Skip to main content

WAGOMBEA WANAWAKE WATAJA ATHARI ZINAZOWEZA KUWAKUMBA IWAPO WATADHALILISHWA




NA ZUHURA JUMA, PEMBA@@@@

KILA kukicha Seirikali, taasisi binafsi na jamii zinapaza sauti zao ili kuhakikisha wanaondoa vitendo vya udhalilishaji ambavyo kwa asilimia kubwa hufanyiwa wanawake na watoto.

Suala la kukemea vitendo vya udhalilishaji sasa limejaa kwenye mioyo ya watu kwa sababu halipewi nafasi katika jamii zetu, licha ya wachache wanaolifanya na kutia aibu Taifa letu.

Tayari wanajamii waliowengi wameshapatiwa elimu na wanajua athari zinazojitokeza iwapo mwananchi atafanyiwa vitendo vya udhalilishaji na ndio maana wapo tayari kuyazungumzia na kuyakemea kwa nguvu zote.

Wanawake wanaogombea ni miongoni mwa wanakumbwa na changamoto za udhalilishaji ambazo hupelekea kuwaathiri kisaikolojia, kimwili, kijamii, kisiasa na kiuchumi.

Mwandishi wa makala haya alitaka kujua ni athari gani zinazowakumba wanawake wanaogombea nafasi za uongozi iwapo watadhalilishwa.

Ibrahim Mustafa Mussa ambae ni Mjumbe wa Kamati ya Siasa wilaya ya Wete kupitia chama cha Mapinduzi CCM anasema, udhalilishaji kwenye vyama unakwaza ushiriki wa wanawake katika siasa kwa sababu wanaweza kuhofia kudhalilishwa na hivyo kupunguza uwakilishi wao katika vyombo vya maamuzi.

Anasema, udhalilishaji kwa wanawake wanaogombea husababisha kuathirika kisaikolojia kwani wanaweza kupata msongo wa mawazo, hofu na kupoteza hali ya kujiamini, jambo ambalo linawaathiri wao na hata familia zao.

‘’Athari nyengine ni kudorora kwa haki za binadamu kwa sababu unapomnyanyasa mtu, unakiuka haki zake za kibinadamu, kwa hiyo hili linaweza kuonyesha kuwa jamii bado haijatoa nafasi sawa kwa jinsia zote kushiriki katika uongozi,’’ anaeleza.

Wanawake huleta mtazamo mpya katika utawala na maendeleo ya kijamii, hivyo ikiwa hawatoshiriki kwa kuhofia kudhalilishwa, basi jamii inakosa mawazo mbadala ambayo yanaweza kusaidia katika maendeleo ya nchi.

Mwananchi Safia Suleiman Iddi mkaazi wa shehia ya Msuka anasema, athari yake ni kuhamasisha matendo ya ukatili wa kijinsia, kwa sababu yanapotokea wanawake huonekana hadharani, hivyo yanaweza kusababisha watu wengine kuona kama ni ya kawaida.

‘’Udhalilishaji huu unaathiri nakudhoofisha demokrasia, wakati mwanamke anapotishwia au kuzuiwa kushiriki siasa kwa hofu ya kudhalilishwa, basi demokrasia inapoteza usawa na uwakilishi mpana wa wanawake,’’ anaeleza.  

Saada Saleh Ali ambae ni Mwenyekiti wa Vijana Wilaya ya Wete kupitia chama cha Mapinduzi CCM anaeleza, udhalilishaji huo unawaathiri sana kwenda hatua nyengine mbele kwa sababu yule wanaemkusudia atawasaidia wakati mwengine ndie unawaendea kwa lengo jengine.

‘’Unajikuta anakuja mtu anakwambia yule anaekusaidia ana lengo fulani na ni baya, hivyo ile hamasa inapungua kwa sababu vile vishawishi ambavyo atakuonesha utaona bora ukae upande kulinda utu wako na heshima yako,’’ anaelezea.

‘’Wakati mwengine yule yule ambae ana viashiria vibaya lakini wewe hujamjua lengo lake, basi watu wataanza kukushutumu, kukusema na kukupakazia kuwa unafanya nae ngono, kwa kweli inauma sana,’’ anahadithia.

Saada anajua, hayo ni miongoni mwa changamoto na hapaswi kukata tamaa, kwani baadhi ya watu wanaamini hawawezi kufanikiwa ikiwa hawajadhalilishwa, jambo ambalo sio kweli.

Anasema, mara nyingi wanaume wanapokuhujumu na kukufikiria vibaya wanashirikiana na wanawake, hali inayosikitisha sana kwani wao walipaswa wawaunge mkono.

