Skip to main content

MICHEWENI WATAKA UTAMADUNI WA JANDO UENDEE ILI WANAUME WAWE WAKAKAMAVU, KUEPUKA UGONJWA WA MISHIPA


 


NA ZUHURA JUMA, PEMBA@@@@

 

JANDO ni kumkata mtoto au kumfanyia tohara kwa kuondosha gozi la juu kwenye uume.

 

Jando au tohara ni kitu cha lazima kwa wanaume hasa jamii ya waislamu kwani humuweka katika hali ya usafi na usalama katika afya yake.

 

Pamoja na kuwa jando/ tohara ni lazima kwa vijana wa kiume na watoto wa kiume, lakini baadhi ya vijiji walifanya kama utamaduni maalumu, hasa pale walipoutekeleza kwa muda maalumu na kuwakusanya pamoja huku zikiambatana na sherehe.

 

Na kila sehemu walikuwa na utaratibu wao wa kuwatia watoto wao wa kiume jandoni, ambao ulikuwa ni utamaduni maalumu wanaojiwekea.

 

Wanajamii wa vijiji vya Micheweni Pemba, ni miongoni mwa watu ambao, jando walilifanya kama utamaduni kwa kuwakusanya watoto wa kiume na kuwaweka sehemu moja, huku kukifanyika shughuli mbali mbali za kimila zilizoambatana na sherehe baada ya kupona kidonda.

 

Hamad Mbwana Shaame mkaazi wa shehia ya Majenzi Wilaya ya Micheweni anaelezea jando mwanzo ilikuwa kama sherehe, ingawa sasa utamaduni huo umepotea katika jamii yao.

 

Walikuwa wanasubiriwa watoto wa kiume mpaka wafikie miaka kumi na kuendelea, ndipo wazee katika mtaa ule hushauriana siku ambayo watawatia jandoni.

 

"Ilikuwa wanaliita ‘kumbi’ watu wa hapa kwetu Micheweni, hivyo walikuwa wanawakusanya watoto angalau kumi na kuwatia kumbini kwa kusubiri kufanyiwa jando," anasema.

 

Hamad anaelezea, walikuwa wanajengewa uwa wa makuti (boma iliyozungushwa makuti) na wanakaa humo wiki mbili mpaka tatu, huku wazazi wa watoto hao wakitayarisha chakula cha kila siku na kuwapelekea kumbini hapo.

 

Wakati anapokwenda mzazi kupeleka chakula, anakuwa na wimbo maalumu anaoimba na wale watoto walimo kumbini wanaitikia.

 

Mkaazi huyo wa Majenzi aliuwimba wimbo huo kuwa ni... ‘cha jumbe... na watoto wanaitikia... too na kije too...’ ambapo huurejea takribani mara tatu.

 

"Ilikuwa chakula kinakusanywa, baadae mzazi mmoja ambae anahusika na wale watoto walimo kumbini anakwenda kukipeleka," anaeleza.

 

Baada ya kupona watoto wale, inapigwa ngoma inayoitwa 'unjuguu' huku wakiwa wamevishwa nguo nzuri na baadae kutolewa kila mmoja kupelekwa kwao.

 

"Na hawa vijana wa kiume na wao tulikuwa tunawaita wari kama vile vijana wa kike kwa sababu na wao ni wapya," anahadithia.

 


Saada Sheha Ali anasema, wazee zamani walikuwa wanafanya hivyo ili watoto wao wajifunze mambo mbali mbali kwa sababu kwenye kumbi hiyo, walikuwa wanaelimishwa na kupewa nasaha ambazo zinawasaidia katika maisha yao ya kila siku.

 

Vijana hao walikuwa wavumilivu kutokana na kuwa wanapotiwa jandoni hawakuwahi kuekewa ganzi, hivyo yale maumivu waliyoyapata yaliwajenga ukakamavu na uvumilivu.

 

"Ndio maana wazee wetu zamani wanapooa wanakaa na wake zao mpaka mmoja anakufa lakini hawaachani, ingawa sasa hivi mtoto anajikuta yuko vizuri tu hajui uchungu, hivyo uvumilivu umekuwa mdogo," anafahamisha.

 

Akitaja vifaa ambavyo vilitumiwa kwa ajili ya kufanyiwa jando kuwa ni visu ambavyo vilikuwa vikifuliwa na kunolewa kwa vinoo.

 

Aliekuwa akiwatahiri (jando) watoto hao, ni mwanaume ambae aliitwa 'mngariba' na walikuwa ni maalumu.

 

Saada Said Kombo ambae ni mkaazi wa Micheweni anasema kumtia mtoto jandoni, wao walikuwa wanaita ‘kukuwaza’.

