Skip to main content

AMINA JUMA: MJASIRIAMALI ALIYEANZIA MBALI ,SASA AANZA KUONA BANDARI, UFUGAJI, KILIMO CHAMTOA

 



NA HANIFA SALIM, PEMBA::

“HALI ya maisha yangu ilikua ni ngumu mno, na wakati mwengine ili kutimiza mahitaji, ilimlazimu muume wangu kuuza kuni,’’.

Ni maneno ya mama mmoja mwenye familia ya watoto watano Amina Juma Salum (40) mkaazi wa kijiji cha Kwawema kilichopo shehia ya Mgogoni wilaya ya Micheweni Pemba.

KABLA YA KUJIAJIRI

Hali ya maisha yake ilikua ngumu kabla ya kuingia katika uanzishaji wa mradi mbali mbali, na hapo ndio mume wake ilimlazimika kutafuta kuni auze, ili kupata chakula walau kwa siku moja.

Shida hata kwa watoto wake kupata elimu, walipokua wanakwenda skuli sare zao zilikua ni chafu, zimechanika na hata michango ya skuli ilikua inawashinda.

“Ninapotokezewa na misiba au harusi nilikua najisikia vibaya mno, kwani nilishindwa kushirikiana na wenzangu katika michango ya kifedha, hadi pale ninaposuka makuti na kuuza ndipo huchangi”, anakumbuka.

 

Maisha hayo yalikua ni ya takribani miaka 17 na ndipo ulipoanza mradi wa kunusuru kaya maskini ambapo alipata fursa ya kujiunga na mradi huo, ambao ulikua chanzo cha mbadilisha kimaisha yake.

Anasema hakufikiria akiwa macho wala kupitikiwa na ndoto, kuwa iko siku atasahau machungu ya maisha, naye kuisha kama wengine.

‘’Watoto wangu hawaifahamu siku waliovaa nguo mpya hasa sikukuu, walikuwa ni kuvaa mitumba ya bei ya chini na viatu vilivyochoka,’’anakumbuka.



Ingawa ndoto zake na hasa kwa kushirikiana na mume wake, alikuwa na ndoto za kufanya mradi wowote ili kuwaokoa watoto wao na hasa kuwapatia haki yao ya elimu.

‘’Nilisema peke yangu siku moja kuwa, kama mimi ni maskini na je watoto wangu nao waishi kwenye maisha kama haya, nikasema hapana lazima nipambane,’’anasema.

MWANGA WA MAISHA YAKE ULIVOANZIA

Anasema, baada ya kufanyiwa udahili juu ya hali yake ya umaskini na kisha aliingizwa kwenye mpango wa kunusuru kaya maskini chini ya Mfuko wa Maendeleo ya Jamii Tanzania TASAF.

 Kwa mara ya kwanza alipata shilingi 42000 kama rukuzu kutoka TASAF alizitumia na nyengine kuziweka hakiba, ambayo kila mwezi ziliongezeka kutokana na uwekaji wake.

“Nilitoa shilingi 10,000 nilimpa mume wangu, kwa ajili ya kununulia chakula, tulikula vizuri kwa siku hiyo, wanangu pia niliwapa pesa ya kutumia skuli kila mmoja shilingi 500 jambo ambalo lilikua ni ajabu kwao,’’ anasema.

Baada ya hapo anasema, alizaa wazo la kufuga kuku, mradi ambao alibaini utawatoa kimaisha, na kuwaondoshea umasikini ambao walikua nao hapo awali.

Mbali na kuwaza wazo hilo, aliamua kujishughulisha na kilimo cha migomba, mihogo, minanasi na mboga mboga za aina mbali mbali, ili kuwa na uhakika wa fedha ndogo ndogo.



 Anafahamisha, walianza kufanya matufali wao wenyewe ambayo walijengea banda dogo la kufugia kuku, kisha wakaomba mabati ambayo yalishatumika kwa ajili ya kuezekea.

KUANZA KWA MRADI

Alinunua kuku mmoja mmoja kulingana na pesa ambayo alikua akiipata kupitia TASAF kila mwezi, waliongezeka kwa kuzaliana hadi kufika kuku 100, kutoa 10 wa awali.

“Hapo nyuma sikua na utaratibu wa kuwanunulia wanangu nguo kinapofika kipindi cha sikukuu, lakini baada ya kuanza mradi huu, kila inapofika mwezi wa Ramadhani tunauza kuku wetu kwa ajili ya kukidhi mahitaji,’’ anasema.       

