Skip to main content

ZEC YAJIGAMBA NA UCHAGUZI JUMUISHI 2025, WATU WENYE ULEMAVU WAHAKIKISHIWA MAZIGIRA RAFIKI

 





 NA MOZA SHAABAN, PEMBA@@@@

OKTOBA 29 mwaka huu, Tanzania itafanya uchaguzi wake mkuu wa saba wa vyama vingi tokea kuasisiwa mwaka 1995.

Mpaka sasa matayarisho mbali mbali yanaendelea kufanyika, kuanzia kwa wananchi, vyama vya siasa tume ya uchaguzi pamoja na serikali kuu.

Kuelekea siku hiyo, wadau wa haki za watu wenye ulemavu wanaendelea kulilia mazingira rafiki ya uchaguzi kwa watu wenye ulemavu.

Kwani sensa ya watu na makazi ya mwaka 2022 imeweka wazi kuwa, Zanzibar ina takriban asilimia 11.4 ya kundi hilo.

Matokeo hayo ya sensa, yanafafanua kuwa aina ya ulemavu unaoongoza ni wa uoni, ambao unachukuwa asilimia 3.6 ya jumla ya watu wenye ulemavu.

Tume ya uchaguzi Zanzibar (ZEC) imesema jumla ya watu 717,557 wameidhinishwa kupiga kura mwaka huu, na kati yao 8,021 ni watu wenye ulemavu.

Hivyo ni muhimu kwao kuwekewa miundombinu rafiki katika vituo vyote vya kupigia kura, ikijumuisha majengo pamoja na vifaa.

Wenyewe wanasema, lazima mazingira hayo yatiliwe maanani, kwa uhitaji wa aina zote za ulemavu, ili kuhakikisha watu wote wanapata haki yao ya msingi ya kupiga kura.

WATU WENYE ULEMAVU

Said Saleh Sultan wa Mtambile Pemba mwenye ulemavu wa viungo anasema, mazingira rafiki kwao katika uchaguzi ni kuhakikisha vituo vya kupigia kura vinaweza kufikiwa.

Anaeleza ufikiwaji huo ni pamoja na kuweka vituo kwenye sehemu ambazo hazina milima na zenye miundombinu jumuishi, itakayo wawezesha wao kupata ushiriki mpana.

 “Mazingira rafiki kwetu ni kuwekewa vituo vya kupigia kura, katika sehemu zisizo na milima, pamoja na zenye miundombinu jumuishi, tutakazoweza kufika tukiwa na viti mwendo ,anasema.

Rehema Juma Makame wa Kukuu Kangani Pemba mwenye ulemavu wa uoni anasema, miundombinu rafiki ya kupigia kura kwao, ni kuwepo kwa karatasi za nukta nundu vituoni.

Adinan Khamis Juma wa Chake Chake mwenye ulemavu wa uziwi anasema, ujumuishi wao katika uchaguzi  ni kuwepo kwa wakalimani wa lugha ya alama katika vituo vya upigaji kura.

Anaeleza kuwa, wakalimani hao watarahisisha  mawasiliano kwenye maeneo ya kutoa huduma zinazo husu upigaji kura.

Saleh Khamis Khalfan wa Mtambile ambae ana  ulemavu wa ngozi anasema, mazingira jumuishi kwa  wenye ulemavu wa aina yake, ni kuwepo foleni kwa ajili yao.



Anaeleza kuwa, utaratibu huo utasaidia kupunguza muda wa kukaa foleni, ambazo mara nyingi hupangwa katika mazingira hatarishi.

Anasema maumbile ya ngozi zao hayahimili jua kali hasa kwa muda mrefu, ambalo linaathari kubwa kwao.

Sisi wenye ulemavu wa ngozi, mazingira rafiki kwetu katika upigaji kura ni kuwepo foleni maalum kwa ajili yetu, ili kupunguza muda wa kusubiria juani”, anafafanua.

              TUME YA UCHAGUZI ZANZIBAR (ZEC)

Mkuu wa Mkurugenzi wa Elimu ya Wapiga Kura na Mawasiliano kwa Umma wa ‘ZEC’ Juma S. Sheha anasema, wamejipanga kuhakikisha watu wenye ulemavu na mahitaji maalum, wanashiriki ipasavyo katika uchaguzi mkuu.

"ZEC imeandaa vitambulisho maalum kwa ajili ya watu wenye mahitaji maalum, wakiwemo watu wenye ulemavu, ili kuwapa kipaumbele wanapofika katika vituo vya kupigia kura, "anaeleza.




Hatua hizo zilizochukuliwa hazikuja tu kama ajali bali serikali, taasisi binafsi na wadau wingine wa kutetea haki za watu wenye ulemavu, wamekuwa wakilipambania hili kwa namna tofauti.

MIKATABA NA SHERIA INAELEKEZA NINI

Mkataba wa Umoja wa Mataifa wa Haki za Watu wenye Ulemavu wa mwaka 2006, Ibara ya 29 inazitaka nchi wanachama, kuweka mazingira rafiki ya watu wenye ulemavu kushiriki katika mchakato wote wa kisiasa.

“Nchi zihakikishe utaratibu wa kupiga kura, vifaa na nyenzo ni sadifu, vinafikika, vinaeleweka na kutumika kwa urahisi, imeeleza sehemu ya ibara hiyo.

 

TUME YA HAKI ZA BINAADAMU

Afisa Mfawidhi wa Tume ya haki za binaadamu na utawala bora Pemba, Suleiman Salim Ahmad anasema, ili kuhakikisha miundombinu rafiki kwa watu wenyeulemavu wa aina zote, tume hufuatilia mwenendo mzima wa uchaguzi.

 Sisi tunafuatilia mwenendo mzima wa uchaguzi kisha tunatoa mapendekezo kwa tume ya uchaguzi nini kifanyike ili watu wenye ulemavu wa aina zote wawe katika mazingira jumuishi,’’ anasema.

JUMUIYA YA WATU WENYE ULEMAVU

Maryam Mohamed Salum Afisa watu wenye ulemavu kutoka Jumuiya ya watu wenye ulemavu Pemba anasema, unapokaribia uchaguzi,  jumuiya hutoa mapendekezo kwa tume ya uchaguzi ili  kuhakikisha unakuwa jumuishi.

Mratibu Baraza la Taifa la watu wenye ulemavu Pemba, Mashavu Juma Mabrouk anasema, baraza hukutana na jumuiya za watu wenye ulemavu na kukusanya maoni yao.

Anasema baada ya kupata maoni hayo, huweka  mapendekezo na ushauri kwa tume ya uchaguzi, juu ya kuimarisha mazingira, vituo vya kupigia kura.

TAMWA ZANZIBAR INAFANYA NINI ?

Meneja programu kutoka Chama cha waandishi wa habari Tanzania TAMWA-Zanzibar Khairat Haji anasema, TAMWA  inatoa mafunzo kwa waandishi wa habari, kuhusu uandishi jumuishi.

Anaeleza kuwa lengo la mafunzo hayo ni kuhakikisha waandishi wanatambua na kutetea haki za watu wenye ulemavu, katika nyanja zote.

Tumetoa mafunzo ya uandishi jumuishi kwa waandishi wa habari, ili waweze kutetea haki za watu wenye ulemavu, ikiwemo hii ya mazingira rafiki katika vituo vya kupigia kura,’’ anaeleza.

 

                                MWISHO

 

 

 

 

 

Comments