Skip to main content

WEMA YAPIGA MARUFUKU MICHANGO KUMUHUSISHA MWANAFUNZI



WAZAZI wa shehia ya Mgogoni Wilaya ya Wete Pemba wamelalamikia tabia ya walimu wa skuli ya Kinyasini kuwarudisha watoto wao skuli kwa ajili ya kuchukua pesa ya kufanyia mitihani, hali ambayo inarudisha nyuma maendeleo yao ya elimu.

Walisema kuwa, hawajakataa kulipa fedha kwa ajili ya mitihani ya watoto wao kwani ni jambo zuri, ingawa kinachowauma ni vile kutolewa wakati masomo, hali ambayo inawakosesha vipindi vinavyoendelea skuli.

Wakizungumza na mwandishi wa habari hizi wazazi hao walisema, wakati mwengine hawana pesa kutokana na hali ngumu ya maisha, hivyo huwapa pesa nusu kupeleka skuli ingawa hurejeshwa tena kwa vile hawajakamilisha, jambo ambalo linawauma sana.

‘’Hatujakataa kulipia kwa sababu tunapenda wafanye mitihani, lakini linalotusikitisha ni hili la kuwatoa watoto skuli waje nyumbani kuchukua pesa, kwa sababu wanakosa masomo na jengine wanaweza kufanyiwa udhalilishaji njiani kwani ni masafa marefu,’’ walisema wazazi hao.

Walisema kuwa, ni kilio kikubwa kwa skuli hiyo, kwani iwapo hawakulipa hawaruhusiwi kufanya mitihani, hiyo hali ambayo inawadhalilisha wanafunzi hao ambao hawajalipa.

Mwananchi Ramadhan Khamis Juma na Maryam Khamis Sharif awalieleza kuwa, kufanya hivyo kunarudisha nyuma maendeleo ya watoto kielimu ambao wanapenda kusoma, hivyo ni vyema wakawaonea huruma kutokana na uwezo wao mdogo kifedha katika familia zao.

‘’Tunapenda sana watoto wasome na wafanyiwe mitihani kwa ajili ya kupimwa lakini hali zetu ni duni na hata tukiwapa pesa nusu basi wanarudishwa na ikiwa hatujaipata haturuhusiwi kufanya mitihani,’’ walieleza.

Bikombo Abdalla Ali na Asha Bakar Omar walisema, watoto wao wanasikitika sana kufanyiwa hivyo na kuwaomba walimu kufanya subra pale ambapo mtoto hajalipa, kwani hilo ni jukumu la wazazi, wao waachwe wasome.

‘’Tunawaomba watuite sisi wazazi japo kwa kuwapa barua watoto au kutupigia simu kwa sababu masafa wanayorudi nyumbani sio madogo wanaweza kukumbana na vishawishi njiani wakadhalilishwa na pia wanakosa masomo mengine,’’ alieleza.

Nae Hanifa Khamis Said aliomba walimu hao inapofanyika mitihani waruhusiwe wanafunzi wote, ili na wale ambao wana hali ngumu katika familia zao wasijisikie vibaya.

Afisa Mdhamini Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Amali Pemba Mohamed Nassor Salim alisema kuwa, Wizara ya Elimu inatoa huduma zote za kielimu bila ya malipo na ndio utaratibu, ingawa wameanzisha Kamati za skuli ambazo miongoni mwa majukumu yake ni kuimarisha ufaulu kwa wanafunzi na kusimamia maendeleo katika skuli zao.

‘’Hivyo zinakuwa na mamlaka ya ndani na wanakaa kujadili vipi tunaweza kuongeza ufaulu wa alama za juu, ukipitia ripoti mbali mbali za ziara zangu changamoto inayowakuta wanakamati ambayo inasababisha kutokufikia malengo ni utoro wa wanafunzi na tunashirikiana kupambana nalo,’’, alisema.

‘’Lakini mkakati mwengine ambao wanautumia sana kuimarisha ufaulu ni mitihani ya mara kwa mara na ni suala la gharama, sisi tunapeleka pesa za uwendeshaji maskulini lakini wanakamati wanaamua kila wiki wanafunzi wafanye mitihani, hivyo hufanya utaratibu wa kuchangisha wazazi na wanakubaliana pamoja,’’ alifafanua.

Alisema pamoja na hayo, Wizara imetoa angalizo kwamba michango yote ambayo kamati na wazazi watakubaliana isimuathiri mtoto, hivyo alikumbusha na kupiga marufuku aina yeyote ya mchango kumuhusisha mwanafunzi.