Moza Massoud Ali ambae ni Mwenyekiti Vijana Mkoa wa Kaskazini Pemba kupitia chama cha ACT Wazalendo anasema, udhalilishaji unawaathiri sana na kurudisha nyuma harakati zao za kugombea kwa sababu ikiwa mwanamme atakukatalia kitu ambacho wewe mwenyewe umejiamulia, anakuwa na nguvu kubwa ya kukuharibia.

‘’Anakupa vitisho na maneno yenye kukukatisha tamaa, hivyo inapelekea kukosa kujiamini kwa sababu unahisi hutofanikiwa,’’ anaeleza.

Zainab Mussa Bakar ambae ni Mwenyekiti wa Wanawake Mkoa wa Kusini Pemba upitia chama cha Demokrasia na Mendeleo CHADEMA anasema, udhalilishaji unawaathiri kisaikolojia kwani wao wamejipanga kufikia sehemu fulani, lakini watu wanawakwamisha hatua tano nyuma kutokana na maneno.

‘’Maneno hayo yanawavunja moyo wanawake, kwa sababu wanaume walikuwa wawaunge mkono kwa nia njema, lakini kwa vile hawako tayari kupitwa na mwanamke, ndio maana wanatukwaza kila sehemu,’’ anafahamisha.

Mratibu wa chama cha Democratic Party (DP) Pemba, Abas Mohamed Khatib anasema, athari yake ni kuwavunja moyo wanawake ambao wa nia ya kugombea, hivyo anakuwa anasitasita kuingia katika harakati za kugombea.

 

‘’Hali hiyo husababisha kila siku kuwa na viongozi hao hao kwenye chama kwani hawabadiliki, jambo ambalo halileti taaswira nzuri kwenye jamii,’’ anaeleza.

 


Nini kifanyike

Maryam Saleh Juma mgombea ubunge kupitia chama cha Ukombozi wa Umma mkaazi wa Vitongoji anasema, anashauri wapatiwe elimu zaidi ya uraia, ya haki, ingawa kwa sasa udhalilishaji umepungua kasi kutokana na elimu hiyo, ukitofautisha na zamani.

‘’Tuwe na sheria ambayo ukimdhalilisha mwanamke anachukuliwa hatua za kisheria papo hapo,’’ anashauri.

Mwananchi Subira Makame Iddi mkaazi wa Kiwani anasema, kunahitajika elimu kwa viongozi na wanachama wa vyama vyote vya siasa, kwa sababu wengine hawajui kwamba mwanamke ukimfanyia jambo fulani anapata athari.

‘’Udhalilishaji upo wa aina nyingi kwa hivyo utakapomfanyia aina yeyote ile ya kumdhalilisha basi unamrudisha mwanamke nyuma katika harakati za kugombea kwani wengine ni woga,’’ anafafanua.

Mohamed Haji Kombo Katibu wa Wilaya Chake Chake chama cha wananchi CUF anasema, wanawapa elimu wanachama wao na kujenga ukaribu, jambo ambalo linasaidia sana katika kujenga uthubutu, kuhoji na kupata fursa ya kusema kinachomkwaza.  

Ili kuona kuwa wanaondosha athari hizo wamekuwa wakitoa fursa sawa za kudhibiti mianya ya udhalilishaji kwa kutoa fomu bure kwa baadhi ya nafasi wanazogombea kwenye chama.

‘’Kwa vile wengine hawana uwezo kifedha, tumeona kuwa wanaweza kujidhalilisha ili tu wapate fomu, hivyo baaadhi ya nafasi tunaondoa malipo mapema bila kujali mapato ambayo tutayakosa,’’ anaeleza.

Mratibu wa chama cha Democratic Party (DP) Pemba, Abas Mohamed Khatib anasema, anaiomba Serikali kuwa karibu na vyama vya siasa, ili vyama visimilikiwe na mtu binafsi, bali wasimamie katiba zinavyowaongoza, hiyo itasaidia kuondoa udhalilishaji.

Mjumbe wa Kamati ya Siasa wilaya ya Wete kupitia chama cha Mapinduzi CCM Ibrahim Mustafa Mussa anasema, ipo haja kwa wananchi kuhamasishwa kuhusu haki zao za kupiga kura na umuhimu wa kushiriki uchaguzi bila vitisho au unyayasaji.

Anasema, pia sheria zinazopinga vitendo vya udhalilishaji ikiwemo unyanyasaji wa kijinsia na lugha za matusi ziimarishe na kutekelezwa kwa haki.

