Skip to main content

MWANAMKE MIAKA 60 PEMBA ANUNUA MTUMBWI KWA RUZUKU YA TASAF

 

                              


NA HAJI NASSOR, PEMBA

BIBI Maryam Bakar Issa miaka 60, mkaazi wa shehia ya Ukunjwi, ni mmoja kati ya walengwa 14,280 wanaopokea fedha za mpango wa kunusuru kaya maskini, kutoka TASAF Pemba.

Mpango huo, kwake ulianza kumfikia miaka minane iliyopita, akipokea kati ya shilingi 30,000 hadi shilingi 44,000 kila baada ya miezi miwili, hutegemeana na kukidhi masharti.

Mpango huo ulikuwa na maana sana kwake, kwa vile mwaka 2013 kabla ya kuingia kwenye ruzuku, alifiliwa na mume wake na kumuachia watoto wawili wadogo, walioanza kumtegemea.

Kilomo cha muhogo, mpunga, migomba na kazi ya uvuvi wa chaza, ndio aliyokuwa kazi yake alikuwa akiitegemea kwa wakati huo kuendesha familia yake.

Maisha yalikuwa mazito, hasa pale anapokwenda pwani na kukosa chaza, vipando bado vichanga na dukani ana deni, na watoto wanahitaji walau mlo mmoja.

“Uwanawake wangu ulikuwa ni pale nnapokwenda pwani na kurudi na chaza, ili niziweke pamoja kwenye njiti za makuti kwa ajili ya biashara, ili nipate unga wa sembe na nyingine kuzifanya kitoweleo cha siku,’’anasema.

Wakati akiwa anavuna muhogo au ndizi, ndio kipindi alichokuwa na uhakika wa mlo wa siku na watoto wake mayatima, ingawa huwa ni kipindi kifupi.

Anasema kipindi cha jua, hutumia miale yake inayopenya kwa juu ya paa la nyumba yake, kufanya shughuli zake kutokana na makuti kuoza.

“Lakini hata usiku kama mwezi unang’aa, sikuwa nahitaji taa, kutokana na miale yake kuingia mwangu bila ya kizuizi, achia mbali mvua haina hodi,’’anasimulia.

Maisha ya kubahatisha, yaliyozaa dhiki, shida, na uchungu, wakati mwengine, yalipelekea watoto wake kusimamishwa masomo, kuanzia madrassa hadi skuli kwa wakati huo.

Hakuwa na tamaa kuwa, iko siku ataishi maisha ya furaha kama wengine, achia mbali kuishi kwenye nyumba ya kisasa yenye huduma za lazima.



BAADA YA KUFIKIWA NA MPANGO WA TASAF

Kwa mara ya kwanza, alipopokea taarifa kutoka kwa Sheha wake wa Ukunjwi, juu ya kuatakiwa kuorodhesha majina ya watoto wake, aliona ni pumbazo la viongozi.

“Nilipofuatwa na Sheha kuwa natakiwa kuandikisha majini ya watoto wangu na kisha nilipwe, nilikuwa na hakika jambo hilo haliwezekani,’’anasimulia.

Maana, anaona kwenye akili yake, ili mtu alipwe kwanza atanguliwe na kufanyakazi, ambapo wakati huo yeye akiwa ameshaanza kupungua nguvu.

Siku ya kujazishwa fomu, anasema ilifika na kisha kusbiria mwisho wa mwezi, ambapo aliahidiwa kulipwa na siku ilipofika, alikuwa mtu wa pili.

“Malipo ya mwanzo nilipotakiwa kwenda kusaini, hata msuwaki na kunawa uso nilisahau siku hiyo, maana ilikuwa roho na moyo wangu haukubali kuwa TASAF, inilipe kabla ya kufanyakazi,’’anahadithia.

Bibi Maryam ambae kwa sasa anatimiza miaka 60, anasema fedha hizo za mwanzo, alinunua mchele na samaki mnene na kula na watoto wake mapema.

