UDHALILISHAJI KWENYE VYAMA UNAVYOWEZA KUKATISHA NDOTO ZA WAGOMBEA WANAWAKE, 'Wanasema: kama una moyo mwepesi hutoboi
IMEANDIKWA NA ZUHURA JUMA, PEMBA
HAKIKA… hakuna safari ya mafanikio iliyokosa vikwazo na misukosuko ndani yake.
Lakini kama mwanadamu hatakiwi kuvunjika moyo ama kukata tamaa kwa kile kinachoitwa kukumbana na vikwazo katika safari yake ya kutafuta mafanikio.
Na ndio maana tumeumbwa na tabia ya kujaribu kila upande, ili tu kuhakikisha unafanikiwa katika maisha yako.
Ili ufanikiwe katika maisha yako lazima uwe tayari kupambana na kuvishinda vikwazo vyote vinavyokupitia mbele yako.
Kwani hakuna mafanikio ya njia rahisi na ndio maana wahenga walisema… ‘jitihada wajada’ wakimaanisha ukijitahidi utafanikiwa.
UDHALILISHAJI UNAOWAKUMBA WAGOMBEA WANAWAKE
Saada Saleh Ali mkaazi wa Chwale ni miongoni mwa wanawake wapambanaji katika kuusaka uongozi bila kujali vikwazo anavyokutana navyo katika kila hatua anayopitia.
Hiyo imemfanya kuwa jasiri na kujiamini huku akifanikiwa kujinyakulia nafasi mbali mbali ndani ya chama chake.
Saada ambae ni Mwenyekiti wa Vijana Wilaya ya Wete kupitia chama cha Mapinduzi CCM anaeleza kwamba, udhalilishaji wa wanawake wakati wa kugombea upo kwa kiasi kikubwa, ingawa anaendelea kupambana ili kufikia anapopataka.
Anasema, mwanamke anaetaka kugombea mara nyingi hukubwa na udhalilishaji wa maneno na udhalilishaji wa kingono, hivyo ikiwa hatokuwa makini kuna hatari ya kujivunjia heshima.
‘’Udhalilishaji wa maneno huwezi kuuwepuka kwa sababu mtu anakutupia tu maneno mabaya, lakini udhalilishaji wa kingono unaweza kuuwepuka kwani una uwezo wa kukataa,’’ anasema kijana huyo.
Anahadithia unapotaka kugombea, kuna wanaume watajitokeza na kukwambia watakusaidia katika hatua zote, ingawa kumbe moyoni mwake ana lengo jengine, hali inayoweza kuwakatisha tamaa wanawake wengi.
‘’Ilinikuta hiyo kwa watu wangu wa karibu, lakini baada ya kuona lengo lao halikufanikiwa wakakataa kusema na mimi, kwa sababu wanakuwa wanakusaidia ingawa wamejiwekea malengo yao, hata kama hajakwambia lakini huwa anaimani kuwa huyu nitamuomba hiki na atanipatia,’’ anahadithia Saada.
‘’Lakini hii ni utayari wa mtu wenyewe, kuna wanawake wengine wanajipeleka wenyewe kwa madhumuni ya kuwa watafanikiwa na kama utakuwa hivyo na mwanaume nae hakai mbali, hivyo akipata anachokihitaji tu kwake anamuacha mkono, ingawa mimi anajipambania mwenyewe tu,’’ anaeleza.
Changamoto nyengine inayowakumba wagombea wanawake ni wanaotoka vijijini, kwani huitwa washamba wasiojua kuvaa, hivyo hushawishiana ili waiwachague kwa vile hawafuati mila za kimagharibi.
Hivyo wanakumbana na maneno machafu na yenye kuwavunja moyo kiasi ambacho wanaweza kukata tamaa ya kuendelea kugombea kwa ngazi nyengine ya uongozi, ingawa yeye mwaka huu amejipanga kugombea ubunge jimbo la Kojani.
‘’Kuna mtu aliniambia kuwa sifai kuwa Mwenyekiti wa Vijana kwa sababu nasitiri wala sijichanganyi kwenye makundi ya wanaumeme na kuniambia ni kheri ningekuwa Mwenyekiti wa Wazazi, kauli hiyo iliniuma sana,’’ anasimulia.
Saada hakuwa peke yake kati ya wanawake wanaokumbana na udhalilishaji, hata Moza Massoud Ali ambae ni Mwenyekiti Vijana Mkoa wa Kaskazini Pemba kupitia chama cha ACT Wazalendo nae ni miongoni wa wahanga wa janga hilo.
Dada huyo mkaazi wa Konde anahadithia, alikuwa anatukanwa na kudharauliwa na wapambe wa mpinzani wake ambae alikuwa mwanaume, jambo ambalo lilimuuma sana ingawa hakukata tamaa bali aligombea na kushinda.
