Skip to main content

WATATU MIKONONI MWA POLISI TUHMA ZA UPIGAJI MAPANGA KENGEJA

 



NA ZUHURA JUMA, PEMBA@@@@

JESHI la Polisi Mkoa wa kusini Pemba, linawashikilia watu watatu kwa tuhuma za kumshambulia mfanyabiashara Maulid Haroub Mpemba na mke wake, katika eneo la Kengeja wilaya ya Mkoani Pemba.

Akizungumza na mwandishi wa habari hizi kwa njia ya simu, Kamanda wa Polisi Mkoa huo Abdalla Hussein Mussa, alisema watuhumiwa hao, walikamatwa katika siku na maeneo tofauti humo.

Aliwataja waliowakamata kuwa ni pamoja na Saleh Mohamed Abdalla ‘Mbambe miaka 33, Mohamed Rashid Mohamed miaka 42 wote wakaazi wa Mjiweni Kengeja na Salum Mohamed Seif ‘Rumbwi miaka 36 mkaazi wa Tumbi Wambaa.



Alisema kuwa, baada ya kupokea taarifa za tukio hilo kutoka kwa wasamaria wema, majira ya saa 7:00 usiku Machi 17 mwaka huu, Jeshi la Polisi liliandaa mitego na kufanikiwa kuwakamata katika maeneo na siku tofauti.

Alisema watuhumiwa hao, wanaodaiwa kumshambulia mfanyabiashara huyo kwa vitu vyenye ncha kali, katika sehemu mbali mbali za mwili wake, huku mke wake wakimshambulia kwa kumpika marungu.

Alieleza kuwa, tukio hilo lilisababisha mfanyabiashara huyo kupata maumivu makali katika mwili wake na hasa eneo la kichwani na kutokwa na damu nyingi, ambapo kisha alikimbizwa hospitali ya Abdalla Mzee Mkoani Pemba kwa matibabu.

“Mfanyabiashara huyu alivamiwa usiku na watu wasiojulikana nyumbani kwake, huku chanzo rasmi kikiwa bado hakijafahamika”, alisema Kamanda huyo.




Baadhi ya wananchi waliokataa kutaja majina yake, walisema walisikia vurumai ndani ya nyumba yake, ingwa hawakujua nini kinaendelea.

Walisema, muda mfupi waliskia gari ikiondoka eneo la tukio na kutokomea sehemu isiyojulikana na kumuacha mfanyabiashara huyo akiwa na majeraha makubwa.

Taarifa kutoka hospitali ya Abdalla Mzee, zinaeleza kuwa baada ya kupokelewa kwa mjeruhi kisha alihamishia hospitali nyingine kwa matibabu zaidi..

                        Mwisho

 

 

Comments