Skip to main content

WAJAWAZITO WAELEZEA MATUNDA KUJIFUNGULIA HOSPITALI, WANAOBAKI MAJUMBANI ROHO MKONONI

 

 


 

HABIBA ZARALI, PEMBA:::

 

LICHA ya serikali kuimarisha huduma za akina mama na watoto mijini na vijijini, ili wajifungulie hospitali, bado jitihada hizo zinaonekana kubezwa na baadhi ya akina mama hao.

 

Tayari Unguja na Pemba serikali imesogeza karibu vituo vya afya na kutowa elimu afya ya uzazi tofauti na zamani, wapo akina mama hujifungulia majumbani wakisaidiwa na wakunga wa jadi.

 

Ni dhahir kuwa akina mama wanapobeza maelekezo hayo na kuamuwa kubakia majumbani hadi kujifunguwa kunaweza kuwaletea madhara yatokanayo na uzazi.

 

Na ndio maana serikali kupitia wizara ya Afya, wakawataka wakunga wa jadi kuwasindikiza mama wajawazito hadi katika vituo vya afya na sio kuwazalisha wakiwa majumbani.

 

Na ndio maana hata Raisi wa Zanzibar Dk. Hussein Ali Mwinyi katika hutuba zake za mara kwa mara, huitaka wizara ya Afya kutowa huduma bora na kuona kwamba kunapunguwa vifo vya mama na mtoto.

 

Uchunguzi wa makala hii umebaini kuwa bado wapo akina mama ambao wanaendelea kupatwa na matatizo yahusuyo uzazi kwa kuamuwa kujifungulia majumbani.

 

MAMA WALIOJIFUNGULIA MAJUMBANI

 

“Bado kidogo nipoteze maisha kutokana na kujifungulia nyumbani, hata hivyo nimepata matatizo makubwa, kwani sijuwi kama nitaweza kubeba tena ujauzito”, hiyo ni kauli ya Fatma Abdalla (39) mkaazi wa Mwambe Mkoani Pemba. 

 

Mwanzoni mwa mwaka 2022, alipojifungua mimba yake ya tano na aliamua kujifungulia nyumbani, kutokana na uzoefu kwamba ameshazoea kujifungulia hapo, ingawa kwa bahati mbaya, mtoto alitoka vibaya na kumsababishia matatizo makubwa.

 

Akionekana mwenye huzuni baada ya kukumbuka mateso aliyoyapata, anasema alikuwa kwa mkunga wa jadi, mtoto alitangulia kutoka makalio, akakwama sehemu ya kichwa na mkono.

 

Anasema mkunga wa jadi hakuwa na namna ya kuweza kumsaidia, ndipo ilipoamuliwa kupelekwa hospitali ya Abdalla Mzee Mkoani, akiwa amechanika.

 

“Niliponea chupu chupu, nilipoteza damu nyingi, nikapoteza fahamu na mguu wangu wa kushoto ukafa ganzi kwa miezi mitatu, sikuweza kusimama,” anaeleza.

 

Zuwena Juma (35) mkaazi wa Chambani anasema, bado kidogo apoteze maisha, lakini huku na huku alimpoteza mtoto wake, baada ya kukaa nyumbani akiona ataweza kujifunguwa mwenyewe.

 

Mtoto wake hakutoka kwa hali ya kawaida, ila baada ya kufikishwa hospitali ya Abdalla Mzee, alifanyiwa upasuwaji  na maisha yake yakaokoka.

 

Sauda Salim (59) mkaazi wa Chake Chake, anaeleza jinsi mkwewe alivyopata tabu, alizalia kwa mkunga wa jadi na kusema kuwa mtoto alitoka vibaya mkunga hakuwa na uwezo tena wa kumsaidia.

 


‘’Kwa hakika nilimuona mkunga akienda huku na kule, ili kuhakikisha anaokoa maisha ya mtoto, lakini hatimae alipoteza maisha na mimi nilikuwa hali mbaya hasa baada ya kupoteza damu nyingi,’’anakumbuka.

