Skip to main content

WANAHABARI ZANZIBAR NA MATUMAINI YA KUPATA SHERIA MPYA YA HABARI

 



NA SALUM VUAI, ZANZIBAR@@@@

KUFUATIA uteuzi wa Mawaziri wapya Zanzibar baada ya uchaguzi mkuu wa Oktoba 29 mwaka huu uliokirudisha madarakani Chama cha Mapinduzi, waandishi wa habari hawakusita kutoa ya moyoni wakieleza matumaini waliyonayo katika kuimarika zaidi kwa sekta ya habari.

Wadau wa habari na waandishi waliozungumza na gazeti hili, wamesema kwa miaka mingi, sekta ya habari visiwani Zanzibar imekuwa ikipata mafanikio kadhaa, ingawa pia wamebainisha  changamoto mbalimbali zinazowabana katika utekelezaji wa majukumu yao.

Wamesifu kuongezeka kwa uhuru wa habari kwa kiasi fulani, lakini wakaeleza kuwa bado baadhi ya watu wanatawaliwa na dhana potofu kwamba waandishi wa habari hawapaswi kuwa marafiki wa kudumu bali ni wa msimu tu hasa pale maslahi yao binafsi yanapohusika.

Kutokana na fikra kama hizo, mara kwa mara waandishi wamekuwa wakinyimwa   taarifa au kuamriwa kutozitangaza hasa ikiwa jambo linalotakiwa linahusu uzembe, hujuma au makosa ya mtu au taasisi inayohojiwa.

Hata Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Barza la Mapinduzi, aliitaja na kuikemea tabia hiyo alipowaapisha mawaziri wapya aliowateua baada ya uchaguzi mkuu, akihoji kwa nini hata taarifa za maendeleo zifichwe.

MUARUBAINI

Ili kuondoa vikwazo hivyo na vyengine vinavyofanana navyo, marekebisho ya sheria ya habari kimekuwa kilio kikubwa kwa waandishi, wakitaka sheria mpya inayokwenda na wakati uliopo na isiyokuwa na masharti yanayoumiza.

Ifahamike kuwa, uhuru wa habari na kutoa maoni, ni miongoni mwa haki za binadamu zilizomo katika mikataba mbalimbali ya kitaifa na kimataifa.

Hiyo inatokana na masuala ya haki hizo za binadamu kuanza kuingizwa katika mikataba hiyo mnamo mwaka 1950 baada ya dunia kuweka Azimio la kuzilinda kimataifa (Universal Declaration of Human Rights-UDHR) lililofikiwa mwaka 1948.

Kama hiyo haitoshi, barani Afrika, suala la haki za binadamu liliainishwa katika mkataba wa Afrika kuhusiana na jambo hilo lililopitishwa mwaka 1981.

Mwenyekiti wa Jumuia ya Waandishi wa Habari za Maendeleo Zanzibar (WAHAMAZA) Hawra Shamte, alisema haki ya uhuru wa kujieleza ambayo pia inahusu haki ya uhuru wa habari inalindwa  chini ya Ibara ya 18 ya Katiba ya Zanzibar.

Ibara hiyo 18 (1) inasema: “Bila ya kuathiri sheria nyengine za nchi, kila mtu anayo haki ya uhuru wa maoni (kujieleza), kutafuta, kupokea na kusambaza habari na mawazo yake kupitia chombo chochote cha habari bila kujali mipaka ya nchi na pia anayo haki na uhuru wa kutoingiliwa mawasiliano yake.

Ibara hiyo hiyo kifungu namba 2, kinasema; “Kila raia anayo haki ya kupewa taarifa wakati wote wa matukio mbalimbali nchini na duniani kwa jumla ambayo ni muhimu kwa maisha na shughuli za wananchi na pia masuala yenye umuhimu kwa jamii.”

Akinukuu mapungufu yaliyomo katika kifungu cha kwanza kama yalivyooneshwa kwenye rasimu ya marekebisho pendekezwa ya sheria ya habari, Hawra alisema kinanyang’anya haki na hivyo kinahitaji kurekebihswa ili kisiume.

