NA MOZA SHAABAN, PEMBA@@@@
KATIKA zama hizi, wanawake wanakabiliwa na
changamoto kadhaa, ikiwemo utelekezwaji.
Ambao kwa kiasi
kikubwa, unaathari za moja kwa moja katika uchumi na ustawi wa maisha yao.
Mara nyingi,
utelekezwaji huo hufanywa na wanaume kutokana na sababu kadhaa, huku wengi wa
wanaotelekezwa, wakitupia lawama ndoa za mke zaidi ya mmoja.
Katika hili, wanawake
wengi waliofanya mahojiano na mwandishi wa makala hii, ambao wamewahi
kutelekezwa walisema, chanzo ni ndoa za mke zaidi ya mmoja.
Huku Afisa ustawi wa
jamii wilaya ya Wete Salma Saleh Hamad akigongea msumari kuwa, katika idadi ya
mashauri ya kesi za utelekezaji wanazopokea ofisini kwao, asilimia 90 yanaonesha
chanzo ni ndoa za mke zaidi ya mmoja.
NINI UTELEKEZAJI FAMILIA?
Ni kule mtu kushindwa kupeleka mahitaji kwa
yule unaepaswa kumpa, hali ya kuwa unauwezo wa kutoa mahitaji hayo.
Utelekezaji unaweza kuwa wa moja kwa moja au
katika huduma za elimu, afya na hata kihisia.
Ingawa Serikali na wadau wengine,
wanaoshughulikia haki za wanawake na watoto wanalipiga vita suala la
utelekezaji, lakini bado, kuna baadhi ya wanaume hawawajibiki kwa chochote,
kuhusu mahitaji ya msingi ya familia zao.
Kwani, wapo wasiotoa huduma zote za lazima na
wengine huenda mbali zaidi, kwa kuzitelekeza kihisia, ikiwa ni pamoja na
kuwatishia, kuwadharau na kuwatenga.
Kwamujibu wa hutuba
ya bajeti ya wizara
ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia Wazee na Watoto ya mwaka 2026/2027 malalamiko 390,
ya matunzo yameripotiwa Unguja na Pemba.
Kati ya hayo 238 yaliripotiwa Unguja na152 kwa
upande wa Pemba.
Hii nikuonyesha wazi kwamba, wapo wanaume
wanakwepa majukumu yao ya msingi na kuyawacha kwa wake zao au waliowahi kua
wake zao, jambo linalozorotesha ustawi
wao kiuchumi.
Katika hili Bishara Guluma Haji (sio jina lake rasmi)
anasema, hali yake ya kiuchumi ilianza kua ngumu, baada ya mumewake aliezaa nae
watoto watatu, kutomshughulikia kwa chochote.
Akasema, kuanzia hapo akawa ombaomba kwa jirani
na wakati mwingine kwa ndugu wa muume, na wapita njia.
Mwingine mkaazai wa Pandani Wete, anasema yeye
hakuachwa, ingawa baada ya muume wake waliezaa watoto wanane, kuongeza mke.
Hili linakwenda sambamba na Fatma Iddi Pandu wa
Micheweni, anasema baada muume wake kutangaaza ndoa, alifika Idara ya Ustawi wa
Jamii, na sasa anaendelea kupokea huduma.
‘’Miaka mitano nyuma alioa Tanga, na hukudu
huduma zilidorora, nikamfuatilia na alikuwa analeda huduma kwa mbinde, hadi
alipoamua kurudi kwangu baada ya kutoa talaka huko,’’anasema.
Kumbe muume huyo, kisha alioa mjini Chakechake,
na kwa siku tano, hakupeleka huduma kwa mke wake mkubwa, ndipo mama huyo
kufikisha lalamiko lake sehemu husika na kufanikiwa.
Hata mwanamke mwingine (hakupenda jina lake
lichapishwe), anasema mwaka 2024, alikopa shilingi 150,000 ili anzishe biashara
ya uji na maandazi, na alishaanza kuresha shilingi 50,000.
Mwanamke huyo, miezi minne baadae, aliachwa na
watoto wanne, na sasa anaendeleza biashara hiyo ingawa, mpango wa kurejesha umekaa
upande.
‘’Kwa hakika biashara inakwenda, lakini kwa
vile sipokea huduma kwa ajili ya watoto, niachouza kinaishia tumboni na
nashindwa kulipa shilingi 100,000,’’anasema.
WANAUME WANAOTUHUMIWA WANASEMAJE
Issa Hassan Mjawiri, akiri kuwa baada ya
kufunga ndoa hakuwa akipeleka huduma, ingawa ilisababishwa na mke wake mkubwa,
kuzikataa.
