Skip to main content

WADAU ZANZIBAR WALIA NA MANENO YA KIUJANJA SHERIA ZA HABARI

 


NA HAJI NASSOR, PEMBA@@@@

KWA zaidi ya miaka 15 sasa wadau wa habari wamekuwa wakipaza sauti zao kutaka sheria mpya na bora ya habari Zanzibar.


Wadau mfano Chama cha waandishi wa habari wanawake Tanzania TAMWA-Zanzibar, Baraza la Habari Tanzania (MCT), na hata ZAMECO wamekuwa wakiungana na waandishi wa habari kuhakikisha sheria moja ya habari inapatikana.


Afisa Program wa uchechemuzi wa sheria za habari Zanzibar kutoka TAMWA-Zanzibar Zaina Mzee, anasema moja ya sababu ya kutaka sheria mpya ya habari, ni kuona zile mbili zilizopo zinafutwa.


‘’Ipo sheria ya Tume ya Utangaazaji Zanzibar nambari 7 ya mwaka 1997, pamoja na marekebisho yake, pamoja na ile ya sheria nambari 5 ya Wakala wa Habari, Magazeti na Vitabu ya mwaka 1988, ambayo imefanyiwa marekebisho mwaka 1997.


 Anasema sheria hizo, zimekuwa na vifungu ambavyo sio rafiki kwa kuimarisha uhuru wa habari, pamoja na uhuru wa kujieleza katika jamii.

 

Anaeleza kuwa, pamoja na ukongwe wake sheria hizo mbili kuu, zinazosimamia vyombo vya habari, zimekuwa zikiwabana waandishi katika kutekeleza haki yao ya kikatiba ya kuuhabarisha umma.

 

‘’Katiba ya Zanzibar ya mwaka 1984, kwenye kifungu cha 18(2) kimeweka wazi suala la kupata, kusambaza habari habari tena bila ya kujali mipaka ya nchi,’’ anasema ilivyoeleza sehemu ya katiba.

 

Mkurugenzi wa TAMWA-Zanzibar Dk. Mzuri Issa Ali anasema kuwa, kwa wakati uliopo sasa Zanzibar na duniani kote, suala la kuwepo vifungu vinavyobana uhuru wa habari na uhuru wa kujieleza havina nafasi.

 

‘’Kwa mfano kwenye sheria mbili hizo, vipo vifungu vilivyompa uwezo mkubwa Waziri wa kulifungia au kuzuia uchapishaji wa gazeti, akihisi kwa maoni yake, kunataka kuchapishwa habari iliyokinyume na maadili,’’ anasema.

 

Mwandishi Salim Said Salim, anasema huu sio wakati tena wa sheria zinazoongoza vyombo vya habari, kumpa uwezo mkubwa Mkurugenzi, au Waziri.


‘’Inashangaaza kuona katika sheria za habari, hadi leo kuna maneno kama waziri anaweza, Mkurugenzi akihisi, Polisi anaweza kupekuwa, haya yote yanaleta ukakasi kwenye kazi za vyombo vya habari,’’anasema.


Mwandishi Khadija Kombo wa ZBC Pemba, anasema ukakasi wa sheria za habari hapa Zanzibar, wakati mwingine huwarejesha nyuma waandishi, kuibua changamoto za wananchi. 


‘’Inawezekana waandishi wa habari wanataka kuibua changamoto kubwa inayowahusu wananchi, lakini vipo vifungu ambavyo vinatishia utendaji wao wa kazi,’’ anasema.



 

Meneja wa redio Jamii Mkoani Said Omar Said, anasema uwepo wa vifungu kandamizi kwenye sheria za habari, wakati mwingine huwakosesha kujiamini waandishi katika utendaji wa kazi zao.

 

Mkurugenzi Uratibu wa Shirika la Magazeti ya Serikali Zanzibar ofisi ya Tanzania bara Juma Khamis Juma, anasema kwenye utekelezaji na tafsiri za vifungu vya sheria, hakutakiwi kuwepo neno lenye utata.


‘’Kwa mfano neno waziri anaweza, akiona inafaa, akihisi na mengine yanayofanana na hayo, huwa ni hatari kuwapo kwenye maelezo ya utekelezaji wa sheria,’’ anasema.


Hata Mkufunzi Mshauri Haura Shamte wakati akiwasilisha vifungu vya sheria za habari vyenye hofu na uhuru wa waandishi alipokuwa Pemba, alisema kuwa sheria hizo sio rafiki kwa waandishi.