Alianza mradi huo ambao ulikua ni kwa kuku 10 na hadi sasa ana wastani wa kuku 100 wa kienyeji, bado anaendelea na biashara hiyo, kwa kushirikiana na mume wake.

Anasema, kwa sasa ana uwezo hata wa kununua pikipiki (Bodaboda) kwa pesa za kuku, anaofuga ikiwa atatamani kubadilisha maisha yake, kwa namna nyengine.

Kwa sasa hivi amepiga hatua kubwa za kimaisha hadi kufikia kusomesha mtoto wake katika skuli za binafsi, kupitia mradi huo wa kuku, jambo ambalo mwanzoni hakulifikiria kwenye maisha yake.

“Naweza hata kuwaita ndugu zangu katika familia, kushirikiana nao katika kujenga mambo mbali mbali, kusaidia familia yangu kwa kifedha na hata mawazo,’’ anaeleza.

Kama akitakiwa kutoa maombi kwa wafadhili wengine au serikali ni kuomba fedha hata za mkopo, ili kutanua banda kwa ajili ya mifugo yake ya kuku.

‘’Ndoto zangu za kuwa na maisha mazuri zimeshaanza kuona bandari na kweli nimeamini zie kauli za viongozi kuwa tujiajiri, kwangu zimeshazaa mafanikioa,’’anasema.

Anawashangaa wanawake wenzake, wanaoendeleza nafasi ya ugolkipa kwenye ndoa, akisema sasa wanaume wa aina hiyo wameshaondoka duniani,’’anafafanua.

Hapa anakusudia kuwataka wanawake na hasa waliomo kwenye ndoa, kuhakikisha wanakuwa na miradi japo midogo ambayo, itasaidia katika huduma za kila siku.

Kwake anasema ijapokuwa TASAF ilikumkuta njiani kuelekea kujiajiria, lakini haisahu ilivyomsukuma mbele na sasa kuwa mwanamke wa aina ya pekee katika familia yao.

MALENGO YA BAADAE

 Malengo yake ya baadae anasema, endapo hatopata msaada, anatamani kukuza mradi wa ufugaji wa kuku wa kienyejia, ili aweze kuajiri wengine kijijini hapo.

Jengine sasa anatamani kuwasafirisha mwenyewe kuku wake kutoka Pemba hadi Unguja, ili atakaporudi abeba mradi kama wa nguo.

‘’Kama mipango na mikakati yangu itafikiwa hapo baade, nataka niwe mfugaji maarufu na mwenye wateja hata wan je ya nchi, kama sisi tunavyokea kuku wa peduwi,’’anasema.

SOKO

Kwake soko la kuku na mayai ya kienyeji yake kama kusukuma mlevi kwenye bonde, hana shaka wala wasi wasi nalo, maana akitangaaza tu wateja wanajaa.

‘’Katika mifugo ambayo haina shaka ya wateja ni kuku wa kienyeji na mayai, yake maana hata mimi kama nahitaji shilingi 100,000 ya haraka nikisema tu, wameshanununuliwa,’’anasema.

Tena achia mbali wale wateja wetu kama wenye hoteli au wanaosafirisha nje ya Pemba, yaani kwa wateja wapo kama mvua.

Kwa sasa soko lake ni eneo la miji ya Wete, Konde na Micheweni ambapo ukiwapeleka maeneo hayo baada ya saa moja, unarudi na fedha.

MUME WAKE

Seif Salum Hamad ni mume na baba wa familia hiyo ya watoto watano anasema, mke wake amekua ni mshauri wake mkubwa na ndie aliyemfunua akili.

Anasema, mafanikio yote ambayo wanayapata ni mashirikiano na masikilizano ambayo wanayo baina yake na mke wake, ndio sababu kubwa iliyopelekea kufikia hapo.

“Katika shughuli zetu za kuendesha maisha tunasaidiana kwenye kilimo na hata ufugaji wa kuku, huduma pia pale ambapo mimi napungukiwa kihuduma, anasaidia ili muradi siku zinakwenda”, anasema.

Kipindi cha sikukuu hakua na uwezo wa kuwanunulia watoto angalau nguo moja tena mpya, lakini baada ya kufanya shughuli hizo amekua ni muume mbele za watu.



Anaona sasa ndoa yake imepata mapana na kurejesha upya, mapenzi, mahaba, masikilizano, uaminifu na kujiamini hasa katika hudumza za kila siku, achia mbali matibabu.

