Skip to main content

ELIMU YA CHANJO YA UVIKO19, KUNDI LA VIZIWI LALAMIKIA KUSAHAULIWA






NA HAJI NASSOR, PEMBA@@@@

MKATABA wa kimataifa wa haki za watu wenye ulemavu, ambao Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania iliusaini Machi mwaka 2007 na kuthibithisha mwaka 2009, unalazimisha huduma za afya kwa watu wenye ulemavu.

Ibara ya 25, inasisitiza nchi wanawachama, watumbue kuwa, watu wenye ulemavu wanayo haki ya kunufaika kwa kiwango cha juu, huduma za afya tena bila ya ubaguzi wowote.

Mkataba ukafafanua kuwa, nchi husika zitachukua hatua zinazostahiki, kuhakikisha watu wenye ulemavu wanapata huduma bora za afya.

‘’Nchi wanachama zitatoa huduma za afya, zinazohitajika kwa watu wenye ulemavu, hasa kutokana na aina ya ulemavu wao, yakiwemo maeneo ya vijijini,’’umefafanua Mkataba huo.

Ukaongeza kuwa, nchi hizo zitawataka wataalamu wa afya, kutoa huduma za kiwango sawa kama watu wenye ulemavu, kama zinavyotolewa kwa watu wengine, ikiwa ni pamoja na misingi ya kutoa ridhaa kwa uhuru na ufahamu wa kutosha.

Mwaka 1983 hadi 1992 hatua mbali mbali zilichukuliwa, ikiwani pamoja na maamuzi ya mwisho ya Umoja wa Mataifa, kuitangaza Disemba 3 ya kila mwaka kuwa ni siku ya kimataifa ya watu wenye ulemavu duniani.

Ambapo siku hiyo pamoja na mambo mengine, kundi la watu wenye ulemavu hujadili, mafanikio na changamoto zao mbali mbali, zikiwemo na huduma za afya.

Kwa mfano katika sherehe za mwaka jana, Mkuu wa mkoa wa kusini Pemba Mattar Zahor Massoud, alipendekeza kuwepo kwa madirisha maalum ya kutolea dawa kwa watu wenye ulemavu kwa hospitali za serikali.

Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania nayo, iliunda Mkakati wa Kitaifa wa Ujumuishi wa mwaka 2010 hadi 2015 na sera ya taifa ya watu wenye ulemavu ya mwaka 2004, ukitaja uhitaji wa lazima wa huduma za afya wa watu wenye ulemavu.

Ipo sera ya kitaifa ya watu wenye ulemavu ya mwaka 2018 kwa upande wa Zanzibar, ambayo nayo kwenye Ibara ya 20, ikasisitiza uimarishwaji wa upatikanaji huduma bora na endelevu kwa watu hao.

Kuhusiana na hatua za kisheria, Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, ilitunga sheria ya Watu wenye Ulemavu ya mwaka 2010, ambapo ilikuja kuharakisha pia suala la huduma bora za afya.

Zanzibar, ambayo ilikuwa na Sheria ya Watu wenye Ulemavu, nambari 9 ya mwaka 2006, ambayo sasa imefutwa na kuwa na sheria mpya nambari 8 ya mwaka 2022.

Kifungu cha 28 (1) (c) cha sheria hiyo, kimeanisha haki ya kupata huduma za afya kwa watu wenye ulemavu, ikiwemo matibabu, matengenezo au marekebisho yanayohusiana na aina ya ulemavu wao.

Tanzania bara pia iliunda Mpango Mkakati wa Sekta ya Afya ambao unatoa mwongozo wa ufikiaji wa huduma za afya kwa makundi yote yakiwemo ya watu wenye ulemavu kama viziwi.

Kwa upande wa Zanzibar, kulikuwa na Mpango Mkakati wa sekta ya afya wa miaka tisa, ambao uliishia mwaka 2019, wenyewe ulitaja hatua za kuchukuliwa, ili kuwakinga na utapia mlo wanawake, watoto na watu wenye ulemavu.

UGONJWA WA CORONA NA CHANJO YAKE

Wakati hayo yakifanyika, Machi 11, 2020, Shirika la Afya Ulimwenguni ‘WHO’ iliiratibisha rasmi ugonjwa COVID-19 kama janga la dunia.

 Hii baada ya ugonjwa huo wa mlipuko wa kuenea kwa kasi duniani kote, ambao huenea kwa haraka katika mataifa na mabara mbali mbali.

Aidha WHO iligundua kuwa, watu 4,291 walikuwa wameshaaga dunia na maelfu zaidi walikuwa wamelazwa hospitalini kwa muda mfupi.