‘’Nimekuwa nikiyakemea kila wakati kwa sababu pesa ile waliyokubaliana wanakamati na wazazi ni dhima na mzazi sio mwanafunzi na tunakataza hata iyo pesa asipewe mtoto kuipeleka bali aipeleke mzazi mwenyewe au waweke utaratibu wa kuifikisha,’’ alikemea Mdhamini huyo.

Alisema kuwa, Wizara ya Elimu haikubaliani na kumuhukumu mtoto kwa sababu mzazi wake hakulipa fedha na hakuna skuli ambayo wataibani ikifanya hivyo na kuiachia salama, bali itachukuliwa hatua stahiki kwani pia inasababisha kumuathiri mtoto kisaikolojia.

Aliwasisitiza makatibu wa Kamati za skuli kuendelea kusimamia hayo kwa kutengeneza kamati ndogo ndogo, ikiwemo ya fedha, itakayosimamia kambi, ya kusimamia maadili ili walimu na wanafunzi wawe na muda mzuri wa kutekeleza majukumu yao ya kielimu.

                                         MWISHO.   

 

Comments

BLOG'S VISITORS

DAKTARI MWENGINE CHAKE CHAKE KULA SIKUKUU POLISI, NI KWA TUHUMA ZA KUMBAKA MGONJWA WAKE

NA WAANDISHI WETU, PEMBA::: DAKTARI anaetoa huduma kwa wagonjwa kituo cha afya cha serikali cha  Gombani wilaya ya Chake Chake Pemba, Is-haka Rashid Hadid, anaendelea kushikiliwa na Jeshi la Polisi Mkoa wa kaskazini Pemba, akituhumiwa kumtorosha na kisha kumbaka mtoto wa mwenye umri wa miaka 16, mkaazi wa Gombani. Daktari huyo miaka 35 ni mkaazi wa Kangagani Wilaya ya Wete mkoani humo, ambapo anadaiwa alimchukua mtoto huyo kutoka kwa rafiki yake, na kumpeleka kwenye nyumba anayoishi eneo la Kangagani. Mtoto aliefanyiwa kitendo hicho alisema kuwa, April 21 mwaka huu alikwenda kituo cha afya Gombani, kwa ajili ya matibabu na baada ya kupatiwa huduma na daktari huyo, alimuomba nambari yake ya simu. Alisema ilipofika usiku, walikuwa wanawasiliana kupitia ujumbe mfupi (sms) kwa lengo la kwenda kuchukua dawa nyingine ambazo kwa mchana huo alizikosa hospitalini hapo. "Nilikwenda hospitali kutibiwa, baada ya kufanya mapele katika sehemu zangu za siri, lakini akaniambia mpaka aje da...

HII KALI MBUNGE ASIYA AMKOGESHA MWANANCHI HADHARANI KISA HICHI HAPA......

  NA HAJI NASSOR, PEMBA MBUNGE wa viti maalum nafasi za wanawake mkoa wa kaskazini Pemba Asiya Sharif Omar, amewataka wananchi wa kijiji cha taifu, shehia ya Kinyasini jimbo la Gando wilaya ya Wete Pemba, kuyalinda miundombinu ya maji safi na salama, ili yawe endelevu kwao. Kauli hiyo ameitoa wakati alipokuwa akizungumza na mwandishi wa habari hizi, mara baada ya kuwasili kijijini humo, na kumkogesha mwananchi mmoja kama ishara ya uzinduzi wa mradi wa maji safi na salama, ulioasisiwa na mbunge wa Jimbo la Gando. Alisema, hawana mbadala kwa sasa bali ni kuilinda miundombinu ya huduma hiyo, hasa baada ya mbunge wa wao Salim Mussa Omar, kuwarejeshea huduma hiyo. Alieleza kuwa, inafahamika kuwa kwa miaka 14 waliikosa huduma hiyo hasa kwa vile viongozi waliokuwepo hawakujali kuwatatulia tatizo hilo, hadi juzi ilipofanywa na mbunge wao. “Baada ya huduma hii sasa kurejeshwa na mbunge wa jimbo la Gando, kazi iliyobakia kwenu wananchi ni kila mmoja kuwa mlinzi wa miundombinu hii,’...

