Skip to main content

DISEMBA 3 YA MWAKA HUU, ITUKUMBUSHE UJUMUISHI KWA KILA JAMBO

 


 NA MOZA SHAABAN, PEMBA@@@@

DISEMBA 3 ya  kila mwaka dunia huadhimisha siku ya kimataifa ya watu wenye ulemavu.

Siku hii ilianza kuadhimishwa mwaka 1992 na umoja wa mataifa, lengo likiwa ni kuongeza uwelewa juu ya mambo yanayo husu watu wenye ulemavu.

Pia  inalenga kutoa elimu kwao na kwa jamii  juu ya haki zao na kuongeza ufahamu juu ya uungwaji mkono kwa ajili ya utu, heshima na ustawi wao.

Historia inaonyesha watu wenye ulemavu walikua na wakati mgumu zaidi kwa miaka iliopita.

Kwakile kinachooeleza kua walikabiliwa na changamoto kadhaa ikiwa ni pamoja na kutelekezwa na  kunyimwa haki zao za msingi ikiwemo ya kuishi.

Hivyo uwepo wa siku hii ni kuthamini na kuenzi utu na heshima ya watu wenye ulemavu ambavyo vilitiwa kapuni kwa miaka mengi.

Hivyo Disemba 3 ni wito wa kukumbatia utofauti wa kimaumbile tulio nao, kuvunja vizuizi na kuhakikisha mustakbali uliojumuishi zaidi kwa watu wote.

Ikizingatiwa kwamba takribani watu bilioni 1.3 duniani kote wana ulemavu mkubwa, sawa na asilimia 16 ya watu  duniani.

Wakati dunia ikiwa na takwimu hizo, Tanzania katika sensa yake ya  watu na makazi ya mwaka 2022,  inafafanua asilimia 11.4 ya watu wote Zanzibar  wana ulemavu.

 Huku ikieleza idadi hiyo imeongezeka kutoka asilimia 5.4 ilivyokuwa katika sensa ya mwaka 2012.

Takwimu hii na ile ya dunia zinasisitiza umuhimu wa kushughulikia changamoto zinazowakabili watu wenye ulemavu na kuhakikisha ulemavu wao hauwi sababu ya kuvunjwa utu na heshima zao.

Izingatiwe kwamba watu wenye ulemavu wana haki sawa na watu wengine, kama zilivyo kaziwa na  sera kanuni na sheria za watu wenye ulemavu.

Hivyo siku ya watu wenye ulemavu ulimwenguni kipekee zaidi imekuja kuwapa fursa ya kupaza sauti pale wanapoona kutokuwepo kwa usawa katika jamii au uvunjwaji wa sheria zinazo wasimamia katika upiganiaji  haki zao.

Kauli mbiu ya mwaka huu inasema “Kua na jamii jumuishi inayo wathamini na kuwapa fursa sawa watu wenye ulemavu katika nyanja zote za maendeleo’.

Yenye maana kuwa kila kitu katika jamii kiwazingatie  watu wenye ulemavu, ili kuwapa thamani na fursa kushiriki  katika nyanja za kimaendeleo, ikiwa ni pamoja  na elimu, afya, siasa na mengineyo.

Kaulimbiu hii inaungana na Sera, Sheria na kanuni mbali mbali zinazo simamia haki za watu wenye ulemavu, ikiwemo ya ujumuishi wao katika nyanja za kimaendeleo.

Mfano  mkataba wa umoja wa kimataifa wa haki za watu wenye ulemavu (2006) ibara ya 19 (b) na (c)  inaeleza kuhusu ushirikishwaji wa watu wenye ulemavu.

Ibara hiyo inataka  watu wenye ulemavu wawe wanapata huduma za aina mbalimbali nyumbani na katika jamii na  misaada binafsi ambayo ni ya lazima katika kuwawezesha kujumuika kwenye jamii.

“Huduma za kijamii na miundombinu kwa ajili ya umma, inapatikane kwa watu wenye ulemavu kwa misingi ya usawa na inayoendana na mahitaji yao”, pia imeeleza sehemu ya mkataba huo.

 

 

Aidha sheria ya watu wenye ulemavu ya Zanzibar ya mwaka 2022 katika kifungu chake cha 32 (d) kinaeleza taratibu za utoaji na uaptikanaji huduma ziwe  zinazingatia mahitaji maalumu ya watu wenye ulemavu.

Hii yote ni kuhakikisha jamii jumuishi, jamoja na kuwathamini watu wenye ulemavu kwa kuwapa fursa sawa katika nyanja zote za maendeleo.

WATU WENYE ULEMAVU

Rehema Juma Makame wa Kukuu Pemba ni mwenye ulemavu wa uoni anasema, jamii jumuishi ni daraja la kupita katika  kuhakikisha  upatikanaji fursa sawa kwa kila mmoja.

