Skip to main content

TUMIENI MATOKEO YA SENSA KUFANYA UTAFITI-BALOZI HAMZA

 




IMEANDIKWA NA ZUHURA JUMA, PEMBA

WALIMU na wanafunzi wa vyuo vikuu kisiwani Pemba wametakiwa kuyatumia matokeo ya sensa katika kufanya shughuli za utafiti, ili kuwarahisishia katika kazi zao za kimasomo na kufundishia.

Akifungua kikao cha usambazaji wa matumizi ya matokeo ya viashiria vya sensa ya watu na makazi ya mwaka 2022 kwa wanafunzi na walimu wa vyuo vikuu kisiwani hapa, Kamisaa wa Sensa Zanzibar Balozi Mohamed Haji Hamza alisema, takwimu za matokeo ya sensa zitawarahisishia kufanya utafiti wa haraka.

Alisema kuwa, ni vyema sensa ikatumika kwa ajili ya kufanya utafiti wa baadae kutokana na matokeo yaliyopatikana, hivyo ipo haja kila wanapofanya utafiti kutumia takwimu hizo kwa maendeleo yao na taifa kwa ujumla.

‘’Sensa ina vitu vingi sana tunavyoweza kuvitumia katika mambo yetu mbali mbali, ikiwemo ya kiutafiti, hivyo tuzitumie takwimu hizi za sensa ya watu na makazi ya mwaka 2022 kwa ajili ya kazi zetu,’’ alisema Balozi huyo.

Aidha aliwahamasisha walimu na wanafunzi hao kuelimisha jamii ili ihamasike kuyatumia matokeo ya sensa kufanya utafiti na vitu vyengine vya kimaendeleo, kwani bila ya takwimu utafiti hauwezi kuwa wa kiwango kizuri.



Kwa upande wake Mtakwimu Mkuu wa Serikali Salum Kassim Ali alisema kuwa, kawaida wanafunzi wanatumia tafiti kwa ajili ya mazoezi (field) katika vyuo vyao, hivyo aliwashauri walimu kuwahamasisha wanafunzi wao kutumia sekondari data kwani ni rahisi.

‘’Tumewaita hapa kuwafahamisha kwamba mnapopewa kazi za utafiti kule vyuoni basi mjitahidi kutumia takwimu ambazo zimepatikana kutokana na matokeo ya sensa, hivyo zitakuwa na thamani na wengine pia watatumia,’’ alieleza.

Akiwasilisha mada katika kikao hicho, Meneja Viwango na Utafiti Zanzibar Hamisa Suleiman alifahamisha kuwa, data zote za hatua ya sekondari zitapatikana kwa kufuata utaratibu unaotakiwa, hivyo ni vyema kwanza kupata kibali ambacho kinahitaji kulipiwa.



‘’Tufuate utaratibu mzuri wakati wa kufanya tafiti zetu na sisi tunaangalia data hizo unazitaka kwa lengo gani, ikiwa utafiti huo una maslahi na nchi yetu kwa maendeleo basi tunakupatia,’’, alisema Meneja huyo.

Nae Mwenyekiti wa sensa Balozi Amina Salim Ali alisema, matokeo ya sensa ni muhimu kwa kufanya tafiti mbali mbali, kwani kuna takwimu ambazo zitawasaidia katika masomo yao.

Kwa upande wao washiriki wa mkutano huo walisema, baada ya kuwasilishwa matokeo hayo ya sensa walibaini kwamba, viashiria vingi vya hatari vinatoka Mkoa wa Kaskazini Pemba, hali ambayo imewapa wasiwasi, hivyo kunahitajika utafiti wa hali ya juu kuweza kujua tatizo.



Mkutano huo wa siku moja umefanyika katika ukumbi wa ZRA Gombani Chake Chake ambao umeandaliwa na Ofisi ya Mtakwimu Mkuu wa Serikali Zanzibar kwa lengo la kuihamasisha jamii kutumia matokeo ya sensa kufanya mambo yao ya kimaendeleo.

                                                     MWISHO.                                                              

                                                              

                                

 

Comments