Skip to main content

MIAKA 10 BAADA YA UJENZI WA BARABARA ZA ‘MCC’ PEMBA, WANAWAKE WAZIFIKIA HUDUMA ZA KIJAMII 'UBWETE'

 




NA HAJI NASSOR, PEMBA

SASA ni majira ya saa 8:00 jioni, jua limeshateguka, vivuli vya miti mikubwa ndio mwemvuli wangu, nipo hapa kituo cha afya cha Uwondwe shehia ya Mtambwe kaskazini, wilaya ya Wete Pemba.

Mbele yangu, namuoma mjamzito, akitokea chumba cha muuguzi wa afya ya mama na mtoto, huku mkononi akiwa na gamba la kliniki, akionekana na tabasamu.

Nilipomkaribia aliniambia, sasa huduma za mama na mtoto, wanazipata ndani ya kituo hicho, na hasa baada ya kumalizika kwa ujenzi wa barabara yao ya Bahanasa- Mtambwe.

Barara hiyo, ni kati ya zile tano (5), ziilizojengwa kwa ufadhili wa Mfuko wa Changamoto za Millenia na watu wa Marekeani ‘MCC’ ikiwa ni ile ya Kipangani- Kangani, Chwale- Likoni, Mzambarau takao pamoja na Pandani hadi Finya zenye urefu wa kilomita 35 kwa ujumla.

Kwa uwepo wa barabara hiyo, wananawake wa Mtambwe, wanasema moja ya huduma zilizoimarika ni upande wa afya ya mama na mtoto, na sasa ni miaka tisa (9), wamesahau machungu, dhiki na shida.

HUDUMA ZA AFYA

Wanawake, wanasema sasa wamesahau kubebwa kwa magunia, gari ya Ng’ombe kupelekwa bandarini kwa ajili ya kuingizwa kwenye mitumbwi, ili kufikishwa hospitali ya wilaya ya Wete.

Hamida Juma Mohamed wa Uwondwe shehia ya Mtambwe kaskazini, anasema hawakuwa na thamani wanapotaka kujifungua, maana wanaume walikuwa ndio gari zao za muda, kwa kuwabeba hadi bandarini, kabla ya kuingizwa kwenye mitumbwi.

‘’Kabla ya ujenzi wa barabara hii, iliyofadhiliwa na ‘MCC’ ilikuwa hapa Mtambwe, hakuna huduma za kujifungulia, tulilazimika kwenda Wete, tena kwa mtumbwi,’’anasema.

Muhudumu wa afya, kituo cha afya Uwondwe Zainab Hassan Shehe, anakiri kuwa, ujenzi wa barabara yao, ndio mwarubaini wa kupatiwa huduma za uzazi kijijini kwao.

‘’Kwa mwezi, tupokea kati ya wajawazito 60 hadi 65, kuwapatia huduma za mama na mtoto, na wanaojifungulia hapa hujitokeza kati ya 10 hadi 15, jambo linalo ni faraja, hasa baada kuwepo kwa barabara hii,’’anasema.

Anaona, mwisho wa wajawazito wa Mtambwe kubebwa kwa magunia, gari za Ng’ombe na vitanda imekoma, baada ya kuwepo wa barabara hiyo na kufuatia kujengwa kwa kituo cha kujifungulia.

Lakini sio Mtambwe pekee, wanawake wanaokiri kuimarika kwa huduma hizo, hata Mwanaisha Bakari Haji wa Kangagani, anasema sasa adha ya kwenda Wete au Chake chake imekwisha.

‘’MCC kutujengea barabara yetu, kutoka Kipangani hadi kijiji kwetu, imetupunguzia machungu ya usafiri, maana ilikuwa gari za Ng’ombe au kubebwa kwenye magunia, ni jambo la kawaida,’’anasema.



Asia Haji Hussein wa Pandani, anasema dhiki kubwa walikuwa wakiipata miaka tisa iliyopita, juu ya kufuata huduma za uzazi Wete na Micheweni, sasa wameshazisahu, baada ya kujengewa barabara yao.

Kama alivyo Asia, hata Mwashamba Kombo Lali wa Finya, anasema watoto wake watatu, amejifungulia kituoni kwao, baada ya serikali kuimarisha huduma za uzazi na hasa uwepo wa barabara kwa kiwango cha lami.

