NA HAJI NASSOR, PEMBA@@@@
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.
Hussein Ali Mwinyi, asubuhi ya leo April 2, 2026, anatarajiwa kuwa mgeni, rasmi
katika uzinduzi wa mbio za mwenge wa uhuru kitaifa, utakaofanyika, uwanja wa michezo
Gombani Chake Chake Pemba.
Taarifa iliyotolewa na Mkuu wa Mkoa wa kusini Pemba, Rashid
Hadid Rashid, kwa vyombo vya habari, ilieleza kuwa, tayari maandalizi yote
yameshakamilika kwa shughuli hiyo ya kitaifa.
Taarifa hiyo ilieleza kuwa, Dk. Mwinyi ataingia kwenye kitabu
cha kumbukumbu kwa zoezi hilo, ambapo kwa mara ya kwanza, lilifanyika zaidi ya miaka
10 iliyopita kisiwani humo.
Mkuu huyo wa mkoa katika taarifa yake, ilifafanua kuwa, Dk.
Mwinyi atawahutubia wananchi watakaohudhuria, pamoja na kuzindua rasmi mbio za
mwenge wa uhuru kitaifa, kwa mwaka 2026.
Alieleza kuwa, wananchi watakaohudhuria kwenye zoezi hilo la
kitaifa, kabla ya Dk. Mwinyi kufanya uzinduzi huo, watashuhudia burudani kadhaa
uwanjani hapo.
Alisema, miongoni mwa wasanii wanaotarajiwa kuzikonga nyonyo za
wananchi hao, ni msanii Dula Makabila kutoka Tanzania bara.
Wasanii wingine ni Mau Mpemba, K-official, Maswaga na vikundi
vya ngoma ya asili ikiwemo Kiumbizi kutoka Pujini.
Ngoma nyingine ambazo zitatumbuiza ni Uringe kutoka Micheweni,
Kwaya Mkoani, Empare na Msewe wa vijana wa Mchanga mdogo wilaya ya Wete.
‘’Wananchi watakaohudhuria hawatakaa bila ya kufurahia, maana
mkoa na kamati zake, umejipanga kumkonga nyonyo kila atakaehudhuria, ili afurahi
nafsi yake,’’alisema kwenye taarifa yake.
Hivyo Mkuu huyo wa Mkoa wa kusini Pemba Rashid Hadid Rashdi,
ameakumbusha wananchi wa makundi yote, kujitokeza kwa wingi kwenye uwanja wa
Gombani, asubuhi hii.
‘’Niyaombe makundi ya kijamii, kama vijana, wazee, wanawake,
watu wenye ulemavu, vikundi vya mazoezi, wasanii, waandishi wa habari, na wanachama
wa vyama vyote, kuhudhuria leo hii,’’alifafanua.
Juzi, Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Hemed Suleiman Abdulla,
alielezea kufurahishwa kwake na maandalizi ya uzinduzi wa mwenge huo.
Hayo aliyasema alipoutembelea uwanja wa michezo Gombani Chakechake,
ambao utatumika kwa shughuli hiyo, ili kujionea maandalizi yalipofikia.
‘’Baada ya kuutembelea uwanja na hata wale watoto wa halaiki na
maeneo mingine muhimu, nimeridhishwa na kamati zote za maandalizi,’’alifafanua.
Hata hivyo, amewakumbusha wananchi wa mkoa wa kusini Pemba na
maeneo mingine, kuhakikisha wanakiunga mkono, chombo hicho cha taifa.
Baada ya uzinduzi huo mkoa wa kusini
Pemba, mwenge wa uhuru, utakimbizwa mikoa yote ya Jamhuri ya Muungano wa
Tanzania na halmashauri 195 na zitafikia kilele chake, Okotoba 14, mwaka huu mkoani
Rukwa.
Ambapo kaulimbiu ya mwenge wa huru kwa
mwaka 2026 ni “Tanzania ni Yetu Sote, Tushikamane kwa Pamoja Kuleta
Maendeleo’’.
Mwisho

.jpg)
.jpg)
Comments
Post a Comment