‘’Mtu anataka ile nafasi usikae, hivyo hukushambulia kwa maneno mabaya ili uvunjike moyo, kilichoniuma ni vile kunifuata na kuniambia nafasi hii nisigombee wananipangia nyengine, lakini mimi sikukubali,’’ anaeleza.
Alikuwa anagombea nafasi ya Mwenyekiti na wao walitaka agombee nafasi ya Mshikafedha, lakini alifuata maamuzi yake, ingawa kutokana na vikwazo alivyovipata baada ya kushinda, alijiuzulu.
Lakini kutokana na kuishi na watu vizuri, vijana wenzake walimtetea na kumsimamia mpaka ile nafasi akarudishwa tena.
Mgombea wa ubunge kupitia chama cha TLP Ziada Hassan Saleh anasema, yeye hajakumbana na udhalilishaji wa aina yeyote kwenye harakati zake za kugombea, ingawa husikia kwa wagombea wengine.
‘’Utasikia wanachama wanaambiwa fulani hafai, musimpe kura akawa kiongozi kwa sababu ana tabia hii na hii na yale maneno huwa ni ya kuumiza moyo kwa kweli,’’ anasema.
Mgombea huyo, ameshagombea ubunge mara sita, ingawa bado hajabahatika na mwaka huu ana nia ya kugombea tena nafasi hiyo.
Zainab Mussa Bakar ambae ni Mwenyekiti wa Wanawake Mkoa wa Kusini Pemba upitia chama cha Demokrasia na Mendeleo CHADEMA anaelezea, udhalilisha unaowakumba sana ni ule wa kudharauliwa kwa kuonekana hawawezi kuongoza, kwani maeno hayo yanaumiza na kuwakatisha tamaa baadhi ya wanawake.
‘’Tunaambiwa maneno yanayotuumiza sana, kwa sababu mwanamme anakwambia nikishakupa kura yangu nitafaidika vipi? na unapomwambia utafaidia na maendeleo ya kwenye jimbo, basi yeye hafurahii kwani anakusudia ngono,’’ anaeleza.
Taasisi mbali mbali ikiwemo TAMWA wanajitahidi kuwaupatia elimu ili wajikingine na vikwazo vinavyowapata ikiwemo udhalilishaji, wawe waaminifu, wasikate tamaa, hivyo inawasaidia sana kwa kila mwanamke ambae yupo makini.
Anasema, wakati mwengine wanawake wanajisababisha wenyewe kuvunjiwa heshima na kudhalilishwa, kutokana na tabia wanazozionyesha.
‘’Pengine utavaa nguzo zisizo za heshima, hivyo utawakaribisha watu kukunyanyasa na kukuvunjia heshima, unapelekea vishawishi, pia wengine wanakwenda wenyewe kwa viongozi kujipendekeza na hasa kwa viti maalumu,’’ anafafanua.
‘’Kuna kipindi niligombea na mume wangu lakini kila mmoja kwa nafasi yake, nilipata tabu sana ya kutupiwa maneno na kuhamasishana mimi nisipewe,’’ anahadithia.
Maryam Saleh Juma mgombea ubunge kupitia chama cha Ukombozi wa Umma mkaazi wa Vitongoji alidhalilishwa na wagombea wa vyama vyengine kwa kumpinga na kuwambia wananchi wasimpe kura, walimchafua kwa maneno machafu.
Wadhalilishaji hao walipita nyumba kwa nyumba kumtilia fitina na kumsema vibaya, hali ambayo ilimdhalilisha sana na hatimae kukosa kura.
Mama huyo anahadithia kuwa, wengine walikuwa wanamwambia afanye nao ngono ili wamsaidie kupiga kampeni, kwani itamsaidia kupata kura nyingi hata kwa wanachama wa vyama vyao.
‘’Kwa vile najitambua niliwaambia kuwa, tumalizeni hili halafu mengine yatafuatia, kwa hiyo wakaacha kuwapigia kampeni kwa wagombea wa vyama vyao, wakanisaidia mimi, ulipomaliza uchaguzi wengine walinichukia sana kwa sababu sikuwafanyia vile walivyotaka na wengine wakaachana nayo,’’ anafafanua.
VIONGOZI WA VYAMA VYA SIASA
Katibu wa Wilaya Chake Chake chama cha wananchi CUF Mohamed Haji Kombo anasema, suala la udhalilishaji kwa wagombea kwenye vyama vingi vya siasa ni jambo la kawaida, ingawa katika chama chake halina nafasi kwa sababu wanashirikisha wote bila ubaguzi.
‘’Sisi tunajifunza yaliyotokea kupitia kwa wenzetu ili na kwetu yasitokee, hivyo maboresho yetu tunayafanya kutokana na zile athari tunazoziona maeneo mengine, tumepambana kuhakikisha hata mianya ya udhalilishaji haijitokezi.
