Skip to main content

MAUWAJI CHAKE CHAKE YAACHA SIMANZI: WANANCHI WASUBIRI KWA HAMU UPELELEZI POLISI

 


NA HAJI NASSOR, PEMBA@@@@

WANANCHI wa shehia ya Mgogoni wilaya ya Chake chake, wameliomba Jeshi la Polisi mkoa wa kusini Pemba, kuharakisha upelelezi wao, ili kumbaini mtu aliyedaiwa kumbaka na kisha kumuua mwanamke mmoja wa kijiji hicho mwenye miaka 55.

Wananchi hao walisema, kitendo alichitendewa mwananchi mwenzao, sio cha kiungwana na kinafaa kulaaniwa na kila mmoja, na kuliomba Jeshi la Polisi kuharakisha upelelezi wao.

Wakizungumza na mwandishi wa habari hizi, walisema wanasikitishwa mno na mzazi mwenzao, kufanyiwa kitendo hicho na kisha mwili wake, ukiwa hauna nguo kutelekezwa kichakani.

Mmoja kati ya wananchi hao, Mohamed Juma Maalim, alisema kilichobakia kwa sasa pamoja na kushirikiana na Jeshi la Polisi, lakini wanalisubiri kuona upelelezi wao unazaa matunda gani.

“Ni kitendo kinachoumiza hadi ndani ya miili yetu, kuona mtu aliyefanya kitendo hicho, hakuishia tu kwenye kumdhalilisha kingono, lakini kisha kuondoa uhai wake,’’alisema.

Nae Khadija Mjaka Makame, alisema walikuwa wamezoeana mno na mama huyo kabla ya kufanyiwa unyama huo, ingawa kwa sasa wamekosa amani ndani ya mioyo yao.

‘’Amani mtaani kwetu imepotea, maana mzazi wetu aliyekuwa mshauri wetu mkuu, amefanyiwa unyama mara mbili, hivyo kwa sasa tunaliangalia Jeshi la Polisi na upelelezi wake,’’alisema.

Kwa upande wake Asha Muhsin Ameir, alisisitiza haja kwa Jeshi la Polisi, kuharakisha upelelezi wao, kwani kwa sasa wanashindwa hata kula na kunywa, kwa kuumwa na tukio hilo.

‘’Kwa sasa hatuna furaha hapa mtaani, maana tukio hili limetuumiza mno, kuona mama yetu huyu asiye na hatia amefanyiwa udhalilishaji na ukatili mkubwa,’’alifafanua.

Mapema Kamanda wa Polisi mkoa wa kusini Pemba, Abdalla Hussein, akiri kutokea kwa tukio hilo, na kusema tayari Jeshi la Polisi limeshaanza upelelezi wa kina.



Alisema, Jeshi litahakikisha kuwa, linawatia mikononi wahusika wa tukio hilo, na kisha kuwafikisha mbele ya vyombo vya sheria, kujibu madai hayo.

Alieleza kuwa, baada ya kupata taarifa ya tukio hilo, walifika eneo la tukio na kuona kuwa, marehemu huyo, hakuwa na hali nzuri, baada ya kufanyiwa ukatili.

‘’Jeshi la Polisi kufanya uchunguzi wa matukio ya kihalifu ni sehemu ya wajibu wetu, na tukio la mama huyo kudaiwa kubakwa na kisha kuuliwa, tunaendelea kulifanyia kazi,’’alifafanua.

Katika hatua nyingine Kamanda huyo wa Polisi mkoa wa kusini Pemba, aliwataka wananchi kuwa watulivu katika kipindi hiki, wakiendelea na uchunguuzi wao.

‘’Kubwa tunaloomba kwa wananchi ni kuhakikisha, wanashirikiana kwa karibu na Jeshi la Polis, ikiwemo kutoa taarifa za siri, pindi wakihisi kuna mtu wanamdhania,’’alifafanua.

Baadhi ya mashuhuda wa tukio hilo, walisema wakati wanakwenda kwenye shughuli zao za kawaida, waliona nguo za marehemu pembezoni mwa mto, katika eneo lisilo mbali na shamba lake.

Walisema, baadae waliposikia taarifa hizo, walirudi tena kushirikiana na wananchi wenzao, waliokuwa wakimtafuta, na kisha kuuona mwili wa marehemu, ukiwa kichana na hauna nguo.

