Skip to main content

MAFUNZO YA UTUNZAJI WA MISITU YA MIKOKO YAANZA RASMI COMMUNITY FORESTS PEMBA

 



BY MUNIRA KAONEKA, ZANZIBAR@@@@

Katika jitihada za kuimarisha uhifadhi wa mikoko na matumizi endelevu ya rasilimali za asili, Jumuiya ya Community Forests Pemba (CFP) imefungua mafunzo maalum kwa Watoa Mafunzo ya Jamii (ToTs) kuhusu uhifadhi wa mikoko na usimamizi wa rasilimali za jamii. Mafunzo haya, yalifanyika kuanzia tarehe 19 hadi 21 Februari katika ofisi za CFP Unguja, na yalilenga kuwawezesha washiriki kuwa viongozi wa uhifadhi wa mazingira katika jamii zao.

Mafunzo haya yameandaliwa ili kuongeza uelewa wa washiriki kuhusu umuhimu wa mikoko, mbinu za kuhifadhi misitu, na namna ya kushiriki katika usimamizi wa rasilimali za asili kwa njia endelevu. Kupitia mafunzo haya, ToTs watapata ujuzi wa vitendo na mbinu za kufundisha ambazo zitawawezesha kuwa mabalozi wa mabadiliko katika maeneo yao.

Akifungua rasmi mafunzo haya, Mkurugenzi Mtendaji wa CFP alisisitiza kuwa uhifadhi wa mikoko ni jukumu la jamii nzima. “Uhifadhi wa mikoko na urejeshwaji wake ni kazi ya pamoja, na ni muhimu kwa maendeleo endelevu. Tunapaswa kuwa mabalozi wa kulinda rasilimali hizi ” alisema. Pia, aliishukuru jamii kwa kujitolea na kushiriki katika juhudi za uhifadhi wa mazingira.


                                          ToT wa mikoko wakipokea mafunzo darasani

Mafunzo haya yalihusisha jumla ya washiriki 35, wakiwemo wanaume wanne (4) na wanawake 31, huku wanawake wakipewa kipaumbele kwa kuwa mara nyingi wao ndio waathirika wakubwa wa mabadiliko ya tabianchi lakini hawashirikishwi ipasavyo katika maamuzi. Washiriki walitoka katika maeneo ya Unguja Ukuu (17) na Uzi (18). Walichaguliwa kwa ujuzi wao na namna wanavyojitolea kwenye utunzaji wa mikoko, wakiwemo wanachama wa kikundi cha uhifadhi wa mikoko cha Unguja Ukuu, Mikoko ni Urithi Wetu.

Mafunzo haya yaliendeshwa na maafisa wa CFP waliobobea katika uhifadhi wa mikoko, wakiwemo Khadija Abdulrahman Hamdu (Afisa wa Mikoko) na John Ngonyani (Afisa wa CoFMA). Washiriki walipata elimu kuhusu:Umuhimu wa mikoko katika mazingira na jamii, Mbinu za uhifadhi na urejeshwaji wa misitu ya mikoko, matumizi endelevu ya rasilimali za mikoko na changamoto zinazokumba uhifadhi wa mikoko na jinsi ya kuzitatua.

Kwa mujibu wa Afisa wa Mikoko kutoka CFP Khadija Hamdu, “Mafunzo haya yatasaidia katika kuengeza ujuzi na uelewa wa wanajamii katika masuala ya mikoko. Pia yatasaidia katika kupunguza athari zitokanazo na uharibifu wa mikoko.”

Baada ya vipindi vya darasani, washiriki watafanya ziara ya mafunzo kwenye misitu ya mikokoi ili kujifunza kwa vitendo mbinu bora za uhifadhi wa mikoko.

Mafunzo yalikua mazuri na tumejifunza mengi na sasa nina ujasiri wa kufanya yale niliyohitaji kufanya (kwenye utunzaji wa mikoko)”alisemaBi.Rukia Haji Hamisi, mvuvi na mkulima kutoka Uzi

Baada ya mafunzo haya, washiriki wanatarajiwa kuwa viongozi wa uhifadhi wa mikoko katika jamii zao kwa kuelimisha wanajamii kuhusu faida za uhifadhi wa mikoko na jinsi inavyoweza kuwanufaisha kiuchumi, kushiriki katika urejeshwaji wa mikoko kwa kupanda miche mipya, na kuhamasisha ushiriki wa wanawake katika uhifadhi wa misitu kupitia nafasi za uongozi.

 


Comments