Anakiri kuwa, fedha alizopewa alielezwa madhumuni yake, ikiwa ni pamoja na kuhakikisha watoto wanakwenda skuli kwa wakati, ununuzi wa vifaa husika.

Kuanzia hapo na mwezi mwengine, Bi Maryam anasema aliamini kuwa sasa, anataka kunusuriwa na umaskini, na elimu ya kuzifanyia shughuli nyingine fedha hizo, ili zizae.

Ilipofika mwaka 2018, anasema huku akiwa anaweka fedha hizo nusu kwenye hisa na watoto wake wakiongezeka umri, alimuita mtoto wake, mwenye miaka 18, kumpa wazo la kununua mtumbwi.

!!!!!...naam siku ikafika, bi Maryam ambae ni mlengwa wa kaya maskini, shehia ya Ukunjwi wilaya ya Wete, kununua mtumbwi kwa shilingi 300,000.

Wapi alikuwa akizitunza fedha hizo na muda gani, nilumuuliza na kusema kuwa, alikuwa akiziweka ndani mwake hadi kutimia kiwango cha ununuzi wa mtumbwi.

Aliacha kununua boda boda wala kuanzisha biashara, akisema kazi ya Ukunjwi ambayo ni rahisi ya yenye kipato cha haraka, ni uvuvi.

Anasema, sasa anaishi kwenye maisha ya furaha na kusahau yale madhila na machungu ya miaka karibu 50, aliyokuwa nayo.

“Mtoto wangu ndie anenivisha, kunilisha asubuhi na jioni na wakati mwengine hunipa fedha hadi kufiki shilingi 100,000 na huku bado naendelea kupokea kutoka TASAF,’’anasema.

Sasa bi Maryam, anasema haikimbii tena michango ya familia iwe ya harusi, ungonjwa au kufiliwa, maana wakati wowote akiba ya shilingi 100,000 hadi shilingi 300,000 kwake sio jambo kubwa.

 

Jee bibi Mrayam ni mvuvi wa mtumbwi, nilipomuuliza alisema alishaacha kuvua chaza kwa miguu miaka minne iliyopita, ingawa alimpa mtoto wake Abdi Abdalla Khamis.

MTOTO WA MLENGWA: ABDI ABDALLA KHAMIS

Yeye shuguli ya uvuvi, alianza mara tu baada ya kumaliza masomo yake darasa la 12, miaka miwili iliyopita, na kisha alipoamua kutaka kufungu ndoa, alitumia gharama wastani wa shilingi milioni 1, zilizotokana na mtumbwi huo.

Abdi, anasema ubunifu wa mama yake kuweka fedha hadi kufikia shilingi 300,000 na kumnunulia mtumbwi, ndio unaompa uhakika wa kuendesha familia yake, na mama yake kwa ujumla.



“Mtumbwi ulizaa mahari yangu ya ndoa ya kwanza, na hadi nilipoa tena mke wa pili shilingi 700,000 zilitoka kwenye mtumbwi ulionunuliwa na mama,’’anasema.

Kwa mwezi mmoja, huwa anakwenda baharini siku 15, kutokana na mabadiliko ya bahari, na hujiingizia kati ya shilingi 50,000 hadi 70,000 ingawa inategemea na bahari ilivyoamka.

Ndio maana, Abdi sasa kwa mwezi mmoja hujipatia kati ya shilingi 750,000 wastani wa shilingi 50,000 kwa siku 15 za mwezi, anazokwenda baharini.

Hapo utaona mvuvi huyo mwenye asili ya fedha za TASAF za shilingi 40,000 za mpango wa kunusuru kaya maskini, kwa mwaka anajipatia shilingi milioni 9,000,000.

Kwa sasa tayari, ameshanunu matofali 1000, kwa thamani ya shilingi milioni 1, akiweka malengo ya kujenga nyumba yao ya familia yenye vyumba vinne, kama lengo la mama yake lilivyo.

Miaka miwili ijayo, anatarajia amalize ujenzi wa nyumba hiyo, na kisha anampango wa kununua boda boda, kwa ajili ya kuongeza pato lake zaidi.