‘’Eeneo alilofanyiwa udhalilishaji na ukatili mama huyu, ndio eneo hilo hilo, alilofanyiwa jaribio la kubakwa kwa mwanafunzi mmoja mkaazi wa Vikutani Wawi, wakati anakwenda skuli mwaka jana,’’alieleza shuhuda mmoja.

Mama huyo anaekisiwa kuwa na umri wa miaka 55, ni mkaazi wa shehia Mgogoni wilaya ya Chake chake, ambapo mwili wake ulipatikana kichakani, majira ya saa 7:00 mchana.

Matukio ya jinai, inaonesha ongezeko la makosa 32, 221 kutoka matukio 574,881 yaliyoripotiwa katika kipindi cha Januari hadi Disemba mwaka2022.

Ikilinganishwa na matukio 607,102 yaliyoripotiwa katika kipindi kama hicho kwa mwaka 2023, ripoti ya Jeshi la Polisi Tanzania ya mwaka 2023 inafafanua.

Ingawa ripoti hiyo ikafafanua kuwa, kati ya matukio hayo ya jinai, mwaka 2022 pekee, kuliripotiwa matukio 2,464 ya watu kuuliwa, na kuwepo punguzo la matukio 161, kwenye mwaka 2023, kati ya matukio 2, 303 waliouliwa kwa Tanzania nzima.

Hata hivyo, kwa upande wa matukio ya ubakaji, ripoti ikaelekeza kuwa, kwa Zanzibar yenye mikoa mitano, kuliripotiwa matukio 44 ya mauwaji na watu 927 waliripotiwa kubakwa.

Kwenye mkoa wa kusini Pemba, mwaka 2023 pekee kuliripotiwa watu wawili (2) waliouawa na 86 waliripotiwa kubakwa, ripoti hiyo ikazidi kufafanua.

Mwisho 

Comments

BLOG'S VISITORS

DAKTARI MWENGINE CHAKE CHAKE KULA SIKUKUU POLISI, NI KWA TUHUMA ZA KUMBAKA MGONJWA WAKE

NA WAANDISHI WETU, PEMBA::: DAKTARI anaetoa huduma kwa wagonjwa kituo cha afya cha serikali cha  Gombani wilaya ya Chake Chake Pemba, Is-haka Rashid Hadid, anaendelea kushikiliwa na Jeshi la Polisi Mkoa wa kaskazini Pemba, akituhumiwa kumtorosha na kisha kumbaka mtoto wa mwenye umri wa miaka 16, mkaazi wa Gombani. Daktari huyo miaka 35 ni mkaazi wa Kangagani Wilaya ya Wete mkoani humo, ambapo anadaiwa alimchukua mtoto huyo kutoka kwa rafiki yake, na kumpeleka kwenye nyumba anayoishi eneo la Kangagani. Mtoto aliefanyiwa kitendo hicho alisema kuwa, April 21 mwaka huu alikwenda kituo cha afya Gombani, kwa ajili ya matibabu na baada ya kupatiwa huduma na daktari huyo, alimuomba nambari yake ya simu. Alisema ilipofika usiku, walikuwa wanawasiliana kupitia ujumbe mfupi (sms) kwa lengo la kwenda kuchukua dawa nyingine ambazo kwa mchana huo alizikosa hospitalini hapo. "Nilikwenda hospitali kutibiwa, baada ya kufanya mapele katika sehemu zangu za siri, lakini akaniambia mpaka aje da...

'MKAPA' NA WENZAKE PEMBA WALAZWA RUMANDE

  NA HAJI NASSOR, PEMBA@@@@ MAHKAMA kuu Zanzibar kisiwani Pemba, chini ya Jaji Ibrahim Mzee Ibrahim, imewapeleka rumande watumuhimwa wanne wanaokabiliwa na tuhuma za kuua kwa makusudi, akiwemo Ali Mussa Omar ‘ Mkapa’ mkaazi wa Wawi wilaya ya Chake chake Pemba. Watuhumiwa wengine walioanza maisha mapya ya rumande ni mtuhumiwa Yassir Mohamed Juma miaka 23, Anuwari Mussa Omar miaka 30 pamoja na mtuhumiwa Yassir Mussa Omar ‘ Makababu ’ miaka 29, wote wakaazi wa shehia ya Wawi, wilaya ya Chake chake Pemba. Awali watuhumiwa hao waliwasili mahakamani hapo, kwa mara ya kwanza, kwa ajili ya kusomewa tuhma zinazowakabili za kumuua kwa maksudi Said Seif Kombo. Ilidaiwa mahakamani hapo na Mwendesha Mashtaka kutoka Ofisi ya Mkurugenzi wa Mashataka Seif Mohamed Khamis akiambatana na mwenzake Mussa Khamis Ali kuwa, watuhumiwa hao kwa pamoja wanadaia kufanya mauwaji hayo kwa maksudi. Ilidai kuwa, watuhumiwa wote kwa pamoja, walitenda kosa hilo Oktoba 16, mwaka huu, baina ya saa 7:00 m...

