Skip to main content

ELIMU YA CHANJO YA UVIKO19, KUNDI LA VIZIWI LALAMIKIA KUSAHAULIWA






NA HAJI NASSOR, PEMBA@@@@

MKATABA wa kimataifa wa haki za watu wenye ulemavu, ambao Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania iliusaini Machi mwaka 2007 na kuthibithisha mwaka 2009, unalazimisha huduma za afya kwa watu wenye ulemavu.

Ibara ya 25, inasisitiza nchi wanawachama, watumbue kuwa, watu wenye ulemavu wanayo haki ya kunufaika kwa kiwango cha juu, huduma za afya tena bila ya ubaguzi wowote.

Mkataba ukafafanua kuwa, nchi husika zitachukua hatua zinazostahiki, kuhakikisha watu wenye ulemavu wanapata huduma bora za afya.

‘’Nchi wanachama zitatoa huduma za afya, zinazohitajika kwa watu wenye ulemavu, hasa kutokana na aina ya ulemavu wao, yakiwemo maeneo ya vijijini,’’umefafanua Mkataba huo.

Ukaongeza kuwa, nchi hizo zitawataka wataalamu wa afya, kutoa huduma za kiwango sawa kama watu wenye ulemavu, kama zinavyotolewa kwa watu wengine, ikiwa ni pamoja na misingi ya kutoa ridhaa kwa uhuru na ufahamu wa kutosha.

Mwaka 1983 hadi 1992 hatua mbali mbali zilichukuliwa, ikiwani pamoja na maamuzi ya mwisho ya Umoja wa Mataifa, kuitangaza Disemba 3 ya kila mwaka kuwa ni siku ya kimataifa ya watu wenye ulemavu duniani.

Ambapo siku hiyo pamoja na mambo mengine, kundi la watu wenye ulemavu hujadili, mafanikio na changamoto zao mbali mbali, zikiwemo na huduma za afya.

Kwa mfano katika sherehe za mwaka jana, Mkuu wa mkoa wa kusini Pemba Mattar Zahor Massoud, alipendekeza kuwepo kwa madirisha maalum ya kutolea dawa kwa watu wenye ulemavu kwa hospitali za serikali.

Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania nayo, iliunda Mkakati wa Kitaifa wa Ujumuishi wa mwaka 2010 hadi 2015 na sera ya taifa ya watu wenye ulemavu ya mwaka 2004, ukitaja uhitaji wa lazima wa huduma za afya wa watu wenye ulemavu.

Ipo sera ya kitaifa ya watu wenye ulemavu ya mwaka 2018 kwa upande wa Zanzibar, ambayo nayo kwenye Ibara ya 20, ikasisitiza uimarishwaji wa upatikanaji huduma bora na endelevu kwa watu hao.

Kuhusiana na hatua za kisheria, Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, ilitunga sheria ya Watu wenye Ulemavu ya mwaka 2010, ambapo ilikuja kuharakisha pia suala la huduma bora za afya.

Zanzibar, ambayo ilikuwa na Sheria ya Watu wenye Ulemavu, nambari 9 ya mwaka 2006, ambayo sasa imefutwa na kuwa na sheria mpya nambari 8 ya mwaka 2022.

Kifungu cha 28 (1) (c) cha sheria hiyo, kimeanisha haki ya kupata huduma za afya kwa watu wenye ulemavu, ikiwemo matibabu, matengenezo au marekebisho yanayohusiana na aina ya ulemavu wao.

Tanzania bara pia iliunda Mpango Mkakati wa Sekta ya Afya ambao unatoa mwongozo wa ufikiaji wa huduma za afya kwa makundi yote yakiwemo ya watu wenye ulemavu kama viziwi.

Kwa upande wa Zanzibar, kulikuwa na Mpango Mkakati wa sekta ya afya wa miaka tisa, ambao uliishia mwaka 2019, wenyewe ulitaja hatua za kuchukuliwa, ili kuwakinga na utapia mlo wanawake, watoto na watu wenye ulemavu.

UGONJWA WA CORONA NA CHANJO YAKE

Wakati hayo yakifanyika, Machi 11, 2020, Shirika la Afya Ulimwenguni ‘WHO’ iliiratibisha rasmi ugonjwa COVID-19 kama janga la dunia.

 Hii baada ya ugonjwa huo wa mlipuko wa kuenea kwa kasi duniani kote, ambao huenea kwa haraka katika mataifa na mabara mbali mbali.

Aidha WHO iligundua kuwa, watu 4,291 walikuwa wameshaaga dunia na maelfu zaidi walikuwa wamelazwa hospitalini kwa muda mfupi.

 

Baada ya janga hilo, wataalamu wa afya waliibuka na chanjo za aina mbali mbali, ambazo baada ya majaribio zikabainika kuwa, zinaweza kuwa kinga.

 

Na hapo sasa wizara ya Afya Zanzibar kwa upande nwake, ilidhamiria hadi ikiingia mwaka 2023 iwe wazanzibari 70 kila 100 wameshapa chanjo za Corona.