 

Anafahamisha, mzazi anapompeleka mwanawe kwa mngariba, humwambia kuwa...tayari mtoto wake anataka kukuwazwa, hivyo anapangiwa muda wa kumpeleka kukatwa huku wakikusanywa pamoja na wenzake.

 

"Wanakuwa watoto wengi, hivyo anachukuliwa mmoja mmoja na kuwekwa kwenye kinu na baadae linavunjwa dafu halafu ndio anakatwa," anaeleza.

 

Baada ya kumaliza kukatwa, ananyweshwa maji ya dafu pale pale ili apate kukojoa haraka, kwani wengine wanapokatwa hukaa mda mrefu hawajapata haja ndogo, jambo ambalo linawaletea maumivu.

 

Anafafanua, zamani walikuwa wakikatwa watu wazima sio watoto wadogo kama siku hizi, ambapo kila mzazi alikuwa anapeleka visu na kulazwa kwenye maji kuanzia usiku mpaka asubuhi, ndipo hutolewa kwa ajili ya kufanyiwa kazi ya kukatia.

 

"Tulikuwa tunawalipa wangariba wetu, lakini kipindi hicho tuliwapa kila mzazi shilingi mia tatu tu lakini ilikuwa ni pesa kubwa," anafafanua.

 

Sharifu Massoud Hamad analielezea jando lilivyokuwa likifanyika zamani kuwa, watoto wa kiume walikuwa wanaachwa mpaka wanakuwa wakubwa, kwani waliamini wanapokatwa wadogo kuna baadhi ya vitu vinaweza kubakia (magozi).

 

Mama huyo anahadithia kuwa, utamaduni huo umeondoka na sasa mtoto anakatwa akiwa ndani ya siku arubaini baada ya kuzaliwa.

 

"Zamani ilikuwa wanaachwa mpaka wanakuwa balekh, wanakusanywa pamoja na kufanyiwa tohara/jando, wanajengewa uwa uliozungushwa makuti au majani ya mgomba makavu," anahadithia mama huyo.

 

"Kulikuwa na nyimbo wanaimbiwa na wao wanaitikia lakini ikiwa watanyamaza kimya chakula kinarudishwa, kwani ilikuwa mpelekaji chakula hawezi kuingia ndani humo bila ya kuitikiwa," anaeleza.

 

Anasema, lengo la kuimbiwa nyimbo hiyo lilikuwa ni kwamba wajifunike nguo kwani walikuwa wanakaa bila nguo, ili wapate upepo na kidonda kikauke haraka.

 

Sheha wa shehia ya Majenzi Faki Kombo Hamad anasema, kulikuwa na mzee ambae kwa hapo kijijini kwao na vijiji jirani walimtumia kwa kuwakata watoto wa kiume.

 

"Tulikuwa tunawekwa pamoja vijana wapatao 20, baadae anachaguliwa mmoja anaitwa kiranja (kiongozi), sasa huyu huchukuliwa mwanzo kwenda kukatwa huku tunamuona," anaeleza sheha huyo.

 

Walikuwa wanawekwa kwenye kinu na baadae wanakuja kaka zao ambao wameshakuwa watu wazima ili kuwafumba macho, hivyo hukaa hapo kumbini mpaka watakapopona ndipo hupelekwa nyumbani kwao.

 

FAIDA YA UTAMADUNI WA JANDO

 

Hamad Mbwana yeye anasema, watu walijuana na kusaidiana sana kwani ikiwa mzazi mmoja hana cha kumlisha mtoto wake, basi anachangiwa na wenzake mpaka anaondoka kumbini.

 

Anasema Sharifu Massoud, watoto hao walikuwa wanakatwa bila ya ganzi, hivyo ilisaidia kwa wale wenye matatizo ya mishipa kuondoka moja kwa moja tofauti na sasa.

 

"Mtoto ikiwa ana mshipa akichomwa sindano tu unakimbia kwa muda ule, likitoka ganzi tu na mshipa unarudi pale pale," anafafanua.

 

"Mwanangu alikuwa na mshipa, hospitali zote nilizimaliza lakini hakupona na alikuwa akivimba, lakini niliambiwa na daktari moja kuwa nimpeleke akakatwe kwa hao wangariba bila ya ganzi, nashkuru sana kwa sababu mpaka leo hii mshipa ule haukuja tena, ulipotea kabisa" anahadithia mama huyo.

 

Muuguzi wa kituo cha afya Maziwa Ng’ombe Wilaya ya Micheweni Aisha Omar Salum anasema, jando ni muhimu kwani inamuepusha mwanaume na magonjwa ya kuambukiza (S.T.I)

 

‘’Unapofanyiwa tohara inamzuia mwanaume kupata maradhi ya kujamiiana kutokana na kuwa uchafua haubakii baada ya kufanya tendo la ndoa’’, anaelezea daktari huyo.