Kwa mfano alihadithia uchaguzi walioufanya wa kutafuta wajumbe wa mkutano mkuu taifa kwamba, kawaida wanahitaji wajumbe 20 ingawa walishiriki wanachama 50, ambapo waliepusha udhalilishaji kwa kutoa fomu bure.
‘’Kwa vile wengine hawana uwezo kifedha, tuliona wanaweza kujidhalilisha ili tu wapate fomu, hivyo tukaliondoa mapema bila kujali mapato ambayo tutayakosa, kwani fomu ni shilingi 10,000,’’ anaeleza.
Abas Mohamed Khatib Mratibu wa chama cha Democratic Party (DP) Pemba anasema, ni mwaka na nusu tangu akae kwenye nafasi hiyo, hivyo hajapokea kesi, ingawa kipindi cha nyuma aliwahi kuwasikia wanawake wakilalamikia udhalilishaji.
Anasema kuwa, udhalilishaji huwa hufanywa na wanaume n ahata wanawake wenzao, kwa kuambiwa maneno mabaya yanayoweza kuwakatisha tamaa ya kuendelea kugombea.
‘’Wanawake nao wanaongoza kuwazdhalilisha wanawake wenzao, kwa sababu ikiwa ndo mara ya kwanza kugombea basi wanawake wenanzake wanamkataa na kumpakazia ubaya,’’ anaeleza.
Kiongozi kutoka chama cha Demokrasia Makini ambae hakutaka jina lake litajwe naeleza, udhalilishaji unatokea sana kwa sababu wao wanapiga kampeni za nyumba kwa nyumba, hivyo baadhi ya wanaume wanawambia waingie ndani ya nyumba zao na hivyo kuwadhalilisha.
‘’Pamoja na nafasi niliyonayo kwenye chama lakini pia nimeshagombea uwakilishi hivyo, tunapata shida kweli mtu anakwambia ingia ndani, ukiingia tu anakunasa,’’ anasema.
Waliwahi kupokea kesi ya kudhalilishwa mgombea kwa hali hiyo, hivyo wanachukua juhudi kubwa ya kutoa elimu na kuwashauri, kuhakikisha changamoto haziwakumbi tena wagombea wa chama chao.
ASASI ZA KIRAIA
Katibu wa Jumuiya ya Utetezi wa Kijinsia na Mazingira Pemba (PEGAO) Dina Juma Makota anasema, kupitia taarifa za wagombea wenyewe wanakiri kukumbana na udhalilishaji wakati wanapogombea nafasi za uongozi.
‘’Kinachonisikitisha mimi hawaripoti popote wanapofanyiwa udhalilishaji, sasa sijui kwa nini na tunajitahidi kuwahamasisha wasikae kimya ili tukomeshe wenye tabia ya kudhalilisha wenzao,’’ anaeleza.
Anasema, hatua mbali mbali wanazichukua kuhakikisha wanaepuka udhalilishaji ikiwepo kuwapatia elimu ya kuwajengea uthubutu wa kuripoti matendo ya udhalilishaji ikiwa yatawatokezea.
Chama cha Waandishi wa Habari Wanawake Tanzania (TAMWA) kwa kushirikiana na Taasisi ya Kitaifa ya Demokrasia (NDI) walifanya tathmini ya kutokomeza uddhalilishaji dhidi ya wanawake katika vyama vya siasa Zanzibar, ambayo iliyofanyika Julai 2024.
Ambapo ripoti hiyo ya tathmini ilieeleza kuwa, asilimia 45 ya wanawake hao walifanyiwa udhalilishaji wa kisaikolojia, asilimia 41 walifanyiwa udhalilishaji wa kiuchumi, asilimia 27 wallifanyiwa vitisho na kutumiwa nguvu, asilimia 25 walifanyiwa ukatili wa kimwili na asilimia 22 walifanyiwa ukatili wa kingono.
‘’Asilimia 48 ya taarifa hizo zilitolewa na wanachama wenzao, asilimia 30 zilitolewa na viongozi wa vyama vya siasa, asilimia 17 kwenye mamlaka na asilimia 35 kwenye familia,’’ ulibaini uchunguzi huo.
Serikali ya Zanzibar na ile ya Tanzania imempa mwanamke fursa mbali mbali, ikiwemo kuwa kiongozi, hivyo si vyema kwa wale wanaowafanyia udhalilishaji wenzao waache kwani kila mmoja ana haki kisheria.
Katiba ya Zanzibar ya mwaka 1984 kwenye kifungu cha 12 (1), sura ya tatu imeeleza kuwa, ‘Watu wote ni sawa mbele ya sheria’, huku katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya mwaka 1977 kwenye Ibara ya 21 ikieleza ikieleza haki ya kila mtanzania kushiriki kwenye shughuli za utawala, suala la kuchagua na kuchguliwa, hivyo kila mmoja ana wajibu wa kuwa kiongozi bila ya kudhalilishwa.
MWISHO.
Comments
Post a Comment