Skip to main content

USAFIRISHAJI HARAMU BINADAMU TANZANIA, WAZAZI WAELEMEWA NA TAMAA, MADALALI MANENO KAMA ASALI

 

 



USAFIRISHAJI HARAMU WA BINADAMU TANZANIA

-Wazazi wakiri tamaa, umaskini vyawaelemea kuwatoa watoto wao

 -Wasema madalali wana maneno ya kumtoa nyoka pangoni

 

HAJI NASSOR, PEMBA::

cell phone:  +255656265945

emali:          hajipembatoday@gmail.com


‘’Mimi baada ya kuona mtoto wa jirani yangu mwaka 2000 alisafirishwa na mtu tunayemjua, na wangu mimi mwaka 2022 nimemtoa, ingawa naarifiwa alishauawa akiwa Oman,’’maneno ya mzazi.

 

Mzazi huyo aliyekataa kuchapishwa jina lake halisi, anasema atakubali kuhojiwa ikiwa mwandishi atatumia jina la Zawadi, kwa ajili ya kufanikisha mazungumzo haya baina yake.

 

Anasema mtoto wake wa kike mwenye miaka 17, baada ya kumaliza masomo, huku akiwa na watoto sita wanaomtegemea, baada ya baba yao kufariki kwenye meli ya Mv. Spice, hakuwa na wasi wasi, kumtoa kwenda Oman.

Anasema alimjia mtu ambae hamfamu, ingawa alimueleza kuwa, alikuwa karibu mno na marehemu mume wake, na hivyo baada ya kuzoea mno kwake, kisha alimuamini.

 

Alimtaja kwa jina moja la Hashim, na ndie aliyemtengenezea pasi ya kusafiria ‘pass port’ baada kumueleza kuwa hana uwezo wa hata shilingi moja, kwa ajili ya maandalizi ya safri ya Oman.

 

Alifikiria mno juu ya safari ya mtoto wake, ingawa anasema Hashim, alimuonesha picha za vijana wengine ambao ameshawapeleka nchini huko, wakiendelea na kazi.

 

‘’Mwandishi usinirikodi wala usinichapishe jina langu,’’ alikuwa akinisisitiza kila wakati mama huyo, mkaazi wa Tumbe wilaya ya Micheweni Pemba.

 

Anasema alivutika mno, na alielezwa na kijana Hashim kuwa, asimueleza mtu yeyote wa familia yake, maana wanaweza kuiharibu safari kwa ushirikina.

 

‘’Hapo mtaa mbele, kuna kijana nilitaka kumsafirisha, ingawa mama yake baada ya kumueleza kila mtu mtoto huyo, alipata uendawazimu,’’ni maneo ya ulaghai aliyoelezwa Zawadi na Hashim.

 

Anasema alitii agizo, hilo na Januari 29, mwaka 2022 mtoto wake alikabidhiwa pasi ya kusafiria, na alipewa shilingi 500,000 na Hashim za kufanyabiashara ndogo ndogo.

 

‘’Wakati anaondoka alielezwa mtoto wangu, yule Hashim kuwa amuite baba na hata akiulizwa uwanja wa ndege aseme ni baba yake mzazi,’’anasema mama huyo.

 

Zawadi anasema siku moja, wakati mtoto wake anajiandaa kuondoka, aliulizwa ikiwa yule Hashim na baba yake kweli, na kumjibu hapana.

 

‘’Ilibidi nimdanganye kuwa ni baba yake, mdogo na nilisisitizwa hata akiulizwa uwanja wa ndege ajibu kama hivyo,’’anakiri mama kumdanganya mtoto wake.

 

BAADA YA KUFIKA OMAN

Mama huyo anasema, mtoto wake ilikuwa kila Ijumaa anawasiliana nae na mwezi Aprili, alitumiwa shilingi 300, 000 kwa fedha za Tanzania, kutoka kwa kijana Hashim.

