Skip to main content

WAZIRI AZINDUA UVUNAJI ZAO LA KARAFUU PEMBA, AWAPA NENO WATOROSHAJI, WIZI

 

 

 


 

 SAID ABDULL-RAMAN, PEMBA

 

WAKULIMA wa zao la Karafuu Kisiwani Pemba, wametakiwa kuvuna zao hilo, lililopevuka na kuacha kuvuna karafuu changa, kwani kufanya hivyo, ni kupoteza ubora wa zao hilo.

 

Hayo yalielezwa na Waziri wa Biashara Maendeleo ya Viwanda Zanzibar Omar Said Shaaban, wakati akizindua zoezi la uvunaji wa zao hilo katika mashamba ya mikarafuu Kichunjuu Mtambili wilaya ya Mkoani Pemba.

 

Alisema, kuwa endapo wakulima wa zao hilo wataweza kuvuna karafuu zinazostahiki, wataweza kupata faida kubwa kwao na kwa Serikali, kwa kule kuliongezea thamano zao hilo.

 

Waziri Shaaban alifahamisha kuwa, kwa mwaka huu Serikali imedhamiria kurudisha hadhi ya zao la karafuu ya Zanzibar, kuwa na ubora wake, ambapo tayari Shirika la biashara la taifa ZSTC limeshakaa na wadau wake.

 

"Mashine ambazo tumeziweka katika vituo vyetu vya kununulia karafuu ziko salama, na zimethibishwa na kuthibitika kwamba zina ubora na wala haziharibu karafuu, kama inavyodaiwa na baadhi ya watu," alisema Waziri huyo.

 

"Katika suala la ubora wa karafuu, hili ni kutokana ushughulikiaji wake kuanzia inapovunwa, uanikaji wake lakini hata matunzo yake, hii ndio njia itakayosaidia kupata karafuu mzuri," alieleza.

 

Sambamba na hayo, alieleza kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, inatambua changamoto zote zilizomo kwenye kilimo cha zap hilo, hivyo Serikali niajadili changamoto hizo na kuhakikisha inahuwisha kilimo hicho.

 

Mapema Waziri Shaaban, aliwatahadharisha wananchi wote ambao wanajushughulisha na wizi wa karafuu na kusema kuwa kwa sasa muarubaini wa tatizo hilo limeshapatikana.

 

"Kwa wale ambao wanajishughulisha na utoroshaji wa Karafuu,(magendo) mbinu zao tumeshazijua, tutaendelea kushirikiana na vikosi vyetu vya ulinzi na usalama ili kuona vitendo hivyo vinathibitiwa," alisema Waziri Shaaban.

 




Nae mkulima wa zao hilo, Hafidh Makame Haji wa Michenzani Mkoani, alisema kuwa, kwa mwaka huu mauzo ya karafuu ni tofauti na miaka iliyopita, hasa katika sehemu ya kupasishia karafuu kutokana na uwekwaji wa mashine maalum.

 

"Kwa wakulima wenzangu tuendelee kuchukuwa hatua za makusudi za kuweka mazingira safi katika mashamba yetu ili tuweze kupata mavuno mazuri," alisema Hafidh.




Comments