 

Baada ya janga hilo, wataalamu wa afya waliibuka na chanjo za aina mbali mbali, ambazo baada ya majaribio zikabainika kuwa, zinaweza kuwa kinga.

 

Na hapo sasa wizara ya Afya Zanzibar kwa upande nwake, ilidhamiria hadi ikiingia mwaka 2023 iwe wazanzibari 70 kila 100 wameshapa chanjo za Corona.

 

Huku hayo yakipangwa, Shirika la Afya Duniani (WHO) lilisema Julai 27, mwaka 2022 kuwa hadi kufikia Julai 25, 2022 jumla ya dozi bilioni 12.24 za chanjo ya Covid-19 zilitolewa duniani kote.

Utoaji wa chanjo dhidi ya Covid-19 hapa nchini ulizinduliwa Julai 28, mwaka 2021 na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan ambapo chanjo aina ya Pfizer, Moderna, Sinopharm, Sinovac na Jansen ziliidhinishwa kutumika.

VIZIWI WANASEMAJE?

Kassim Issa Khamis mkaazi wa Kisiwa cha Makoongwe wilaya ya Mkoani akizungumza na wandishi wa habari hii, chini ya mkalimani wake, anasema hajapata elimu ya ugonjwa wa Uviko 19.

Anasema, hana taarifa rasmi za kujikinga na janga hilo, bali amekuwa akipewa taarifa za juu juu na familia yake.

‘’Kwa kuitwa na wizara ya Afya, sisi watu wenye uziwi hapa wilaya ya Mkoani bado, bali wengine wanakwenda wakirudi wanatueleza japo juu juu,’’anasema.

Mayasa Mkombe Mgando nae wa Kisiwani humo, anasema wao wamesahauliwa kwenye elimu ya Uviko 19, hivyo wameshindwa kufanya uamuzi kuhusu kuchanjo.

Idrissa Khamis Khamis wa Kisiwa Panza, wilaya ya Mkoani, anasema amekuwa akishiriki kwenye shughuli kadhaa za kijamii, ingawa kwenye elimu ya Uviko 19, wameachwa.

‘’Mimi ni kiongozi wa wenzangu wenye uziwi katika shehia tatu, ikiwemo ya Kisiwa Panza, lakini wizara ya Afya ilitusahau kutupa elimu ya moja kwa moja,’’anasema.

‘’Natamani hasa nipate elimu ya umuhimu wa chanjo, ili kisha nifanye uamuzi wa kuchanja ama laa, lakini sasa elimu niliyonayo ni kupitia kwenye baraza zetu za mazungumzo,’’anasema.

Maryam Ali Kombo wa kisiwa cha Makoongwe, anasema hana elimu ya kutosha juu ya namna ya kujikinga na Uviko 19, kwani hajawahi kuitwa na watendaji wa wizara kumpa elimu.



‘’Sisi ni wanachama wa chama cha viziwi Zanzibar ‘CHAVIZA’ lakini hatujawahi kualikwa, chini ya mkalimani wetu,’’anasema.

Mama mmoja mwenye vijana wawili wote viziwi mkaazi wa Kisiwa cha Shamiani wilaya ya Mkoani, anasema sio elimu ya Uviko19, ambayo wamekuwa wakisauliwa, lakini hata shughuli nyingine za kijamii.

‘’Hata ukiona na sisi tumeshirikishwa kikamilifu, basi iwe CHAVIZA, wamepata mradi, lakini vyenginevyo huwa vigumu kupata taarifa rasmi,’’anasema.

Sheha wa shehia ya Kisiwa Panza Haji Ali Shaali, anasema anaowahudumu wa afya shehiani mwake, lakini hawana utaalamu wa kuzungumza na viziwi.

‘’Ninao viziwi wastani 15 kwenye shehia yangu, lakini wote hawajafikiwa na elimu ya Uviko19, na kuachwa nyuma katika vita dhidi ya ungonjwa huu,’’ anasema.

Muhudumu wa afya shehiani humo ‘CHV’ Haroub Makame Bakar, anasema ilikuwa vigumu kuwafikishia elimu viziwi, kutokana na wao kukosa mafunzo ya lugha ya alama.

‘’Sisi ‘CHV’ tupo watano kwenye shehia, lakini hakuna hata mmoja ambae anaelimu japo ndogo ya lugha ya alama, hivyo basi elimu ya Uviko19 haikuwafikia viziwi,’’anasema.

Mkalimani pekee wa lugha ya alama Pemba Asha Suleiman, anasema hajawahi kualikwa na wizara ya Afya au wahudumu wa afya, ili kuwa makalimani wakati elimu ya kujikinga na Uviko19, ikietolewa.