 

MASHUHUDA

Munira Mohamed Ali (55) Mkaazi wa Kengeja, anatoa ushuhuda kwa aliyoyaona kwa jirani yake alivohangaika tokea majira ya saa 12:00 asubuhi, hadi saa 4:00 asubuhi, ambapo bado zalio halikutoka.

 

Anasema alimuona mama huyo akipoteza damu nyingi, ndipo walipoamua kumpeleka hospitali ya Abdalla Mzee Mkoani, akiwa na hali mbaya.

 

“Mtu akisha jiona kashazaa mimba tatu au nne hujiona mzoefu hukataa kujifungulia hospitali, hubahatisha kwa kujifungua nyumbani, jambo ambalo ni hatari,”anasema, Munira.

 

Hafidh Mohamed (30) Mkaazi wa Msuka Wilaya ya Micheweni anasema, wanaume wana jukumu la kuwahimiza wake zao kuzalia hospitali, ili kujiepusha na matatizo.

 

 

 “Mimi siwezi kusahau tokea siku niliyomuona jirani yangu anavyoteseka, tukiwa tunamkimbiza hospitali baada ya kukaa siku nzima, kwa mkunga wa jadi bila ya kujifunguwa na kupoteza gharama kubwa zisizo za lazima,’’anakumbuka.

 

Hassina Issa Omar wa Mtambile, ambae ni mkunga anasema, wakati mwengine huamshwa usiku kati, na hushwindwa kuwarejesha wazazi.

 

‘’Tumeshaelekezwa kuwa, mama yeyote asijifungulie nyumbani, lakini wapo wakaidi na wakati ndio hao wanaotufikia mikononi mwetu,’’anasema.

 

Mohamed Kombo wa Mwambe anasema mara nyingi ni ukaidi wa wanawake wenyewe, kwenda hospitali mapema na hatimae hujikalia mpaka wakafikwa na matatizo.

 


WALIOJIFUNGULIA HOSPITAL

Awena Abdalla wa Kiwani Mkoani, anasema moja ya jambo linalomshawishi kujifungulia hospitali ni huduma za lazima kama kuangalia uwingi wa damu.

 

‘’Hii ni mimba yangu ya nne, zote najifungulia hospitali, maana hata mume wangu na mama mzazi hakubali wazo la kwenda kwa mkunga,’’anasema.

 

Siti Othman Mohamed wa Kengeja, anasema faida anayoiyona anapojifungulia hospitali ni kupata dawa za kuhimiza uzazi.

‘’Niliwahi mimba yangu ya sita, kujifungulia kwa shangazi yangu, alitumia nguvu wakati nataka kujifungua, na baadae, nilikimbizwa hospitali kwa matibabu,’’anasema.

 

Hata Aisha Haji Ibrahimu wa Mtuhaliwa, anasema ushauri nasihi na huduma bila ya malipo, ndio jambo kubwa linalomvutia kujifungulia hospitali.

 

‘’Lakini hata ikitokezea unaukosefu wa damu, mtoto amekwama au umepata kifafa, wataalamu wanakushughulikia na hayo ukiwa nyumbani ni kukikaribia kifo,’’anasema.  

 

WATAALAMU WA AFYA WANASEMAJE

 

Muhudumu wa mama na watoto, hospitali ya Abdalla Mzee Pemba, Rabia Mohamed Ussi, anasema tatizo kubwa linalo gharimu maisha ya akina mama na watoto wakati wa kujifungua, ni kucheleweshwa kufikishwa hospitali.

 

“Mama anapokuja hospita huwa hali imesha kuwa mbaya pamoja na juhudi tunakazochukua basi utakuta anapoteza maisha mama au mtoto na mara nyingine wote wawili, “anasema.

 

Kwa mwaka 2020 akina mama 286 walijifunguwa kwa njia ya upasuaji, kati yao 27 walifanyiwa upasuaji kwa njia ya dharua ili kuokoa maisha yao na watoto, lakini hata hivyo watoto 7 na mama mmoja walipoteza maisha.

