Skip to main content

SHAMATA AZINDUA SOKO LA KISASA MTAMBILE

 



NA HAJI NASSOR, PEMBA@@@@

WAZIRI wa Kilimo, Umwagiliaji, Maliasili na Mifugo Zanzibar Shamata Shaame Khamis, amewaagiza wakulima wa ndizi wilaya ya Mkoani, kuepukana na vishoka wa biashara hiyo, na badala yake walitumie soko jipya la Mtambile, ili kupata bei kubwa.



Waziri Shamata aliyasema hayo jana, mara baada ya ufunguzi wa soko la mboga na matunda la Mtambile wilaya ya Mkoani, ikiwa ni sehemu za shamra shamra za miaka 60 ya Mapinduzi Zanzibar ya mwaka 1964.

Alisema, kuanzia sasa waachane na wanunuzi wa ndizi wanaowalalia kibei, na badala yake sasa walitumie soko hilo, ili kuzipandisha thamani ndizi zao.




Alieleza kuwa, ndani ya soko hilo mtakuwa na mnada maalum wa mazao mbali mbali, ikiwemo ndizi, muhogo, matikti, nyanya, chungwa na ndimu, hivyo ni wajibu kwa wakulima hao, kulitumia soko hilo.

Waziri Shamata, alisema kwa muda mrefu, wakulima walikuwa wanalaliwa kibei na wachuuzi wanaosafirisha bidhaa hiyo nje ya kisiwa cha Pemba, kwa kueleza kuwa kunaanguko la bei.

‘’Niwatake wakulima wa ndizi, sasa iwe basi kulaliwa bei na njooni hapa ndani ya soko jipya, na muuze bidhaa hiyo na mtapata bei, maana patakuwa na ushindani wa bei,’’alieleza.

Hata hivyo Waziri huyo, aliliagiza baraza la mji wa Mkoani, kutenga bajeti maalum, kwa ajili ya matengenezo madogo madogo ya soko hilo hapo baadae.

‘’Leo (jana) tumelifungua soko hili, linang’ara na linapendeza, sasa ni wajibu kwa Baraza la mji Mkoani, kuanzia sasa kujiwekea bajeti maalum, kwa ajili ya matengenezo,’’alifafanua.

Aidha amewataka wafanyabiashara wote na hasa wale waliokuwa wakianyabiashara zao pembezoni mwa barabara, sasa kuhamia ndani ya soko hilo.

Katika hatua nyingine, Waziri huyo wa Umwagiliaji, Maliasili, na Mifugo, alisema kufanyika kwa Mapinduzi ya Zanzibar ya mwaka 1964, yamewakomboa wananchi kiuchumi.

Alisema kuwa, kabla ya kufanyika kwa Mapinduzi hayo, wananchi wa Zanzibar, hawakuwa na nafasi ya kulima na kuuza kwa bidhaa zao kwa thamani, jambo lililowazidishia unyonge.

‘’Tukiwa ndani ya miaka 60 ya Mapinduzi ya Zanzibar, lazima tuwakumbuke waasisiwa wa taifa hili, akiwemo rais wa kwanza wa Zanzibar, marehemu Abied Amani Karume na mwenzake kwa kujitolea,’’alisema.

Hivyo amewataka wananchi, kuendelea kuiunga mkono serikali ya awamu ya nane, ambayo inaendelea kutekeleza dhana ya mapinduzi daima kwa vitendo, kwa kujenga miradi mikubwa ya maendeleo.

Kwa upande wake, Katibu mkuu Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa, serikali za Mitaa na Idara Maalum za SMZ Issa Mahafudhi, alisema ujenzi wa soko hilo, ni utekeleza wa ahadi ya Rais wa Zanzibar, wakati alipokutana na wajasiriamali.

Hata hivyo alisema, mji wa Mtambile umekuwa na ongezeko la watu kila mwaka, na sasa kuchukua nafasi ya tatu kwa idadi ya watu, baada ya Chambani yenye wakaazi 7,460, Kengeja 7,202 na Mtambile 7,000.


‘’Hivyo uwepo wa soko hili, limeandana na mahitaji ya wananchi kwa muda mrefu na hasa suala la changamoto, iliyopo ya wafanyabiashara kuendesha shughuli zao pembezoni mwa barabara,’’alifafanua.

 Mkuu wa Mkoa wa kusini Pemba, Mattar Zahor Massoud, alisema serikali inampango wa kujenga soko jingine kama hilo, katika eneo shehia ya Kengeja, ili kukidhi mahitaji ya wajasiriamali.

Akizungumzia Mapinduzi ya Zanzibar ya mwaka 1964, alisema yalifanyika kwa lengo la kuwapa heshima wazalendo wa taifa hili, ikiwemo kujitambua kiutu na kiuchumi.





‘’Leo tukiadhimisha miaka 60, kila mmoja ni shuhuda kuwa, ameyapata matunda ya mapinduzi, iwe kwenye sekta ya elimu, afya, barabara, maji safi na salama,’’alifafanua.

Soko hilo la matunda na mboga la Mtambile inavyo vikuta 40, milango 13 ya maduka, ambapo ujenzi wake ulianza mwishoni mwa mwaka 2022, na kumalizika mwezi Julai mwaka huu.

Ujenzi huo umepitia hatua tatu, ikiwemo ukataji mlima, ujenzi wa soko lenyewe na uweka saruji chini nje ya soko hilo, lenye vyoo vinane, kikiwemo cha watu wenye ulemavu.

Aidha ujenzi huo, umegharimu zaidi ya shilingi milioni 5.88 ambapo ni fedha zinazotokana na makusanyo ya baraza la mji Mkoani, kupitia serikali kuu.

Shamra shamra hizo za miaka 60 ya Mapinduzi ya Zanzibar zitaendelea tena kesho, eneo la Makangale ambapo Waziri wa Biashara na Maendeleo ya Viwanda Zanzibar Omar Said Shaaban atalifungua tangi la maji safi na salama.

                           Mwisho 

Comments