Skip to main content

ULINZI SHIRIKISHI NG'AMBWA CHAKE CHAKE WAPUNGUZA WIZI KIDOGO

 



NA HAJI NASSOR, PEMBA@@@@

WANANCHI wa kijiji cha Vikunguni shehia ya Ng’ambwa wilaya ya Chake chake Pemba, wamekiri kupungua kidogo kwa vitendo vya wizi wa mifungu na mazao, baada ya ulinzi shirikishi kuimarika shehiani humo.

Walisema, ijapokuwa bado wapo baadhi ya wananchi wamekuwa wakiidharau na kukebehi uwepo wa ulinzi shirikishi, lakini vitendo vya wizi wa Ng’ombe na mazao umeanza kupungua kwa kasi.

Wakizungumza na waandishi wa habari waliofika kijijini hapo kusikiliza kero zao, walisema sasa mifugo imekuwa salama kwa kiasi fulani.

Walisema, kwa sasa wanalala kwa amani na wanaweza kukaa hadi miezi mitatu bila ya kusikia uwepo wa wizi wa mifugo na mazao kama ilivyokuwa miaka iliyopita.

Mwananchi Khamis Ali Khamis, anasema kabla ya ulinzi shirikishi kuimarishwa, kila mwezi kulikuwa wizi wa Ng’ombe kati ya watano hadai saba.

‘’Kwa sasa unaweza kukaa miezi mitatu, ukasikia tukio moja la wizi wa Ng’ombe kwetu sisi hali hiyo, tunasema afadhali mno tofauti na zamani,’’alisema.



Kwa upande wake mfugaji Mohamed Mkubwa Mohamed, alieleza kuwa walifikia wakati wanapolala wao ndio walipokuwa wakiilaza mifugo yao.

‘’Ilikuwa lazima Ng’ombe au Mbuzi umlaze chini ya dirisha la nyumba yako, maana ukimuacha malishoni siku ya pili ukienda ameshaibiwa,’’anafafanua.

Wakulima Leluu Suleiman Said, Saada Suleiman Omar na Mtumwa Ali Omar, walisema ijapokuwa wizi haujaondoka moja kwa moja, lakini wanalima na kuvuna mazao mapevu.

Walisema, katika kijiji chao cha Vikunguni ndizi, muhogo, mananasi ilikuwa sio rahisi kuvunwa mapevu, maana vijana wao walikuwa wakiyaiba.



‘’Kwa mfano kama wizi wa Ng’ombe na mazao mara nyingi hufanyika nyakati za usiku au siku ya Ijumaa wakati waumini na dini ya kiislamu wakiwa kwenye ibada,’’wanasema.

Vijana Issa Khamis Issa, Kombo Juma Hassan na Mundhiri Ilyasa Hilali wanasema, moja ya eneo ambalo linapaswa kudhibitiwa ni matumizi ya dawa za kulevya.

‘’Ingawa jambo hili vijana wa shehia moja na nyingine huchanganyika, lakini kama hawa wa Ng’ambwa watadhibitiwa inaweza kuwa mwarubaini kwa vitendo vya wizi,’’wanasema.

Sheha wa shehia Ng’ambwa Issa Rihani Abass, amesema alimua kuelekeza nguvu katika ulinzi shirikishi, ili kupunguza vitendo vya jinai shehiani humo.


‘’Ni kweli baada ya kuteuliwa kushika nafasi hii, moja ya changamoto niliyoiona ilikuwa ni wizi wa macho macho, sasa tukajipanga na wananchi na ndio maana kuna afadhali,’’anafafanua.

Hata hivyo alisema, bado dhamira yake hasa ya hapo baadae ni kuona shehia ya Ng’ambwa wananchi wanalala bila ya hofu, pamoja na wakulima na wafugaji kuendesha shughuli zao kwa amani.





Mkuu wa wilaya ya Chake chake Abdalla Rashid Ali, amekuwa akirejea kuali yake kwa wananchi, kuwa njia moja nzuri ya kuzuia uhalifu kwenye maeneo yao ni kuiunga mkono Polisi Jamii.

Shehia ya Ng’ambwa wilaya ya Chake chake inao wakaazi 2500, inazo huduma za kijamii kama afya, elimu, mawasiliano ya simu na huduma za barabara kwa kiwango cha kifusi.

                                  Mwisho

 

Comments