
NA HABIBA ZARALI PEMBA@@@@
Mara nyingi ndoto
hizo, hukwama si kwa sababu ya ukosefu wa uwezo, bali ni vikwazo, vinavyotokana
na mitazamo hasi ya jamii, unyanyapaa na kukosekana kwa mifumo jumuishi.
Katika kipindi
ambacho dunia inaendelea kusisitiza usawa wa kijinsia, haki za binadamu na
maendeleo jumuishi, wanawake vijana wenye ulemavu, bado ni miongoni mwa makundi
yanayokabiliwa na changamoto kubwa za kutoshirikishwa.
Licha ya kuwa na
uwezo, elimu na vipaji, wengi wao hukosa nafasi, kutokana na mazingira
yasiyowawezesha kushiriki kwa usawa.
Awena Khamis Rashid, mwenye ulemavu wa ngozi (albino), kutoka mkoa wa kaskazini
Pemba, anasema wao mara nyingi, hushirikishwa kwa jina tu, lakini si kwa
vitendo.
Maana hupewa
mwaliko kwenye mikutano, warsha na majukwaa mbalimbali, lakini maoni yao
hayapewi uzito unaostahili, wingine.
“Wakati mwingine,
tunaitwa kwenye mikutano ili kuonekana tumeshirikishwa tu, lakini mawazo yetu
hayaingii katika maamuzi ya mwisho,’’anasema.
Katija Mbarouk Ali
kutoka wilaya ya Wete, mwenye ulemavu wa viungo, anasema changamoto kubwa
wanayokutana nayo, si uwezo wao, bali mtazamo funyu wa jamii, unaowafanya
waonekane hawafai kuwa viongozi.
“Pamoja na kujitolea kwetu, bado jamii inatuchukulia kuwa watu wasio na uwezo,
na wasiostahili kupewa nafasi yoyote,’’anafafanua.
Hali hiyo wakati
mwingine, hutufanya wakose ushirikiano unapojitokeza katika nafasi za uongozi
au vikao ngazi ya shehia.
Amekuwa akishiriki
katika nafasi mbalimbali za uongozi, ikiwemo kuwa mjumbe wa Jumuiya ya Watu
Wenye Ulemavu wilaya ya Wete, mjumbe wa Baraza la Vijana Taifa, Katibu wa
Kikundi cha Elimu Mkombozi Wete, msaidizi wa sheria na mjumbe katika ngazi
mbalimbali za kijamii.
Aliwahi kugombea
nafasi ya uwakilishi wa viti maalum mwaka 2015, na mwaka 2025 aligombea nafasi
ya uwakilishi wa Jimbo la Kojani, ingawa hakufanikiwa kushika hatamu.
Mkasi Simai Makame,
mwenye ulemavu wa kuona kutoka wilaya ya Mkoani, anasema wakati mwingine watu
wenye ulemavu, hualikwa kwenye mikutano kama sehemu ya kutimiza idadi ya washiriki,
na sio vyenginevyo.
Anasema changamoto hizo zilianza tangu akiwa mdogo, ambapo aliwahi kufungiwa
ndani, kwa miaka kadhaa kutokana na imani kuwa, ulemavu wake ulimfanya ashindwe
kufanya jambo lolote.
“Nilionekana siwezi
lolote, lakini baada ya kutolewa ndani na kupelekwa skuli, nilianza kuamini
uwezo wangu, leo najishughulisha na kazi zangu na najitegemea,” anasema.
Mratibu wa Baraza
la Taifa la Watu Wenye Ulemavu Zanzibar upande wa Pemba, Mashavu Juma Mabrouk,
anasema wanawake wenye ulemavu, wana uwezo mkubwa wa kuwa viongozi, iwapo
watawezeshwa na kuaminiwa.
“Wanawake wenye ulemavu wana uwezo wa kuongoza kama watu wengine,
kinachohitajika ni kuondoa vikwazo vinavyowazuia kushiriki kikamilifu, katika
maendeleo na maamuzi,” anasema.
Kwa mujibu wa Ofisi
ya Mtakwimu Mkuu wa serikali (OCGS), kwenye taarifa yake mwaka 2024, inaonesha
kuwa mwaka 2023, Zanzibar ilikuwa na watu 8,100 wenye ulemavu waliosajiliwa,
wakiwemo wanawake 3,838 na wanaume 4,262.
Afisa Programu wa ‘WYDE’ kutoka TAMWA, Sophia Ngalapi, anasema ushiriki wa
wanawake wenye ulemavu katika uongozi una umuhimu mkubwa, kwa sababu huwapa
nafasi ya kuwakilisha mahitaji ya makundi ambayo mara nyingi husahaulika.