 

Kwa mwaka 2021 waliojifunguwa kwa upasuaji ni 310 kati yao 39 wamefanyiwa upasuaji wa dharura ambapo wamama 18 wamepoteza watoto na mama wanne wamepoteza maisha.

 

“Kati ya hao mama waliofanyiwa upasuaji kwa dharura walifika hospitali wakiwa wanamwaga damu nyingi, watoto kutokeza mkono mwanzo na kodi ya mtoto kutoka nje”,alisema.

 

Amina Ali Mbarouk, ambaye pia ni Muhudumu wa Mama na watoto katika hospitali hiyo, anasema licha ya kuwa wanapewa elimu lakini bado wapo akina mama hawajaamuwa kujifungulia hospitali.

 

“Matatizo kama ya kukwama kwa zalio, kuchanika msamba, yote haya husababisha mama kutokwa na damu nyingi, mkunga wa jadi hawezi kumsaidia,”anasema, Amina.

 

Ofisa muuguzi wa Wilaya ya Mkoani Pemba Moza Muhamed Ali anasema wakunga wa jadi hawaruhusiwi kuzalisha majumbani, isipokuwa wanahimizwa kuwaongoza hadi hospitali, kwani kuna matatizo mengi ya uzazi yanayoweza kujitokeza na hushindwa kuyakabili.

 

“Changamoto ambazo wanapozalisha nyumbani hushindwa kuzikabili ni pamoja na mzazi kumwaga damu kwa wingi, kupasuka fuko, mtoto kutanguliza makalio ,mkono ama kiungo chochote”,anasema

 

Ofisa Mdhamini Wizara ya Afya Pemba Khamis Bilali Ali anawasisitiza akina mama kwenda katika vituo vya afya mara tu wanapojigunduwa na ujauzito.

 

Hii anasema ni kwa ajili ya kupata huduma za awali na elimu ili kuweza kulea mimba kwa hali ya usalama pamoja na afya yake kwa ujumla.

 

Anasema, Serikali imeamua kuwasogezea karibu huduma hiyo, kwa kuongeza vituo mbali mbali vyenye madaraja ya pili kila wilaya, na kwa sasa Zanzibar ina Mtandao mzuri wa vituo vya Afya.

 

“Kwa sasa kuna wadau wa maendeleo ambao wamejitokeza na wanaendeleza kusaidia eneo la mama na mtoto, ili kupata huduma ambazo ni za bora sahihi na kwa wakati,’’anafafanua.

Mdhamini Bilali anawataja wadau kuwa ni hawa wa wanaokujana mradi wa M-mama ambao utawanufaisha kina mama kufika hospitali mapema, kujifungulia spitali na kupunguza vifo vya mama na mtoto.

 

WAKUNGA WA JADI WANASEMAJE

Wahida Mohamed Saidi wa Mkanyageni anasema wizara ya afya imeshawapa elimu ya kuwasindikiza wazazi hospitali kabla kuwazalisha ili kunusuru matatizo wanayoyapata.

 

“Akina mama wengi hupuuza kwenda spitali mapema na kujikalia majumbani mpaka hali inapokuwa mbaya, jambo ambalo hulazikmika kuwazalisha majumbani bila ya kutarajia,”anasema.

 

Siti Khamis Juma wa Mwambe anasema juhudi kubwa wanayoifanya ya kuelimisha akina mama kwenda hospitali mapema, ingawa bado wapo wanaokaidi.

 

Anasema husuburia mpaka hali ikawa tete na wakati mwingine hufanya makusudi wala si kwa bahati mbaya kama wanavyosingizia.

 

“Wapo wazazi wenye tabia ya kutuita wakiwa hali mbaya na dalili zote za kutaka kuzaa zimeshajionesha, ndipo kama binadaamu huona tusaidie kuzalisha lakini huku tukijitayarisha kuwakimbiza haraka hospitali maana kuna matatizo yakiwatokezea hatuyawezi,”alisema.

