Skip to main content

KUMBE NJIA HII NI RAHISI KWA WANAWAKE KUKOSA KIZAZI NA HATIMAE KIFO

 


    

NA ZUHURA JUMA, PEMBA@@@@

UTOAJI mimba ni jambo lisilokubalika.

Lakini na hata jamii, serikali na sheria za nchi ya Zanzibar na Tanzania kwa ujumla, linakatazwa.

Ingawa sheria kwa upande mmoja hata hizo za dini, zinakubali, kutoa mimba, ikiwa mtaalamu wa afyua alishathibitisha, mimba hiyo kubakia ni madhara makubwa zaidi.

Jamii zetu kumekuwa na baadhi ya wanawake na wakati mwingine wakishirikiana na wanaume, katika utoaji wa mimba usio salama, kwa sababu wanazozijua wao wawili tu.

Jambo hili limetajwa na wataalamu wa afya kuwa, huhatarisha maisha yake, fuko lake la uzazi na wakati mwingine kifo.

‘’Hali hii inatokana na kuwa dini yetu ya kiislamu pamoja na sheria za nchi haziruhusu kutoa mimba, labda kuwe kuna tatizo la kumuhatarishia maisha,’’ anafafanua Mratibu wa Afya ya Uzazi Pemba Dk. Rehema Abdalla Abeid.

Hivyo kwa vile wanatoa kwa matakwa yao bila kuwepo sababu za msingi, hawaendi hospitali na hutumia njia za kienyeji, jambo ambalo ni hatari kwa maisha yao.

Utoaji wa mimba unaweza kusababisha utasa hasa kwa wale wanaotoa mimba nyingi au mara kwa mara, kwani hupelekea kuharibika fuko la uzazi na hatimae hutolewa kabisa.

Kwa nini wanawake wanatoa mimba?

Dk. Rehema anasema ni kwamba, mbebaji wa mimba ile huwa hajajipanga, hivyo hakuitarajia na ndio maana anaamua kuitoa bila kujali athari inayoweza kumpata.

‘’Lakini mimi husema, hiyo mimba huwa ameitarajia kwa sababu anaenda kukutana na mwanaume huku akijua hatumii uzazi wa mpango, sasa atarajie nini kama sio mimba?,’’ alihoji.

Anasema, wengine hutoa mimba kwa kupoteza ushahidi hasa kwa wasichana ambao hawajaolewa na wajane, kwani sio utamaduni wa jamii yao kubeba ujauzito kabla ya kuolewa.

‘’Wanakosa elimu ya uzazi salama, hivyo wanashindwa kujua sehemu sahihi ya kwenda na wengine wanajua ingawa wanaona aibu kwenda hospitali,’’ anasema.

Dk. Rehema anasema, wanapokwenda hospitali huwa tayari mimba imeshatoka na amepata madhara ambayo yanahatarisha maisha yake na hivyo husema kuwa, ameharibu.

Wazazi na watoto wenyewe hawapo wawazi kusema ukweli, ingawa kwa uzoefu walionao wanabaini kwamba, mwanamke huyo ametoa mimba na kumletea madhara.

‘’Wanapokuja na wazazi wao wanasema mtoto wao ameharibu na sisi tunatekeleza jukumu letu la kumtibu, kwani hatuwezi kujua kama ni mwanandoa ama la,’’ anafahamisha.

Amina Hamad Ali mkaazi wa Pujini anasema, wanaotoa mimba huwa na sababu tofauti ingawa wasio na waume wamekuwa wakitoa mimba kiholela, jambo ambalo ni hatari.

‘’Mimba inapokuwa na matatizo unaambiwa hospitali na madaktari ndio wanayoitoa, lakini hawa wanaobeba mimba wasizozitarajia huwa hawajulikani, ndio maana wanatumia njia za kienyeji kutoa,’’ anaeleza.

Athari za utoaji mimba

Dk. Rehema anasema, mwanamke anaetoa mimba ana uwezo mkubwa wa kuchanika fuko lake la uzazi, kwani hutumia madawa ya kienyeji na vifaa visivyostaki.

Anasema, kutokana na ukali wa madawa hayo na yasiyo na kiwango, hulisababishia fuko la uzazi madhara ikiwemo kuchunika na hatimae kutoboka kabisa.

