Skip to main content

KIDUTANI WAPITISHA KANUNI KUSIMAMIA MALEZI YA VIJANA WAO

 


 NA MOZA SHAABAN, PEMBA @@@@

KAMATI ya maadili na taaluma ya kijiji cha Kidutani shehia ya Chumbageni Wilaya ya Mkoani Pemba, imepitisha kanuni 19 zitakazowaongoza katika kusimamia malezi ya watoto na vijana.

Akizungumza kijijini hapo  katika kikao cha kupitisha kanuni hizo kilichoandaliwa na  kamati hiyo Mwakilishi wa sheha ambae pia ni Mratibu wa kamati ya maadili ya shehia hiyo Abrahman Mohamed Khamis alisema, Ofisi ya sheha ipo tayari kushirikiana na wanakijiji  katika kusimamia kanuni hizo.

Alisema ni vyema wananchi kutoa ushirikiano wa kutosha kwa kamati hiyo, ili lengo liweze kufanikiwa, huku akiwataka wanakamati hao iwapo patakua na kikwazo chochote katika utekelezaji majukumu yao, kupeleka changamoto zao kwa sheha.

"Ofisi ya sheha ipo tayari kushirikiana na nyinyi katika hili, naomba na wananchi mutoe ushirikiano wa kutosha ili kufanikisha jambo hili, na iwapo patatokezea kikwazo  katika utendaji kazi wenu musisite kuripoti kwa sheha", alieleza.

Nae Mjumbe wa Sheha wa Shehia ya Chumbageni Juma Shaaban Jabir alisema, hatua iliyochukuliwa na wanakikijiji hao, ni nzuri kwani itasaidia kutatua changamoto za kimaadili katika shehia yao, huku akisisitiza kamati hiyo kua endelevu.

Aliongeza kua huenda kijiji hicho kikawa mfano nzuri na wakuigwa ndani ya shehia hiyo na hata shehia nyingine, huku akitoa wito kwa kamati hiyo kuweka pembeni itikadi zao za kisiasa na badala yake wafanye kazi kwa maslahi ya kijiji hicho.

Akizungumza katika kikao hicho  Mkaguzi Msaidizi wa Jeshi la polisi  Abdallah Mohamed Abdallah alisema, iwapo mtu yeyote atapingana na kanuni hizo kwa makusudi, ni vyema kamati kumripoti kwa kwao, kwa lengo la kuchukuliwa hatua zaidi, huku akiitaka jamii kutoa mashirikiano ya kutosha kwa jeshi hilo.


Nae Mwenyekiti wa kamati hiyo Machano Ali Makame, alipongeza ushirikiano wanaoupata kutoka kwa jamii na uongozi wa shehia, ambapo alifafanua kua tokea kuanza kamati hiyo wanafunzi 25 wameanza kusoma, baada ya kupewa vitabu vya aina tofauti vikiwemo vya kumjua Muumba wao kutoka katika kamati hiyo.

Akisoma kanuni 19 zilizopitishwa katika kikao hicho Mshauri Eelekezi wa kamati hiyo Haji Nassor Mohamed alisema, kanuni hizo ni pamoja na marufuku ya kutembea usiku zaidi ya saa nne kwa asiekua na dharura, marufuku ya ukataji nywele usio zingatia maadili pamoja na uvaaji nguo za mbano.





Huku kanuni nyengine zikiwa ni marufuku ya uvutaji sigara, unywaji  pombe na madawa ya kulevya, upigaji ngoma ovyo pamoja na kanuni inayotaka futarisho kwa wanakijiji kila mwaka mara moja kwa lengo la kuwaunganisha.

Kamati ya maadili na taatuma ya kijiji cha Kidutani shehia ya Chumbageni,  ilioanzishwa mienzi minne iliopita, ikiwa na wajumbe 12 wakiwemo wanaume na wanawake, na imepitisha kanuni 19 itakazozisimamia katika utendaji kazi wake, ambazo zitasainiwa na sheha wa shehia hiyo, Kamanda wa polisi wa Wilaya ya Mkoani pamoja na Mkuu wa wilaya hiyo.

                                                                MWISHO

 

 

 

Comments