‘’Baada ya kumalizika kwa ujenzi wa barabara yetu, sasa huduma za afya zipo saa 24, lazima tuwashukuru MCC na serikali ya Mapinduzi, kwa kushirikiana katika hili,’’anasema.

Bakar Faki Pandu ‘85’ mkaazi wa Chwale Madenajni, barabara ya Likoni hadi bandari ya Kojani, anasema huduma za afya zilizorota, na waliopokuwa wakitaka kumsafirisha mgonjwa kwenda hospitali ya Wete.

‘’Ujenzi wa barabara hii ya MCC kwetu wananchi wa Chwale, Likoni na Kojani imekuja kutuimarishia usafiri, na hasa tunapokwenda kwenye hospitali iwe cha Chake chake Wete,’’anaema.

Na hata Mwakame Hija Hamad, anasema aliwahi kuzaa njiani mwaka 2012, kutokana usumbufu wa barabara waliokuwa nao, ingawa sasa imekuwa mtelezo kwao.

Aisha Ussi Hamad, anasema pamoja na kuimarisha huduma za afya Kisiwa cha Kojani, lakini hata wanapokuwa na kesi kubwa za kwenda hospitali za Wete au Chake chake, usafiri upo saa 24.

‘’Kabla ya ujenzi wa barabara hii, ilikuwa ukipata tatizo la kwenda hospitali za Wete, kunausumbufu mara mbili, moja usafiri wa mtumbwi na kisha unakumbana na ubovu wa barabara, lakini sasa shida tumeisahau,’’anasema.

Suleiman Makame Issa wa Kojani, anasema usafiri na usafirishaji umekuwa rahisi kwao, iwe kwa wanaokwenda mjini, hospitali au kufuata huduma nyingine, makao makuu ya serikali ya wilaya.

‘’Sasa tunalala Kisiwa cha Kojani na kuwahi shughuli kama za matibabu hospitali kuu za Wete au Chake chake, jambo ambalo, lilikuwa ni adimu kwa miaka kadhaa,’’anasema.

HUDUMA ZA ELIMU

Mwalimu mkuu msaidizi wa skuli ya Msingi Uwondwe, akihudumu miaka 31 sasa, Maryam Ali Hamad, anasema sasa wamekuwa na majengo ya kisasa na kutanua wigo, wa upatikanaji elimu.


‘’Sasa skuli imeongezewa majengo, kutoka matatu ya awali hadi matano, hivyo hata idadi ya wanafunzi nayo imeongezeka, lakini hata huduma za umeme zimeimarika,’’anasema.

Anakumbuka, wakati anasoma skulini hapo, wanafunzi wenzake walikuwa wakichelewa kwa saa moja, na hasa kwa siku za mvua, kutokana na uchakavu wa barabara yao.

Wanafunzi Khamis Juma Ali, Omar Haji Omar, Is-haka Mjaka Sauod na mwenzake Khadija Kombo Yussuf wa skuli za Pandani, Finya, Uwondwe, Kangagani, wanasema barabara imewasaidi kuendeleza ushirikiano na skuli nyingine.

‘’Kila muda tunapokea wanafunzi na ugeni wa tasisi nyingine, kutokana na kuwepo kwa barabara ya uhakika, jambo ambalo limetuamsha ari ya kusoma kwa kushindana,’’anasema.

Afisa Mdhamini wizara ya Elimu na Mafunzo ya Amali Pemba Mohamed Nassor Salim, anasema uwepo wa barabara hizo, kwao zimerahisisha usafirishaji wa vifaa vya ujenzi wa skuli na vitabu vya kujisomea.

‘’Gharama ya kusafirishia vifaa kama vitabu, chaki, mitihani na vifaa vya ujenzi imeondoka hasa kuanzia mwaka 2014, baada ya udunguzi wa barabara tano za mkoa wa kaskazini Pemba, ‘’anaeleza.

HUDUMA ZA UMEME

Afisa Mawasiliano na Huduma kwa wateja wa Shirika la Umeme Zazibar ‘ZECO’ tawi la Pemba Haji Khatib Haji, anasema barabara hizo zimechangia kwa asilimia 100, usambaazaji wa huduma ya umeme vijijini.

‘’Vijiji vya Kangagani tumesambaaza umeme eneo lenye wa urefu wa kilomita 2, sambamba kufanya matengenezo, kupeleka umeme wa njia kuu na mdogo wa kilomita 3.5 kisiwa cha Kojani pamoja na Likoni Chwale, kwa kutumia barabara za MCC,’’anasema.