“Hapo ilipoelezwa katika kifungu hicho cha Katiba, maneno; “Bila kuathiri sheria nyengine yoyote ya nchi”, kinamaanisha kuwa, kufurahia uhuru wa kujieleza, kutafuta, kusambaza habari, kunategemea sheria nyengine za nchi,” alisema.

Aliitaja pia Ibara ya 24 ya Katiba ya Zanzibar inayosomeka, “Haki za binadamu na uhuru, kanuni zake ambazo zimeainishwa katika Katiba hii, hazitatekelezwa na mtu kwa namna ambayo itasababisha kuingiliwa au kukandamiza haki na uhuru wa watu wengine au maslahi ya umma.”

Mwenyekiti huyo alisema aya iliyotajwa hapo juu, inaweka bayana kwamba  haki na uhuru huo unaweza kuwekewa mipaka na sheria iliyotungwa na Baraza la Wawakilishi  ikiwa kizuizi hicho ni cha lazima.

Shamte alionesha wasiwasi kuwa kifungu hicho kinatoa nafasi kwa Baraza la Wawakilishi kuweka mipaka ya kufurahia uhuru wowote ikiwa ni pamoja na ule wa kujieleza.

“Kwa uhitaji wa sheria mpya ya habari hapa Zanzibar, uko ulazima Katiba hiyo pia ifanyiwe marekebisho ya haraka na ni wajibu wa waandishi  kuchagiza  jambo hilo lifanyike sasa bila ya ajizi,” alibainisha.

Ni wazi uharaka huo ni muhimu kwa kuwa zipo sheria nyengine nyingi zinazoathiri uhuru wa habari na haki ya kujieleza, kwa mfano sheria za usalama wa Taifa, Baraza la Wawakilishi, Takwimu na ile ya makosa ya mtandaoni ambayo imetungwa Tanzania Bara na haijaridhiwa Zanzibar lakini inatumika.

Kauthar Is-Hak, mwandishi na ofisa habari mwandamizi Idara ya Habari Maelezo Zanzibar, alishauri sheria ijayo ijumuishe pia maeneo yanayokataza matumizi makubwa ya nguvu kwa wanahabari iwapo  kwa bahati mbaya, watabainika kutangaza taarifa zinazohisiwa kwenda kinyume na sheria za nchi, au kwa upande mmoja kutopendezewa tu kutolewa kwake.

Kwa kuwa dunia inakwenda haraka katika maendeleo ya teknolojia ya habari, amesema ni vyema sheria mpya izingatie mabadiliko hayo.

“Dunia ya sasa ni tofauti na kale ambapo teknolojia mpya imeshika kasi na ndio inayowaleta watu pamoja kwa muda mfupi na haraka zaidi. Mitandao ya kijamii imerahisisha mawasiliano na hakuna kitu kinachoweza kufichwa,” alifafanua.

Ofisa huyo alisema ingawa uhuru una mipaka, lakini huu si wakati wa kufungana midomo, akisema dunia ilipofika, ni vigumu kuwadhibiti watu wasitoe joto lao.

Hata hivyo, alieleza kuwa jambo la muhimu  sheria isiwabane watu kwa kuwa tu wanagusa mambo yasiyofaa ambayo watendaji hawataki  yadhihirishwe hata kama ni kwa maslahi mapana ya umma.

ADHABU KWA VYOMBO VYA HABARI

Mjumbe wa Kamati ya Wataalamu wa Habari Zanzibar (ZAMECO) Jabir Idrissa Yunus, aligusia suala la adhabu kwa waandishi wa habari na vyombo vinavyokutwa na makosa ya kimaadili.

Alisema jambo hilo linahitaji kutazamwa kwa jicho la tatu ili kuhakikisha adhabu zinazotolewa hazimuathiri mtu asiyehusika, mathalan kukifungia chombo cha habari kwa kosa binafsi la mwandishi.

Alieleza kuwa, kufungia chombo cha habari kwa kosa linalomhusu mwandishi si haki. Kwanza adhabu yenyewe ni kubwa sana na kufanya hivyo ni kuadhibu wanaokitegemea kihabari.

