Skip to main content

MEYA JIJI LA CHAKE CHAKE: 'NJOONI MJIFUNZE KWA 'GOMBANI FITNESS CLUB'

 


NA HAJI NASSOR, PEMBA@@@@

MEYA wa jiji la Chake chake Hamad Abdalla Hamad, amevitaka vilabu vyingine vya mazoezi kisiwani Pemba, kuiga mfano unaofanywa na wenzao wa ‘Gombani Fitness club’ kwa kule kuwa karibu na jamii.

Hayo aliyasema leo Machi 30, 2024 mara baada ya kumalizika kwa futari, iliyoandaliwa na klabu hiyo, iliyojumuisha wawakilishi wa vikundi vya mazoezi vya Pemba, watoto mayatima na waumini wengine na dini ya kiislamu na kufanyika ukumbi wa ZRA Gombani.

Alisema, Gombani Fitness Club, imekuwa karibu mno na jamii, kwa kule kujumuika katika shughuli za umma kama za usafi, uchangiaji damu na futari ya kila mwaka.






Alieleza kuwa, klabu hiyo haipo tu kwa ajili yakufanya mazoezi pekee, kama vilivyo vilabu vyingine, bali wanakwenda mbali zaidi, kwa kuwa karibu na jamii kivitendo.

‘’Mfano huu wa futari mlioiandaa, kuchangia kwenu damu kwenye shughuli mbali mbali za umma, kushiriki usafi ni mambo ya kuigwa na vilabu vyingine,’’alieleza.

Aidha alieleza kuwa, ibada walioifanya ya kufutarisha watu wa mkaundi mbali mbali wakiwemo mayatimu na watu wenye kipato cha chini, wamejikusanyia fadhila kubwa, mbele ya Muumba.

‘’Muumba wetu ameshatuahidi malipo makubwa kwa mtu anayemfutarisha mwenzake hata kwa tone la maji au kukokwa moja ya tende, na utamaduni huu uendelee,’’alifafanua.

Katika hatua nyingine, Meya huyo wa jiji la Chake chake Hamad Abdalla Hamad, alisema mazoezi bado yatendelea kuwa ndio ngao kubwa kwa afya bora ya mwanadamu, hivyo kila mmoja anaowajibu huo.



Mapema Makamu Mwenyekiti wa Gombani Fitness Club Hamad Ali Malengo, alisema klabu yao, itaendelea na utamaduni huo kila mwaka, ili kuyakushanya makundi mbali mbali, kweye futari kama hiyo.



‘’Tunaahidi kuwa, sisi Gombani Fitness Club, kila mwaka utamaduni huu tutauendeleza, na tutaendelea kuchukua watu wa  makundi mbali mbali, ili kujumuika nao,’’alieleza.

Katibu wa klabu hiyo Khalfan Amour Mohamed, alisema futari ya mwaka huu walioandaa, imetanua wigo kwa kuvishirikisha vilabu vyote vikuu vya mazoezi vya wilaya nne za Pemba.




Alieleza kuwa, waliamua kufanya hivyo, ili kuongeza urafiki, umoja na mshikamani baina yao na vilabu vyingine vya mazozi kisiwani humo.

‘’Ndio maana hata mara hii, futari yetu imechukua watoto mayatima, viongozi wa dini, watu wenye kipato cha chini, wanachama wetu na wanachama wa vilabu vyingine hapa kisiwani Pemba,’’alieleza.










Miongoni mwa waalikwa wengine ni Afisa Mdhami wizara ya Utalii na Mambo ya Kale Pemba, Afisa Mdhamini wizara ya Ujenzi, Mawasiliano na Usafirishaji, viongozi wa dini, watu maarufu, waandishi wa habari, watu wenye mahitaji maalum na mayatima.

                                          Mwisho

Comments