‘’Zana wanazotumia sio sahihi, hivyo fuko la uzazi linaweza kutoboka na kupata tatizo jengine ikiwemo kutolewa kwa kizazi na wakati mwengine kumsababishia kifo,’’ anafafanua.

Pia anaweza kupata saratani ya shingo ya kizazi na ikiwa haikutibiwa mapema inaenea kwenye fuko la uzazi na hatimae kutolewa kizazi na kumsababishia kifo pale saratani inapoenea mwilini.

Athari nyengine ni kuwa na safura, kupata matatizo kwenye via vya uzazi kutokana na viungo vya uzazi kutokuhimili pamoja na kutengwa na jamii.

Anasema, ingawa wanapofika hospitali hawasemi kwamba wametoa mimba, lakini wanabaini kutokana na kuona viashiria vya bakteria ambao ni tofauti na vya yule alieharibu.

Anasimulia kuwa, waliotoa mimba wanakuwa na dalili ya harufu mbaya, kutokwa na maji machafu, homa kali, nemonia, hivyo wanatibiwa kama wagonjwa walioharibu, ingawa wao wanakuwa katika hali ya hatari.

‘’Huko mitaani kuna madaktari ambao hawajasoma ndio wanaowatoa mimba wanawake na wengine wanatumia njia za asili kwa kushauriwa na watu tofauti, hii ni hatari kwao,’’ anaeleza.

‘’Kama hawa wasichana wanaoenda kukutana na wapenzi wao bila kutumia kinga yeyote watarajie nini? matokeo yake anatoa mimba kwa njia zisizo sahihi,’’ anafafanua.

Dk. Robert Shokolo akitoa mafunzo kwa waandishi wa habari jijini Dodoma anasema, utoaji wa mimba husababisha madhara mbali mbali kama vile, ugonjwa wa fistula, kumwagika damu, kutoboka kwa fuko la uzazi, kubakia tishu ambazo husababisha viungo kukatwa.

Lailat Mohamed Shaali mkaazi wa Michenzani wilaya ya Mkoani anasema, utoaji wa mimba unaweza kupoteza maisha ya wanawake wengi, hivyo elimu inahitajika zaidi.

‘’Kwenye hichi kijiji chetu kuna msichana alibeba ujauzito na kuutoa kwa kutumia dawa za miti shamba, alihatarisha maisha yake kwa sababu mimba ilikuwa na miezi mitano, hivyo alifikia kunuka na kila mtu alimjua,’’ anahadithia.

Maryam Said Hamad (sio jina lake halisi) mwenye miaka 46 mkaazi wa Fuoni Unguja anahadithia alivyohatarisha maisha yake baada ya kutumia njia za kienyeji kutoa mimba.

Dada huyo mwenye mume na watoto wanne anaelezea, alitoa ujauzito kwa sababu hakuwa tayari kuzaa kwa muda huo, hivyo akaamua kuwafuata watu wake wa karibu kumsaidia dawa.

‘’Kila mmoja alinishauri dawa yake, nilianza kutumia moja moja na ikiwa hainifai nabadilisha, hivyo nilijikuta nimetumia dawa nyingi kutoa mimba hiyo, lakini nilikuwa hali mbaya na karibu ya nipoteze maisha,’’ anasema.

Hakuamini kuwa, kuna siku angerudi katika hali yake ya kawaida, kwani kwa hatua aliyofikia kipindi hicho alijutia kwa nini aliamua kutoa mimba na kusema, ni kheri angebaki nayo kwa vile hakuwa na tatizo la kiafya.

Kutokana na funzo alilolipata, dada huyo anawanasihi wenzake wasitumie dawa za kienyeji na wala wasitumie njia ambazo sio sahihi, kwani watapoteza maisha yao.

Mmoja ambae hakutaka jina lake litajwe, alimshuhudia madhara yaliyomkuta jirani ambae alitoa mimba kwa sababu tu mtoto alienae hajafikia miaka miwili, alikuwa ni mwenye kutia huzuni.