Kadhalika, alisema ni busara kushughulika na mwandishi kwa kutumia njia za kuelimisha zaidi maana wakati mwengine makosa hutokana na sifa ya kibinadamu, kuikosea au bahati mbaya.

“Kwa mfano, madaktari na wauguzi nao hukosea. Je, ifungiwe hospitali yote? Na upande wetu tunayo Mabaraza ya Usuluhishi, basi na yatumike kusahihishana," alishauri.

"Juzi tu hapa tumesikia mgogoro kati ya Rais
Trump wa Marekani na BBC. Wakosaji ni Idara ya Habari ya  BBC, halijafungiwa shirika, mtendaji mmoja ndio amejiuzulu, Shirika linaendelea na kazi. Ndivyo nasi tunapaswa kwenda." 

Alihitimisaha kuwa kusema kuwa, mchezo wa kufungia-fungia ukiendekezwa, itakuja siku watu wataamka asubuhi hakuna hata gazeti moja mtaani, na rediio/televisheni zote zimefungwa.

Alitaka nchi isifike huko na sheria ijayo isiweke ugumu kama huo.

WATU WENYE ULEMAVU

Jumuiya ya vyama vya watu wenye ulemavu ni miongoni mwa wadau wakubwa wa habari, hivyo mwandishi wa makala haya alizungumza na Mratibu wa Chama cha Watu Wasioona Zanzibar (ZANAB) Adil Mohammed Ali kujua maoni yao kwa ujumla.

Alikumbusha kuwa, Zanzibar ilikuwa na sheria namba 5 ya usajili wa wakala wa habari, magazeti na vitabu ya mwaja 1988 ambayo ilionekana na mapungufu yaliyoikuwa yakikwamisha haki ya uhuru wa vyombo vya habari na uandishi.

Alisema hata baada ya kurekebishwa, bado imeonekana sheria iliyopo sasa haitekelezeki vizuri.

Adil alikiri kuwa huu ni wakati muafaka Zanzibar ipate sheria mpya ya habari ili kukidhi matakwa ya uhuru wa kujieleza na kuwa na serikali inayoendeshwa kwa misingi ya uwazi na ukweli.

Alisema, waandishi wa habari ni wadau wa maendeleo, na pia ni jicho linaloona mbali na ni sauti ya wasiokuwa na sauti wanaoweza kuleta mabadiliko chanya kimaendeleo.

WIZARA YA HABARI

Akizungumza katika mahojiano na televisheni ya Shirika la Utangazaji Zanzibar (ZBC), Waziri wa Habari, Sanaa, Utamaduni na Michezo Riziki Pembe Juma, aliahidi kulianyia kazi suala la upatikanaji sheria mpya ya habari.

Alisema anaelewa kuwa ombi hilo ni la miaka mingi na kwamba hatua zimekuwa zikichukuliwa kuipitia na kuichambua rasimu katika ngazi tofauti, akisema kazi iliyobaki ni kuipeleka Baraza la Wawakilishi ikajadiliwe kuhitimisha mchakato.

Bila shaka, kauli hii ya Mhe. Waziri inawapa wanahabari matumaini makubwa kwamba, marathoni ya kusaka sheria mpya, itafikia mfundani kipindi kifupi kijacho.

BARAZA LA HABARI

Suala la uchechemuzi kwa waandishi wa habari kote Tanzania ili kuwajengea uwezo wa kuyatetea kitaalamu mambo yanayowahusu, ni sehemu ya mipango ya Baraza la Habari Tanzania (MCT).

 

Makongamano na mafunzo mbalimbali yamekuwa yakiandaliwa na MCT ili kuinua uelewa  wa  waandishi na wahariri, si tu kuandika kwa weledi, bali kuweza kuchambua kitaalamu masuala yanayogusa ustawi wa taifa na dunia kwa jumla.

 

Kwa mfano kuanzia Septemba 8, 2025, MCT iliendesha mafunzo ya siku tano ya wahariri na waandishi wa magazeti, radio televisheni na mtandaoni, yaliyofanyika katika Michenzani Mall mjini Unguja.