Siku moja, mtoto huyo alimueleza mama yake, anatamani kurudi kutokana na ugumu wa kazi, ingawa alimtaka awe mstahamalivu.

 

Na siku nyingine alimueleza kuwa, anataka kurudi kwao Pemba Micheweni, akielezea kukosa muda hata wa kumpuzika, akimtaka kama analipwa, aendelee.

 

Kuanzia mwezi Julai mwaka huu 2022, anasema alikuwa akiwasiliana nae kila mwezi mara moja, tena chini ya ulinzi wa bosi wake wa kazi, tena kwa dakika tatu.

 

‘’Wasiwasi uliniingia na sasa yule Hashima hana tena mawasiliano na mimi, na mtoto wangu alikuwa tukiwasiliana haoneshi furaha, kumbe alianza kupata mateso,’’anasema.

 

Mama Zawadi anasema, siku moja mtoto wake, aliiba simu na kumeleza kuwa, sasa analazwa na kijana wa kiarabu, ambapo usiku humfanya kama mke wake.

 

‘’Siku moja wakati anambaka aliambia alimtafuna shavu, na kumueleza kuwa, yeye hakujia kazi hiyo, na asubuhi yake alipigwa na baba mwenye nyumba,’’anasema.

Kwa mara ya mwisho mwezi Oktoba 2022, alipigiwa simu na tajiri wa mtoto wake, kuwa anaumwa sana na amelazwa hospitali na baada ya wiki, alielezwa kuwa amefariki.

 

‘’Sina hakika mwandishi kuwa, mtoto wangu wa kike ameshauliwa, ameolewa, anatumikishwa, anajiuza au amechinjwa, mimi nipo nipo tu,’’anaeleza.

 

Anasema hawezi kwenda popote kueleza hayo, maana hakumshirikisha mtu yeyote ndani ya familia yake, wala Polisi kama agizo la dalali lilivyokuwa.

 

MAJIRANI

Jirani wa mama huyo, anasema wao wanachofahamu ni kuwa mtoto huyo, anaendelea na masomo chuoni Tanzania bara, kama alivyowaeleza mwenyewe (mama mtoto).

 

Kijana Omar Haji Mcha wa Tumbe, anasema mwaka 2019, nae alifuatwa na kijana mwengine, ambae ni dalali, juu ya safari ya Qatar, ingawa baada kuieleza familia alizuiwa.


NINI BIASHARA HARAMU YA USAFIRISHAJI BINADAMU?

 Biashara haramu ya binadamu ni kusafirisha, kuhamisha, kuweka au kupokea, kuhifadhi mtu lengo la kuwanyonya, kuwakandamiza na kunyimwa huru wao.

 

WAHANGA

Radhia Issa Haji wa Mgogoni Wawi Chake chake, anasema mateso makubwa aliyapata kuamua kutorudi tena, ni kukosa muda wa mapunziko.

 

‘’Hata siku ambazo mmepanga kuwa ni za mapunziko, unahamishiwa nyumba yako ya kawaida, inapelekwa kwa mama yake au baba yake tajiri wako,ukifika ni kazi tu,’’anasimulia.

 

Lililomuumiza zaidi, ni kutakiwa kuwa huru, kushikwa na kuchezewa chezewa na baba mwenye nyumba, au watoto wake wa kike.

 

Haitham Aleyi Manssour wa Wete Pemba, anasema vijana wasing’anganie sana safari za nje, na hasa eneo ambalo ukiamua kutaka kurudi ni shida.

 

Mama mzazi wa mtoto mmoja wa kiume anaeishi shehia ya Makoongwe wilaya ya Mkoani anasema, kama sio dawa na dua aliyoitumia, hadi leo ingekuwa mtoto wake hajarudi.

 

‘’Tulisikia anatumikishwa na kinyume na kazi yake ya awali, tulimuomba dalali amrejeshe lakini aligoma, ingawa tulitumia dawa na sasa amerudi yuko Dar-es Salaam,’’anasimulia.    

