Skip to main content

WADAU HAKI ZA BINAADAMU PEMBA:' UTEKELEZAJI SHERIA ZA WATU WENYE ULEMAVU BADO KITENDAWILI’

 



NA HAJI NASSOR, PEMBA@@@@

WADAU wa haki za binaadamu kisiwani Pemba, wamegundua kuwa Zanzibar inazosheria, kanuni na sera nzuri kwa ajili ya watu wa wenye ulemavu, ingawa changamoto kubwa ni utekelezaji wake kwa vitendo.

Walisema, kwa mfano ipo sheria na sera, inayotaka kila jengo la umma, liwe ni njia maalum kwa ajili ya watu wenye ulemavu, ingawa changamoto ni kutotekelezwa na mamlaka wakati wa ujenzi.

Wakizungumza kwenye kikao kazi, kilichoandaliwa na Mwemvuli wa asasi za kiraia Pemba ‘PACSO’ chenye lengo la kupitisha changamoto za kisheria kwa wanawake, watu wenye ulemavu na vijana, kilichofanyika leo Disemba 16, 2023 skuli ya maandalizi Madungu Chake chake.

Walisema, hata suala la ajira kwa kundi hilo, limewekwa katika sheria kama ilivyo suala la haki nyingine za kibinaadamu, ingawa shida ni utekelezaji wake.

Mmoja kati ya wadau hao, Khalfan Amour Mohamed kutoka Jumuiya kwa ajili ya watu wenye ulemavu wa akili ‘ZAPDD’ Pemba, alisema inashangaaza kuona majengo ya umma, hayana njia za kutembea kwa watu wenye ulemavu.




‘’Hii bado ni changamoto, utakuta jengo la ghorofa la serikali, chini imewekwa njia maaluma ‘rams’ kwa ajili ya watu wenye ulemavu, lakini haikuzingatia ofisi zilizoko juu,’’alisema.

Nae Salim Abdalla Salim, alisema kwa mfano waliandikia barua kadhaa wakati wa ujenzi wa soko jipya la Machomane Chake chake, ingawa hakuna lililozingatiwa.

‘’Leo soko la Machomane limemalizika, kakini bado kwa mtu mwenye ulemavu hasa wa viungo, hawezi kuyatembelea maduka yote yliomo humo, hii sio sababu ya sheria, ni utekelezaji tu,’’alisema.


Kwa upande wake Mwache Juma Abdalla, alisema kama sheria zitatekelezwa kama zilivyo, kundi la watu wenye ulemavu wataneemeka na haki zao.

‘’Sheria zipo nzuri, ikiwemo kuwekwa kwa alama za barabarani, adhabu kwa atakaemuigiza au kumkebehi mtu mwenye ulemavu na hata masuala ya ajira, ingawa shida ni kwenye utekelezaji,’’alieleza.



Nae mshiriki Khadija Sultan, alieleza kuwa, wakati umefika sasa kwa wadau wa haki za watu wenye ulemavu, kuungana pamoja, ili kuhakikisha, vifungu vya sheria vilivyopitishwa vinatekelezwa.

Akifungua kikao hicho, Makamu Mwenyekiti wa ‘PACSO’ Nassor Suleiman, alisema wamekuwa wakizichambua changamoto za kisheria na kisera, zinazowakwaza watu wenye ulemavu, vijana na wanawake.




‘’Lengo ni kuona makundi hayo ambayo ni sehemu ya jamii, wanafaidi haki na fursa zao, kama ilivyo kwa makundi mbali mbali, yaliopo katika jamii husika,’’alifafanua.

Mratibu wa miradi kutoka ‘PACSO’ Mohamed Najim Omar, alisema katika kikao cha kwanza, makundi ya wanawake, vijana na watu wenye ulemavu, waliibua changamoto za kisheria, ambazo kupitia kikao kitaangaliwa kwa kina.

‘’Kikao cha leo ‘jana’ kitachambua na kuona kwa kina, ikiwa yale yliyoibuliwa hapo awali, ni kweli ni changamoto za kisheria, kisera ama kikanuni,’’alifafanua.



Akielezea yaliojiri yatokanyo na kikao cha kwanza, Mratibu huyo alisema ni pamoja na kifungu cha 116 cha Sheria ya Adhabu nambari 6 ya mwaka 2018, juu ya kupewa dhamana aliyemlawiti mtu mwenye ulemavu wa akili.

Jingine alisema ni kutotekelezwa kwa uwekwaji wa miundombinu rafiki kwenye majengo ya umma, kwa ajili ya watu wenye ulemavu na hasa wa viungo.

Aidha lieleza kuwa, kwa upande wa wanawake ni kutokuwepo kwa sheria maalum, inayozungumzia masuala mbali mbali ya wanawake, ikiwemo suala la uongozi katika taasisi.

‘’Lakini hata kundi la vijana, walitaka kanuni ya kuwa na uzoefu, kama sharti la kuajiriwa hasa kwenye sekta za umma, liondolewe ili kuwe haki, wanaotoka vyuoni moja kwa moja waajirike,’’alieleza.

Mwanasheria Ali Hamad, alisema, hakuna kifungu kinachooelezea uzoefu kama sharti la kupata ajira, ama kukosa ajira na hasa katika sekta za umma.



Aidha alifafanua, hakuna mgongano wa hukumu unaotolewa tofauti ikiwa mtu atapatikana na hatia ya kumdhalilisha mtu mwenye ulemavu, kwani makosa kadhaa ya jinai yanafasiriwa kwenye sheri ya Adhabu.

Akifunga kikao hicho, Mwenyekiti wa PACSO Mohamed Ali Khamis, alisema kuwa, maoni ambayo yatapatikana katika kikao hicho, watayaandika vyema na kuyasilisha kwa Jumuiya ya wanawake wanawake wenye ulemavu Zanzibar, ambao nao watakeleza mradi kama huo, ngazi ya kitaifa.



‘’Kwenye mradi huu PASCO, inatekeleza ngazi ya kanda (zone), ingawa wenzetu wa ‘JUWAUZA’ wanatekeleza ngazi ya kitaifa na kisha maoni hayo, watayafikisha kwa viongozi wa kitaifa,’’alieleza.

Mwisho

Comments