‘’Alisema kama natakaoa nikaoe, lakini kwa vile
yule mwandani wangu ni alidai ni mshirikiana, hatopokea huduma yoyote kutoka
kwangu, ingawa baadae alishitaki serikalini,’’anaeleza.
Uledi Makame Hamdu wa Micheweni, anasema sio
kweli kwamba wanapokwenda dago hushindwa kuacha huduama kama wanawake wanavyo
dai, bali ni kutupaka matope.
‘’Kwa mfano mimi huondoka hadi siku 90, kwenda
Tanga, lakini kwa mara ya mwsiho niliporudi dukani, nililipa shilingi 300,000
za chakuka na huduma nyingine,’’anasema.
Kumbe, anakiri kuwa wingi wa wanawake
wanapokwenda kuoa ama dago, huwa na wanalilia wivu, kwamba huwenda tukarudi na
wake tukitoka safari.
Kombo Ali Kombo wa Kiuyu Mbutuni, anakiri kuwa
yeye akiondoa haachi huduma kamili, ingawa anapofika eneo la uvuvi hutuma fedha
skili wiki mara moja.
‘’Ni kweli kwa wiki mbili za mwanzo, ndanu
huacha mchele na sembe tupu, maana fedha ninayopaswa kuwaachia huifanya nauli,
lakini kisha huwa natuma,’’anaelekeza.
Ingawa Jongo Hakim Makame, anasema wapo baadhi
ya wavuvi wenzake, wamekuwa wazito kuzihudumia familia zao, wakiwa na madau
yasio na msingi, kama kuacha shamba la migomba na mihogo.
JE NINI ATHARI YAKE?
Mratibu wanawake na watoto shehia ya
Maziwang’ombe wilaya ya Micheweni, Nusura Ali Mbara anasema, kutokujua nini
utelekezaji na athari zake ni moja ya sababu zinazopelekea hali hiyo.
Anasema wanaume wengi hawana uelewa wa kutosha
juu ya madhara ya kutelekeza familia, ndipo baadhi yao huziacha familia zao,
bila huduma kwa kishingizio cha kutafuta maisha.
Khamis Shaame Khamis wa Maziwang’ombe anasema,
kukosa upendo, huruma na uadilifu inapelekea wanaume kutelekeza familia zao,
tena hasa baada ya kuoa mke zaidi ya mmoja.
Anafafanua kuwa, iwapo mtu atakosa uadilifu na
huruma kwa familia yake ni rahisi, kuikimbia hata katika kipindi ambacho
wanamuhitaji zaidi.
Aisha Haji Kombo, anasema moja ya athari hizo
ni kuwakosesha watoto haki za kula na elimu kuzorotesha afya zao.
Mayasa Hassan Hussein ‘bi mayaa’ anasema
huwakosesha wanawake haki ya mapunziko na saa 24 kuwa maeneo ya msako wa
huduma.
ATHARI ZAKE NI ZIPI KWA UCHUMI WA MWANAMKE?
Mkaazi Micheweni Pemba Bishara (sio jina lake
halisi) anasema, kuoa mke zaidi ya mmoja ni miongoni mwa sababu za utelekezaji
familia.
Anafafanua hali hio huongeza wingi wa majukumu
na kusababisha hali ngumu ya maisha
inayompelekea, mtu kushindwa kumudu mahitaji ya msingi ya wanaomtegemea.
‘’Baba watoto wangu alikua hana kazi maalumu
yakumuingizia kipato, wakati tushapata watoto watatu akaongeza mke, kisha majukumu
yakamzidi, akaanza kutunyima huduma za msingi,’’ anaeleza.
Bisimba Khamis Mwinyi mkaazi wa Micheweni Pemba
anasema, ni kukosa muda wa kutosha kufanya shughuli za kujiendeleza kiuchumi, kama biashara ndogo.
Anaeleza kuwa mwanamke alietelekezwa hua na majukumu ya ziada, yanayomkosesha nafasi na
fursa muhimu za kiuchumi kama kilimo,
biashara na ujasiriamali.
Kwa upande wake Khatib Sharif Hassan wa
Micheweni Pemba anaona, athari nyengine ni kutengwa na jamii, hasa yanapokuja
masuala ya biashara.
Anafafanua kua, mara nyingi utelekezwaji
huambatana na unyanyapaa wa kijamii, ambapo jamii huacha kumshirikisha mwanamke,
alietelekezwa kwa kisingizio cha kukosa muda na uwezo wa kufanya vizuri.
Mwanasaikolojia Fatma Mohamed Khalfan anasema,
utelekezaji familia, humpotezea muelekeo mwanamke kwa kumfanya aangalie zaidi
namna ya kuziba pengo lililowachwa badala ya kuwa mchumi.