 

ATHARI ZINAZOWEZA KUJITOKEZA IWAPO WATOTO HAWAKUFANYIWA TOHARA

 

Muuguzi huyo anasema, athari inayojitokeza iwapo mwanaume hakufanyiwa tohara au kutiwa jandoni, anaweza kupata maradhi ya kujamiiana, kwani anapofanya tendo la ndoa uchafu unabaki ndani yake.

 

Anasema, mwanaume anapofanyiwa tohara huwa anakatwa gozi katika sehemu ndogo ya uume wake, hivyo ikiwa halikutolewa, yale maji maji baada ya kujamiiana yanabakia jambo ambalo ni hatari kwa afya yake.

 

‘’Anaweza hata kupata saratani kwenye tenzi dume kutokana na uchafu huo ambao hubakia kila anapojamiiana’’, anafafanua.

 

NINI KIFANYIKE?

 

Hamad Mbwana anasema, mambo mengine yanapaswa kubakia, pamoja na kuwa jamii inaenda na utandawazi lakini jando la pamoja linahitaji kurudishwa.

 

"Hata kama ataitwa daktari kuwatahiri lakini wawekwe kama zamani, hii itasaidia sana kujuana na kushirikiana," anaeleza.

 

Dk. Aisha anasema, ni vyema kuendelea kufanyiwa jando watoto wakiwa wadogo ili wakikua wajione tayari wameshafanyiwa, kwani wanapofanyiwa wakubwa inawaathiri kisaikolojia.

 

‘’Kwa vile inakuwa ni wakubwa tayari, wanajiona kama wanadhalilishwa, hivyo wanaathirika kisaikolojia, kwa hiyo kutiwa jandoni wakiwa wadogo ’’ anafahamisha.

 

                                                           MWISHO.

 

 

Comments

BLOG'S VISITORS

DAKTARI MWENGINE CHAKE CHAKE KULA SIKUKUU POLISI, NI KWA TUHUMA ZA KUMBAKA MGONJWA WAKE

NA WAANDISHI WETU, PEMBA::: DAKTARI anaetoa huduma kwa wagonjwa kituo cha afya cha serikali cha  Gombani wilaya ya Chake Chake Pemba, Is-haka Rashid Hadid, anaendelea kushikiliwa na Jeshi la Polisi Mkoa wa kaskazini Pemba, akituhumiwa kumtorosha na kisha kumbaka mtoto wa mwenye umri wa miaka 16, mkaazi wa Gombani. Daktari huyo miaka 35 ni mkaazi wa Kangagani Wilaya ya Wete mkoani humo, ambapo anadaiwa alimchukua mtoto huyo kutoka kwa rafiki yake, na kumpeleka kwenye nyumba anayoishi eneo la Kangagani. Mtoto aliefanyiwa kitendo hicho alisema kuwa, April 21 mwaka huu alikwenda kituo cha afya Gombani, kwa ajili ya matibabu na baada ya kupatiwa huduma na daktari huyo, alimuomba nambari yake ya simu. Alisema ilipofika usiku, walikuwa wanawasiliana kupitia ujumbe mfupi (sms) kwa lengo la kwenda kuchukua dawa nyingine ambazo kwa mchana huo alizikosa hospitalini hapo. "Nilikwenda hospitali kutibiwa, baada ya kufanya mapele katika sehemu zangu za siri, lakini akaniambia mpaka aje da...

HII KALI MBUNGE ASIYA AMKOGESHA MWANANCHI HADHARANI KISA HICHI HAPA......

  NA HAJI NASSOR, PEMBA MBUNGE wa viti maalum nafasi za wanawake mkoa wa kaskazini Pemba Asiya Sharif Omar, amewataka wananchi wa kijiji cha taifu, shehia ya Kinyasini jimbo la Gando wilaya ya Wete Pemba, kuyalinda miundombinu ya maji safi na salama, ili yawe endelevu kwao. Kauli hiyo ameitoa wakati alipokuwa akizungumza na mwandishi wa habari hizi, mara baada ya kuwasili kijijini humo, na kumkogesha mwananchi mmoja kama ishara ya uzinduzi wa mradi wa maji safi na salama, ulioasisiwa na mbunge wa Jimbo la Gando. Alisema, hawana mbadala kwa sasa bali ni kuilinda miundombinu ya huduma hiyo, hasa baada ya mbunge wa wao Salim Mussa Omar, kuwarejeshea huduma hiyo. Alieleza kuwa, inafahamika kuwa kwa miaka 14 waliikosa huduma hiyo hasa kwa vile viongozi waliokuwepo hawakujali kuwatatulia tatizo hilo, hadi juzi ilipofanywa na mbunge wao. “Baada ya huduma hii sasa kurejeshwa na mbunge wa jimbo la Gando, kazi iliyobakia kwenu wananchi ni kila mmoja kuwa mlinzi wa miundombinu hii,’...