HII KALI MBUNGE ASIYA AMKOGESHA MWANANCHI HADHARANI KISA HICHI HAPA......

  NA HAJI NASSOR, PEMBA MBUNGE wa viti maalum nafasi za wanawake mkoa wa kaskazini Pemba Asiya Sharif Omar, amewataka wananchi wa kijiji cha taifu, shehia ya Kinyasini jimbo la Gando wilaya ya Wete Pemba, kuyalinda miundombinu ya maji safi na salama, ili yawe endelevu kwao. Kauli hiyo ameitoa wakati alipokuwa akizungumza na mwandishi wa habari hizi, mara baada ya kuwasili kijijini humo, na kumkogesha mwananchi mmoja kama ishara ya uzinduzi wa mradi wa maji safi na salama, ulioasisiwa na mbunge wa Jimbo la Gando. Alisema, hawana mbadala kwa sasa bali ni kuilinda miundombinu ya huduma hiyo, hasa baada ya mbunge wa wao Salim Mussa Omar, kuwarejeshea huduma hiyo. Alieleza kuwa, inafahamika kuwa kwa miaka 14 waliikosa huduma hiyo hasa kwa vile viongozi waliokuwepo hawakujali kuwatatulia tatizo hilo, hadi juzi ilipofanywa na mbunge wao. “Baada ya huduma hii sasa kurejeshwa na mbunge wa jimbo la Gando, kazi iliyobakia kwenu wananchi ni kila mmoja kuwa mlinzi wa miundombinu hii,’...

…….SUZA WATOA USHAURI WA ADHABU YA KUNYONGWA

  NA HAJI NASSOR, PEMBA@@@@ WANAFUNZI wanaosomea uwalimu Chuo cha taifa cha Zanzibar ‘SUZA’ kampasi ya Benjamin Wiliam Mkapa Wete Pemba, wamependekeza adhabu ya kunyongwa hadi kufa, kwa mtu atakaetiwa hatiani, kwa kosa la dawa za kulevya. Walisema, haiingii akili kuona, mahkama imeshamtia hatiani mtu kwa kukutwa na dawa za kulevya, ambazo huathiri nguvu kazi ya taifa na kisha, kupewa hukumu ya kifungo pekee. Wakizungumza leo Juni 26, 2024 kwenye kongamano la vyuo vikuu, juu ya masuala ya msaada wa kisheria, kuelekea wiki ya msaada wa kisheria Zanzibar, lililofanyika Chuoni hapo, walisema wakati umefika sasa kutolewa kwa hukumu hiyo. Walipendekeza kuwa, ni vyema kwa mtu anayetiwa hatiani asibakie chuo cha Mafunzo pekee kuitia tena hasara serikali kwa chakula na wakati mwingine matibabu, wakati tayari ameshasababisha madhara, kwa vijana. Mshiriki Juma Nafasi Juma, alifafanua kuwa kama mtu ameamua kuliumiza taifa kwa kuingiza, kusafirisha, kusambaaza dawa za kulevya, hivyo n...

HABARI ZA HIVI PUNDE

 TAARIFA za hivi punde, zilizofikia ofisi ya Pemba Today, zinaeleza kuwa, Jeshi la Polisi mkoa wa kaskazini Pemba, linamshikilia askari mwenzao, kwa tuhuma za ubakaji ndani ya moja ya kituo cha Polisi kisiwani Pemba Muume wa mwanamke aliyedai kubakwa na Mwanamke mwenyewe, wamedai kutokea kwa tendo hilo, na huku Kaimu Kamanda wa Polisi mkoa wa kaskazini Pemba, akithibitisha kupokea kwa lalamiko hilo.... Kwa taarifa zaidi ya tukio hili endelea kufuatilia mtandao huu, ambao kukuhabarisha ni fahari yetu...