Skip to main content

VIZIWI WATAMANI KAMPENI JUMUISHI, TAMWA -ZANZIBAR YATOA RAI KWA VYAMA

 

 
NA MOZA SHAABAN, PEMBA@@@@

ZANZIBAR ipo ndani ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mashariki mwa Afrika.

Ni miongoni mwa nchi zinazopata viongozi wake kupitia mchakato wa upigaji kura.

Ambapo kila baada ya miaka mitano wananchi wake, wenye sifa zilizotajwa kikatiba, hupiga kura ili kuchagua kiongozi wamtakae.

Mchakato huo humjumuisha kila mtu, ilimradi awe ametimia miaka 18 na asiwe mwenye changamoto ya ufahamu ama akili.

Izingatiwe kwamba, upigaji kura ni haki ya kikatiba ya kila Mzanzibari, kwani katiba ya Zanzibar ya mwaka 1984, kifungu cha 7(1) kimetoa haki hiyo.

Kwamba ‘’Mzanzibari alietimiza umri wa miaka 18 anayo haki ya kupiga kura katika uchaguzi unaofanywa Zanzibar,’’kimefafanua.

Kwa kulizingatia hilo, Tume ya uchaguzi Zanzibar ZEC, imeidhinisha jumla ya wazanzibari 717, 557 kushiriki katika uchaguzi mkuu Oktoba 29 mwaka huu.

Huku taarifa kutoka tume hiyo zikieleza kwamba, kati ya hao  watu wenye ulemavu 8,021 wanatarajiwa kushiriki katika zoezi hilo hapa Zanzibar.



Watu wenye ulemavu wa uziwi wakiwa ni miongoni mwa wapiga kura hao, wanahaki ya kupata sera wakati wa kampeni kutoka katika vyama vyao.

WENYEWE WANASEMAJE?

Fatma Kombo Omar wa Kengeja Pemba ni mmoja wa watu wenye ulemavu wa uziwi, akiwa na mkalimani wake anasema, ingawa vyama vyote viko katika mchakato wa kunadi sera, hadi sasa ni sera za chama kimoja tu, ndio zilizomfikia.

Kumbe vyama vyingine vilivyo bakia, hupokea sera zao kutoka kwa watu wanaomzunguka na si kutoka kwa wagombea wenyewe.

“Ingawa kushiriki katika kampeni ni haki ya kila mmoja, lakini mazingira sio rafiki kwetu, na hadi sasa ni sera za chama kimoja tu ndio zilizonifikia,’’anaeleza.

Anaona bado ni vigumu kwao kupata sera za wagombea wote, kama ilivyo kwa watu wingine wasio na ulemavu wa uziwi.

Adinan Khamis Juma wa Chake Chake Pemba ni mtu mwenye ulemavu wa uziwi anasema, pamoja na kuwepo kwa mikataba, sheria na kanuni zinazotaka ujumuishi, ikiwemo siasa, bado hali si shwari kwao.

 Anafafanua kua, amekua akishiriki katika mikutano hayo, ingawa hakuna anachoelewa na hurudi akiwa hana alichofahamu, kwani hakuna mkalimani wa lugha za alama.

Hata Zuhura Haji Mohamed wa Mtambile, anasema wapo wagombea wanao watumia watu wa karibu wawafikishie sera zao, lakini  bado haitoshi.



“Bado ujumuishi wetu katika kampeni ni chanagamoto, na baadhi ya wagombea hutumia watu wetu wa karibu watufikishie sera zao, lakini hatupati ujumbe kamili,”anaeleza.

JAMII INASEMAJE?

Asia Shaib Saleh wa Mjimbini Pemba, anasema ujumuishi   kwa viziwi katika kampeni, bado ni changamoto na wanawachagua wagombea sio kwa kulewa na sera zao.

Anaeleza kua, jamii ndio inayofanya kazi kuwaeleza sera za vyama tofauti,  kazi ambayo ilipaswa kufanywa na wenyewe wanasiasa.

Saleh Bakkar wa Kengeja anasema, mara nyingi watu wenye ulemavu wa uziwi, hukataa kushiriki katika mikutano ya siasa, kwa vile hakuna mazingira rafiki kwao.