‘’Vyama vya siasa viwajibike kwa matendo ya wanachama wao na kuhakikisha wanazingatia maadili ya uchaguzi, hiyo itasaidia uwajibikaji bora kwa wagombea na vyama vya siasa,’’ anafafanua.

Katibu wa Jumuiya ya Utetezi wa Kijinsia na Mazingira Pemba (PEGAO) Dina Juma Makota anaeleza, viongozi wa dini na jamii washirikishwe katika kuhamasisha maadili mema wakati wa kampeni na uchaguzi.

‘’Pia waandishi wa habari watumie kalamu zao vizuri kuelimisha jamii na wanawake juu ya kuthamini na kuwa na heshima ya hali ya juu, ili kuondosha dhana potofu ya kuwa wanawake wanaogombea wanafanya uhuni,’’ anaeleza Katibu huyo.

Afisa Mkuu wa Mahusiano kutoka chama cha Waandishi wa habari Wanawake Tanzania Zanzibar (TAMWA) Sofia Ngalapi anasema, wamekuwa wakitoa elimu mara kwa mara ili wanawake wajiamini na kujiepusha na matendo ambayo yatamfanya aonekane amekosa heshima.

 

‘’Tunajitahidi sana kuwaelimisha kuhusu mchakato mzima wa kugombea na uchaguzi, hivyo tunaamini kwamba mafunzo tunayowapa yatawasaidia kupambana na changamoto mbali mbali zinazowakumba,’’ anasema.

 

Katiba ya Zanzibar ya mwaka 1984 kwenye kifungu cha 12 (1), sura ya tatu imeeleza kuwa, ‘Watu wote ni sawa mbele ya sheria’, huku katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya mwaka 1977 kwenye Ibara ya 21 ikieleza ikieleza haki ya kila mtanzania kushiriki kwenye shughuli za utawala, suala la kuchagua na kuchguliwa, hivyo kila mmoja ana wajibu wa kuwa kiongozi bila ya kudhalilishwa.

 

                                 MWISHO.

Comments

BLOG'S VISITORS

DAKTARI MWENGINE CHAKE CHAKE KULA SIKUKUU POLISI, NI KWA TUHUMA ZA KUMBAKA MGONJWA WAKE

NA WAANDISHI WETU, PEMBA::: DAKTARI anaetoa huduma kwa wagonjwa kituo cha afya cha serikali cha  Gombani wilaya ya Chake Chake Pemba, Is-haka Rashid Hadid, anaendelea kushikiliwa na Jeshi la Polisi Mkoa wa kaskazini Pemba, akituhumiwa kumtorosha na kisha kumbaka mtoto wa mwenye umri wa miaka 16, mkaazi wa Gombani. Daktari huyo miaka 35 ni mkaazi wa Kangagani Wilaya ya Wete mkoani humo, ambapo anadaiwa alimchukua mtoto huyo kutoka kwa rafiki yake, na kumpeleka kwenye nyumba anayoishi eneo la Kangagani. Mtoto aliefanyiwa kitendo hicho alisema kuwa, April 21 mwaka huu alikwenda kituo cha afya Gombani, kwa ajili ya matibabu na baada ya kupatiwa huduma na daktari huyo, alimuomba nambari yake ya simu. Alisema ilipofika usiku, walikuwa wanawasiliana kupitia ujumbe mfupi (sms) kwa lengo la kwenda kuchukua dawa nyingine ambazo kwa mchana huo alizikosa hospitalini hapo. "Nilikwenda hospitali kutibiwa, baada ya kufanya mapele katika sehemu zangu za siri, lakini akaniambia mpaka aje da...

'MKAPA' NA WENZAKE PEMBA WALAZWA RUMANDE

  NA HAJI NASSOR, PEMBA@@@@ MAHKAMA kuu Zanzibar kisiwani Pemba, chini ya Jaji Ibrahim Mzee Ibrahim, imewapeleka rumande watumuhimwa wanne wanaokabiliwa na tuhuma za kuua kwa makusudi, akiwemo Ali Mussa Omar ‘ Mkapa’ mkaazi wa Wawi wilaya ya Chake chake Pemba. Watuhumiwa wengine walioanza maisha mapya ya rumande ni mtuhumiwa Yassir Mohamed Juma miaka 23, Anuwari Mussa Omar miaka 30 pamoja na mtuhumiwa Yassir Mussa Omar ‘ Makababu ’ miaka 29, wote wakaazi wa shehia ya Wawi, wilaya ya Chake chake Pemba. Awali watuhumiwa hao waliwasili mahakamani hapo, kwa mara ya kwanza, kwa ajili ya kusomewa tuhma zinazowakabili za kumuua kwa maksudi Said Seif Kombo. Ilidaiwa mahakamani hapo na Mwendesha Mashtaka kutoka Ofisi ya Mkurugenzi wa Mashataka Seif Mohamed Khamis akiambatana na mwenzake Mussa Khamis Ali kuwa, watuhumiwa hao kwa pamoja wanadaia kufanya mauwaji hayo kwa maksudi. Ilidai kuwa, watuhumiwa wote kwa pamoja, walitenda kosa hilo Oktoba 16, mwaka huu, baina ya saa 7:00 m...

