Skip to main content

WAANDIKISHENI WATOTO WENYE ULEMAVU SKULI "MDHAMINI ELIMU"

 


NA MOZA SHAABAN, PEMBA

WAZAZI na walezi wenye watoto wenye ulemavu wametakiwa kuwaandikisha watoto hao skuli kwa mwaka wa masomo unaotarajiwa kuanza 2026, ili kuhakikisha upatikanaji wa haki ya msingi ya elimu kwa watoto hao.

Wito huo umetolewa na Afisa mdhamini Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Amali  Pemba Mohamed Nassor Salim wakati akizungumza na mwandishi wa habari hizi, alisema zoezi la uandikishaji wanafunzi wapya kwa mwaka wa masomo 2026 linaendelea kwa watoto wote waliofikia umri wakiwemo wenye ulemavu.

Alisema wakati umefika kwa wazazi, walezi jamii na serikali za shehia kuhakikisha watoto wenye ulemavu wanapata haki yao ya msingi ya elimu, kwa kuhakikisha wanandikishwa skuli bila kujali mahala wanapoishi au aina ya ulemavu walionao.

Aliongeza serikali kupitia wizara ya elimu imeandaa mazingira rafiki kwa watoto wenye ulemavu ambao wanaishi katika mazingira magumu, kwa kuwajengea skuli maalumu inayotoa elimu mjumuisho ili kuhakikisha wanapata haki yao ya msingi ya elimu kama ilivyo kwa watoto wengine.

" Ili kuhakikisha kila mtoto wa Zanzibar anapata haki yake ya msingi ya elimu kama zinavyoeleza sheria na sera, serikali inaendelea  kuweka mazingira rafiki kwa watoto wote wakiwemo wenye ulemavu, na tumejenga skuli ya elimu mjumuisho na tunaendelea kusajili wanafunzi wenye sifa, hivyo ni muhimu jamii kuunga mkono hili  kwa kuhakikisha watoto hao wanaandikishwa, " alieleza.

Alisema kwa mwaka wa masomo 2026 ambao uandikishaji wake unaendelea, skuli ya elimu mjumuisho iliopo pujini kwa mara ya kwanza itakua na darasa la elimu ya maandalizi, huku lengo likiwa ni kuhakikisha watoto wote wanapata haki sawa ya elimu.

Aidha alisema kua, ili kuhakikisha jamii inakua na muamko zaidi kuhusu ulazima wa upatikanaji elimu kwa watoto wenye ulemavu, wizara imeanzisha kampeni ya kushajihisha jamii kulitimiza hilo kwa kushirikiana na viongozi wa shehia.

Alisema ni vyema wazazi kitumia fursa hiyo ya uwepo wa skuli ya elimu mjumuisho ya Pujini Chake chake Pemba kwa kuwaandikisha watoto wenye ulemavu, kwani kuna miundombinu rafiki kwa ajili ya kufundishia na kujifunzia.

Nae Mwalimu wa wanafunzi wenye ulemavu wa uoni na uoni hafifu kutoka skuli ya Elimu  Mjumuisho Pujini  Hanifa Abeid Ali alisema, kuelekea mwaka wa masomo 2026 wameshasajili wanafunzi wapya 30 ambao wanaulemavu wa aina mbali mbali.

Akitoa wito kwa wazazi wenye watoto wenye ulemavu ambao hawajawaandikisha na umri umesharuhusu mwalimu huyo  alisema, ni vyema kuwaandikisha watoto wao skuli ili kupata haki yao ya msingi ya elimu, kwani ulemavu si sababu ya mtoto kutosoma.

Nae mwalimu Anipae Amiri Manallah kutoka skuli hio  aliiomba wizara ya elimu kuendelea kuboresha miundombinu ya skuli hiyo kwa kuongeza vifaa vya kujifunzia na kufundishia pamoja na waalimu ili lengo la utoaji elimu bora liweze kufikiwa.

Skuli ya elimu Mjumuisho Pujini imajumla ya wanafunzi 76 wenye ulemavu wa aina tano, ukiwemo ulemavu wa uoni /uoni hafifu, Uziwi, Viungo, Albino na Matamshi, na hadi sasa inawanafunzi wa darasa la kwanza hadi la tano.

Aidha kwa mujibu wa sera ya elimu ya Zanzibar inasema wizara ya Elimu itahakikisha haki na fursa za elimu inazotoa kwa wazanzibari wotewote,  zinatolewa kwa misingi ile ile kwa watu wenye ulemavu.

                                                                     MWISHO

Comments