Skip to main content

WANANCHI TUMBE PEMBA WAKATA TAMAA FIDIA ZAO

 



NA HAJI NASSOR, PEMBA::

WANANCHI wa shehia za Tumbe Magharibi na Mashariki wilaya ya Micheweni Pemba, wamesema wameshakata tamaa, juu ya kulipwa fidia za vipando vyao, vilivyoharibiwa na Shirika la Umeme la Zanzibar ‘ZECO’ wakati lilipokuwa likipelekea huduma ya umeme soko la samaki Tumbe.

 

Walisema uharivu huo ambao umefanywa tokea mwaka juzi, na kufanyia uhakiki mara mbili, lakini kutokana na muda kuwa mrefu, hawana tena tamaa juu ya kulipwa fidia zao.

 

Wakizungumza na mwandishi wa habari hizi kwa nyakati tofuati, walisema wamekuwa wakipewa ahadi zisizotekeleza na mlipaji, ambae ni wizara ya Uchumi wa Buluu zaidia ya mwaka mmoja na nusu sasa.

 

Mmoja kati ya wananchi hao Halima Haji Khalid (90), alisema aliharibiwa Miembe, Mibirimbi, Mifenesi, mihogo na migomba ingawa hadi sasa alichopewa ni ahadi.

 

‘’Mimi mmoja kati ya waathirika wa kuharibiwa vipando vyangu, wakati ZECO linasafisha njia kwa ajili ya kupeleka huduma ya umeme soko la samaki Tumbe, lakini hadi leo sijalipwa.’’alieleza.

Nae Ali Kale alisema, pamoja na kuharibiwa kwa vipando vyake alivyokuwa akivitegemea mfano minazi na mifenesi, lakini hadi sasa hajapata fidia zake.

 


Nae Khadija Makame Shamata, alisema haamini tena kuwa kuna siku atalipwa fidia yake, kutokana na kupewa ahadi hewa kila muda kutoka wizara ya Uchumi wa buluu.

 

‘’Tupo zaidi ya wananchi 35 ambao tuliharibiwa vipando vyetu vichanga wakati ZECO inapeleka huduma ya umeme soko la samaki Tumbe, lakini hadi sasa hatujalipwa,’’alieleza.

 

Kwa upande wake Aisha Issa Mjaka, alisema alielezwa kuwa watalipwa fidia zao wakati wowote, ingawa kutokana na muda kuwa mkubwa, kwa sasa hana tena tamaa.

 

Kaimu sheha wa shehia ya Tumbe Mashariki Omar Ali Omar alikiri kuwepo kwa shida hiyo, na kusema mara ya mwisho uongozi wa uchumi wa Buluu Zanzibar uliwaahidi kuwalipa fidia wananchi hao mwezi Mei mwaka huu.

 

‘’Kikao cha mwisho kilifanyika mwezi Aprili mwaka huu, ndani ya soko la samaki la Tumbe, baina ya waathirika na uongozi wa wizara ya Uchumi wa Buluu na Uvuvi, na ahadi ikatolewa kuwa mwezi Mei watalipwa, lakini hadi sasa bado,’’alieleza.

Alisema taarifa za kuwa wananchi wa shehua yake hawajalipwa fididi hizo ameshazifikisha kwa uongozi wa wilaya ya Micheweni, kwa muda mrefu sasa.

 

Mkuu wa wilaya ya Micheweni Mgeni Khatib Yahya, alikiri kuwepo kwa taarifa hiyo, na kusema tayari ameifikisha shirika la umeme la Zanzibar ‘ZECO’ ofisi ya Pemba.

 


Alisema, mara ya mwisho aliahidiwa kuwa, mpango wa kulipwa kwa fidia hizo umeshawekwa sawa na wakati wowote wananchi hao watalipwa.

 

‘’Ni kweli wananchi wa shehia za Tumbe Mashariki na Magharibi walioharibiwa vipando vyao, wakati wa upelekaji umeme soko la samaki Tumbe hawajalipwa, na taarifa hizi nshazifikisha ZECO,’’alieleza.

 

Meneja wa shirika la Umeme la Zanzibar ZECO tawi la Pemba Mohamed Juma, alikiri kuwa deni hilo kwa wananchi hao halijalipwa, ingawa wao sio wahusika.

 

‘’Sisi ZECO tulipewa kazi ya kufikisha huduma ya umeme soko la samakini Tumbe na wizara ya Uchumi wa Buluu na Uvuvi, na hao ndio tuliokubaliana kuwa walipe fidia,’’alieleza.

 

Meneja huyo alieleza kuwa hata wananchi wanalijua hilo, kuwa walipaji sio ‘ZECO ‘bali na wizara ya Uchumi wa Buluu na Uvuvi, kama makubaliano yalivyofikiwa.

 

Afisa Mdhamini wizara ya Uchumi wa Buluu Pemba Dk. Salum Mohamed Hamza, alikiri kuwa hadi sasa fidia hiyo haijalipwa, ingawa nia bado ipo.

 

Alisema kwa sasa wanaisubiri wizara ya Fedha na Mipango Zanzibar, maana ndio walipaji wakuu wa madeni yote ya serikali, kwa mujibu wa maelekezo ya ripoti ya Mdhibiti na Mkaguzi mkuu wa hesabu za serikali.

 

‘’Sisi tunaisubiri wizara ya fedha, baada ya kumaliza taratibu zao, kama watutingizia sisi fedha tutawalipa fidia zao wananchi, na kama watalipa wenyewe pia sawa,’’alieleza.

 

Aidha alieleza kuwa, wastani wa shilingi milioni 60 hadi 70 ndio ambazo zikadiriwa kulipwa na hasa baada ya kufanya tathmini ya mara ya pili, ambayo ya mara kwanza ilikuwa na makosa kadhaa.

 

‘’Wamo baadhi ya wananchi watalipwa katia ya shilingi milioni 4, wengine hadi 6, na hii itawashangaaza wananchi, maana wao walitarajia kupata kidogo, lakini kwa tathimini ya mtathimini mkuu kutoka wizara ya Ardhi fidia zimeongezeka,’’alieleza.

 

Sehemu eneo la kuuzia samaki la soko hilo lilifunguliwa na Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Hussein Ali Mwinyi Julai 26, mwaka huu.

                        Mwisho

Comments