Skip to main content

WANANCHI MTEGA WAWI WAKARABATI BARABARA YAO KWA MATOFALI

 



NA HAJI NASSOR, PEMBA @@@@

WANANCHI wa kijiji cha Mtega, shehia ya Wawi wilaya ya Chake chake Pemba, wameamua kuikarabati barabara yao yenye urefu wa kilomita 2.5, kwa kutumia matofali ya fuuwe na mawe, baada ya kuharibika kwa mvua, inayoendelea kunyesha.

Mwandishi wa habari hizi, aliwashuhudia wananchi hao, wakiwa kwenye eneo la barabara hiyo, wakiikarabati barabara hiyo, kwa kutumia vipande vya matofali na mawe, ili iweze kupitika.

Wananchi hao walisema, uamuzi huo umekuja kufuatia kukosa misaada kutoka mamla husika, hali iliyopekea mvua kuathiri barabara yao.

Mwenyekiti wa kamati ya maendeleo ya kijiji hicho, Khamis Haji, alisema barabara hiyo imeharibika mno, kufuatia mvua zinazoendelea kunyesha nchini kote.

Alieleza kuwa, juzi Mei 4, kamati iliikagua barabara hiyo, na kufikia uamuzi wa kutafuta matofali na mawe, ili kuikarabati katika maeneo, yalioathiriwa zaidi na mvua.

‘’Hivi sasa, kama atatokezea mgonjwa ama mzazi anataka kwenda hospitali, inabidi tutumie gari za Ng’ombe au tutumie magunia hadi njia kuu,’’alieleza.

Mwenyekiti huyo alieleza kuwa, kwa sasa kwenye kijiji chao cha Mtega hakufika, gari wala chombo chochote cha maringi mawili, kutokana na kukatika na kuchimbika kwa barabara yao.

Wakati huo huo, Mwenyekiti huyo amepiga marufuku tabia ya baadhi ya wananchi kuchota mchanga kwenye barabara hiyo, na kusema, atakaepatikana atafikishwa mbele ya vyombo vya sheria.



‘’Wapo baadhi ya wananchi wenzetu, kwa maksudi huchimba mchanga kwenye barabara hii, hivyo tunawataka kila mmoja awe mlinzi kwa mwenzake,’’alifafanua.

Katika hatua nyingine, amemtaka Mbunge na Mwakilishi wa Jimbo la Wawi, kuzitekeleza ahadi walizoziweka za kuwapatia kifusi kwenye bara bara hiyo.

Mshika fedha wa Kamati hiyo, Mwalimu Juma Yahya, alisema kusita kwa mchango wa shilingi 50,000 kwa kila nyumba, ambazo ilikuwa ni kwa ajili ya ununuzi wa kifusi, kumesababisha uchakavu wa barabara hiyo.

‘’Kama lile zoezi la uchangiaji wa fedha, kwa ajili ya ununuzi wa kifusi twengelikamilisha kabla ya mvua, leo barabara yetu isingeharibika sana,’’alieleza.

Hata hivyo, amewakumbusha wananchi wa kijiji cha Mtega na wengine, kuendelea kutoa michango yao, ili kufanikisha ununuzi wa kifusi, mara mvua zitakapomalizika.

Mjumbe wa kamati hiyo Rashid Ali Mussa, alisema lazima katika kipindi hichi cha mvua, mkazo wa kuifanyia ukarabati barabara hiyo uwekwe, na wananchi wenyewe bila ya kutegemea ufadhili.

Nao Ibrahim Mohamed Ali, Hassan Abdalla na Khamis Khatib walisema, lazima kila mmoja, awe mlinzi kwa mwenzake, juu ya suala la uchimbaji wa mchanga kwenye barabara yao.




Bara bara ya kijiji cha Mtega, shehia ya Wawi wilaya ya Chake chake, iliyoanzia Wawi kwa Gerei, yenye urefu wa kilomita 2.5 kupitia mtega uwanja wa mpira, hadi mwanzo wa kambi za Jeshi la wananchi, iliasisiwa mwaka 2016 na wananchi wenyewe.

                        Mwisho                                                                 

 

 

Comments