 

Huku hayo yakipangwa, Shirika la Afya Duniani (WHO) lilisema Julai 27, mwaka 2022 kuwa hadi kufikia Julai 25, 2022 jumla ya dozi bilioni 12.24 za chanjo ya Covid-19 zilitolewa duniani kote.

Utoaji wa chanjo dhidi ya Covid-19 hapa nchini ulizinduliwa Julai 28, mwaka 2021 na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan ambapo chanjo aina ya Pfizer, Moderna, Sinopharm, Sinovac na Jansen ziliidhinishwa kutumika.

VIZIWI WANASEMAJE?

Kassim Issa Khamis mkaazi wa Kisiwa cha Makoongwe wilaya ya Mkoani akizungumza na wandishi wa habari hii, chini ya mkalimani wake, anasema hajapata elimu ya ugonjwa wa Uviko 19.

Anasema, hana taarifa rasmi za kujikinga na janga hilo, bali amekuwa akipewa taarifa za juu juu na familia yake.

‘’Kwa kuitwa na wizara ya Afya, sisi watu wenye uziwi hapa wilaya ya Mkoani bado, bali wengine wanakwenda wakirudi wanatueleza japo juu juu,’’anasema.

Mayasa Mkombe Mgando nae wa Kisiwani humo, anasema wao wamesahauliwa kwenye elimu ya Uviko 19, hivyo wameshindwa kufanya uamuzi kuhusu kuchanjo.

Idrissa Khamis Khamis wa Kisiwa Panza, wilaya ya Mkoani, anasema amekuwa akishiriki kwenye shughuli kadhaa za kijamii, ingawa kwenye elimu ya Uviko 19, wameachwa.

‘’Mimi ni kiongozi wa wenzangu wenye uziwi katika shehia tatu, ikiwemo ya Kisiwa Panza, lakini wizara ya Afya ilitusahau kutupa elimu ya moja kwa moja,’’anasema.

‘’Natamani hasa nipate elimu ya umuhimu wa chanjo, ili kisha nifanye uamuzi wa kuchanja ama laa, lakini sasa elimu niliyonayo ni kupitia kwenye baraza zetu za mazungumzo,’’anasema.

Maryam Ali Kombo wa kisiwa cha Makoongwe, anasema hana elimu ya kutosha juu ya namna ya kujikinga na Uviko 19, kwani hajawahi kuitwa na watendaji wa wizara kumpa elimu.



‘’Sisi ni wanachama wa chama cha viziwi Zanzibar ‘CHAVIZA’ lakini hatujawahi kualikwa, chini ya mkalimani wetu,’’anasema.

Mama mmoja mwenye vijana wawili wote viziwi mkaazi wa Kisiwa cha Shamiani wilaya ya Mkoani, anasema sio elimu ya Uviko19, ambayo wamekuwa wakisauliwa, lakini hata shughuli nyingine za kijamii.

‘’Hata ukiona na sisi tumeshirikishwa kikamilifu, basi iwe CHAVIZA, wamepata mradi, lakini vyenginevyo huwa vigumu kupata taarifa rasmi,’’anasema.

Sheha wa shehia ya Kisiwa Panza Haji Ali Shaali, anasema anaowahudumu wa afya shehiani mwake, lakini hawana utaalamu wa kuzungumza na viziwi.

‘’Ninao viziwi wastani 15 kwenye shehia yangu, lakini wote hawajafikiwa na elimu ya Uviko19, na kuachwa nyuma katika vita dhidi ya ungonjwa huu,’’ anasema.

Muhudumu wa afya shehiani humo ‘CHV’ Haroub Makame Bakar, anasema ilikuwa vigumu kuwafikishia elimu viziwi, kutokana na wao kukosa mafunzo ya lugha ya alama.

‘’Sisi ‘CHV’ tupo watano kwenye shehia, lakini hakuna hata mmoja ambae anaelimu japo ndogo ya lugha ya alama, hivyo basi elimu ya Uviko19 haikuwafikia viziwi,’’anasema.

Mkalimani pekee wa lugha ya alama Pemba Asha Suleiman, anasema hajawahi kualikwa na wizara ya Afya au wahudumu wa afya, ili kuwa makalimani wakati elimu ya kujikinga na Uviko19, ikietolewa.

‘’Tume za uchaguzi huwa wananialika au Idara ya Katiba na Msaada wa Kisheria, kwamba viziwi washiriki, lakini kwa hilo la elimu ya Uviko19 bado,’’anasema.

Mwenyeikiti wa Chama cha Viziwi wilaya ya Chake chake Mohamed Khamis Shehe, anasema hakuna hata mkutano mmoja, waliowahi kualikwa wa utoaji elimu ya Uviko19.

Mjumbe wa Umoja wa Watu wenye Ulemavu Zanzibar, Hidaya Mjaka Ali, anakiri kuwa, elimu ya Uviko19 kwa watu wenye uziwi, haikuwepo moja kwa moja kwao.

‘’Ni kweli wizara ya Afya hasa Pemba, imeyafikia makundi yote, lakini kwa wenzetu wenye uziwi kwa mkutano wao peke yao, hilo halijafanyika,’’anasema.