 

VIONGOZI WA DINI

Sheikh Said Ahmad wa ofisi ya Mufti anasema, dini inakataza kwaza kufanya hadaa pili kumuuza mtu, maana huo ni ukatili na udhalilishaji.

 

Mchungaji Benjamen Kisssanga, anasema ukiristo unakerwa na kulalamikia mno, tendo la madali kuwafanyiwa ghilba wazazi au vijana.

 

WANAHARAKATI

Safia Saleh Sultan wa Kituo cha Huduma za Sheria Zanzibar ‘ZLSC’ anasema, utaratibu wa kazi za nje ya nchi uko wazi, ni vyema jamii ikaufuata.

 

‘’Kisheria ni kosa kufanya hadaa au kuupinda uaminifu, maana katiba zinaeleza binadamu wote ni sawa mbele ya sheria, hivyo kama kuna mtu anaipinda ni kosa,’’anasema.

 

Mratibu wa TAMWA Zanzibar ofisi ya Pemba Fat-hya Mussa Omar, anasema huo ni aina mwengine wa ukatili na udhalilishaji wa watoto, ambao unapaswa kukemewa.

 

‘’Hivi sasa dunia iko katika siku 16 za kupinga ukatili na udhalilishaji, hivyo jamiii iache tamaa na kuingia katika mitego kama hiyo,’’anasema.

 

Edwin Mugambila ambae ni Mkurugenzi Mtendaji wa tasisi ya Tanzania Relief Initiatives ‘TRI’ kila watoto 100 ambao ni wa biashara haramu ya binadamu 65 ni wasichana na wanawake.

 

Ambapo anaeleza kuwa, wahanga hao wameajiriwa na kunyonywa kingono, taarifa za mfano wa jimbo la Marekani kupambana biashara haramu ya binadamu, inasema kwamba, wale wanaojihusisha na biashara haramu ya binadamu wanapata kiasi kikubwa cha fedha kama dola bilioni 150 kwa mwaka.

 

Ambapo hiyo, imeifanya kuwa biashara haramu ya tatu yenye faida zaidi, ikitanguliwa na dawa za kulevya na uuzaji wa silaha haramu.

 

Naibu Balozi wa umoja wa nchi za Ulaya ‘EU’ Elimo Rossetti akizungumza kwenye mafunzo ya waandishi wa habari na wanaharakati wa haki za binadamu mjini Zanzibar, alisema Tanzania imekuwa lango la biashara hiyo.

 

‘’Sio kama serikali ya Tanzania haichukii biashara hii haramu, hapana bali kimaumbile na jinsi ilivyopakana na nchi kadhaa, ndio maana wahanga wanapitishwa na wakienda kutumikishwa,’’anasema.

 

Ndio maana anasema, mafunzo hayo kwa waandishi, yatawazindua wananchi na serikali kuzidi kupanga mikakati ya kupunguza biashara haramu ya kusafirisha binadamu.



 

NJIA ZINAZOTUMIKA KUWASAFIRISHA WAHANGA

Kwa sasa njia za kielektroniki, kama face book, watsap, email, tovuti huwaunganisha madalali na vijana na kisha huombwa picha kwa ajili ya kutengenezewa pasi ya kusafiria.

 

Wapo wanaosafirishwa kwa kutumia njia halili za uwanja wa ndege, boti, au gari kutoka nchi moja kwenda nyingine, na wakati mwengine wakiwa wadogo hufanywa baba na mtoto.

 


TAKWIMU ZA NDANI

Ripoti ya Jeshi la Polisi Tanzania ya mwaka 2020, ilipokea matukio 25 ya watoto kusafirishwa, kwa njia za kwenda kuuzwa nje za nchi.

 

Kati ya watoto hao 25, wa kike walikuwa watano (5) huku wa kiume wakiwa 20, ambapo mkoa wa kipolisi wa Temeke uliongozwa kwa kuripoti watoto wanane (8) ukifuatiwa na mkoa wa Manyara watoto wanne (4).