'MKAPA' NA WENZAKE PEMBA WALAZWA RUMANDE

  NA HAJI NASSOR, PEMBA@@@@ MAHKAMA kuu Zanzibar kisiwani Pemba, chini ya Jaji Ibrahim Mzee Ibrahim, imewapeleka rumande watumuhimwa wanne wanaokabiliwa na tuhuma za kuua kwa makusudi, akiwemo Ali Mussa Omar ‘ Mkapa’ mkaazi wa Wawi wilaya ya Chake chake Pemba. Watuhumiwa wengine walioanza maisha mapya ya rumande ni mtuhumiwa Yassir Mohamed Juma miaka 23, Anuwari Mussa Omar miaka 30 pamoja na mtuhumiwa Yassir Mussa Omar ‘ Makababu ’ miaka 29, wote wakaazi wa shehia ya Wawi, wilaya ya Chake chake Pemba. Awali watuhumiwa hao waliwasili mahakamani hapo, kwa mara ya kwanza, kwa ajili ya kusomewa tuhma zinazowakabili za kumuua kwa maksudi Said Seif Kombo. Ilidaiwa mahakamani hapo na Mwendesha Mashtaka kutoka Ofisi ya Mkurugenzi wa Mashataka Seif Mohamed Khamis akiambatana na mwenzake Mussa Khamis Ali kuwa, watuhumiwa hao kwa pamoja wanadaia kufanya mauwaji hayo kwa maksudi. Ilidai kuwa, watuhumiwa wote kwa pamoja, walitenda kosa hilo Oktoba 16, mwaka huu, baina ya saa 7:00 m...

TUHMA ZA DAKTARI PEMBA KUCHIWA HURU: POLISI KASKAZINI KUTOA TAARIFA RASMI LEO

  NA HAJI NASSOR, PEMBA KAMANDA wa Polisi mkoa wa kaskazini Pemba, Juma Saad Khamis, amesema leo Mei 9, mwaka huu atatoa taarifa rasmi, juu ya kuendelea kumshikilia au kumpa dhamana ya Polisi, daktari wa Kituo cha Afya Gombani Is-haka Rashid Hadid, anayetuhumiwa kwa ubakaji. Alisema, kwa vile alikuwa katika mapumziko mafupi, haelewi jambo lolote linaloendelea kwa mtuhumiwa huyo, juu ya kuendelea kushikiliwa kwake kituoni hapo. Alieleza kuwa, leo Mei 6 (jana), hajapata taarifa za ndani za mtuhumiwa, huyo na kuwataka wananchi na wanaharakati, wasubirie hadi Jumatatu ijayo. Akizungumza na waandishi wa habari kwa nyakati tofauti Kamanda huyo, alisema hana taarifa zozote za kupewa dhamana mtuhumiwa ndani ya kituo chake cha Polisi au kuendelea kuwepo. ‘’Ilikuwa mimi sipo kazini kwa muda, kuanzia anakamatwa hadi anafikishwa Polisi, kwa sasa siwezi kueleza jambo lolote kwa mtuhumiwa huyo, hadi Jumatatu,’’alieleza. Aidha Kamanda huyo alieleza kuwa, kwa sasa hawezi kutoa uf...

MADAKTARI KUTOKA CHINA WAOKOA MAISHA YA MTOTO PEMBA

  HABIBA ZARALI, PEMBA TIMU ya 32 ya madaktari wa kichina katika hospitali ya Abdalla Mzee Mkoani wamefanikiwa kufanya upasuaji mkubwa wa mtoto mwenye umri wa miaka 15 mkaazi wa Chole Kengeja, baada ya kuchomwa na jiti sehemu ya njia zake za mfumo wa uzazi. Mtoto huyo ambae alianguka hivi karibuni katika mti na baadae kuchomwa na jiti hilo na kumsababishia kutokwa na damu nyingi katika sehemu ya nyonga, alifanyiwa upasuaji uliodumu kwa muda wa saa tatu na   kuokolewa maisha yake. Akizungumza mara baada ya operesheni huo kiongozi wa timu hiyo Dr Jiang Jinhua, alisema mara baada ya mtoto huyo kufikishwa hospitalini hapo na kufanyiwa vipimo na kuonekana   ilibidi apatiwe rufaa ya kwenda katika hospitali nzuri yenye kutibu tatizo lake huko nchini Kuwado ambapo haikuwezekana kutokana na hali ya umaskini wa f amilia ya mtoto huyo . Alisema timu ya madaktari hao itaendelea kutowa huduma za matibabu   kwa wananchi kisiwani humo,   ili kuwaondolea gharama ya kuta...