 

mwisho

 

Comments

BLOG'S VISITORS

DAKTARI MWENGINE CHAKE CHAKE KULA SIKUKUU POLISI, NI KWA TUHUMA ZA KUMBAKA MGONJWA WAKE

NA WAANDISHI WETU, PEMBA::: DAKTARI anaetoa huduma kwa wagonjwa kituo cha afya cha serikali cha  Gombani wilaya ya Chake Chake Pemba, Is-haka Rashid Hadid, anaendelea kushikiliwa na Jeshi la Polisi Mkoa wa kaskazini Pemba, akituhumiwa kumtorosha na kisha kumbaka mtoto wa mwenye umri wa miaka 16, mkaazi wa Gombani. Daktari huyo miaka 35 ni mkaazi wa Kangagani Wilaya ya Wete mkoani humo, ambapo anadaiwa alimchukua mtoto huyo kutoka kwa rafiki yake, na kumpeleka kwenye nyumba anayoishi eneo la Kangagani. Mtoto aliefanyiwa kitendo hicho alisema kuwa, April 21 mwaka huu alikwenda kituo cha afya Gombani, kwa ajili ya matibabu na baada ya kupatiwa huduma na daktari huyo, alimuomba nambari yake ya simu. Alisema ilipofika usiku, walikuwa wanawasiliana kupitia ujumbe mfupi (sms) kwa lengo la kwenda kuchukua dawa nyingine ambazo kwa mchana huo alizikosa hospitalini hapo. "Nilikwenda hospitali kutibiwa, baada ya kufanya mapele katika sehemu zangu za siri, lakini akaniambia mpaka aje da

'MKAPA' NA WENZAKE PEMBA WALAZWA RUMANDE

  NA HAJI NASSOR, PEMBA@@@@ MAHKAMA kuu Zanzibar kisiwani Pemba, chini ya Jaji Ibrahim Mzee Ibrahim, imewapeleka rumande watumuhimwa wanne wanaokabiliwa na tuhuma za kuua kwa makusudi, akiwemo Ali Mussa Omar ‘ Mkapa’ mkaazi wa Wawi wilaya ya Chake chake Pemba. Watuhumiwa wengine walioanza maisha mapya ya rumande ni mtuhumiwa Yassir Mohamed Juma miaka 23, Anuwari Mussa Omar miaka 30 pamoja na mtuhumiwa Yassir Mussa Omar ‘ Makababu ’ miaka 29, wote wakaazi wa shehia ya Wawi, wilaya ya Chake chake Pemba. Awali watuhumiwa hao waliwasili mahakamani hapo, kwa mara ya kwanza, kwa ajili ya kusomewa tuhma zinazowakabili za kumuua kwa maksudi Said Seif Kombo. Ilidaiwa mahakamani hapo na Mwendesha Mashtaka kutoka Ofisi ya Mkurugenzi wa Mashataka Seif Mohamed Khamis akiambatana na mwenzake Mussa Khamis Ali kuwa, watuhumiwa hao kwa pamoja wanadaia kufanya mauwaji hayo kwa maksudi. Ilidai kuwa, watuhumiwa wote kwa pamoja, walitenda kosa hilo Oktoba 16, mwaka huu, baina ya saa 7:00 mchan

HII KALI MBUNGE ASIYA AMKOGESHA MWANANCHI HADHARANI KISA HICHI HAPA......