‘’Sasa kupitia mke wangu nimeamini kuwa, wanawake wakiamua ni wachumi, watafutaji, wawekaji akiba na wanaojali familia,’’anasema kwa furaha.

Anasema kwa sasa anajiamini kwa kuwa kila shilingi 100, inayotumika katika huduma za lazima pamoja na ada ya mtoto wao anayesoma skuli binafi, basi shilingi 70 ni za mke wake.

‘’Mimi sasa najiamini kama ntapata safari ya kikazi hadi mwezi mmoja, mke wangu anauwezo wa kuiendesha familia n ahata wageni wakitokezea,’’anasema.

Malengo yake ni kuwasomesha watoto wake hadi kufika vyuo vikuu na kuendesha maisha yao kwa shughuli nyengine kama vile kujenga nyumba kubwa ya kisasa.

Anawashauri wanaume wenzake washirikiane na wake zao ili wabuni miradi mbali mbali itakayowaondoshea umasikini na kuwaendeshea maisha yao ya kila siku.

MAJIRANI

Omar Haji Khamis na Fatma Hija Othman wanasema, familia hiyo imeibuka ghafla na leo kuwa mfano wa kuigwa kijijini kwao kimaendeleo.

‘’Kwa hakika jembe na ufugaji kama ukidhamiria haumtupi mtu, maana mfano wa hayo ni Amina na Mume wake, walianza kama utani kufuga kuku 10, leo wanahesabu 100,’’anasema Omar.

Kwa sasa inapofika kipindi cha sikukuu au mtu anapohitaji kuku, imekuwa rahisi wao kufika kwa Amina na kununua kwa ajili ya kukamilisha mahitaji. 

SHEHA

Sheha wa shehia ya Mgogoni Said Hamad Khamis anasema, shehia hiyo ina wakaazi 4,326 ambao wanajishughulisha na shughuli mbali mbali za kijamii na kiuchumi.

Kwake jambo la kujivunia ni kuona baadhi ya wananchi  akiwemo Amina Juma, wanafanya shughuli zao za kijamii na kiuchumi ambazo zinawasaidia katika maisha yao ya kila siku.

‘’Kwa ninavyomfami Amina Juma Salum na mume wake, leo nikisikia wanaisha kwenye maisha mazuri kwa sababu ya ufugaji na kilimo, hii ni furaha maana wameyatekeleza kwa vitendo maagizo ya serikali,’’anasema.

“Katika shehia yangu ni mwanamke ninae muamini kati ya wale ambao wanajishughulisha na harakati mbali mbali ili kuhakikisha wanapata maendeleo”, anasema.

Anaiomba serikali iendelee kuongeza nguvu kwa wanawake ambao wanajighulisha na kazi mbali mbali ikiwemo ujasiriamali, kilimo na ufugaji ili waweze kuondokana na utegemezi na hali ngumu za kimaisha.

WANAHARAKATI

Afisa miradi kutoka TAMWA Pemba Asha Mussa Omar, anaseme wamekuwa wakitoa elimu kwa wanawake, ili kubuni miradi ya kujiendesha kimaisha, badala ya kutegemea familia kwa kila kitu.

Hassina Issa Shehe wa Mchanga mdogo, anasema miradi wanayoifanya wanawake, imekuja kuimarisha ndoa na mahusiano mema kwa familia.



TASAF

 Mratibu wa TASAF Pemba Mussa Said, anasema wapo walengwa 14, 280 kwa Pemba ambao wanaendelea kupata fedha za kunusuriwa na umaskini.

Walengwa hao wapo kwenye shehia 78, ikiwemo ya Mgogoni, ambapo tayari shilingi bilioni 14. 4 zimeshwafikia.

‘’Mtu kama Amina Juma ndio hasa malengo ya TASAF ya kumtoa mwananchi katika unyonge, na kumleta kwenye taa, ili nae aishi maisha mazuri,’’anasema Mratibu.



“TASAF inaorodha ya zaidi ya walengwa 50,000 kutoka wastani wa walengwa 15 kila shehia, kati ya shehia 78, ambao wamenzisha miradi ya kujikwamua.

Mratibu Mussa anabainisha kuwa, kwa mwaka 2014/2015 walengwa hao wa kunusuru kaya maskini, waliibua miradi ya kijamii 41, idadi iliongozeka mwaka uliofuata kwa kufikia miradi 84.

 

                                       MWISHO.

Comments