‘’Haiwezekani kuwa hadi leo, tuwe na sheria inayompa uwezo mkubwa mtu mmoja kwa sababu ya cheo chake, au kuwapo kwa maneno yanayokinzana na msingi wa demokrasia,’’anasema.




Wananchi Khamis Iddi Mabrouk na mwenzake Issa Haji Khamis wa Kangagani Mkoani, wanasema waandishi wasipokuwa huru, hata wananchi hawatokuwa huru, hawatakuwa na uwezo wa kufanya uamuzi sahihi wa mambo yanayowahusu kwa sababu ya kukosa taarifa za ukweli na uwazi.


Hidaya Mjaka Ali wa Vitongoji mwenye ulemavu wa viungo, anasema, wanavitarajia mno vyombo vya habari, kuibua changamoto za kundi lao, ingawa kinyume chake ni kukosa haki zao.


Mwanasheria wa serikali wa kujitegemea Khalfan Amour Mohamed, anasema kwamba, sio sahihi kifungu hicho kuwepo kwa sababu, kuweka sentensikama ‘kwa maoni yake’ katika sheria, ni hatari sana kwa mustakabali wa demokrasia na haki za wananchi.


 VIFUNGU VYA SHERIA ZA HABARI VINAVYOUTETEMESHA UHURU WA HABARI ZANZIBAR

Sheria ya Tume ya Utangazaji Zanzibar nambari 7 ya mwaka 1997, kwenye kifungu chake cha 13 (5) kimeutia doa uhuru wa habari Zanzibar.


Kikaeleza kuwa, ‘’mtu yeyote asiyeridhika na uamuzi wa Tume  kutoa au kataka maombi, anaweza kukata rufaa kwa Waziri kwa namna ya njia itakavyoelezwa na kanuni,’’kinaeleza.


Ambapo hapa, muomba leseni, anapokataliwa na Katibu Mtendaji wa Tume, akate rufaa kwa Waziri, ambae ndie aliyemteua au kusababisha kupatikana kwa Katibu huyo.


Kifungu kingine chenye maneno yenye ukakasi kwa ukuaji wa uhuru wa habari ni cha 27 (1), ambapo waziri husika au mwingine aliyeidhinishwa, anaweza kutoa amri kumtaka mpewa leseni, atangaze jambo lolote ambalo kwa maoni ya Waziri, lina maslahi kwa umma au usalama wa taifa.


Hapa wadau wa habari wanasema, kifungu hicho kipo kishari shari, maana kimebainisha uwezo wa Waziri, kumlazimisha mpewa leseni kutangaza jambo ambalo anaona tu ni kwa maslahi ya umma au usalama wa taifa.


Aliyekuwa Mdhamini wa Baraza la Habaeri Tanzania ‘MCT’ Zanzibar Shifaa Said Hassan, anasema neno kwa maslahi ya umma, sheria hiyo haijalitafsiri, hivyo waziri anaweza kutumia mwanya huo, kutangaza jambo analoona yeye kuwa ni maslahi ya umma.


Hata Mkurugenzi Mtendaji wa Chama cha Waandishi wa Habari Wanawake Tanzania TAMWA- Zanzibar Dk. Mzuri Issa Ali, anasema, neno usalama wa taifa, sheria hiyo kwenye vifungu vyake 30 na sehemu sita halikutajwa.


‘’Hapa mpewa leseni, amewekwa njia panda, maana Waziri akiamka vibaya anaweza kutumia mwanya huo, na kutoa tangazo ambalo halina maslahi na nchi, huku sheria ikimlinda,’’anasema.


Afisa Programu kutoka TAMWA Zanzibar Zaina Mzee, anasema kupata habari ni haki ya kikatiba, sheria zinazosimamia ni vyema zisiwe na maneno au maelezo yanayoashiria kumpa mtu mmoja uwezo, kama vile anajiamulia kufanya mambo yake binafsi.


Mwandishi wa Mwanahalisi mtandaoni Jabir Idrissa, anasema athari kubwa inayotokana na sheria hiyo kandamizi ni wawekezaji katika sekta ya habari, kukosa hamu ya kuwekeza (kwanini wanakosa hamu hiyo? Dadavua), na kundi kubwa la vijana kukosa ajira.