‘’Alikonda sana, hawezi kula, muda wote anaumwa, kwa kweli ilimfanyia shida, hivyo tutambue kuwa hili jambo ni hatari tusilifanye na ikiwa mtu ana matatizo basi afike hospitali,’’ anaeleza.

Msaidizi Katibu Mufti Pemba Sheikh Said Ahmad anafafanua, asili ya utoaji wa mimba ni haramu hasa baada ya kufikia miezi minne kwani tayari mtoto huyo ameshapulizwa roho, hivyo inapotolewa maana yake umeua nafsi.

Na unapoua kiumbe (nafsi) ni dhambi kubwa kuliko fadhaa yeyote ambayo inaweza kuikumba dunia, hivyo kila mmoja anapaswa kujua uzito wa dhambi hiyo kabla hajaifanya.

Suratul-Maida aya ya 32 imeeleza kuwa… ‘Mtu ambae ataua nafsi kwa makusudi iliyokuwa haijaua, dhambi yake ni sawa na mtu alieua watu wote duniani’.

‘’Aya hiyo inaonesha wazi kwamba, kuuwa kiumbe kisicho na hatia ni dhambi kubwa, isipokuwa ikiwa kuna sababu ambazo zikimtokezea mwanamke zinaweza kuhatarisha usalama wake, tena athibitishe daktari kuwa ana tatizo,’’ anasema.

Padri wa Kanisa la Anglicana Wete Essau Mhecha anasema, bibilia inaeleza kwenye kitabu cha mwanzo 9.6 kuwa, ‘Atakae mwaga damu ya mwanadamu, damu yake huyo itamwagwa na mwanadamu, maana kwa mfano wake Mungu alimfanya mwanadamu’

Padri anafafanua, maandiko hayo yanajenga msingi kwamba uhai wa mwanadamu ni zawadi kutoka kwa Mungu, na wenye thamani, hivyo mtu anapotoa mimba kwa makusudi ni uuaji na ni dhambi.

Nini kifanyike

Dk. Rehema aliwataka wanawake wajipange wanapotaka kubeba mimba kwa kutumia njia za uzazi wa mpango na sio kuhatarisha maisha yao kwa kuzitoa.

‘’Kwa vile dini yetu inakataza kufanya mapenzi kabla ya ndoa, tujitahidi kufuata maelekezo hayo ili tusipate mimba ambazo mwisho wake ni kuzitoa,’’ anasema.

Lailat anashauri kuacha uzinifu au watakapopata mimba wasizitoe, kwani ni makosa na pia hawezi kujua kiumbe alichonacho kitakuwa na faida gani katika maisha ya Duniani na Akhera.

Sheikh Said Ahmad anawataka wazazi kujikita katika malezi ya kiislamu ambayo yatamsaidia mtoto kukua katika hali ya kujitambua na kujizuia kujiingiza katika dhambi.

‘’Kuna wanaofanya tendo la ndoa nje ya sheria ambao huficha aibu na wingine wana upungufu wa imani tu, kwa sababu ameshatenda dhambi ya kwanza na baadae anajiingiza kwenye dhambi mbaya zaidi ya kuuwa nafsi,’’ anafahamisha.

Mkufunzi wa kitaifa wa Afya ya Uzazi Mgeni Kisesa wakati akizungunza kwenye mafunzo na waandishi wa habari jijini Dodoma mwaka jana anaeleza, kila mwaka wanawake wa kitanzania milioni 1 hupata mimba zisizotarajiwa, ambapo asilimia 39 huishia kwenye utoaji, huku mimba zinazotolewa kwa njia isiyo salama zikiwa ni 405,000.

Kwa mujibu wa gazeti la habari leo la online la Julai 13, 2023 lilieleza, kila baada ya dakika 8 mwanamke mmoja hufariki kwa kutoa mimba, ambapo wanawake wa bara la Afrika ndio wanaoongoza.

Mtandao huo unaeleza, kila dakika moja kuna wanawake wanne ambao wanatoa mimba kwa njia isiyo salama, ambapo wanawake milioni 56 hutoa mimba, huku watatu kati ya wanne wapo bara la Afrika.

Katika juhudi za kutoa elimu, Afisa Programu kutoka Chama Cha Waandishi wa Habari Tanzania Zanzibar (TAMWA) Zaina Abdalla Mzee anafahamisha, walifanya utafiti na kuona kuna haja ya kutoa elimu kwa wanajamii, pamoja na waandishi wa habari.