‘’Unajua fedha za TASAF ambazo mama anendelea kupata zimefika pahala ndipo, maana awali aliponikabdhi mtumbwi niliona kama vile sio sahihi, lakini sasa matunda yapo,’’anasema.

  SHEHA                                                                                               

Sheha wa shehia ya Ukunjwi Mkongwe Kassande Khamis, anasema, walengwa kama bibi Maryam kwenye shehia yake wapo zaidi ya 10.

Hao wamejiongeza na wamekuwa mfano wa kuukimbia umaskini, kwa kule kujiajiri wenyewe, kama ilivyo azma ya TASAF, kupitia mpango huo.

Shehia ya Ukunjwi yenye wakaazi 3,429 ingawa waliomo kwenye mpango huo walikuwa 239 na kwa sasa wanaondelea ni 215 baada ya wengine kufariki.

Vipo vikundi 12 vilivyoundwa na walengwa wa kaya maskini, ikihusishwa wananchi 240, ambao fedha zao wameamua kuzikukuza.

“Kwa hakika TASAF shehiani mwangu, inaendelea kuacha alama, maana sasa wapo wananchi wanaojenga nyumba za kudumu, walioanzisha miradi ya kimaendeleo kama ufugaji, mtumbwi na kilimo,’’anasema.

Anajivunia mlengwa kama bibi Maryam licha ya umri wake, lakini amebuni mradi wa mtumbwi, ambao sasa unamsaidia kimaisha.

TASAF

Mratibu wa TASAF Pemba Mussa Said, anasema wapo walengwa 14,280 kwa Pemba ambao wanaendelea kupata fedha za kunusuriwa na umaskini.

Walengwa hao wapo kwenye shehia 78 ikiwemo ya Ukunjwi, Tumbe Mashariki, Mgogoni, Kiwani, Ndagoni, Makangale  ambapo tayari shilingi bilioni 14. 4 zimeshwafikia.

Mtu kama bi Maryam ndio hasa ametimiza yale, malengo ya TASAF, ya kumtoa mwananchi katika unyonge wa kipato na chakula na kumleta kwenye taa.

“TASAF inaorodhesha ya zaidi ya walengwa 50,000 kutoka wastani wa walengwa 15 kila shehia, kati ya shehia 78, ambao wamenzisha miradi ya kujikwamua.

“Mtu kama bi Fatma wa Tumbe anaemiliki nyumba, Amina wa Mgogoni na mwenzake Mfake wenye mifugo, hatuna shaka, hawawezi kurudi tena kwenye umaskini wa kipato, wanafikia 50,000 kwa Pemba yote,’’anaeleza.

Mratibu Mussa anabainisha kuwa, kwa mwaka 2014/2015 walengwa hao wa kunusuru kaya maskini, waliibua miradi ya kijamii 41, idadi iliongozeka mwaka uliofuata kwa kufikia miradi 84.

Mwaka 2017/2018 walijukuta na miradi mengine ya kijamii 21, inayuhusisha upandaji miti kama vile Makangale, uazishwaji wa vitalu na ujenzi wa matuta ya kinga maji ya bahari Ndagoni, Kiwani, Micheweni na Tumbe.



Achia mbali idadi ya watu 50,000 waliojiwekeza wenyewe, vipo vikundi 942 vikizaa walengwa 12,000 vilivyoanzishwa, kuanzia mwaka 2014 hadi 2019, ingawa vilivyosajiliwa ni 700.

WANANCHI WA UKUNJWI

Imani Haji Khamis, anasema bibi Maryam ameona mbali kwa kule kumnunulia mtoto wake mtumbwi, kwa ajili ya kuendeleza sekta ya uvuvi.

Omar Hassan Shaibu anasema, moja ya shughuli adhimu ya shehia ya Ukunjwi ni bahari, hivyo wazo la bi Maryam kutumia fedha zake katika eneo hilo, hazikupotea.

Kazija Idd Abdi anasema, bi Maryam hakuamua kuingia kwenye ushirika wowote, na tulidhani anaweza kupotea njia kwenye kujikwamua na umaskini, lakini ni tofauti.