 

Mikoa ya Mbye na Simiyu, iliripoti idadi ya watoto watatu (3) kila mkoa, ingawa kwa mwaka huo wa 2020 mikoa mitano ya Zanzibar, jeshi la Polisi halikuripoti tukio lolote.

Ingawa masheha sita wa wilaya ya Micheweni waliripoti watoto 12, kwa mwaka huo, kuondoka kinyume na sheria.

''Hawa tumewabaini baada ya waalimu wa skuli kulalamikia kuwa wananafunzi ni wao ni watoro, na tulipowaabili wazazi walieleza kuwa, wako nchini Kenya,''anasema sheha mmoja.



TAKWIMU ZA NJE

 Kulingana na Ripoti ya hali ya kimataifa ya Idara ya Jimbo la Merika juu ya usafirishaji haramu wa binadamu, kuanzia mwezi Juni, 2021 hadi Juni 2022, kulikuwa na kesi 185 zilizoripotiwa za zikihusishwa kuwa ni za Tanzania.

 

Ambapo kati ya kesi hizo, 113 tu ndio ambazo zilichunguzwa na wahalifu 13 pekee ndio waliotiwa hatiani, ambao wote walilipa faini badala ya kifungo.

 

JUHUDI ZA SERIKALI NI ZIPI

Mkurugenzi wa Ustawi wa Jamii Zanzibar Adalla Saleh Omar, anasema moja ya mikakati ya serikali ni kushirikiana na mashirika ya kimataifa kama EU, UNFPA ili kuwajengea uwezo wananchi.

 

 Lakini hata serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tazania  imeonyesha msukumo mkubwa wa kuzuia biashara hiyo, kwani Oktoba 2021, bunge ilifanyia marekebisho sheria ya ‘TIP, kuandikwa upya ya marekebisho ya na kuingizwa jaribio la kusafirisha kuwa ni kosa tofauti na zamani.

 

Juhudi nyingine ni serikali kuanzisha nyumba tatu salama, kwa ajili ya waathirika, moja ikiwa Zanzibar, moja ya Dar es salaam na nyingine Dodoma.

 

Hata hivyo, Kamanda wa Polisi mkoa wa kaskazini Pemba Juma Saadi, anasema lazima wazazi waamke, na kuwatilia shaka watu wanaowaendea wakitaka watoto.

 

Kamishna wa Uhamiaji Zanzibar  Hassan Ali Hassan, amenukuliwa akisema, lazima jamii iamke na kufuata sheria za usafiri na usafirishaji.

 

‘’Sisi uhamiaji tunampa mtu pasi ya kusafiria, kwa mujibu wa maelezo yake au kama ni mtoto msimamizi wake, sasa dalali akidanganya huo ni kosa ikibainika,’’anasema.


 ATHARI YA BIASHARA HII

Moja ya athari ya biashara haramu ya usafirishaji binadamu kama ilivyotajwa na Mkuu wa wilaya ya Micheweni Mgeni Khatib Yahaya, ni vifo visivyotarajiwa kwa wahanga

Mama ambae mtoto wake amesharudi Misri hivi karibuni, anasema athari kubwa ni vitendo vya ukatili na udhalilishaji.

Muhanga wa biashara hiyo, mwene miaka 22, anasema maslahi duni na kazi nzito, ndio jambo ambalo linajitokeza.



NINI KIFANYIKE

Afisa Mfawidhi wa Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora Pemba Suleiman Salim Ahmad anasema, elimu ya tahadhari kwa wazazi na vijana, ndio suluhisho.

Kijana Omar Haji Omar ambe mdogo wake ni muhanga wa biashara hiyo, anapendekeza sheria kwa wahalifu wa biashara hiyo, iondoe ulipaji wa fani, bali iwe ni kifungo. 

Mratibu wa Jumuiya ya wasioona Pemba 'ZANAB' Suleiman Mansour Suleiman, anasema ziwekwe sheria kali kwa wazazi watakabainika kuwasafirisha watoto wao kwa kushirikiana na madalali.