  NA HAJI NASSOR, PEMBA MBUNGE wa viti maalum nafasi za wanawake mkoa wa kaskazini Pemba Asiya Sharif Omar, amewataka wananchi wa kijiji cha taifu, shehia ya Kinyasini jimbo la Gando wilaya ya Wete Pemba, kuyalinda miundombinu ya maji safi na salama, ili yawe endelevu kwao. Kauli hiyo ameitoa wakati alipokuwa akizungumza na mwandishi wa habari hizi, mara baada ya kuwasili kijijini humo, na kumkogesha mwananchi mmoja kama ishara ya uzinduzi wa mradi wa maji safi na salama, ulioasisiwa na mbunge wa Jimbo la Gando. Alisema, hawana mbadala kwa sasa bali ni kuilinda miundombinu ya huduma hiyo, hasa baada ya mbunge wa wao Salim Mussa Omar, kuwarejeshea huduma hiyo. Alieleza kuwa, inafahamika kuwa kwa miaka 14 waliikosa huduma hiyo hasa kwa vile viongozi waliokuwepo hawakujali kuwatatulia tatizo hilo, hadi juzi ilipofanywa na mbunge wao. “Baada ya huduma hii sasa kurejeshwa na mbunge wa jimbo la Gando, kazi iliyobakia kwenu wananchi ni kila mmoja kuwa mlinzi wa miundombinu hii,’’ali

TUHMA ZA DAKTARI PEMBA KUCHIWA HURU: POLISI KASKAZINI KUTOA TAARIFA RASMI LEO

  NA HAJI NASSOR, PEMBA KAMANDA wa Polisi mkoa wa kaskazini Pemba, Juma Saad Khamis, amesema leo Mei 9, mwaka huu atatoa taarifa rasmi, juu ya kuendelea kumshikilia au kumpa dhamana ya Polisi, daktari wa Kituo cha Afya Gombani Is-haka Rashid Hadid, anayetuhumiwa kwa ubakaji. Alisema, kwa vile alikuwa katika mapumziko mafupi, haelewi jambo lolote linaloendelea kwa mtuhumiwa huyo, juu ya kuendelea kushikiliwa kwake kituoni hapo. Alieleza kuwa, leo Mei 6 (jana), hajapata taarifa za ndani za mtuhumiwa, huyo na kuwataka wananchi na wanaharakati, wasubirie hadi Jumatatu ijayo. Akizungumza na waandishi wa habari kwa nyakati tofauti Kamanda huyo, alisema hana taarifa zozote za kupewa dhamana mtuhumiwa ndani ya kituo chake cha Polisi au kuendelea kuwepo. ‘’Ilikuwa mimi sipo kazini kwa muda, kuanzia anakamatwa hadi anafikishwa Polisi, kwa sasa siwezi kueleza jambo lolote kwa mtuhumiwa huyo, hadi Jumatatu,’’alieleza. Aidha Kamanda huyo alieleza kuwa, kwa sasa hawezi kutoa ufafan

MADAKTARI KUTOKA CHINA WAOKOA MAISHA YA MTOTO PEMBA

  HABIBA ZARALI, PEMBA TIMU ya 32 ya madaktari wa kichina katika hospitali ya Abdalla Mzee Mkoani wamefanikiwa kufanya upasuaji mkubwa wa mtoto mwenye umri wa miaka 15 mkaazi wa Chole Kengeja, baada ya kuchomwa na jiti sehemu ya njia zake za mfumo wa uzazi. Mtoto huyo ambae alianguka hivi karibuni katika mti na baadae kuchomwa na jiti hilo na kumsababishia kutokwa na damu nyingi katika sehemu ya nyonga, alifanyiwa upasuaji uliodumu kwa muda wa saa tatu na   kuokolewa maisha yake. Akizungumza mara baada ya operesheni huo kiongozi wa timu hiyo Dr Jiang Jinhua, alisema mara baada ya mtoto huyo kufikishwa hospitalini hapo na kufanyiwa vipimo na kuonekana   ilibidi apatiwe rufaa ya kwenda katika hospitali nzuri yenye kutibu tatizo lake huko nchini Kuwado ambapo haikuwezekana kutokana na hali ya umaskini wa f amilia ya mtoto huyo . Alisema timu ya madaktari hao itaendelea kutowa huduma za matibabu   kwa wananchi kisiwani humo,   ili kuwaondolea gharama ya kutafuta matibabu nje ya nch