Mtoto wake ameshaanza ujenzi kupitia mtumbwi, ameshaoa pia lakini anaendesha maisha yake kwa uzuri, maana anavua peke yake anachokipata hagawani na mwengine.

                     Mwisho            

 

 

Comments

BLOG'S VISITORS

DAKTARI MWENGINE CHAKE CHAKE KULA SIKUKUU POLISI, NI KWA TUHUMA ZA KUMBAKA MGONJWA WAKE

NA WAANDISHI WETU, PEMBA::: DAKTARI anaetoa huduma kwa wagonjwa kituo cha afya cha serikali cha  Gombani wilaya ya Chake Chake Pemba, Is-haka Rashid Hadid, anaendelea kushikiliwa na Jeshi la Polisi Mkoa wa kaskazini Pemba, akituhumiwa kumtorosha na kisha kumbaka mtoto wa mwenye umri wa miaka 16, mkaazi wa Gombani. Daktari huyo miaka 35 ni mkaazi wa Kangagani Wilaya ya Wete mkoani humo, ambapo anadaiwa alimchukua mtoto huyo kutoka kwa rafiki yake, na kumpeleka kwenye nyumba anayoishi eneo la Kangagani. Mtoto aliefanyiwa kitendo hicho alisema kuwa, April 21 mwaka huu alikwenda kituo cha afya Gombani, kwa ajili ya matibabu na baada ya kupatiwa huduma na daktari huyo, alimuomba nambari yake ya simu. Alisema ilipofika usiku, walikuwa wanawasiliana kupitia ujumbe mfupi (sms) kwa lengo la kwenda kuchukua dawa nyingine ambazo kwa mchana huo alizikosa hospitalini hapo. "Nilikwenda hospitali kutibiwa, baada ya kufanya mapele katika sehemu zangu za siri, lakini akaniambia mpaka aje da

'MKAPA' NA WENZAKE PEMBA WALAZWA RUMANDE

  NA HAJI NASSOR, PEMBA@@@@ MAHKAMA kuu Zanzibar kisiwani Pemba, chini ya Jaji Ibrahim Mzee Ibrahim, imewapeleka rumande watumuhimwa wanne wanaokabiliwa na tuhuma za kuua kwa makusudi, akiwemo Ali Mussa Omar ‘ Mkapa’ mkaazi wa Wawi wilaya ya Chake chake Pemba. Watuhumiwa wengine walioanza maisha mapya ya rumande ni mtuhumiwa Yassir Mohamed Juma miaka 23, Anuwari Mussa Omar miaka 30 pamoja na mtuhumiwa Yassir Mussa Omar ‘ Makababu ’ miaka 29, wote wakaazi wa shehia ya Wawi, wilaya ya Chake chake Pemba. Awali watuhumiwa hao waliwasili mahakamani hapo, kwa mara ya kwanza, kwa ajili ya kusomewa tuhma zinazowakabili za kumuua kwa maksudi Said Seif Kombo. Ilidaiwa mahakamani hapo na Mwendesha Mashtaka kutoka Ofisi ya Mkurugenzi wa Mashataka Seif Mohamed Khamis akiambatana na mwenzake Mussa Khamis Ali kuwa, watuhumiwa hao kwa pamoja wanadaia kufanya mauwaji hayo kwa maksudi. Ilidai kuwa, watuhumiwa wote kwa pamoja, walitenda kosa hilo Oktoba 16, mwaka huu, baina ya saa 7:00 mchan

HII KALI MBUNGE ASIYA AMKOGESHA MWANANCHI HADHARANI KISA HICHI HAPA......