                Mwisho     

 

Comments

BLOG'S VISITORS

DAKTARI MWENGINE CHAKE CHAKE KULA SIKUKUU POLISI, NI KWA TUHUMA ZA KUMBAKA MGONJWA WAKE

NA WAANDISHI WETU, PEMBA::: DAKTARI anaetoa huduma kwa wagonjwa kituo cha afya cha serikali cha  Gombani wilaya ya Chake Chake Pemba, Is-haka Rashid Hadid, anaendelea kushikiliwa na Jeshi la Polisi Mkoa wa kaskazini Pemba, akituhumiwa kumtorosha na kisha kumbaka mtoto wa mwenye umri wa miaka 16, mkaazi wa Gombani. Daktari huyo miaka 35 ni mkaazi wa Kangagani Wilaya ya Wete mkoani humo, ambapo anadaiwa alimchukua mtoto huyo kutoka kwa rafiki yake, na kumpeleka kwenye nyumba anayoishi eneo la Kangagani. Mtoto aliefanyiwa kitendo hicho alisema kuwa, April 21 mwaka huu alikwenda kituo cha afya Gombani, kwa ajili ya matibabu na baada ya kupatiwa huduma na daktari huyo, alimuomba nambari yake ya simu. Alisema ilipofika usiku, walikuwa wanawasiliana kupitia ujumbe mfupi (sms) kwa lengo la kwenda kuchukua dawa nyingine ambazo kwa mchana huo alizikosa hospitalini hapo. "Nilikwenda hospitali kutibiwa, baada ya kufanya mapele katika sehemu zangu za siri, lakini akaniambia mpaka aje da

'MKAPA' NA WENZAKE PEMBA WALAZWA RUMANDE

  NA HAJI NASSOR, PEMBA@@@@ MAHKAMA kuu Zanzibar kisiwani Pemba, chini ya Jaji Ibrahim Mzee Ibrahim, imewapeleka rumande watumuhimwa wanne wanaokabiliwa na tuhuma za kuua kwa makusudi, akiwemo Ali Mussa Omar ‘ Mkapa’ mkaazi wa Wawi wilaya ya Chake chake Pemba. Watuhumiwa wengine walioanza maisha mapya ya rumande ni mtuhumiwa Yassir Mohamed Juma miaka 23, Anuwari Mussa Omar miaka 30 pamoja na mtuhumiwa Yassir Mussa Omar ‘ Makababu ’ miaka 29, wote wakaazi wa shehia ya Wawi, wilaya ya Chake chake Pemba. Awali watuhumiwa hao waliwasili mahakamani hapo, kwa mara ya kwanza, kwa ajili ya kusomewa tuhma zinazowakabili za kumuua kwa maksudi Said Seif Kombo. Ilidaiwa mahakamani hapo na Mwendesha Mashtaka kutoka Ofisi ya Mkurugenzi wa Mashataka Seif Mohamed Khamis akiambatana na mwenzake Mussa Khamis Ali kuwa, watuhumiwa hao kwa pamoja wanadaia kufanya mauwaji hayo kwa maksudi. Ilidai kuwa, watuhumiwa wote kwa pamoja, walitenda kosa hilo Oktoba 16, mwaka huu, baina ya saa 7:00 mchan

HII KALI MBUNGE ASIYA AMKOGESHA MWANANCHI HADHARANI KISA HICHI HAPA......