Kwa muda mrefu, walikuwa wanashindwa kuwafikishia huduma hiyo wateja waao, hiyo ni kutokana na miundombinu kuwa chakavu na hasa uzito wa gari na vifaa vyao.

Upande mwengine anasema, barabara ya Bahanasa- Mtambwe mwishoni  2020 /2021, waliitumia wakati wanasafirishia vifaa vya huduma ya umeme wa sola, kwa wananchi wa kisiwa cha Kokota wilaya ya Wete.

Wananchi Omar Khamis Haji na mwenzake Siti Omar Hamdu wa Finya wanasema, kwa vyovyote vile, uwepo wa barabara yao kwa kiwango cha lami, kwao imerahisisha kuunga huduma ya umeme.

Asha Haji Hamza wanasema, sasa imekuwa rahisi kwake, anapokuwa na changamoto kwenye shirika la umeme, kufuatilia mjini Chake chake au Wete, na hapo kabla ya ujenzi wa barabara, lilikuwa zito kwake.   

HUDUMA ZA KISHERIA

Mratibu wa Kituo cha Huduma za Sheria Zanzibar ZLSC tawi Pemba, Safia Saleh Sultan, anasema kabla ya kufunguliwa kwa barabara hizo mwaka 2014, walikuwa wakipokea wanawake kati ya watano (5) hadi 10 kwa mwezi, waliyokuwa wakihitaji masaada wa kisheria.

‘’Baada ya kufunguliwa, sasa wanawake wamehamasika na tumekuwa tukiwapokea kati ya 35 hadi 40 kwa mwezi, kutoka vijiji vya Kangagani, Kojani, Mtambwe, Finya na Pandani zilimopita barabara za MCC,’’anasema.

Mwananchi wa Mzambarau takao, Moza Abass Mohamed anaona uwepo wa barabara hiyo, imerahisishia kufuatilia hudumza kisheria, kituo cha Polisi Wete.

‘’Mwaka 2019, niliibiwa ndizi na kuku wangu saba, lakini kwa vile barabara ipo vyema, nilihamasika kufika kituo cha Polisi, kufuatilia haki zangu, lakini kwa zamani, isingekuwa kuwa rahisi,’’anasema.  

Mratibu wa wanawake na watoto shehia ya Kangagani Awena Salim Kombo, anasema wanawake sasa wanafika kituo cha Polisi Mchanga mdogo, wanapokutana na changamoto za kisheria.

‘’Hata usiku sasa mtu anakodi bajaji au boda boda na kupeleka malalamiko yake, ambapo zamani kwa uchakavu wa barabara haikuwa rahisi hata kidogo,’’anasema.

SERIKALINI

Afisa Mdhamini wizara ya Ujenzi, Mawasiliano na Uchukuzi Pemba Ibrahim Saleh Juma, anasema tokea kufunguliwa kwa barabara hizo, miaka tisa (9) iliyopita hawajawahi kuzifanyia matengenezo, kutokana na uimara wake.

‘’Matengenezo tuliyoyafanya, ni barabara ya Bahanasa- Mtambwe kwenye daraja, baada ya kuharibika kutokana na mvua kubwa iliyonyesha mwaka 2017 na kwa sasa barabara zote tano, ziko madhubuti,’’anasema.

Aliyekuwa kuwa Mhandisi mkaazi wa ujenzi wa barabara Pemba, wakati wa ujenzi wa barabara za MCC, Khamis Massoud Khamis, anasema uimara wa barabara hizo, ulitokana na aina ya ujenzi.

Ujenzi wa barabara hizo umetofautiana na nyingine, maana tabaka mbili za juu ‘sub base and base’ zilichanganywa kokoto nyembamba na saruji, kwa ujazo wa mita moja, kwa mfuko mmoja wa saruji.

Barabara za ‘MCC’ hazikutumia utaalamu wa lami moto ‘asphalt congreatE’ bali zilitumia mfumo wa lami ya kuchemsha ‘surface dressing’ na kisha humwagwa, baada ya muda humiminiwa kokoto zenye ujazo wa milimita 15 hadi 20, na kuzama kwenye lami hiyo.

‘’Baada ya kushindiliwa hadi kuzama kwa kokoto, humwagwa tena lami zikiwa na kokoto ndogo ndogo, zenye ujazo kati ya milimita 8 hadi 10, lengo ni kuziba nafasi ilizoachwa wazi na kokoto kubwa za awali,’’anafafanua.