Hata hivyo, bado wanawake wengi wenye ulemavu hukosa fursa za elimu bora, mafunzo ya uongozi, ajira, mikopo na nafasi za kushiriki, katika vyombo vya maamuzi
Shirika la Afya
Duniani (WHO), linaarifu kuwa, zaidi ya watu bilioni 1.3 duniani wanaishi na
aina fulani ya ulemavu, sawa na takribani asilimia 16 ya idadi ya watu duniani.
Hali hiyo inaonyesha
umuhimu wa kujenga jamii inayojumuisha watu wote, katika nyanja mbalimbali za
maisha.
Shirika la Umoja wa
Mataifa la Wanawake (UN Women) linaeleza kuwa, wanawake wenye ulemavu
hukabiliwa na changamoto za ubaguzi unaotokana na jinsia pamoja na ule
unaotokana na ulemavu wao.
Hali hiyo
imechangia kundi hilo, kuwa na uwakilishi mdogo katika nafasi za uongozi, ajira
na maamuzi.
Nalo Shirika la
Kazi Duniani (ILO), linabainisha kuwa, wanawake wenye ulemavu wako katika
hatari kubwa zaidi ya kukosa ajira na fursa za kujitegemea, kiuchumi kuliko
wanawake wasio na ulemavu.
Aidha, UNICEF
inaeleza kuwa elimu jumuishi ni msingi muhimu wa kuwawezesha watoto na vijana
wenye ulemavu, kushiriki kikamilifu katika maisha ya baadaye.
Sheria ya Watu
Wenye Ulemavu Na. 8 ya mwaka 2022 inatambua haki ya watu wenye ulemavu kupata
fursa sawa katika elimu, ajira, huduma za jamii na ushiriki katika maendeleo
bila ubaguzi.
Sera ya Taifa ya Watu
Wenye Ulemavu ya mwaka 2004, kwenye ibara zake kadhaa, inalenga kuondoa vikwazo
vinavyowazuia kushiriki kikamilifu katika maendeleo.
Katika ngazi ya
kimataifa, Tanzania imeridhia Mkataba wa Umoja wa Mataifa wa Haki za Watu Wenye
Ulemavu (CRPD), wa mwaka 2006 ambao unatambua haki za wanawake wenye ulemavu
kushiriki katika maisha ya kisiasa na maamuzi ya umma.
HATUA ZINAZOCHUKULIWA
Mkuu wa Idara ya
Maendeleo ya Jamii, Jinsia na Watoto Pemba, Mwanaisha Ali Massoud, anasema serikali
imeendelea kuweka programu za kuwawezesha wanawake wenye ulemavu, kwa kuwapatia
mafunzo ya uongozi, mikopo na fursa katika vikundi vya kiuchumi.
“Hakuna mtu
anayepaswa kuachwa nyuma katika masuala ya kiuchumi, kisiasa, uongozi na
kijamii,” anasema.
TAMWA Zanzibar
inasisitiza kuwa hatua inayohitajika sasa si kutunga sheria mpya pekee, bali kuhakikisha
sheria zilizopo zinatekelezwa kikamilifu.
Shirika hilo linashauri kuongeza uwakilishi wa wanawake wenye ulemavu katika
taasisi za umma, vyama vya siasa, sekta binafsi na kamati za maendeleo.
Pia linashauri
kuimarishwa kwa elimu jumuishi, teknolojia saidizi, lugha ya alama, miundombinu
rafiki na kampeni za kuondoa unyanyapaa.
Awena Khamis Rashid anasema watu wenye ulemavu wangepewa nafasi maalumu za
uwakilishi ili waweze kusimamia changamoto zao katika ngazi za maamuzi.
Naye Mwanaisha Ali Massoud anasisitiza umuhimu wa kuwaandaa watoto wenye
ulemavu tangu wakiwa wadogo kupitia familia, shule na mabaraza ya watoto ili
wajenge kujiamini na uwezo wa kushiriki katika uongozi baadaye.
HITIMISHO
Wanawake vijana
wenye ulemavu si kundi la kuhurumiwa, bali ni nguvu muhimu katika ujenzi wa
jamii na taifa.
Changamoto
inayowakabili si ukosefu wa uwezo, bali ni vikwazo vya kijamii, kimazingira na
kimfumo vinavyowazuia kutumia uwezo wao kikamilifu.
Kuwapa nafasi
wanawake wenye ulemavu katika uongozi na maamuzi si hisani, bali ni haki yao ya
msingi.
Zanzibar na
Tanzania kwa ujumla zitafikia maendeleo jumuishi pale kila mwananchi
atakapopewa nafasi sawa ya kushiriki na kuchangia katika maendeleo ya taifa.
MWISHO



Comments
Post a Comment