 ‘’Tuligundua elimu hii bado haijawafikia vizuri wanawake, na ndio maana tukawataka wanahabari watoe elimu ya satratani ya mlango wa kizazi, uzazi wa mpango, mabadiliko ya tabia kwa vijana, ushiriki wa wanaume kwenda kliniki na wake zao,’’ anafafanua.

Inashauriwa kwamba linapomfika mwanamke tatizo kwennye ujauzito, afike hospitali ilia pate ushauri nasaha.

                                         MWISHO.

Comments

BLOG'S VISITORS

DAKTARI MWENGINE CHAKE CHAKE KULA SIKUKUU POLISI, NI KWA TUHUMA ZA KUMBAKA MGONJWA WAKE

NA WAANDISHI WETU, PEMBA::: DAKTARI anaetoa huduma kwa wagonjwa kituo cha afya cha serikali cha  Gombani wilaya ya Chake Chake Pemba, Is-haka Rashid Hadid, anaendelea kushikiliwa na Jeshi la Polisi Mkoa wa kaskazini Pemba, akituhumiwa kumtorosha na kisha kumbaka mtoto wa mwenye umri wa miaka 16, mkaazi wa Gombani. Daktari huyo miaka 35 ni mkaazi wa Kangagani Wilaya ya Wete mkoani humo, ambapo anadaiwa alimchukua mtoto huyo kutoka kwa rafiki yake, na kumpeleka kwenye nyumba anayoishi eneo la Kangagani. Mtoto aliefanyiwa kitendo hicho alisema kuwa, April 21 mwaka huu alikwenda kituo cha afya Gombani, kwa ajili ya matibabu na baada ya kupatiwa huduma na daktari huyo, alimuomba nambari yake ya simu. Alisema ilipofika usiku, walikuwa wanawasiliana kupitia ujumbe mfupi (sms) kwa lengo la kwenda kuchukua dawa nyingine ambazo kwa mchana huo alizikosa hospitalini hapo. "Nilikwenda hospitali kutibiwa, baada ya kufanya mapele katika sehemu zangu za siri, lakini akaniambia mpaka aje da...

HII KALI MBUNGE ASIYA AMKOGESHA MWANANCHI HADHARANI KISA HICHI HAPA......

  NA HAJI NASSOR, PEMBA MBUNGE wa viti maalum nafasi za wanawake mkoa wa kaskazini Pemba Asiya Sharif Omar, amewataka wananchi wa kijiji cha taifu, shehia ya Kinyasini jimbo la Gando wilaya ya Wete Pemba, kuyalinda miundombinu ya maji safi na salama, ili yawe endelevu kwao. Kauli hiyo ameitoa wakati alipokuwa akizungumza na mwandishi wa habari hizi, mara baada ya kuwasili kijijini humo, na kumkogesha mwananchi mmoja kama ishara ya uzinduzi wa mradi wa maji safi na salama, ulioasisiwa na mbunge wa Jimbo la Gando. Alisema, hawana mbadala kwa sasa bali ni kuilinda miundombinu ya huduma hiyo, hasa baada ya mbunge wa wao Salim Mussa Omar, kuwarejeshea huduma hiyo. Alieleza kuwa, inafahamika kuwa kwa miaka 14 waliikosa huduma hiyo hasa kwa vile viongozi waliokuwepo hawakujali kuwatatulia tatizo hilo, hadi juzi ilipofanywa na mbunge wao. “Baada ya huduma hii sasa kurejeshwa na mbunge wa jimbo la Gando, kazi iliyobakia kwenu wananchi ni kila mmoja kuwa mlinzi wa miundombinu hii,’...

