Skip to main content

JAJI IBRAHIM ATUPILIA MBALI RUFAA KESI DAWA ZA KULEVYA

 


NA MARYAM NASSOR, PEMBA @@@@       

HUKUMU ya rufaa ya dawa za kulevya inayohusisha kete 1,678 iliyowasilishwa mahakama kuu Zanzibar, kanda ya Pemba, imekataliwa na Jaji wa mahakama hiyo, Ibrahim Mzee Ibrahim, baada ya kubaini kuwa, upande wa mashtaka tokea awali, ulithibitisha kosa pasi na shaka yoyote.

Jaji Ibrahim akitoa uamuzi wa rufaa hiyo na baada ya kujiridhisha, aliamuru mshtakiwa huyo Zubeir Jerad Said wa Bopwe Pemba, kutumikia chuoa cha mafunzo, kwa muda wa miaka 10, kama alivyohukumiwa awali mahakama ya mkoa.

 Alisema kuwa, mahakama yake imeitupilia mbali rufaa hiyo, kutokana na kuwa upande wa mashtaka, ulikuwa na mashahidi ambao walitoa ushahidi wa wazi na wakuaminika, hivyo hawezi kuipindua hukumu hiyo.

 

Jaji huyo alisema kuwa, mshtakiwa alikamatwa na na dawa hizo na kupewa jina la kielelezo ‘pw3 na pw4’, ambacho ni mfuko wa dawa za kulevya aina ya heroin kete uliokuwa na 1, 678  zenye uzito wa  gramu 41.53.

 Alieleza kuwa, wakili wa utetezi Abeid Mohamed Said wakati anaomba rufaa, aliieleza mahakama sababu ya rufaa, kuwa mteja wake, hakupatiwa haki kutokana na ushahidi uliyotolewa na kumtia hatiani, haukufikia kiwango au ulichezewa.

Wakili wa utetezi alidai kuwa, ukamataji wa mteja wake, haukufuata sheria na ulikuwa kinyume na kifungu cha 35 (1) na (4) cha sheria namba7 ya mwaka 2018.

Alidai kuwa, mteja wake alikamatwa hadharani na askari waliokuwa kwenye doria, lakini hawakuita shahidi  huru hata mmoja, ili kushuhudia kitendo hicho, hivyo inaoneshaa askari Polisi hao walikuwa na nia mbaya.

“Mteja wangu alikamatwa hadharani na Polisi waliyokuwa doria, lakini baada ya kumkamata hawakuita shahidi huru ambae angeshuhudia tukio hilo,” alidai wakili huyo.

 Aidha, alidai kuwa, pia mnyororo wa kesi ulikatika, hiyo inathibitishwa na kuwa vielelezo vilivyopewa majina ya ‘pw3 na pw4’ kwani kulikuwa hakuna ushahidi wa maelezo wapi kielelezo hicho kilihifadhiwa, mara baada ya kufikishwa kituoni.

Hivyo, kwa mantiki hiyo, wakili Abeid, aliiomba mahakama hiyo, itupilie mbali  hukumu hiyo, adhabu ibatilishwe na mteja wake achiwe huru.

Akijibu, tuhuma hizo, Mwendesha mashtaka wa Serikali Juma Ali, alisema kuwa ni kweli mshtakiwa alikamatwa hadharani, ingawa ilikuwa ni usiku majira ya saa 4:00 hivyo, ilikuwa vigumu kumpata mtu huru kwa wakati huo.



Alidai kuwa, muomba rufaa huyo, ushahidi ulimtia hatiani moja kwa moja, kutokana na kuwa alikamatwa na mfuko wa kete 1,678, aliyokuwa kautia ndani ya fulana yake.

Aidha alidai kuwa, mnyonyoro wa kesi haukukatika, mara baada ya mtuhumiwa kukamatwa na kufikishwa Polisi, pamoja na kielelezo chake, alikabidhiwa askari aliyekuwepo na ilipofika asubuhi, alikabidhiwa mtunza vielelezo na kupewa namba WIR2008/2021.

Alidai, kuhusiana na kukiukwa kwa kifungu cha 35(4) cha sheria namba 7 ya mwaka 2018 alidai kuwa, kifungu hicho hakijakiukwa, kwani mara nyingine sio lazima kufuatwa kwa kifungu hicho, hasa kutokana na mtuhumiwa hakubainisha ni watu wapi wapewe taarifa, kuwa yeye yupo kituoni.

 Baada ya kuupitia ushahidi huo, Jaji Ibrahim alisema kuwa, ameupitia kwa umakini  mkubwa ushahidi huo na kujiridhisha, kwa kuona upande wa mashtaka, ulifanikiwa kuthibitisha tuhuma hizo pasi na shaka, kwani ulikuwa na nafasi nzuri ya kuwaona mashahidi katika mazingira hayo.

Kwa mantiki hiyo, rufaa hiyo imekataliwa na mshtakiwa anatakiwa kutumikia kifungo chake cha miaka 10 chuo cha mafunzo, alichohukumiwa na mahakama ya Mkoa hapo awali.

Shauri hilo lilifunguliwa Juni 16, mwaka 2021, katika mahakama ya mkoa na mshtakiwa ni Zubeir Jerad Said (30) mkaazi wa Bopwe wilaya ya Wete Pemba.

Mshitakiwa huyo, alipatikana na dawa hizo, Juni 6, mwaka 2021 eneo la Bopwe majira ya saa 4:00 usiku, ambapo bila ya halali,   alipatikana na kete 1,678 zenye uzito wa gramu 41,53.

Kupatikana na dawa za kulevya, kinyume na kifungu cha 21 (1) (d) cha sheria za Mamlaka ya kudhibiti na kupambana na dawa za kulevya Zanzibar, cha sheria namba 8 ya mwaka 2021, sheria za Zanzibar.

                                    MWISHO

  

Comments