 

Mafunzo hayo yalilenga kuimarisha uwezo wa kitaaluma na kisheria, namna ya kung’amua taarifa zisizo sahihi (misinformation), taarifa za uongo (disinformation) , hotuba na matamshi ya chuki (hate speeches) kuelekea uchaguzi mkuu uliopita.

 

Aidha, Novemba 17-19, MCT iliandaa mafunzo kama hayo kwa waandishi na wahariri wanachama wa Kamati ya Wataalamu wa Habari Zanzibar (ZAMECO) Mnarani Mapinduzi Square, kuelimisha mbinu za utetezi (Advocacy) katika masuala na maslahi ya wanahabari.

 

 

 

Comments

BLOG'S VISITORS

DAKTARI MWENGINE CHAKE CHAKE KULA SIKUKUU POLISI, NI KWA TUHUMA ZA KUMBAKA MGONJWA WAKE

NA WAANDISHI WETU, PEMBA::: DAKTARI anaetoa huduma kwa wagonjwa kituo cha afya cha serikali cha  Gombani wilaya ya Chake Chake Pemba, Is-haka Rashid Hadid, anaendelea kushikiliwa na Jeshi la Polisi Mkoa wa kaskazini Pemba, akituhumiwa kumtorosha na kisha kumbaka mtoto wa mwenye umri wa miaka 16, mkaazi wa Gombani. Daktari huyo miaka 35 ni mkaazi wa Kangagani Wilaya ya Wete mkoani humo, ambapo anadaiwa alimchukua mtoto huyo kutoka kwa rafiki yake, na kumpeleka kwenye nyumba anayoishi eneo la Kangagani. Mtoto aliefanyiwa kitendo hicho alisema kuwa, April 21 mwaka huu alikwenda kituo cha afya Gombani, kwa ajili ya matibabu na baada ya kupatiwa huduma na daktari huyo, alimuomba nambari yake ya simu. Alisema ilipofika usiku, walikuwa wanawasiliana kupitia ujumbe mfupi (sms) kwa lengo la kwenda kuchukua dawa nyingine ambazo kwa mchana huo alizikosa hospitalini hapo. "Nilikwenda hospitali kutibiwa, baada ya kufanya mapele katika sehemu zangu za siri, lakini akaniambia mpaka aje da...

HII KALI MBUNGE ASIYA AMKOGESHA MWANANCHI HADHARANI KISA HICHI HAPA......

  NA HAJI NASSOR, PEMBA MBUNGE wa viti maalum nafasi za wanawake mkoa wa kaskazini Pemba Asiya Sharif Omar, amewataka wananchi wa kijiji cha taifu, shehia ya Kinyasini jimbo la Gando wilaya ya Wete Pemba, kuyalinda miundombinu ya maji safi na salama, ili yawe endelevu kwao. Kauli hiyo ameitoa wakati alipokuwa akizungumza na mwandishi wa habari hizi, mara baada ya kuwasili kijijini humo, na kumkogesha mwananchi mmoja kama ishara ya uzinduzi wa mradi wa maji safi na salama, ulioasisiwa na mbunge wa Jimbo la Gando. Alisema, hawana mbadala kwa sasa bali ni kuilinda miundombinu ya huduma hiyo, hasa baada ya mbunge wa wao Salim Mussa Omar, kuwarejeshea huduma hiyo. Alieleza kuwa, inafahamika kuwa kwa miaka 14 waliikosa huduma hiyo hasa kwa vile viongozi waliokuwepo hawakujali kuwatatulia tatizo hilo, hadi juzi ilipofanywa na mbunge wao. “Baada ya huduma hii sasa kurejeshwa na mbunge wa jimbo la Gando, kazi iliyobakia kwenu wananchi ni kila mmoja kuwa mlinzi wa miundombinu hii,’...