Jengine ni kutumia shilingi bilioni 1.1 kwa urefu wa kilomita 1, wakati ujenzi wa barabara za kawaida kwa urefu huo, hutumia gharama ya shilingi bilioni 1.

‘’Ujenzi wa aina hii ya barabara za MCC, hutakiwa kufanyiwa matengenezo kila baada ya miaka 10, ingawa kwa kwetu zinaweza kuzidi kutokana na kutokuwepo kwa gari, nyingi zenye uzito wa zaidi tani 15, kama uhimili wa barabara hizi inavyotakiwa,’’anasema.

Aliyewahi kuwa Afisa Mdhamini wa wizara hiyo Hamad Ahmed Baucha, anasema barabara hizo, zilisimamiwa na wenyewe kuanzia uchoraji wa michoro, hadi kwenye ulipaji wa fidia.

                                  Mwisho

Comments

BLOG'S VISITORS

DAKTARI MWENGINE CHAKE CHAKE KULA SIKUKUU POLISI, NI KWA TUHUMA ZA KUMBAKA MGONJWA WAKE

NA WAANDISHI WETU, PEMBA::: DAKTARI anaetoa huduma kwa wagonjwa kituo cha afya cha serikali cha  Gombani wilaya ya Chake Chake Pemba, Is-haka Rashid Hadid, anaendelea kushikiliwa na Jeshi la Polisi Mkoa wa kaskazini Pemba, akituhumiwa kumtorosha na kisha kumbaka mtoto wa mwenye umri wa miaka 16, mkaazi wa Gombani. Daktari huyo miaka 35 ni mkaazi wa Kangagani Wilaya ya Wete mkoani humo, ambapo anadaiwa alimchukua mtoto huyo kutoka kwa rafiki yake, na kumpeleka kwenye nyumba anayoishi eneo la Kangagani. Mtoto aliefanyiwa kitendo hicho alisema kuwa, April 21 mwaka huu alikwenda kituo cha afya Gombani, kwa ajili ya matibabu na baada ya kupatiwa huduma na daktari huyo, alimuomba nambari yake ya simu. Alisema ilipofika usiku, walikuwa wanawasiliana kupitia ujumbe mfupi (sms) kwa lengo la kwenda kuchukua dawa nyingine ambazo kwa mchana huo alizikosa hospitalini hapo. "Nilikwenda hospitali kutibiwa, baada ya kufanya mapele katika sehemu zangu za siri, lakini akaniambia mpaka aje da

'MKAPA' NA WENZAKE PEMBA WALAZWA RUMANDE

  NA HAJI NASSOR, PEMBA@@@@ MAHKAMA kuu Zanzibar kisiwani Pemba, chini ya Jaji Ibrahim Mzee Ibrahim, imewapeleka rumande watumuhimwa wanne wanaokabiliwa na tuhuma za kuua kwa makusudi, akiwemo Ali Mussa Omar ‘ Mkapa’ mkaazi wa Wawi wilaya ya Chake chake Pemba. Watuhumiwa wengine walioanza maisha mapya ya rumande ni mtuhumiwa Yassir Mohamed Juma miaka 23, Anuwari Mussa Omar miaka 30 pamoja na mtuhumiwa Yassir Mussa Omar ‘ Makababu ’ miaka 29, wote wakaazi wa shehia ya Wawi, wilaya ya Chake chake Pemba. Awali watuhumiwa hao waliwasili mahakamani hapo, kwa mara ya kwanza, kwa ajili ya kusomewa tuhma zinazowakabili za kumuua kwa maksudi Said Seif Kombo. Ilidaiwa mahakamani hapo na Mwendesha Mashtaka kutoka Ofisi ya Mkurugenzi wa Mashataka Seif Mohamed Khamis akiambatana na mwenzake Mussa Khamis Ali kuwa, watuhumiwa hao kwa pamoja wanadaia kufanya mauwaji hayo kwa maksudi. Ilidai kuwa, watuhumiwa wote kwa pamoja, walitenda kosa hilo Oktoba 16, mwaka huu, baina ya saa 7:00 mchan

HII KALI MBUNGE ASIYA AMKOGESHA MWANANCHI HADHARANI KISA HICHI HAPA......

