Skip to main content

SHEHA CHUMBAGENI LEO KUWAONGOZA WANANCHI KIDUTANI UPITISHWAJI KANUNI ZA KIJIJI

 



NA HAJI NASSOR, PEMBA@@@@

SHEHA wa Chumbageni wilaya ya Mkoani, Mgeni Othman Shaame, jioni ya leo anatarajiwa kuwaongoza wanachi wa kijiji cha Kidutani, kuzipitisha sheria ndogondogo, zitakazowaongoza wananchi hao, ili kujenga tabia njema.

Akizungumza na mwandishi wa habari hizi, Katibu wa kamati ya elimu na maadali ya kijiji hicho Machano Ali Makame, alisema jioni ya leo, kijijini hapo watakuwa na ugeni wa shehia yao.

Alisema kuwa, sheha huyo pamoja na ujumbe wake akiwemo askari wa shehia, watakutana na wananchi hao, na kuzijadili kwa mara ya mwisho kanuni, hizo kabla ya kuzipitisha rasmi.

Alieleza kuwa, kijiji hicho kimeamua kuanzisha kanuni hizo, ili kuwasawaidia vijana kuwaelekeza kwenye maadili mema, ili wawe raia bora wa taifa hili.

‘’Ni kweli jioni ya leo, Sheha wa Chumbageni ataungana na wananchi wa kijiji cha Kiduatani, ili kuzipitisha kanuni, ambazo zilianzishwa na wananchi wenyewe,’’alisema.

Mwenyekiti wa kamati hiyo Mwalimu Saleh Abdalla Mohamed, alisema moja ya kanuni ambazo zitarajiwa kupitishwa, ni kusitisha muda wa kuranda ovyo mitaani hapo nyakati za usiku.

Alieleza kuwa nyingine ni kupiga marufuku matumizi ya sigara kwa watoto, pombe, upigaji ngoma, wizi, uvaaji wa nguo za mbano, ukataji nywele usio wa maadili.

‘’Kanuni nyingine ambayo jioni ya leo sheha atazikagua na kuzipitisha pamoja na wananchi wenyewe, ni uvaaji za suruali juu ya magoti kwa wanaume, vigenge hatarishi na kuwarejesha masomoni walioacha,’’alifafanua.

Kwa upande wake Katib wa sheha wa shehia  hiyo, Abdalla Salim Juma, alisema maandalizi yote kwa ajili ya mkutano huo wa jioni ya leo, yameshakamilika.

Alisema, tayari wajumbe wa sheha, askari wa shehia na sheha mwenyewe, wameshaarifiwa kwa ajili ya kuhudhuria mkutano huo wa leo.

‘’Ni kweli wananchi wenzetu wa kijiji cha Kidutani, waliamua kuanzisha kanuni, ambazo leo uongozi wa shehia ya Chumbageni, unakwenda kukutana na wananchi na kuzipitisha kwa pamoja,’’alifafanua.

Baadhi ya wananchi wa Kidutani, akiwemo Juma Abassi Ali, alisema wanatamani haraka mkutano huo, ufanyike na kanuni hizo, zianze kazi.

Nae Time Pandu Makame, alisema kijiji hicho ingawa kina wananchi kidogo, lakini kimekuwa kikitumbukia kwenye wizi wa mifugo, utoro wa wanafunzi pamoja na tabia nyingine chafu.

Hivi karibuni Mkuu wa wilaya ya Mkoani Miza Hassan Faki, aliwataka wananchi, kuendelea kuzifufua polisi jamii, ambazo huwa ni masaada mkubwa wa kuzuia uhalifu.

                Mwisho  

 

Comments