'MKAPA' NA WENZAKE PEMBA WALAZWA RUMANDE

  NA HAJI NASSOR, PEMBA@@@@ MAHKAMA kuu Zanzibar kisiwani Pemba, chini ya Jaji Ibrahim Mzee Ibrahim, imewapeleka rumande watumuhimwa wanne wanaokabiliwa na tuhuma za kuua kwa makusudi, akiwemo Ali Mussa Omar ‘ Mkapa’ mkaazi wa Wawi wilaya ya Chake chake Pemba. Watuhumiwa wengine walioanza maisha mapya ya rumande ni mtuhumiwa Yassir Mohamed Juma miaka 23, Anuwari Mussa Omar miaka 30 pamoja na mtuhumiwa Yassir Mussa Omar ‘ Makababu ’ miaka 29, wote wakaazi wa shehia ya Wawi, wilaya ya Chake chake Pemba. Awali watuhumiwa hao waliwasili mahakamani hapo, kwa mara ya kwanza, kwa ajili ya kusomewa tuhma zinazowakabili za kumuua kwa maksudi Said Seif Kombo. Ilidaiwa mahakamani hapo na Mwendesha Mashtaka kutoka Ofisi ya Mkurugenzi wa Mashataka Seif Mohamed Khamis akiambatana na mwenzake Mussa Khamis Ali kuwa, watuhumiwa hao kwa pamoja wanadaia kufanya mauwaji hayo kwa maksudi. Ilidai kuwa, watuhumiwa wote kwa pamoja, walitenda kosa hilo Oktoba 16, mwaka huu, baina ya saa 7:00 m...

TUHMA ZA DAKTARI PEMBA KUCHIWA HURU: POLISI KASKAZINI KUTOA TAARIFA RASMI LEO

  NA HAJI NASSOR, PEMBA KAMANDA wa Polisi mkoa wa kaskazini Pemba, Juma Saad Khamis, amesema leo Mei 9, mwaka huu atatoa taarifa rasmi, juu ya kuendelea kumshikilia au kumpa dhamana ya Polisi, daktari wa Kituo cha Afya Gombani Is-haka Rashid Hadid, anayetuhumiwa kwa ubakaji. Alisema, kwa vile alikuwa katika mapumziko mafupi, haelewi jambo lolote linaloendelea kwa mtuhumiwa huyo, juu ya kuendelea kushikiliwa kwake kituoni hapo. Alieleza kuwa, leo Mei 6 (jana), hajapata taarifa za ndani za mtuhumiwa, huyo na kuwataka wananchi na wanaharakati, wasubirie hadi Jumatatu ijayo. Akizungumza na waandishi wa habari kwa nyakati tofauti Kamanda huyo, alisema hana taarifa zozote za kupewa dhamana mtuhumiwa ndani ya kituo chake cha Polisi au kuendelea kuwepo. ‘’Ilikuwa mimi sipo kazini kwa muda, kuanzia anakamatwa hadi anafikishwa Polisi, kwa sasa siwezi kueleza jambo lolote kwa mtuhumiwa huyo, hadi Jumatatu,’’alieleza. Aidha Kamanda huyo alieleza kuwa, kwa sasa hawezi kutoa uf...

MADAKTARI KUTOKA CHINA WAOKOA MAISHA YA MTOTO PEMBA

  HABIBA ZARALI, PEMBA TIMU ya 32 ya madaktari wa kichina katika hospitali ya Abdalla Mzee Mkoani wamefanikiwa kufanya upasuaji mkubwa wa mtoto mwenye umri wa miaka 15 mkaazi wa Chole Kengeja, baada ya kuchomwa na jiti sehemu ya njia zake za mfumo wa uzazi. Mtoto huyo ambae alianguka hivi karibuni katika mti na baadae kuchomwa na jiti hilo na kumsababishia kutokwa na damu nyingi katika sehemu ya nyonga, alifanyiwa upasuaji uliodumu kwa muda wa saa tatu na   kuokolewa maisha yake. Akizungumza mara baada ya operesheni huo kiongozi wa timu hiyo Dr Jiang Jinhua, alisema mara baada ya mtoto huyo kufikishwa hospitalini hapo na kufanyiwa vipimo na kuonekana   ilibidi apatiwe rufaa ya kwenda katika hospitali nzuri yenye kutibu tatizo lake huko nchini Kuwado ambapo haikuwezekana kutokana na hali ya umaskini wa f amilia ya mtoto huyo . Alisema timu ya madaktari hao itaendelea kutowa huduma za matibabu   kwa wananchi kisiwani humo,   ili kuwaondolea gharama ya kuta...