Skip to main content

WAALIMU, WANAFUNZI WESHA WATAKIWA KUONGEZA JUHUDI MAPAMBANO DHIDI YA UDHALILISHAJI

 



NA ASHA ABDALLA, PEMBA@@@@

WAALIMU na wanafunzi wa skuli ya msingi ya Wesha wilaya ya Chake chake Pemba, wamesahauriwa kuongeza juhudi za kupambana na vitendo vya udhalilishaji, ili wanawake na watoto wabaki salama kwa vitendo hivyo.

 

Hayo yameelezwa na Mshauri nasaha kutoka kitengo cha mkono kwa mkono cha hospitali ya Chake chake Asha Massoud, wakati akitoa mafunzo kwa wanafunzi hao, juu ya dhana ya kupambana na udhalilishaji, mafunzo yaliyofanyika skulini hapo.

 

Alisema kuwa, kupitia mafunzo anaamini wanafunzi na waalimu hao, wameshapata njia sahihi ya kuongeza juhudi za mapambano dhidi ya udhalilishaji.

 

Alieleza kuwa, kila mmoja na kwa nafasi yake, anatakiwa kukemea na kutoa elimu ya kujikinga na masuala la udhalilishaji, ili jamii na hasa kundi la wanawake na Watoto libaki salama.

 


‘’Kwanza niwatake waalimu na wanafunzi wa skuli hii ya Msingi Wesha, kuhakikisha wanaongeza makali ya kukemea na kutoa taarifa wanapoona viashiria vya udhalilishaji kwa mmoja wao,’’alifafanua.

 

Akizungumzia mbinu zinazotumiwa na wadhalilishaji na hasa kwa waatoto Mshauri nasaha huyo, alisema moja wapo ni kupewa zawadi mfano wa pesa au pipi.

 

Alifahamisha kuwa,  mwanafunzi yoyote asikubali kuitwa na mtu amsiyemjua na kukubali kupokea pesa au kitu chochote, kwani kufanya hivyo ni kuwakaribisha wahalifu hao.

 

 "Kitendo cha udhalilishaji, kwa miaka hii hakifanywi na mtu wa mbali, bali ni wale wazazi na walezi au wakati mwengine hata majirani, lakini wote hawa wakianza ishara ni vyema mkatoa taarifa,"alisema.

 



Wakati huo huo, Mshauri huyo nasaha kutok kitengo cha Mkono kwa mkono cha Hospitali ya Chake chake Asha Massoud, amewasisitiza wanafunzi hao, kuacha kuitana majina mabaya au kupigana, kwani vitendo hivyo ni sehemu ya udhalilishaji.

 

Nae Afisa Mshauri kutoka kitengo cha mkono kwa mkono cha hospitali ya Chake chake,Tatu Abass, alisema moja ya madhara makubwa kwa mtoto aliyefanyiwa vitendo vya udhalilishaji ni kukosa elimu, kupoteza afya yake na kukosa hamu ya kujiendeleza.

 



Hata hivyo, amewakumbusha Watoto wa kike, kujilinda na athari za mimba za umri mdogo, kwani athari yake moja kubwa ni kupoteza uhai, kutoakana na viungo vyake vya uzazi kutokuwa tayari kuhimili vishindo vya mimba.

 

"Mtu yeyote aliyefanyiwa udhalilishaji, anaweza kupata maradhi mbali mbali, mfano ukimwi, kwani anayemfanyia huwa hujui afya yake,’’alifafanua.

 

 Kwa upande Mshauri nasaha kutoka kitendo hichi hicho, Kurthumu Khamiss Msabaha, alisema kua kuna njia mbali mbali za kujikinga na udhalilishaji, ikiwemo kutokutumia simu ukiwa bado ni mwanafunzi na kuzurura ovyo ovyo katika maeneo mbali mbali.

 

Nae Polisi kutoka dawati la jinsia la wanawake na watoto katika kituo cha Polisi Chake chake Salama Omar, aliwataka wanafunzi, kuendelea kutoa taarifa wanapoona wanataka kufanyiwa vitendo vya udhalilishaji.

 

"Musimuamini mtu yoyote ambae humjui undani wake, kwani itapelekea kuja kukufanyiwa kitendo kibaya, ambacho hujakitarajia katika Maisha yako, nakukuvunjia malengo yako," alieleza.

 

Kwa upande wake Mwalimu mkuu wa skuli hiyo Mafunda Sudi Sabur, alikishukuru kitengo hicho kwakuwapa mafunzo hayo na kuahidi kuyafanyiakazi kwa wengine, ili elimu hiyo isambae.

 

Hata hivyo aliwawambia wanafunzi wake, wawe mabalozi kwa wenzao, ambao hawapo katika mafunzo hayo, ili kuona kila mmoja amepata uwelewa.

 

                            Mwisho

 

Comments