  NA HAJI NASSOR, PEMBA MBUNGE wa viti maalum nafasi za wanawake mkoa wa kaskazini Pemba Asiya Sharif Omar, amewataka wananchi wa kijiji cha taifu, shehia ya Kinyasini jimbo la Gando wilaya ya Wete Pemba, kuyalinda miundombinu ya maji safi na salama, ili yawe endelevu kwao. Kauli hiyo ameitoa wakati alipokuwa akizungumza na mwandishi wa habari hizi, mara baada ya kuwasili kijijini humo, na kumkogesha mwananchi mmoja kama ishara ya uzinduzi wa mradi wa maji safi na salama, ulioasisiwa na mbunge wa Jimbo la Gando. Alisema, hawana mbadala kwa sasa bali ni kuilinda miundombinu ya huduma hiyo, hasa baada ya mbunge wa wao Salim Mussa Omar, kuwarejeshea huduma hiyo. Alieleza kuwa, inafahamika kuwa kwa miaka 14 waliikosa huduma hiyo hasa kwa vile viongozi waliokuwepo hawakujali kuwatatulia tatizo hilo, hadi juzi ilipofanywa na mbunge wao. “Baada ya huduma hii sasa kurejeshwa na mbunge wa jimbo la Gando, kazi iliyobakia kwenu wananchi ni kila mmoja kuwa mlinzi wa miundombinu hii,’’ali

TUHMA ZA DAKTARI PEMBA KUCHIWA HURU: POLISI KASKAZINI KUTOA TAARIFA RASMI LEO

  NA HAJI NASSOR, PEMBA KAMANDA wa Polisi mkoa wa kaskazini Pemba, Juma Saad Khamis, amesema leo Mei 9, mwaka huu atatoa taarifa rasmi, juu ya kuendelea kumshikilia au kumpa dhamana ya Polisi, daktari wa Kituo cha Afya Gombani Is-haka Rashid Hadid, anayetuhumiwa kwa ubakaji. Alisema, kwa vile alikuwa katika mapumziko mafupi, haelewi jambo lolote linaloendelea kwa mtuhumiwa huyo, juu ya kuendelea kushikiliwa kwake kituoni hapo. Alieleza kuwa, leo Mei 6 (jana), hajapata taarifa za ndani za mtuhumiwa, huyo na kuwataka wananchi na wanaharakati, wasubirie hadi Jumatatu ijayo. Akizungumza na waandishi wa habari kwa nyakati tofauti Kamanda huyo, alisema hana taarifa zozote za kupewa dhamana mtuhumiwa ndani ya kituo chake cha Polisi au kuendelea kuwepo. ‘’Ilikuwa mimi sipo kazini kwa muda, kuanzia anakamatwa hadi anafikishwa Polisi, kwa sasa siwezi kueleza jambo lolote kwa mtuhumiwa huyo, hadi Jumatatu,’’alieleza. Aidha Kamanda huyo alieleza kuwa, kwa sasa hawezi kutoa ufafan

MADAKTARI KUTOKA CHINA WAOKOA MAISHA YA MTOTO PEMBA

  HABIBA ZARALI, PEMBA TIMU ya 32 ya madaktari wa kichina katika hospitali ya Abdalla Mzee Mkoani wamefanikiwa kufanya upasuaji mkubwa wa mtoto mwenye umri wa miaka 15 mkaazi wa Chole Kengeja, baada ya kuchomwa na jiti sehemu ya njia zake za mfumo wa uzazi. Mtoto huyo ambae alianguka hivi karibuni katika mti na baadae kuchomwa na jiti hilo na kumsababishia kutokwa na damu nyingi katika sehemu ya nyonga, alifanyiwa upasuaji uliodumu kwa muda wa saa tatu na   kuokolewa maisha yake. Akizungumza mara baada ya operesheni huo kiongozi wa timu hiyo Dr Jiang Jinhua, alisema mara baada ya mtoto huyo kufikishwa hospitalini hapo na kufanyiwa vipimo na kuonekana   ilibidi apatiwe rufaa ya kwenda katika hospitali nzuri yenye kutibu tatizo lake huko nchini Kuwado ambapo haikuwezekana kutokana na hali ya umaskini wa f amilia ya mtoto huyo . Alisema timu ya madaktari hao itaendelea kutowa huduma za matibabu   kwa wananchi kisiwani humo,   ili kuwaondolea gharama ya kutafuta matibabu nje ya nch