Skip to main content

'ZITUMIENI KIVITENDO SIKU ZA MWEZI MTUKUFU ZILIZOBAKIA MTAPA NEEMA’

 



NA HAJI NASSOR, PEMBA@@@@

WAUMINI wa dini ya kiislamu kisiwani Pemba, wametakiwa kuzitumia kimipango, siku zilizobakia za mwezi mtukufu wa Ramadhan, ili kujikurubisha kwa Muumba na kupata fadhila zake.

Hayo yalielezwa na Msaidizi wa Katibu wa ofisi ya Mufti Zanzibar, ofisi ya Pemba Sheikh Said Ahmad Mohamed, wakati alipokuwa akitoa shukran kwa waumini, walioshiriki sawala wa Ijumaa, na Rais wa Zanzibar Dk. Hussein Ali Mwinyi, Machomanne Chake chake Pemba.

Alisema, sio sahihi kuwa mwezi mtukufu wa Ramadhan umekwisha, bali siku zilizobakia zinaweza kumkomboa muumini na kupata malipo makubwa, iwapo atajipangia ratiba nzuri.

Alieleza kuwa, kwa fadhali za mwezi huu, muumini hawezi kupoteza jambo hata kwa siku moja, ikiwa ataamua kujikurubisha kwa vitendo Muumba, kama wanavyofanya baadhi yao.

Sheikh Said alieleza kuwa, siku moja katika mwezi mtukufu wa Ramadhan inathamani zaidi ya mara moja, kuliko siku nyingine, hivyo sio sahihi kuwa Ramadhan imekwisha na hakuna muda wa kufanya ibada.

‘’Kama Khatib wa swala ya Ijumaa alivyosema, kwenye hutuba zake, kuwa muda wa kufanya ibada bado upo ndani ya mwezi huu, na wala sio sahihi kuwa siku za Ramadhan zimekwisha,’’alieleza.

Katika hatua nyingine, Msaidizi huyo wa Katib wa ofisi ya Mufti Pemba sheikh Said Ahmad Mohamed, aliwataka waumini kuendelea kuombeana mema na kusaidiana miongoni mwao.

‘’Mwezi huu mtukufu hutujia sisi waumini wa dini ya kiislam mara moja kila mwaka, hivyo inatupasa kuongeza bidii ya kuombeana na kusaidiana kwa vitendo, ili kufikia malengo yetu,’’alifafanua.


Mapema Khatib wa swala ya Ijumaa katika  mskiti huo, alisema waumini hawanabudi katika suala la kuongeza bidi, katika ibada zao mbali mbali, katika mwezi mtukufu wa Ramadhan.

Alieleza kuwa, yapo malipo makubwa kwa kila muuimini anayefanya mema, ambayo Muumba ameyahidi kwa waja wake, fursa ambayo huja mara moja kila mwaka.

‘’Mwezi mtukufu wa Ramadhan ni hidaya kwa waumini wa dini ya kiislamu, kwani wema unaoutenda katika miezi mingine, malipo yake huwa ya kawaida, ingawa katika mwezi huu huongezeka,’’alieleza.

Baadhi ya waumini wa dini ya kiislamu waliohidhuria swala hiyo ya Ijumaa, waliwataka waumini wenzao, kuongeza kasi ya utendaji wa ibada na kusahau michezo isiyo na tija.

Mohamed Khamis Juma, alisema kwa siku zilizobakia sio za mtu kufanya vitendo vya anasa, kama kushirki michezo ya karata, bao na kuangalia michezo ya isiyo natija ya tv.

Omar Haji Mohamed, alisema bado kuna kasi ndogo ya waumini wa dini ya kiislamu, wanaoshiriki katika vikao vitakatifu vikiwemo vya baada ya swala ya Al-fajiri, Al-aasiri na wanaojitokeza ni wale wenye umri mkubwa pekee.

‘’Kwenye madarsa ya misikitini iwe ni baada ya swala za Alf-ajiri, Adhuhuri au ishaa wanaoonekana kwa wingi ni wazee, lakini vijana wamekuwa wakifanya shughuli nyingine mabadala,’’alieleza.

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Hussein Ali Mwinyi, alikuwa kisiwani Pemba kwa ziara ya siku mbili ya futurisho, ambapo tayari wananchi wa mikoa miwili ya kaskazini na kusini, wameshajumuika nae.

                           Mwisho

Comments