‘’Tume za uchaguzi huwa wananialika au Idara ya Katiba na Msaada wa Kisheria, kwamba viziwi washiriki, lakini kwa hilo la elimu ya Uviko19 bado,’’anasema.

Mwenyeikiti wa Chama cha Viziwi wilaya ya Chake chake Mohamed Khamis Shehe, anasema hakuna hata mkutano mmoja, waliowahi kualikwa wa utoaji elimu ya Uviko19.

Mjumbe wa Umoja wa Watu wenye Ulemavu Zanzibar, Hidaya Mjaka Ali, anakiri kuwa, elimu ya Uviko19 kwa watu wenye uziwi, haikuwepo moja kwa moja kwao.

‘’Ni kweli wizara ya Afya hasa Pemba, imeyafikia makundi yote, lakini kwa wenzetu wenye uziwi kwa mkutano wao peke yao, hilo halijafanyika,’’anasema.

Mratibu wa Baraza la Taifa la watu wenye Ulemavu Mashavu Juma Mabrouk, anakiri kuwa wizara ya Afya haikuwahi kuliita kundi la watu wenye uziwi, kuwapa elimu hiyo.   

‘’Mbinu tulioitumia kwa watu wenye uziwi, ili wafikiwe na elimu ya Uviko19, ni kuwatumia maafisa wa Baraza, ambao wameshapata elimu na kukutana na viziwi,’’anasema.

Changamoto inayojitokeza kuwa ni uwepo wa viziwi zaidi ya 400 kisiwani Pemba, ingawa kuwepo kwa mkalimani mmoja anayetambulika.

Anakiri kuwa ile elimu rasmi ya Uviko19 na hasa inayoambatana chanjo kutoka kwa wataalamu wa afya, watu wenye uziwi imefika kwa kundi dogo mno.

WIZARA YA AFYA

Afisa Mdhamini wizara ya Afya Pemba Khamis Bilali Ali, anasema walichokifanya ni kukutana na wakuu wa Jumuiya za watu wenye ulemavu, ili kuwapa elimu.

‘’Naamini katika elimu ya kujikinga na Uviko19, hakuna mtu aliyeachwa nyuma, na hasa wenzetu wa makundi maalum, tulikuwa na mkakati malum,’’anasema.

Eneo jingine, hadi leo hii wameweka utamaduni wa kuyataka makundi yote, yawaalike wataalamu wa afya popote walipo ili wapatiwe elimu ya Uviko19.

‘’Inawezekana kwa mfano wenye uziwi wapo kisiwani na kufika mjini ni shida, kwa mujibu wa mazingira yao, sasa wawasiliane na maafisa wetu wa afya wa wilaya na watafuatwa walipo,’’anasema.

Ingawa upande mmoja, Mratibu wa kitengo cha elimu ya Chanjo cha wizaara hiyo Pemba Bakar Hamad, anasema utaratibu wao ulikuwa ni kuyaenda makundi kuyapa elimu.



''Kwa mfano tulikwenda kwa vikosi vya ulinzi na usalama, wanafunzi wa skuli, vyuo vikuu, waandishi wa habari, wakulima, watumishi wa umma na viongozi wa dini,’’anasema.

Hivyo anasema hakumbuki kuwa na mpango maalum kwa ajili ya watu wenye ulemavu wa uziwi peke yao, bali walikuwa na mikutano ya elimu kwa makundi mchanganyiko.

NINI ATHARI YAKE?

Himid Mcha Khamis kiziwi mkaazi wa kisiwa kidogo cha Fundo wilaya ya Wete, anasema ni kuwa rahisi wao kushambuliwa na uogonjwa wa Corona au mengine ya mfumo wa hewa.

Aisha Haji Makame wa kisiwa cha Makoongwe, anasema wamevunjiwa haki zao ambazo zimeainisha kwenye mikataba na sheria mbali mbali.

Afisa Mdhamini wizara ya Afya Khamis Bilali Ali, anasema moja ni kukumbuwa na maambukizo kwa wepesi, kama hawakuwa na elimu ya kujikinga.

Afisa wa Chama cha Viziwi wilaya ya Chake chake Mohamed Khamis Shehe, anasema ni kuwaweka wao katika msingi wa kukumbwa na magonjwa.

NINI KIFANYIKE?

Mratibu wa Baraza la Taifa la watu wenye uleavu Zanzibar Mashavu Juma Mabrouk, anasema ni wizara ya Afya kurudi kwa kundi la watu wenye ulemavu, ili kuliemisha.

