Skip to main content

‘NILIPATA ULEMAVU KWA UCHAKAVU WA BARABARA NILIPOKUWA MJAMZITO’

 



NA HAJI NASSOR, PEMBA:

WANAWAKE wenye ulemavu wa shehia za Michungwani na Wesha wilaya ya Chake Chake Pemba, wamelezea kuchoshwa na vifo vya watoto wao wachanga na sulubu ya kujifungua njiani, wakati wanapopelekwa hospitali, kutokana na uchakavu wa muda mrefu wa barabara yao.

Walisema, imekuwa ni kawaida kwa mwaka kupata vifo vya watoto wachanga kati ya viwili hadi vitatu, au akinamama wajawazito kupata matatizo wakati wanapojifungua kutokana kuchelewa kufika hospitali za Wesha na ya Chake Chake.

Wakizungumza na waandishi wa habari wa vyombo mbali mbali, walisema barabara yao imekua ikichangia kwa asilimia 100 vifo vvya watoto wachanga na wazazi, kutokana na uchakavu wake unaokwamisha gari kupita kwa kasi.

Walisema, matatizo zaidi huwakumba katika kipindi cha mvua, kwa vile barabara hiyo, hujaa mashimo yenye kina kirefu ambayo hairuhusu hata gari ya Ng’ombe kupita kwa utulivu.



Mmoja kati ya wanawake hao mwenye ulemavu wa viungo Raya Salim Khamis, alisema suala la wao na wagonjwa wengine kwenye kijiji chao kupata misuko suko inayotokana na barabara yao, ni  jambo la kawaida hasa kila inapofika kipindi cha mvua.

Alisema yeye mwaka 1990, aliwahi kubebwa kwa gunia kutokana Birikau hadi barabara kuu, na alipofika katikati ya safari, alijifungua.

“Kwa uchakavu wa barabara yetu kwa mwaka huo, nilimpoteza mtoto wangu na mimi mwenye nilipata ulemavu wa mguu uliosababishwa na uchungu mzito, kwa kule kuchelewa kufika hospitali,’’alisema.

Nae Halima Kassim Juma mwenye ulemvu wa uziwi, alisema sasa zaidi ya miaka 40 amekuwa akishuhudia dhiki ya barabara yao, jambo ambalo hata yeye ameshawahi kupoteza mtoto, baada ya kujifungua kwake nyakati za usiku.

“Niliumwa na uchungu wa kujifungua nyakati za usiku mkubwa, na nikajifungua nyumbani na asubuhi nilipelekwa hospiatali na mwangu alifariki, baada ya kupoteza damu nyingi,’’alieleza.

Aidha mama huyo alisema, alianza yeye kubebwa kwa magunia na vitanda kupelekwa hospitali kwa kifungua, na sasa zamu imekuwa ya watoto wake wanapokuwa wajawazito.

Hata hivyo Hussan Yussuf Hamad (39) wa Tondooni shehia ya Wesha, alisema tokea afahamu yeye barabara yao imekuwa na usumbufu, jambo linalowapa dhiki hasa wajawazito na wa wagonjwa.

“Baba yangu alikuwa ni mgonjwa wa pumu na alikuwa akibebwa kwa kitanda kutoka hapa kijijini hadi barabara kuu, na sasa ni muda mrefu hadi leo, kadhia ikiendelea,’’alieleza.

Massoud Seif Massoud na Khamis Ali Said walisema dhiki ya barabara hiyo, imekuwa ni jambo la kawaida kwao, na waathirika ni wanawake hasa wenye ulemavu.

Walisema, kila Mbunge na Mwakilishi anayefika kijijini kwao, huwaahidi kuwatengenezea barabara hiyo kwa kiwango cha kifusi, ingawa baada ya kupata nafasi hizo hushindwa kutekeleza.

Naibu sheha wa shehia ya Michungwani wilaya ya Chake Chake Amina Hamad Fakih, alisema hawajakata tamaa, lakini wameanza kupata wasi wasi na utekelezaji wa ahadi za viongozi juu ya ujenzi wa barabara yao.

Alisema, amekuwa akishirikiana na sheha mwenzake wa shehia ya Wesha kupeleka taarifa kila wakati ofisi ya wilaya na baraza na mji wa Chake Chake juu ya ubovu wa barabara hiyo, ingawa bado wanaendelea kuteseka.

Mkuu wa wilaya ya Chake Chake Rashid Hadid Ali, alisema kwa sasa barabara hiyo pamoja na nyingine zilizomo wilayani humo, zimeshaingizwa kwenye mpango wa kujengwa kwa kiwango cha lami.

Alisema barabara za Birikau- Kijangwani, Wesha Ndagoni na ile ya Gombani- Michungwani zinaangalia kwa karibu na tayari hata kwenye mpango wa wilaya, zimeshawekewa mkakati wa kujengwa kwa kiwango cha lami.



“Kwa mfano kama sisi Mei 22, mwaka huu baada ya kuharibika vibaya barabara hiyo, tulishirikiana na baraza la Mji na wizara husika ya barabara, kuifanyia matengenezo na sasa iko vizuri,’’aleleza.

Hivi karibuni Afisa Mdhamini wizara ya Ujenzi, Mawasiliano na Usafirishaji Pemba Ibrahim Saleh Juma, alisema kwa barabara za ndani wahusika wakuu ni halmashauri au mabaraza ya miji, ingawa wakati mwengine huzijenga hata kwa kiwango cha lami.

Barabara ya Kijangwani- Birikau iliyomo baina ya majimbo ya Chake Chake na Ziwani ambayo ina urefu wa wastani wa kilomita 3.7 imeasisiwa zaidi ya miaka 50 iliyopita, ingawa bado kwa siku za mvua hairuhusu gari kupita.

                                  Mwisho    

Comments