  NA HAJI NASSOR, PEMBA MBUNGE wa viti maalum nafasi za wanawake mkoa wa kaskazini Pemba Asiya Sharif Omar, amewataka wananchi wa kijiji cha taifu, shehia ya Kinyasini jimbo la Gando wilaya ya Wete Pemba, kuyalinda miundombinu ya maji safi na salama, ili yawe endelevu kwao. Kauli hiyo ameitoa wakati alipokuwa akizungumza na mwandishi wa habari hizi, mara baada ya kuwasili kijijini humo, na kumkogesha mwananchi mmoja kama ishara ya uzinduzi wa mradi wa maji safi na salama, ulioasisiwa na mbunge wa Jimbo la Gando. Alisema, hawana mbadala kwa sasa bali ni kuilinda miundombinu ya huduma hiyo, hasa baada ya mbunge wa wao Salim Mussa Omar, kuwarejeshea huduma hiyo. Alieleza kuwa, inafahamika kuwa kwa miaka 14 waliikosa huduma hiyo hasa kwa vile viongozi waliokuwepo hawakujali kuwatatulia tatizo hilo, hadi juzi ilipofanywa na mbunge wao. “Baada ya huduma hii sasa kurejeshwa na mbunge wa jimbo la Gando, kazi iliyobakia kwenu wananchi ni kila mmoja kuwa mlinzi wa miundombinu hii,’’ali

TUHMA ZA DAKTARI PEMBA KUCHIWA HURU: POLISI KASKAZINI KUTOA TAARIFA RASMI LEO

  NA HAJI NASSOR, PEMBA KAMANDA wa Polisi mkoa wa kaskazini Pemba, Juma Saad Khamis, amesema leo Mei 9, mwaka huu atatoa taarifa rasmi, juu ya kuendelea kumshikilia au kumpa dhamana ya Polisi, daktari wa Kituo cha Afya Gombani Is-haka Rashid Hadid, anayetuhumiwa kwa ubakaji. Alisema, kwa vile alikuwa katika mapumziko mafupi, haelewi jambo lolote linaloendelea kwa mtuhumiwa huyo, juu ya kuendelea kushikiliwa kwake kituoni hapo. Alieleza kuwa, leo Mei 6 (jana), hajapata taarifa za ndani za mtuhumiwa, huyo na kuwataka wananchi na wanaharakati, wasubirie hadi Jumatatu ijayo. Akizungumza na waandishi wa habari kwa nyakati tofauti Kamanda huyo, alisema hana taarifa zozote za kupewa dhamana mtuhumiwa ndani ya kituo chake cha Polisi au kuendelea kuwepo. ‘’Ilikuwa mimi sipo kazini kwa muda, kuanzia anakamatwa hadi anafikishwa Polisi, kwa sasa siwezi kueleza jambo lolote kwa mtuhumiwa huyo, hadi Jumatatu,’’alieleza. Aidha Kamanda huyo alieleza kuwa, kwa sasa hawezi kutoa ufafan

MADAKTARI KUTOKA CHINA WAOKOA MAISHA YA MTOTO PEMBA

  HABIBA ZARALI, PEMBA TIMU ya 32 ya madaktari wa kichina katika hospitali ya Abdalla Mzee Mkoani wamefanikiwa kufanya upasuaji mkubwa wa mtoto mwenye umri wa miaka 15 mkaazi wa Chole Kengeja, baada ya kuchomwa na jiti sehemu ya njia zake za mfumo wa uzazi. Mtoto huyo ambae alianguka hivi karibuni katika mti na baadae kuchomwa na jiti hilo na kumsababishia kutokwa na damu nyingi katika sehemu ya nyonga, alifanyiwa upasuaji uliodumu kwa muda wa saa tatu na   kuokolewa maisha yake. Akizungumza mara baada ya operesheni huo kiongozi wa timu hiyo Dr Jiang Jinhua, alisema mara baada ya mtoto huyo kufikishwa hospitalini hapo na kufanyiwa vipimo na kuonekana   ilibidi apatiwe rufaa ya kwenda katika hospitali nzuri yenye kutibu tatizo lake huko nchini Kuwado ambapo haikuwezekana kutokana na hali ya umaskini wa f amilia ya mtoto huyo . Alisema timu ya madaktari hao itaendelea kutowa huduma za matibabu   kwa wananchi kisiwani humo,   ili kuwaondolea gharama ya kutafuta matibabu nje ya nch