Mwashamba Haji Mrisho mwenye uziwi mkaazi wa Chake chake, anasema nguvu ya elimu sasa ielekezwe kwa wenzao waliko vijijini.

Mkalimani wa lugha ya alama Pemba Asha Suleiman, anashauri vipindi na taarifa zote za kwenye tv zinapoendeshwa, kuwepo kwa mkalimani maalum.

Jengine ni jamii na hata watu wenye ulemavu wenyewe, kusomea lugha ya alama na ukalimani, kuwasaidia wananchi wenzao wenye uziwi.     

Mzazi mweye kijana mwenye uziwi, anasema ni kutekelezwa kwa sheria kama zilivyo, ili kundi hilo lipate haki zao.

TAKWIMU YA WALIOCHANJA

Katika kipindi cha tarehe 29 Oktoba hadi 02 Disemba, 2022, jumla ya visa vipya 442 vimethibitika kuwa na maambukizi ya Uviko19.

Imebainika kuwa, idadi hii ni kubwa ukilinganisha na takwimu za mwezi uliopita ambapo kulikuwa na visa vipya 272, sawa na ongezeko la asilimia 62.5.

Hadi kufikia tarehe 02 Desemba 2022, jumla ya watu milioni 29,123,387 kati ya walengwa 30,740,928 ambao ni sawa na asilimia 94.7 wamepata dozi kamili ya chanjo ya UVIKO- 19.

                              Mwisho

Comments

BLOG'S VISITORS

DAKTARI MWENGINE CHAKE CHAKE KULA SIKUKUU POLISI, NI KWA TUHUMA ZA KUMBAKA MGONJWA WAKE

NA WAANDISHI WETU, PEMBA::: DAKTARI anaetoa huduma kwa wagonjwa kituo cha afya cha serikali cha  Gombani wilaya ya Chake Chake Pemba, Is-haka Rashid Hadid, anaendelea kushikiliwa na Jeshi la Polisi Mkoa wa kaskazini Pemba, akituhumiwa kumtorosha na kisha kumbaka mtoto wa mwenye umri wa miaka 16, mkaazi wa Gombani. Daktari huyo miaka 35 ni mkaazi wa Kangagani Wilaya ya Wete mkoani humo, ambapo anadaiwa alimchukua mtoto huyo kutoka kwa rafiki yake, na kumpeleka kwenye nyumba anayoishi eneo la Kangagani. Mtoto aliefanyiwa kitendo hicho alisema kuwa, April 21 mwaka huu alikwenda kituo cha afya Gombani, kwa ajili ya matibabu na baada ya kupatiwa huduma na daktari huyo, alimuomba nambari yake ya simu. Alisema ilipofika usiku, walikuwa wanawasiliana kupitia ujumbe mfupi (sms) kwa lengo la kwenda kuchukua dawa nyingine ambazo kwa mchana huo alizikosa hospitalini hapo. "Nilikwenda hospitali kutibiwa, baada ya kufanya mapele katika sehemu zangu za siri, lakini akaniambia mpaka aje da

'MKAPA' NA WENZAKE PEMBA WALAZWA RUMANDE

  NA HAJI NASSOR, PEMBA@@@@ MAHKAMA kuu Zanzibar kisiwani Pemba, chini ya Jaji Ibrahim Mzee Ibrahim, imewapeleka rumande watumuhimwa wanne wanaokabiliwa na tuhuma za kuua kwa makusudi, akiwemo Ali Mussa Omar ‘ Mkapa’ mkaazi wa Wawi wilaya ya Chake chake Pemba. Watuhumiwa wengine walioanza maisha mapya ya rumande ni mtuhumiwa Yassir Mohamed Juma miaka 23, Anuwari Mussa Omar miaka 30 pamoja na mtuhumiwa Yassir Mussa Omar ‘ Makababu ’ miaka 29, wote wakaazi wa shehia ya Wawi, wilaya ya Chake chake Pemba. Awali watuhumiwa hao waliwasili mahakamani hapo, kwa mara ya kwanza, kwa ajili ya kusomewa tuhma zinazowakabili za kumuua kwa maksudi Said Seif Kombo. Ilidaiwa mahakamani hapo na Mwendesha Mashtaka kutoka Ofisi ya Mkurugenzi wa Mashataka Seif Mohamed Khamis akiambatana na mwenzake Mussa Khamis Ali kuwa, watuhumiwa hao kwa pamoja wanadaia kufanya mauwaji hayo kwa maksudi. Ilidai kuwa, watuhumiwa wote kwa pamoja, walitenda kosa hilo Oktoba 16, mwaka huu, baina ya saa 7:00 mchan

HII KALI MBUNGE ASIYA AMKOGESHA MWANANCHI HADHARANI KISA HICHI HAPA......