HII KALI MBUNGE ASIYA AMKOGESHA MWANANCHI HADHARANI KISA HICHI HAPA......

  NA HAJI NASSOR, PEMBA MBUNGE wa viti maalum nafasi za wanawake mkoa wa kaskazini Pemba Asiya Sharif Omar, amewataka wananchi wa kijiji cha taifu, shehia ya Kinyasini jimbo la Gando wilaya ya Wete Pemba, kuyalinda miundombinu ya maji safi na salama, ili yawe endelevu kwao. Kauli hiyo ameitoa wakati alipokuwa akizungumza na mwandishi wa habari hizi, mara baada ya kuwasili kijijini humo, na kumkogesha mwananchi mmoja kama ishara ya uzinduzi wa mradi wa maji safi na salama, ulioasisiwa na mbunge wa Jimbo la Gando. Alisema, hawana mbadala kwa sasa bali ni kuilinda miundombinu ya huduma hiyo, hasa baada ya mbunge wa wao Salim Mussa Omar, kuwarejeshea huduma hiyo. Alieleza kuwa, inafahamika kuwa kwa miaka 14 waliikosa huduma hiyo hasa kwa vile viongozi waliokuwepo hawakujali kuwatatulia tatizo hilo, hadi juzi ilipofanywa na mbunge wao. “Baada ya huduma hii sasa kurejeshwa na mbunge wa jimbo la Gando, kazi iliyobakia kwenu wananchi ni kila mmoja kuwa mlinzi wa miundombinu hii,’...

…….SUZA WATOA USHAURI WA ADHABU YA KUNYONGWA

  NA HAJI NASSOR, PEMBA@@@@ WANAFUNZI wanaosomea uwalimu Chuo cha taifa cha Zanzibar ‘SUZA’ kampasi ya Benjamin Wiliam Mkapa Wete Pemba, wamependekeza adhabu ya kunyongwa hadi kufa, kwa mtu atakaetiwa hatiani, kwa kosa la dawa za kulevya. Walisema, haiingii akili kuona, mahkama imeshamtia hatiani mtu kwa kukutwa na dawa za kulevya, ambazo huathiri nguvu kazi ya taifa na kisha, kupewa hukumu ya kifungo pekee. Wakizungumza leo Juni 26, 2024 kwenye kongamano la vyuo vikuu, juu ya masuala ya msaada wa kisheria, kuelekea wiki ya msaada wa kisheria Zanzibar, lililofanyika Chuoni hapo, walisema wakati umefika sasa kutolewa kwa hukumu hiyo. Walipendekeza kuwa, ni vyema kwa mtu anayetiwa hatiani asibakie chuo cha Mafunzo pekee kuitia tena hasara serikali kwa chakula na wakati mwingine matibabu, wakati tayari ameshasababisha madhara, kwa vijana. Mshiriki Juma Nafasi Juma, alifafanua kuwa kama mtu ameamua kuliumiza taifa kwa kuingiza, kusafirisha, kusambaaza dawa za kulevya, hivyo n...

HABARI ZA HIVI PUNDE

 TAARIFA za hivi punde, zilizofikia ofisi ya Pemba Today, zinaeleza kuwa, Jeshi la Polisi mkoa wa kaskazini Pemba, linamshikilia askari mwenzao, kwa tuhuma za ubakaji ndani ya moja ya kituo cha Polisi kisiwani Pemba Muume wa mwanamke aliyedai kubakwa na Mwanamke mwenyewe, wamedai kutokea kwa tendo hilo, na huku Kaimu Kamanda wa Polisi mkoa wa kaskazini Pemba, akithibitisha kupokea kwa lalamiko hilo.... Kwa taarifa zaidi ya tukio hili endelea kufuatilia mtandao huu, ambao kukuhabarisha ni fahari yetu...