Mwenyekiti wa Klabu ya Waandishi wa Habari Zanzibar ‘ZPC’ Abdalla Mfaume, anasema kazi yao kubwa ni kuzisemea sheria na vifungu kandamizi, ili waandishi wa habari wafanyekazi zao kama ilivyo, kwa makundi mengine.

Rahma Suleiman mwandishi wa Gazeti la Nipashe, anashauri kuwa waandishi na wadau wa habari, waungane kushinikiza mswada wa sheria ya Huduma za Habari unapelekwa Barazani.


 WIZARA YA HABARI

Waziri wa Wizara ya Habari, Vijana na Utamaduni Tabia Maulid Mwita, anasema anaamini kuwa Muswada wa sheria mpya ya Habari Zanzibar wakati wowote utapelekwa Baraza la Wawakilishi kujadiliwa.


‘’Na hata maoni ya wadau yamo kama yalivyopendekezwa, hapa kubwa naomba niendelee kuwepo katika nafasi hii, ili nihakikishe hilo linafanyika kwa haraka,’’anasema.

 

                                                       MWISHO.

 

Comments

BLOG'S VISITORS

DAKTARI MWENGINE CHAKE CHAKE KULA SIKUKUU POLISI, NI KWA TUHUMA ZA KUMBAKA MGONJWA WAKE

NA WAANDISHI WETU, PEMBA::: DAKTARI anaetoa huduma kwa wagonjwa kituo cha afya cha serikali cha  Gombani wilaya ya Chake Chake Pemba, Is-haka Rashid Hadid, anaendelea kushikiliwa na Jeshi la Polisi Mkoa wa kaskazini Pemba, akituhumiwa kumtorosha na kisha kumbaka mtoto wa mwenye umri wa miaka 16, mkaazi wa Gombani. Daktari huyo miaka 35 ni mkaazi wa Kangagani Wilaya ya Wete mkoani humo, ambapo anadaiwa alimchukua mtoto huyo kutoka kwa rafiki yake, na kumpeleka kwenye nyumba anayoishi eneo la Kangagani. Mtoto aliefanyiwa kitendo hicho alisema kuwa, April 21 mwaka huu alikwenda kituo cha afya Gombani, kwa ajili ya matibabu na baada ya kupatiwa huduma na daktari huyo, alimuomba nambari yake ya simu. Alisema ilipofika usiku, walikuwa wanawasiliana kupitia ujumbe mfupi (sms) kwa lengo la kwenda kuchukua dawa nyingine ambazo kwa mchana huo alizikosa hospitalini hapo. "Nilikwenda hospitali kutibiwa, baada ya kufanya mapele katika sehemu zangu za siri, lakini akaniambia mpaka aje da...

'MKAPA' NA WENZAKE PEMBA WALAZWA RUMANDE

  NA HAJI NASSOR, PEMBA@@@@ MAHKAMA kuu Zanzibar kisiwani Pemba, chini ya Jaji Ibrahim Mzee Ibrahim, imewapeleka rumande watumuhimwa wanne wanaokabiliwa na tuhuma za kuua kwa makusudi, akiwemo Ali Mussa Omar ‘ Mkapa’ mkaazi wa Wawi wilaya ya Chake chake Pemba. Watuhumiwa wengine walioanza maisha mapya ya rumande ni mtuhumiwa Yassir Mohamed Juma miaka 23, Anuwari Mussa Omar miaka 30 pamoja na mtuhumiwa Yassir Mussa Omar ‘ Makababu ’ miaka 29, wote wakaazi wa shehia ya Wawi, wilaya ya Chake chake Pemba. Awali watuhumiwa hao waliwasili mahakamani hapo, kwa mara ya kwanza, kwa ajili ya kusomewa tuhma zinazowakabili za kumuua kwa maksudi Said Seif Kombo. Ilidaiwa mahakamani hapo na Mwendesha Mashtaka kutoka Ofisi ya Mkurugenzi wa Mashataka Seif Mohamed Khamis akiambatana na mwenzake Mussa Khamis Ali kuwa, watuhumiwa hao kwa pamoja wanadaia kufanya mauwaji hayo kwa maksudi. Ilidai kuwa, watuhumiwa wote kwa pamoja, walitenda kosa hilo Oktoba 16, mwaka huu, baina ya saa 7:00 m...

HII KALI MBUNGE ASIYA AMKOGESHA MWANANCHI HADHARANI KISA HICHI HAPA......