  NA HAJI NASSOR, PEMBA MBUNGE wa viti maalum nafasi za wanawake mkoa wa kaskazini Pemba Asiya Sharif Omar, amewataka wananchi wa kijiji cha taifu, shehia ya Kinyasini jimbo la Gando wilaya ya Wete Pemba, kuyalinda miundombinu ya maji safi na salama, ili yawe endelevu kwao. Kauli hiyo ameitoa wakati alipokuwa akizungumza na mwandishi wa habari hizi, mara baada ya kuwasili kijijini humo, na kumkogesha mwananchi mmoja kama ishara ya uzinduzi wa mradi wa maji safi na salama, ulioasisiwa na mbunge wa Jimbo la Gando. Alisema, hawana mbadala kwa sasa bali ni kuilinda miundombinu ya huduma hiyo, hasa baada ya mbunge wa wao Salim Mussa Omar, kuwarejeshea huduma hiyo. Alieleza kuwa, inafahamika kuwa kwa miaka 14 waliikosa huduma hiyo hasa kwa vile viongozi waliokuwepo hawakujali kuwatatulia tatizo hilo, hadi juzi ilipofanywa na mbunge wao. “Baada ya huduma hii sasa kurejeshwa na mbunge wa jimbo la Gando, kazi iliyobakia kwenu wananchi ni kila mmoja kuwa mlinzi wa miundombinu hii,’’ali

TUHMA ZA DAKTARI PEMBA KUCHIWA HURU: POLISI KASKAZINI KUTOA TAARIFA RASMI LEO

  NA HAJI NASSOR, PEMBA KAMANDA wa Polisi mkoa wa kaskazini Pemba, Juma Saad Khamis, amesema leo Mei 9, mwaka huu atatoa taarifa rasmi, juu ya kuendelea kumshikilia au kumpa dhamana ya Polisi, daktari wa Kituo cha Afya Gombani Is-haka Rashid Hadid, anayetuhumiwa kwa ubakaji. Alisema, kwa vile alikuwa katika mapumziko mafupi, haelewi jambo lolote linaloendelea kwa mtuhumiwa huyo, juu ya kuendelea kushikiliwa kwake kituoni hapo. Alieleza kuwa, leo Mei 6 (jana), hajapata taarifa za ndani za mtuhumiwa, huyo na kuwataka wananchi na wanaharakati, wasubirie hadi Jumatatu ijayo. Akizungumza na waandishi wa habari kwa nyakati tofauti Kamanda huyo, alisema hana taarifa zozote za kupewa dhamana mtuhumiwa ndani ya kituo chake cha Polisi au kuendelea kuwepo. ‘’Ilikuwa mimi sipo kazini kwa muda, kuanzia anakamatwa hadi anafikishwa Polisi, kwa sasa siwezi kueleza jambo lolote kwa mtuhumiwa huyo, hadi Jumatatu,’’alieleza. Aidha Kamanda huyo alieleza kuwa, kwa sasa hawezi kutoa ufafan

MADAKTARI KUTOKA CHINA WAOKOA MAISHA YA MTOTO PEMBA

  HABIBA ZARALI, PEMBA TIMU ya 32 ya madaktari wa kichina katika hospitali ya Abdalla Mzee Mkoani wamefanikiwa kufanya upasuaji mkubwa wa mtoto mwenye umri wa miaka 15 mkaazi wa Chole Kengeja, baada ya kuchomwa na jiti sehemu ya njia zake za mfumo wa uzazi. Mtoto huyo ambae alianguka hivi karibuni katika mti na baadae kuchomwa na jiti hilo na kumsababishia kutokwa na damu nyingi katika sehemu ya nyonga, alifanyiwa upasuaji uliodumu kwa muda wa saa tatu na   kuokolewa maisha yake. Akizungumza mara baada ya operesheni huo kiongozi wa timu hiyo Dr Jiang Jinhua, alisema mara baada ya mtoto huyo kufikishwa hospitalini hapo na kufanyiwa vipimo na kuonekana   ilibidi apatiwe rufaa ya kwenda katika hospitali nzuri yenye kutibu tatizo lake huko nchini Kuwado ambapo haikuwezekana kutokana na hali ya umaskini wa f amilia ya mtoto huyo . Alisema timu ya madaktari hao itaendelea kutowa huduma za matibabu   kwa wananchi kisiwani humo,   ili kuwaondolea gharama ya kutafuta matibabu nje ya nch