Na Muandishi Wetu Zanzibar
Mwenyekiti wa Kamati yaMapngo
wa Kitaifa wa Kutokomeza Ukatili dhidi
ya Wanawake na Watoto, ambaye pia ni Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Katiba,
Sheria, Utumishi na Utawala Bora, Mhe. Haroun Ali Suleiman, amewataka wadau
wanaojihusisha na masuala ya ukatili na udhalilishaji kufanya kazi kwa weledi
na ushirikiano ili kutokomeza vitendo hivyo katika jamii.
Mhe. Haroun alitoa wito huo
jana wakati wa uzinduzi wa Kamati ya Kitaifa ya ngazi ya Mawaziri uliofanyika
katika Ukumbi wa Hoteli ya Golden Tulip Airport, Zanzibar.
Alisema kuwa lengo la kuundwa
kwa kamati hiyo ni kuimarisha ushirikiano kati ya taasisi mbalimbali katika
kupambana na vitendo vya ukatili na udhalilishaji dhidi ya wanawake na watoto,
kwa lengo la kupunguza na hatimaye kuvimaliza kabisa.
Aidha, aliitaka kamati hiyo
kutekeleza majukumu yake kwa bidii, kuweka mikakati madhubuti na kuhakikisha
sheria pamoja na sera zilizopo zinatekelezwa ipasavyo ili kulinda haki za
wanawake na watoto.
Kwa upande wake, Mwenyekiti
Mwenza wa Kamati hiyo ambaye pia ni Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee
na Watoto, Mhe. Anna Athanas Paul, alisema Wizara yake itaendelea kushirikiana
na wadau wa maendeleo katika kuimarisha mifumo ya ulinzi wa jamii.
Alisema Serikali kupitia
Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto itaendelea kutoa elimu
kuhusu haki za wanawake, watoto na wananchi kwa ujumla ili kujenga jamii yenye
kupinga vitendo vya ukatili na udhalilishaji.
Naye Afisa Programu za Jinsia
kutoka Shirika la Umoja wa Mataifa la Idadi ya Watu (UNFPA), Ali Haji Hamadi,
alisema shirika hilo litaendelea kushirikiana na Serikali katika kusaidia
utekelezaji wa programu zinazolenga kulinda haki, afya na ustawi wa wanawake,
watoto na vijana.
Katika uzinduzi huo, Mkuu wa
Divisheni ya Watoto, Mohammed, aliwasilisha muhtasari wa Mpango wa Kitaifa wa
Kutokomeza Ukatili dhidi ya Wanawake na Watoto wa miaka mitano (2025–2030),
akieleza mpangilio wa utekelezaji wake, ushirikiano wa sekta mbalimbali na
wadau wa maendeleo, pamoja na mfumo wa uratibu, ufuatiliaji na tathmini ya
mpango huo.
Kwa upande wa Mkuu wa
Divisheni ya Maendeleo ya Jamii, ndugu Omar Haji, aliwasilisha muundo na
majukumu ya Kamati hiyo. Alieleza kuwa Kamati itaongozwa na Waziri
anayeshughulikia masuala ya sheria, ndie mwenyekiti huku Waziri anayesimamia
masuala ya jinsia akiwa Mwenyekiti Mwenza, kamati hiyo inawajumuisha Wizara,na
taasisi za Kiserikali na binafsi na washirika wa maendeleo.
Alisema miongoni mwa majukumu
makuu ya Kamati hiyo ni kutoa mwongozo wa kisera, kuhakikisha afua zinaendana
na mikakati ya kitaifa, kushawishi ugawaji wa bajeti kwa ajili ya utekelezaji
wa mpango kazi, kusimamia usimamizi wa kesi za ukatili na kuhakikisha mashitaka
yanawasilishwa na kuendeshwa kwa wakati.
Uzinduzi wa Kamati ya Kitaifa ya Kutokomeza
Ukatili na Udhalilishaji dhidi ya Wanawake na Watoto ulihudhuriwa na viongozi
na wadau mbalimbali, wakiwemo mawaziri, wakuu wa mikoa na wilaya, Jeshi la
Polisi, Ofisi ya Mufti Mkuu wa Zanzibar, Ofisi ya Mkurugenzi wa Mashtaka (DPP),
pamoja na washirika wa maendeleo wakiwemo UNICEF, UNFPA na UN Women.
Mwisho
Comments
Post a Comment