Anasema, uchumi wa mwanamke huwa rahisi kukua,
ikiwa kwa wale waliokwenye ndoa au mahusiano wataimiziwa huduma za msingi.
“Kiuhalisia saikolojia ya mama hubadilika punde
tu baada ya kutelekezwa, kama alikua mtafutaji mzuri hubadili muelekeo na
kujikita zaidi, kuziba pengo la malezi,’’anaanisha.
Afisa ustawi wa jamii Salma Saleh Hamad
anasema, utelekezaji hupelea umaskini uliokithiri kwa mwanamke, kwani anapoteza
fursa ya kuwekeza katika biashara au njia nyengine za kujiingizia kipato.
‘’Inawezekana ipo mikopo ya masharti nafuu,
lakini mwanamke aliyetelekezwa na hasa akiwa na watoto, macho yake hayoni na
akili yake haibaugui, anachojali na kuihuduma familia,’’anasema.
JE SHERIA ZINASEMAJE?
Sheria zote duniani zinapinga utelekezaji wa watoto kutokana na msingi
kwamba, bado wanategemea malezi na huduma kutoka kwa wazee au walezi wao.
Ina maana kwamba, matendo mabaya dhidi ya watoto yanakemewa na sheria za kimataifa, za kikanda na sheria
za nchi husika.
Mfano Mkataba wa Kimataifa wa
haki za Watoto Duniani (CONVENTION
OF THE RIGHTS OF THE CHILDREN)
wa mwaka 1989, ulianza kutumika 1990, kifungu cha 9 kinasisitiza nchi
wanachama wa Umoja wa Mataifa kuhakikisha watoto, hawatelekezwi.
Na kifungu cha 19 cha Mkataba wa haki na Ustawi wa Watoto wa Afrika wa
mwaka 1999, kinaelezea
kila mtoto anayohaki ya kufurahia na kunufaika na malezi bora ya wazazi, ana
haki ya kuishi na mzazi au wazazi wake.
Sheria ya Watoto
Zanzibar, namba 11 ya 2011 kifungu cha 9 (1) kinaelekeza haki ya mtoto kuishi na wazazi
wake, walezi au familia, ili akue kwa upendo na mazingira salama.
MITANDAO YA KIJAMII IMERIPOTI NINI?
Mitandao ya kijamii imeripoti
kua zaidi ya robo tatu ya wanawake wote duniani, hupoteza kipato na kushindwa
kujitegemea kimaisha, kutokana na kuachiwa mzigo wa malezi na migogoro ya
kifamilia.
NINI KIFANYIKE?
Mratibu wanawake na watoto Maziwang’ombe Nusura
Ali Mbara anasema, elimu juu ya athari za utelekezaji wa familia itolewe ili
kutokomeza suala hili.
Afisa ustawi wa jamii Salma Saleh Hamad anasema
ni vyema kwa kina mama kuripoti na kutoa mashirikiano ya kutosha kwa vyombo vya
sheria, ili kudhibiti hali hii.
Mkuu wa mkoa wa kaskazini Pemba Mgeni Khatib
Yahya anasema, kwa vile serikali kupitia ofisi ya mufti hutoa mafunzo ya ndoa,
yanayo wakumbusha wanandoa wajibu wao, ni vizuri wakayatumia, ili kila mmoja atimize
majukumu yake.
Afisa pragramu wa mradi wa kupambana na ukatili
na unyanyasaji wa kijinsia dhidi ya wanawake na watoto kutoka TAMWA- Zanzibar
Asiya Hakim Makame, ametahadharisha kuhusu chanagmoto ya utelekezazi na madhara yake kwa uchumi wa
mwanake.
Anasema changamoto hiyo, ni miongoni mwa zinazosababisha
udhalilishaji kwa wanawake na watoto, pamoja na anguko la kiuchumi.
Anashauri wanawake, kutoyafumbia macho matendo
ya utelekezaji na badala yake waripoti, katika mamlaka husika ili hatua zaidi
zichukuliwe.
MTAZAMO
WA DINI
Sheikh Said
Ahmad Mohamed anasema, ni kosa kwa mume kuitelekeza familia yake, kwa sababu yeyote
ile.
Anaeleza kuwa, wanahitajika wanaume kutoa
matumizi kwa ajili ya wake zao na familia zao, kama ilivyopokelewa kutoka kwa
Abdallah bin Amru kwamba…
"Inatosha mtu katika dhambi kuwatupa
wale ambao anawajibika yeye kuwapatia matumizi"
Ikiwa na maana kwamba, kuwapatia matumizi wale
unaowajibika kuwapa, ni kheri kubwa.
MWISHO



Comments
Post a Comment