'MKAPA' NA WENZAKE PEMBA WALAZWA RUMANDE

  NA HAJI NASSOR, PEMBA@@@@ MAHKAMA kuu Zanzibar kisiwani Pemba, chini ya Jaji Ibrahim Mzee Ibrahim, imewapeleka rumande watumuhimwa wanne wanaokabiliwa na tuhuma za kuua kwa makusudi, akiwemo Ali Mussa Omar ‘ Mkapa’ mkaazi wa Wawi wilaya ya Chake chake Pemba. Watuhumiwa wengine walioanza maisha mapya ya rumande ni mtuhumiwa Yassir Mohamed Juma miaka 23, Anuwari Mussa Omar miaka 30 pamoja na mtuhumiwa Yassir Mussa Omar ‘ Makababu ’ miaka 29, wote wakaazi wa shehia ya Wawi, wilaya ya Chake chake Pemba. Awali watuhumiwa hao waliwasili mahakamani hapo, kwa mara ya kwanza, kwa ajili ya kusomewa tuhma zinazowakabili za kumuua kwa maksudi Said Seif Kombo. Ilidaiwa mahakamani hapo na Mwendesha Mashtaka kutoka Ofisi ya Mkurugenzi wa Mashataka Seif Mohamed Khamis akiambatana na mwenzake Mussa Khamis Ali kuwa, watuhumiwa hao kwa pamoja wanadaia kufanya mauwaji hayo kwa maksudi. Ilidai kuwa, watuhumiwa wote kwa pamoja, walitenda kosa hilo Oktoba 16, mwaka huu, baina ya saa 7:00 m...

TUHMA ZA DAKTARI PEMBA KUCHIWA HURU: POLISI KASKAZINI KUTOA TAARIFA RASMI LEO

  NA HAJI NASSOR, PEMBA KAMANDA wa Polisi mkoa wa kaskazini Pemba, Juma Saad Khamis, amesema leo Mei 9, mwaka huu atatoa taarifa rasmi, juu ya kuendelea kumshikilia au kumpa dhamana ya Polisi, daktari wa Kituo cha Afya Gombani Is-haka Rashid Hadid, anayetuhumiwa kwa ubakaji. Alisema, kwa vile alikuwa katika mapumziko mafupi, haelewi jambo lolote linaloendelea kwa mtuhumiwa huyo, juu ya kuendelea kushikiliwa kwake kituoni hapo. Alieleza kuwa, leo Mei 6 (jana), hajapata taarifa za ndani za mtuhumiwa, huyo na kuwataka wananchi na wanaharakati, wasubirie hadi Jumatatu ijayo. Akizungumza na waandishi wa habari kwa nyakati tofauti Kamanda huyo, alisema hana taarifa zozote za kupewa dhamana mtuhumiwa ndani ya kituo chake cha Polisi au kuendelea kuwepo. ‘’Ilikuwa mimi sipo kazini kwa muda, kuanzia anakamatwa hadi anafikishwa Polisi, kwa sasa siwezi kueleza jambo lolote kwa mtuhumiwa huyo, hadi Jumatatu,’’alieleza. Aidha Kamanda huyo alieleza kuwa, kwa sasa hawezi kutoa uf...

MADAKTARI KUTOKA CHINA WAOKOA MAISHA YA MTOTO PEMBA

  HABIBA ZARALI, PEMBA TIMU ya 32 ya madaktari wa kichina katika hospitali ya Abdalla Mzee Mkoani wamefanikiwa kufanya upasuaji mkubwa wa mtoto mwenye umri wa miaka 15 mkaazi wa Chole Kengeja, baada ya kuchomwa na jiti sehemu ya njia zake za mfumo wa uzazi. Mtoto huyo ambae alianguka hivi karibuni katika mti na baadae kuchomwa na jiti hilo na kumsababishia kutokwa na damu nyingi katika sehemu ya nyonga, alifanyiwa upasuaji uliodumu kwa muda wa saa tatu na   kuokolewa maisha yake. Akizungumza mara baada ya operesheni huo kiongozi wa timu hiyo Dr Jiang Jinhua, alisema mara baada ya mtoto huyo kufikishwa hospitalini hapo na kufanyiwa vipimo na kuonekana   ilibidi apatiwe rufaa ya kwenda katika hospitali nzuri yenye kutibu tatizo lake huko nchini Kuwado ambapo haikuwezekana kutokana na hali ya umaskini wa f amilia ya mtoto huyo . Alisema timu ya madaktari hao itaendelea kutowa huduma za matibabu   kwa wananchi kisiwani humo,   ili kuwaondolea gharama ya kuta...