  NA HAJI NASSOR, PEMBA MBUNGE wa viti maalum nafasi za wanawake mkoa wa kaskazini Pemba Asiya Sharif Omar, amewataka wananchi wa kijiji cha taifu, shehia ya Kinyasini jimbo la Gando wilaya ya Wete Pemba, kuyalinda miundombinu ya maji safi na salama, ili yawe endelevu kwao. Kauli hiyo ameitoa wakati alipokuwa akizungumza na mwandishi wa habari hizi, mara baada ya kuwasili kijijini humo, na kumkogesha mwananchi mmoja kama ishara ya uzinduzi wa mradi wa maji safi na salama, ulioasisiwa na mbunge wa Jimbo la Gando. Alisema, hawana mbadala kwa sasa bali ni kuilinda miundombinu ya huduma hiyo, hasa baada ya mbunge wa wao Salim Mussa Omar, kuwarejeshea huduma hiyo. Alieleza kuwa, inafahamika kuwa kwa miaka 14 waliikosa huduma hiyo hasa kwa vile viongozi waliokuwepo hawakujali kuwatatulia tatizo hilo, hadi juzi ilipofanywa na mbunge wao. “Baada ya huduma hii sasa kurejeshwa na mbunge wa jimbo la Gando, kazi iliyobakia kwenu wananchi ni kila mmoja kuwa mlinzi wa miundombinu hii,’...

…….SUZA WATOA USHAURI WA ADHABU YA KUNYONGWA

  NA HAJI NASSOR, PEMBA@@@@ WANAFUNZI wanaosomea uwalimu Chuo cha taifa cha Zanzibar ‘SUZA’ kampasi ya Benjamin Wiliam Mkapa Wete Pemba, wamependekeza adhabu ya kunyongwa hadi kufa, kwa mtu atakaetiwa hatiani, kwa kosa la dawa za kulevya. Walisema, haiingii akili kuona, mahkama imeshamtia hatiani mtu kwa kukutwa na dawa za kulevya, ambazo huathiri nguvu kazi ya taifa na kisha, kupewa hukumu ya kifungo pekee. Wakizungumza leo Juni 26, 2024 kwenye kongamano la vyuo vikuu, juu ya masuala ya msaada wa kisheria, kuelekea wiki ya msaada wa kisheria Zanzibar, lililofanyika Chuoni hapo, walisema wakati umefika sasa kutolewa kwa hukumu hiyo. Walipendekeza kuwa, ni vyema kwa mtu anayetiwa hatiani asibakie chuo cha Mafunzo pekee kuitia tena hasara serikali kwa chakula na wakati mwingine matibabu, wakati tayari ameshasababisha madhara, kwa vijana. Mshiriki Juma Nafasi Juma, alifafanua kuwa kama mtu ameamua kuliumiza taifa kwa kuingiza, kusafirisha, kusambaaza dawa za kulevya, hivyo n...

TUHMA ZA DAKTARI PEMBA KUCHIWA HURU: POLISI KASKAZINI KUTOA TAARIFA RASMI LEO

  NA HAJI NASSOR, PEMBA KAMANDA wa Polisi mkoa wa kaskazini Pemba, Juma Saad Khamis, amesema leo Mei 9, mwaka huu atatoa taarifa rasmi, juu ya kuendelea kumshikilia au kumpa dhamana ya Polisi, daktari wa Kituo cha Afya Gombani Is-haka Rashid Hadid, anayetuhumiwa kwa ubakaji. Alisema, kwa vile alikuwa katika mapumziko mafupi, haelewi jambo lolote linaloendelea kwa mtuhumiwa huyo, juu ya kuendelea kushikiliwa kwake kituoni hapo. Alieleza kuwa, leo Mei 6 (jana), hajapata taarifa za ndani za mtuhumiwa, huyo na kuwataka wananchi na wanaharakati, wasubirie hadi Jumatatu ijayo. Akizungumza na waandishi wa habari kwa nyakati tofauti Kamanda huyo, alisema hana taarifa zozote za kupewa dhamana mtuhumiwa ndani ya kituo chake cha Polisi au kuendelea kuwepo. ‘’Ilikuwa mimi sipo kazini kwa muda, kuanzia anakamatwa hadi anafikishwa Polisi, kwa sasa siwezi kueleza jambo lolote kwa mtuhumiwa huyo, hadi Jumatatu,’’alieleza. Aidha Kamanda huyo alieleza kuwa, kwa sasa hawezi kutoa uf...