  NA HAJI NASSOR, PEMBA MBUNGE wa viti maalum nafasi za wanawake mkoa wa kaskazini Pemba Asiya Sharif Omar, amewataka wananchi wa kijiji cha taifu, shehia ya Kinyasini jimbo la Gando wilaya ya Wete Pemba, kuyalinda miundombinu ya maji safi na salama, ili yawe endelevu kwao. Kauli hiyo ameitoa wakati alipokuwa akizungumza na mwandishi wa habari hizi, mara baada ya kuwasili kijijini humo, na kumkogesha mwananchi mmoja kama ishara ya uzinduzi wa mradi wa maji safi na salama, ulioasisiwa na mbunge wa Jimbo la Gando. Alisema, hawana mbadala kwa sasa bali ni kuilinda miundombinu ya huduma hiyo, hasa baada ya mbunge wa wao Salim Mussa Omar, kuwarejeshea huduma hiyo. Alieleza kuwa, inafahamika kuwa kwa miaka 14 waliikosa huduma hiyo hasa kwa vile viongozi waliokuwepo hawakujali kuwatatulia tatizo hilo, hadi juzi ilipofanywa na mbunge wao. “Baada ya huduma hii sasa kurejeshwa na mbunge wa jimbo la Gando, kazi iliyobakia kwenu wananchi ni kila mmoja kuwa mlinzi wa miundombinu hii,’’ali

TUHMA ZA DAKTARI PEMBA KUCHIWA HURU: POLISI KASKAZINI KUTOA TAARIFA RASMI LEO

  NA HAJI NASSOR, PEMBA KAMANDA wa Polisi mkoa wa kaskazini Pemba, Juma Saad Khamis, amesema leo Mei 9, mwaka huu atatoa taarifa rasmi, juu ya kuendelea kumshikilia au kumpa dhamana ya Polisi, daktari wa Kituo cha Afya Gombani Is-haka Rashid Hadid, anayetuhumiwa kwa ubakaji. Alisema, kwa vile alikuwa katika mapumziko mafupi, haelewi jambo lolote linaloendelea kwa mtuhumiwa huyo, juu ya kuendelea kushikiliwa kwake kituoni hapo. Alieleza kuwa, leo Mei 6 (jana), hajapata taarifa za ndani za mtuhumiwa, huyo na kuwataka wananchi na wanaharakati, wasubirie hadi Jumatatu ijayo. Akizungumza na waandishi wa habari kwa nyakati tofauti Kamanda huyo, alisema hana taarifa zozote za kupewa dhamana mtuhumiwa ndani ya kituo chake cha Polisi au kuendelea kuwepo. ‘’Ilikuwa mimi sipo kazini kwa muda, kuanzia anakamatwa hadi anafikishwa Polisi, kwa sasa siwezi kueleza jambo lolote kwa mtuhumiwa huyo, hadi Jumatatu,’’alieleza. Aidha Kamanda huyo alieleza kuwa, kwa sasa hawezi kutoa ufafan

MADAKTARI KUTOKA CHINA WAOKOA MAISHA YA MTOTO PEMBA

  HABIBA ZARALI, PEMBA TIMU ya 32 ya madaktari wa kichina katika hospitali ya Abdalla Mzee Mkoani wamefanikiwa kufanya upasuaji mkubwa wa mtoto mwenye umri wa miaka 15 mkaazi wa Chole Kengeja, baada ya kuchomwa na jiti sehemu ya njia zake za mfumo wa uzazi. Mtoto huyo ambae alianguka hivi karibuni katika mti na baadae kuchomwa na jiti hilo na kumsababishia kutokwa na damu nyingi katika sehemu ya nyonga, alifanyiwa upasuaji uliodumu kwa muda wa saa tatu na   kuokolewa maisha yake. Akizungumza mara baada ya operesheni huo kiongozi wa timu hiyo Dr Jiang Jinhua, alisema mara baada ya mtoto huyo kufikishwa hospitalini hapo na kufanyiwa vipimo na kuonekana   ilibidi apatiwe rufaa ya kwenda katika hospitali nzuri yenye kutibu tatizo lake huko nchini Kuwado ambapo haikuwezekana kutokana na hali ya umaskini wa f amilia ya mtoto huyo . Alisema timu ya madaktari hao itaendelea kutowa huduma za matibabu   kwa wananchi kisiwani humo,   ili kuwaondolea gharama ya kutafuta matibabu nje ya nch