Skip to main content

WANANCHI PEMBA WADAI KULAZIMISHWA CHANJO YA CORONA, WIZARA YATOA TAMKO

 



NA HAJI NASSOR, PEMBA:::

WIZARA ya Afya Zanzibar, imepiga marufuku kwa daktari yeyote, kumlazimisha mwananchi kuchoma chanjo ya kinga ya Corona, na badala yake, chanjo hiyo itaendelea kuwa ya hiari ya mtu binafsi.

Akizungumza na mwandishi wa habari hizi kwa njia ya simu Januari 13, 2023, Waziri wa wizara hiyo Zanzibar, Nassor Ahmed Mazurui, alisema hakuna mtu yeyote, mwenye mamlaka ya kumlazimisha mwengine, kuchanja chanjo hiyo.

Alisema, bado kila mtu yuko huru ama kuamua kuchanja au kukataa kufanya hivyo, kwani suala la kinga ni la hiari ya mtu binafsi, na sio kumlazimisha kama ilivyozuka kwa baadhi ya madaktari kulalamikiwa.

Alisema bado msimamo wa wizara ya Afya, ni kuona chanjo hiyo inakuwa ya hiari, na wala hukuna daktari yeyote wala mfanyakazi wa wizara, mwenye nguvu na mamlaka ya kumlazimisha mtu kuchanja.

‘’Kama kuna daktari anawalazimisha watu kuchanja chanjo ya Corona, hilo ni kosa kisheria, maana bado msimamo wa serikali kuwa chanjo hiyo, ni hiari,’’alisema.

Hata hivyo Waziri huyo wa Afya wa Zanzibar Nassor Ahmed Mazurui, alisema atafuatilia kwa karibu katika hospitali zote za Unguja na Pemba, ili kujua kuna madaktari wamekuwa wakiwalazimisha wananchi kuchanja.

Katika hatua nyingine, Waziri huyo alisema, wanachopaswa kufanya madaktari na wahudumu wengine wa afya, ni kuwaelimisha wananchi, juu ya faida za chanjo hiyo.

‘’Lakini pia wanaweza kuwaeleza wananchi athari za mtu asiyechanja, aina za chanjo zilizokubaliwa, ipi unachoma mara moja na ipi mara mbili, lakini sio kuwalazimisha,’’alisema.

Hayo yamekuja hivi karibuni, baada ya baadhi ya wananchi kisiwani Pemba, kulalamikia tabia iliyozushwa, na baadhi ya madaktari, kuwalazimisha kuchoma chanjo ya Corona.

Wakizungumza na mwandishi wa habari hizi kwa masharti ya kutochapishwa majina yao walisema, kwa wanaokataa wamekuwa wakielezwa kuwa, wanaweza kukosa matibabu pindi watakapokwenda hospitalini.

Walisema wamekuwa, wakilalamika, kutokana na amri ya madaktari hao, ambao baadhi yao wamekuwa wakipita majumbani na kuwalazimisha kwenda kuchanja.



Wananchi wa shehia za Mwambe, Kengeja, Msingini Chake chake, Kwale, Ole, Micheweni, Wawi, Kiuyu Mbuyuni na Mtambwe wamesema, wamelazimishwa kuchanjwa, chanjo ya corona.

Vijana Omar Haji Khamis na mwenzake Nadia Issa Ali wa Kengeja, waliotaka majina yao yachapishwe, walisema juzi waliporudi kwenye safari zao, walikuta ujumbe unaowataka kufika hospitali kupata chanjo.

‘’Niliposema kuwa mimi siendi, tuliambiwa na waliotupa salamu, kuwa hata matatibabu mengine huwenda nayo tukayakosa,’’alisema Omar.

Kadika Mkubwa Mashiri na mwenzake Assa Khamis Mohamed wa Mtambwe walisema, wao waliwashuhudia madaktari wakipita nyumba hadi nyumba, sio tu kuwashawishi bali ni kuwalazimisha.

Akizungumza hivi karibuni, Afisa Mdhamini wizara ya Afya Pemba Khamis Bilali Ali, amerejea kauli yake, ya kuwaomba wananchi kupata chanjo hiyo, ili kujikinga na corona.

‘’Corona bado ipo, na zipo njia kadhaa za kujikinga na ugonjwa huo, ikiwa ni pamoja na chanjo, kunawa mikono kwa sabuni na maji tiririka kila baada ya muda na kuacha mikusanyiko isiyo ya msingi,’’alieleza.



Katika hatua nyingine Afisa Mdhamini huyo, alisema ambao hawastahiki kupata chanjo hiyo ni watoto waliochini ya miaka umri wa 18 na wale ambao sindano zinawadhuru pekee.

Mwezi Machi 11, 2020 Shirika la Afya Ulimwengini ‘WHO’ itangaaza kuwa ugonjwa Corona kuwa ni janga, la taifa hii ilitokana na kasi yake ya kuua na kusambaa.

Kisha WHO ikiwashauri wananchi kujiinga kwa kupata chanjo ambayo ni dawa ya kibaologia iliyokubaliwa na wataalamu wa afya, kwa lengo la kukinga, kujenga, ulinzi wa mwili na ugonjwa fulani husika kwa mujibu wa aina chanjo.

Hivi karibuni kituo cha Ulaya cha kudhibiti na kuzuwia magonjwa (ECDC) na ‘WHO’ wanakadiria kuwa watu 470,000 wenye umri wa zaidi ya miaka 60, wamenusurika kifo katika nchi 33 kote barani Ulaya, tangu chanjo hiyo ilipoanza kutolewa.

                      Mwisho

 

Comments