'MKAPA' NA WENZAKE PEMBA WALAZWA RUMANDE

  NA HAJI NASSOR, PEMBA@@@@ MAHKAMA kuu Zanzibar kisiwani Pemba, chini ya Jaji Ibrahim Mzee Ibrahim, imewapeleka rumande watumuhimwa wanne wanaokabiliwa na tuhuma za kuua kwa makusudi, akiwemo Ali Mussa Omar ‘ Mkapa’ mkaazi wa Wawi wilaya ya Chake chake Pemba. Watuhumiwa wengine walioanza maisha mapya ya rumande ni mtuhumiwa Yassir Mohamed Juma miaka 23, Anuwari Mussa Omar miaka 30 pamoja na mtuhumiwa Yassir Mussa Omar ‘ Makababu ’ miaka 29, wote wakaazi wa shehia ya Wawi, wilaya ya Chake chake Pemba. Awali watuhumiwa hao waliwasili mahakamani hapo, kwa mara ya kwanza, kwa ajili ya kusomewa tuhma zinazowakabili za kumuua kwa maksudi Said Seif Kombo. Ilidaiwa mahakamani hapo na Mwendesha Mashtaka kutoka Ofisi ya Mkurugenzi wa Mashataka Seif Mohamed Khamis akiambatana na mwenzake Mussa Khamis Ali kuwa, watuhumiwa hao kwa pamoja wanadaia kufanya mauwaji hayo kwa maksudi. Ilidai kuwa, watuhumiwa wote kwa pamoja, walitenda kosa hilo Oktoba 16, mwaka huu, baina ya saa 7:00 m...

TUHMA ZA DAKTARI PEMBA KUCHIWA HURU: POLISI KASKAZINI KUTOA TAARIFA RASMI LEO

  NA HAJI NASSOR, PEMBA KAMANDA wa Polisi mkoa wa kaskazini Pemba, Juma Saad Khamis, amesema leo Mei 9, mwaka huu atatoa taarifa rasmi, juu ya kuendelea kumshikilia au kumpa dhamana ya Polisi, daktari wa Kituo cha Afya Gombani Is-haka Rashid Hadid, anayetuhumiwa kwa ubakaji. Alisema, kwa vile alikuwa katika mapumziko mafupi, haelewi jambo lolote linaloendelea kwa mtuhumiwa huyo, juu ya kuendelea kushikiliwa kwake kituoni hapo. Alieleza kuwa, leo Mei 6 (jana), hajapata taarifa za ndani za mtuhumiwa, huyo na kuwataka wananchi na wanaharakati, wasubirie hadi Jumatatu ijayo. Akizungumza na waandishi wa habari kwa nyakati tofauti Kamanda huyo, alisema hana taarifa zozote za kupewa dhamana mtuhumiwa ndani ya kituo chake cha Polisi au kuendelea kuwepo. ‘’Ilikuwa mimi sipo kazini kwa muda, kuanzia anakamatwa hadi anafikishwa Polisi, kwa sasa siwezi kueleza jambo lolote kwa mtuhumiwa huyo, hadi Jumatatu,’’alieleza. Aidha Kamanda huyo alieleza kuwa, kwa sasa hawezi kutoa uf...

MADAKTARI KUTOKA CHINA WAOKOA MAISHA YA MTOTO PEMBA

  HABIBA ZARALI, PEMBA TIMU ya 32 ya madaktari wa kichina katika hospitali ya Abdalla Mzee Mkoani wamefanikiwa kufanya upasuaji mkubwa wa mtoto mwenye umri wa miaka 15 mkaazi wa Chole Kengeja, baada ya kuchomwa na jiti sehemu ya njia zake za mfumo wa uzazi. Mtoto huyo ambae alianguka hivi karibuni katika mti na baadae kuchomwa na jiti hilo na kumsababishia kutokwa na damu nyingi katika sehemu ya nyonga, alifanyiwa upasuaji uliodumu kwa muda wa saa tatu na   kuokolewa maisha yake. Akizungumza mara baada ya operesheni huo kiongozi wa timu hiyo Dr Jiang Jinhua, alisema mara baada ya mtoto huyo kufikishwa hospitalini hapo na kufanyiwa vipimo na kuonekana   ilibidi apatiwe rufaa ya kwenda katika hospitali nzuri yenye kutibu tatizo lake huko nchini Kuwado ambapo haikuwezekana kutokana na hali ya umaskini wa f amilia ya mtoto huyo . Alisema timu ya madaktari hao itaendelea kutowa huduma za matibabu   kwa wananchi kisiwani humo,   ili kuwaondolea gharama ya kuta...