Mratibu wa Baraza la Taifa la watu wenye Ulemavu Mashavu Juma Mabrouk, anakiri kuwa wizara ya Afya haikuwahi kuliita kundi la watu wenye uziwi, kuwapa elimu hiyo.   

‘’Mbinu tulioitumia kwa watu wenye uziwi, ili wafikiwe na elimu ya Uviko19, ni kuwatumia maafisa wa Baraza, ambao wameshapata elimu na kukutana na viziwi,’’anasema.

Changamoto inayojitokeza kuwa ni uwepo wa viziwi zaidi ya 400 kisiwani Pemba, ingawa kuwepo kwa mkalimani mmoja anayetambulika.

Anakiri kuwa ile elimu rasmi ya Uviko19 na hasa inayoambatana chanjo kutoka kwa wataalamu wa afya, watu wenye uziwi imefika kwa kundi dogo mno.

WIZARA YA AFYA

Afisa Mdhamini wizara ya Afya Pemba Khamis Bilali Ali, anasema walichokifanya ni kukutana na wakuu wa Jumuiya za watu wenye ulemavu, ili kuwapa elimu.

‘’Naamini katika elimu ya kujikinga na Uviko19, hakuna mtu aliyeachwa nyuma, na hasa wenzetu wa makundi maalum, tulikuwa na mkakati malum,’’anasema.

Eneo jingine, hadi leo hii wameweka utamaduni wa kuyataka makundi yote, yawaalike wataalamu wa afya popote walipo ili wapatiwe elimu ya Uviko19.

‘’Inawezekana kwa mfano wenye uziwi wapo kisiwani na kufika mjini ni shida, kwa mujibu wa mazingira yao, sasa wawasiliane na maafisa wetu wa afya wa wilaya na watafuatwa walipo,’’anasema.

Ingawa upande mmoja, Mratibu wa kitengo cha elimu ya Chanjo cha wizaara hiyo Pemba Bakar Hamad, anasema utaratibu wao ulikuwa ni kuyaenda makundi kuyapa elimu.



''Kwa mfano tulikwenda kwa vikosi vya ulinzi na usalama, wanafunzi wa skuli, vyuo vikuu, waandishi wa habari, wakulima, watumishi wa umma na viongozi wa dini,’’anasema.

Hivyo anasema hakumbuki kuwa na mpango maalum kwa ajili ya watu wenye ulemavu wa uziwi peke yao, bali walikuwa na mikutano ya elimu kwa makundi mchanganyiko.

NINI ATHARI YAKE?

Himid Mcha Khamis kiziwi mkaazi wa kisiwa kidogo cha Fundo wilaya ya Wete, anasema ni kuwa rahisi wao kushambuliwa na uogonjwa wa Corona au mengine ya mfumo wa hewa.

Aisha Haji Makame wa kisiwa cha Makoongwe, anasema wamevunjiwa haki zao ambazo zimeainisha kwenye mikataba na sheria mbali mbali.

Afisa Mdhamini wizara ya Afya Khamis Bilali Ali, anasema moja ni kukumbuwa na maambukizo kwa wepesi, kama hawakuwa na elimu ya kujikinga.

Afisa wa Chama cha Viziwi wilaya ya Chake chake Mohamed Khamis Shehe, anasema ni kuwaweka wao katika msingi wa kukumbwa na magonjwa.

NINI KIFANYIKE?

Mratibu wa Baraza la Taifa la watu wenye uleavu Zanzibar Mashavu Juma Mabrouk, anasema ni wizara ya Afya kurudi kwa kundi la watu wenye ulemavu, ili kuliemisha.

Mwashamba Haji Mrisho mwenye uziwi mkaazi wa Chake chake, anasema nguvu ya elimu sasa ielekezwe kwa wenzao waliko vijijini.

Mkalimani wa lugha ya alama Pemba Asha Suleiman, anashauri vipindi na taarifa zote za kwenye tv zinapoendeshwa, kuwepo kwa mkalimani maalum.

Jengine ni jamii na hata watu wenye ulemavu wenyewe, kusomea lugha ya alama na ukalimani, kuwasaidia wananchi wenzao wenye uziwi.     

Mzazi mweye kijana mwenye uziwi, anasema ni kutekelezwa kwa sheria kama zilivyo, ili kundi hilo lipate haki zao.

TAKWIMU YA WALIOCHANJA

Katika kipindi cha tarehe 29 Oktoba hadi 02 Disemba, 2022, jumla ya visa vipya 442 vimethibitika kuwa na maambukizi ya Uviko19.

Imebainika kuwa, idadi hii ni kubwa ukilinganisha na takwimu za mwezi uliopita ambapo kulikuwa na visa vipya 272, sawa na ongezeko la asilimia 62.5.

Hadi kufikia tarehe 02 Desemba 2022, jumla ya watu milioni 29,123,387 kati ya walengwa 30,740,928 ambao ni sawa na asilimia 94.7 wamepata dozi kamili ya chanjo ya UVIKO- 19.

                              Mwisho

Comments