Anasema kama kaulimbiu inavyooeleza, kua na jamii jumuishi inayowathamini watu wenye ulemavu, utekelezaji wake utarahisisha usawa na upatikanaji haki zao za msingi ambayo ndio kiu yao kubwa.

Hidaya Mjaka Ali ni mwenye ulemavu wa viungo anasema,  kaulimbiu hii itasaidia kujenga uwelewa kwa jamii na nchi kwa ujumla kwamba, watu wenye ulemavu wanapaswa kujumuishwa katika safari zote za maendeleo.

Anaeleza jamii jumuishi itatoa fursa na haki sawa kwa watu wenye ulemavu, ambayo ni hatua muhimu katika kufikia maendeleo.

“Jamii jumuishi ni fursa ya upatikanaji wa haki sawa na ni hatua muhimu ya kufikia maendeleo, kwani bila kuwepo kwa ujumuishi ni ngumu kulifikia fursa zilizopo”, alieleza.

Anasema jamii jumuishi inamaanisha kuwa watu wenye ulemavu wana fursa sawa za kupata elimu, ajira, huduma za afya na mengineyo.

Amina Khamis Khalfan wa Mtambile Pemba ni mwenye ulemavu wa ualbino anasema, kuwa na jamii jumuishi ni fursa kwao kujiimarisha kiuchumi, kwani kutawawezesha kufanya shughuli zao za kiuchumi bila vizuizi.

Anasema ikiwa miundombinu ya masoko, usafiri, elimu afya na mengineyo yatakua jumuishi kwa watu wote, kutawapa fursa ya kuendesha shughuli zao za kimaendeleo bila vizuizi na maendeleo yatapatikana.

JAMII

Adam Mbarouk Juma wa Mbuguani Mkoani Pemba anasema, kunaumuhimu wa kua na jamii jumuishi na inayowathamini watu wenye ulemavu, kwani itawapa fursa ya kushiriki kikamilifu katika masuala mbali mbali ya kimaendeleo.

Sada Mohamed Amour wa Mjimbini Pemba anasema, jamii inapaswa kuondoa vikwazo kwa watu wenye ulemavu  vya kuzifikia fursa mbali mbali kama wanavyo zifikia wengine.

“Watu nwenye ulemavu huchangia pakubwa katika kila nyanja ya maisha iwe ni sanaa, sayansi, michezo au teknolojia, ni vizuri waondolewe vikwazo na wathaminiwe ili washiriki kwa uhuru”, alieleza Sada.

JUMUIYA ZA WATU WENYE ULAVU

Maryam Mohamed Salum Afisa watu wenye ulemavu Pemba kutoka “UWZ” anasema, kila kitu kinachohusu jamii lazima kihusishe ujumuishi wa watu wenye ulemavu hapo ndipo jamii jumuishi ipatikane.

Anasema hii ni kuhakikisha elimu, Afya, miundombinu, kazi na  kila sehemu inayohusu haki ya msingi ya binaadamu  inakidhi mahitaji ya kila mtu, hapo ndipo fursa sawa katika maendeleo itapatikana.

Mashavu Juma Mabrouk Mratibu baraza la watu wenye ulemavu Pemba anasema, siku ya watu wenye ulemavu ulimwenguni ni fursa ya kuitambulisha jamii  haki za  watu wenye ulemavu, ambazo ndio msingi imara wa kupatikana jamii jumuishi.

Anasema kila mmoja katika jamii kuanzia familia hadi serikali kuu, inajukumu la kuhakikisha tunakua na jamii jumuishi, ili kujenga thamani na kutoa fursa sawa kwa watu wenye ulemavu katika maendeleo.

HITIMISHO

Siku ya watu wenye ulemavu duniani 2025 ni ukumbusho kwamba ujumuishaji sio tu tukio la siku moja lakini ni ahadi  ya maisha  ya kila siku.

Hivyo ni vyema kwa watu binafsi, mashirika, na serikali kuvunja vizuizi na kujenga jamii ambapo kila mtu bila kujali uwezo wa maisha anaweza kustawi.

Katika kufikia hilo ni vizuri kuboresha ufikiaji katika maeneo ya umma, kuajiri watu wenye ulemavu katika majukumu ya maana, na kuelimisha jamii kuhusu thamani ya ushirikishwaji wa watu hao katika maendeleo.

Kwa vile siku ya Kimataifa ya Watu Wenye Ulemavu huangazia changamoto na fursa katika kuunda ulimwengu unaojumuisha zaidi, ni vizuri kuzifanyia kazi changamoto hizo ili kuhakikisha usawa katika jamii.

MWISHO

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

Comments