“Wenzetu wenye ulemavu wa uziwi, mara nyingi hawashiriki ipasavyo mikutano ya kampeni, kwa kukosekana kwa mazingira rafiki kwao, ikiwemo wakalimani wa lugha ya alama,’’anasema.

 VYAMA VYA SIASA VINASEMAJE?

Katibu wake wa CCM mkoa wa kusini Pemba Kajoro Vyohoroko anasema, katika kampeni za mwaka huu, mikutano yao ya hadhara ya wagombea urais, wameweka wakalimani wa lugha ya alama, ili kuhakikisha ujumuishi.



‘’Kwa miaka iliopita, kundi hili hatukulizingatia ipasavyo, ingawa mwaka huu mikutano yote ya kampeni za wagombea wa urais wa Tanzania na Zanzibar, tumeweka wakalimani wa lugha ya alama,’’anafafanua.

Mohamed Abdallah ni Mwenyekiti wa chama cha ACT –Wazalendo mkoa wa kusini Pemba anasema, hadi sasa chama hicho hutumia watu wa karibu, na watu wenye ulemavu wa uziwi katika kufikisha sera.

 ‘’Kwasasa chama hakina mazingira rafiki kwa watu wenye ulemavu wa uziwi, katika kuhakikisha wanapata sera za chama, na badala yake tunawatumia watu wao wa karibu,’’ anaeleza.



MIKATABA/SHERIA NA SERA

Mkataba wa Umoja wa Mataifa wa watu wenye uleamu (CRPD,2006) Ibara ya 9, inazitaka  nchi wanachama, zihakikishe zimeweka utaratibu wa watu wenye ulemavu, kufikia huduma zote pamoja na mawasiliano na teknolojia.

Malengo 17 ya Maendeleo Endelevu ya Dunia ya mwaka 2020/2030 yenye shabaha 169, shabaha 11 inagusia watu wenye ulemavu wa aina zote.

Katiba ya Zanzibar ya mwaka 1984, kifungu cha 12 (1) kimeweka wazi kua, watu wote ni sawa mbele ya sheria.

Huku mabano (4) na (5) vikieleza kua, hakuna mtu yeyote atakae baguliwa kwa utaifa wake, kabila, jinsia, ulemavu, pahala alipotokea, muelekeo wa kisiasa, rangi au dini.

Ndio maana Sheria ya watu wenye ulemavu nambari 8 ya Zanzibar ya mwaka 2022, kifungu chake cha 29 kinaeleza umuhimu wa watu wenye ulemavu, kufikia miundombinu pamoja na taarifa, mawasiliano na  haki zote za msingi.

NINI ATHARI YAKE?

Zainab Mohamed Ali wa Chake Chake, mwenye ulemavu wa uziwi anasema, moja ya athari zinazojitokeza ni kutowachagua viongozi wawatakao.



Afisa Mfawidhi Tume ya Haki za Binaadamu na Utawala Bora Pemba Suleiman Salim Ahmad anasema, ni  watu hao kukosa haki yao ya kikatiba ya kupiga kura.

NINI KIFANYIKE?

Yumna Mbarouk Yussuf na Mbarouk Ali Juma wa Pemba wanasema, yvama vyote vya siasa viandae mazingira rafki kwa kuweka wakalimani wa lugha ya alama katika mikutano yote.

Katibu Mkuu wa Chama cha Viziwi Zanzibar ‘CHAVIZA’ Yahya Hamed Seif anasema, ili kuhakikisha ujumuishi wao katika kampeni za vyama vya siasa, vyama vibuni njia za kuwajumuisha.

Kaimu Mratibu wa chama cha waandishi wa habari wanawake TAMWA-Zanzibar Ofisi za Pemba Amina Ahmed Mohamed anasema, ni vyema vyama vyote vya siasa kuweka wakalimani wa lugha ya alama.



Jingine, ni kwa wadau wa haki za watu wenye ulemavu, kuendelea kupaza sauti, ili sheria ya uchaguzi na ile ya vyama vya siasa iwe na kifungu lazimishi juu ya kuwatumia wakalimani.

                                           MWISHO

 

Comments