Skip to main content

WADAU WATAKA SHERIA ZINAZOGUSA TASNIA YA HABARI KUFANYIWA MAREKEBISHO, WASEMA ZIMEEGEMEA SERIKALINI ZAIDI

 



 

NA MWANDISHI MAALUM, ZANZIBAR

KILA raia katika nchi hii anastahili kupata haki zake za msingi za kila siku awe mtu mwenye ulemavu au asiye na ulemavu, Mwanamke na mwanamme, watoto, wazee na vijana.

Hivyo basi panapozungumzwa haki ni kwamba makundi yote yana haki katika jamii na taifa kwa ujumla.

Kwa mfano katiba zote mbili za Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na ile ya Zanzibar zimezungumzia waziwazi haki za msingi kwa raia wote bila ya ubaguzi.

Hivi karibuni Wanaharakati na wadau wa masuala ya habari walipitia baadhi ya sheria zinazohusiana na habari ikiwa ni pamoja na kuangalia, kujadili, kushauri na kupendekeza utendaji mzuri wa usimamizi wa mchakato mzima na mwenendo wa sheria zinazogusa vyombo vya habari na wanahabari kwa ujumla.

SHERIA ZINAZOGUSA TASNIA YA HABARI

Miongoni mwa sheria hizo ni kuangalia Mianya ya kisheria katika Sheria ya Usajili wa Wakala wa Habari, Magazeti na Vitabu namba 5 ya mwaka 1988 iliyofanyiwa marekebisho na Sheria No.8 ya 1997 sambamba na Sheria ya Tume ya Utangazaji ya Zanzibar namba 7 ya mwaka 1997 kama ilivyorekebishwa na sheria namba 1 ya mwaka 2010.

Kama inavyoeleweka kuwa Haki ya Uhuru wa kujieleza  Ibara ya 18 ya katiba ya Zanzibar 18(1) imezungumza Bila ya kuathiri sheria zinazohusika za nchi, kila mtu anayo haki ya uhuru wa maoni na kutafuta, kupokea, kutoa au kusambaza habari na mawazo yake kupitia chombo chochote cha habari bila ya kujali mipaka ya nchi na pia ana haki ya mawasiliano yake kutoingiliwa.

Hivyo wadau hao walisema neno “bila kuathiri sheria za nchi” irekebishwe kwa sababu inaondosha uhuru wa kujieleza na haki ya kupata habari.

Akitoa maoni yake mwandishi mkongwe na mkufunzi wa mambo ya habari hapa Zanzibar Salim Said Salim, alisema kuwa kifungu hichi kinaonesha ni namna gani jinsi sentensi hii inavyokiuka uhuru wa kujieleza kuhusiana na sheria nyingine za nchi.

“Ipo haja ya kuangaliwa upya kifungu hichi kwani kinanyima haki za raia kujieleza na kutoa maoni yao”, alisema.

Kuhusana na Uteuzi wa Msajili Kifungu cha 3 – Waziri, kwa taarifa katika Gazeti la Serikali, atamteua Msajili wa Vitabu na Magazeti kutekeleza majukumu na kutekeleza mamlaka aliyopewa Msajili na Sheria hii na kanuni zozote zitakazotungwa chini yake, na anaweza kuteua Naibu Msajili ambaye atapatikana kwa maelekezo ya Msajili. 

Kwa mukhtadha huu Sheria inampa Waziri mamlaka ya kuteua Msajili wa Vitabu na Magazeti. Lakini iko kimya juu ya sifa na uzoefu.

Hivyo Said Salim alisema Msajili asihusishwe katika uteuzi wa naibu msajili na kusema kuwa ni vyema kwa nafasi ya Msajili itangazwe na achaguliwe kwa mujibu wa sifa. Mfano awe mwanasheria au mtu mwenye taaluma ya habari na mawasiliano ya umma.

Sambamba na hilo, lakini wadau kwa pamoja walisema ni vyema sifa za msajili zinapaswa kuainishwa katika sheria.

“Kazi ya uteuzi wa Naibu Msajili pia ifanywe kwa kuzingatia weledi (sifa zake zielezwe kwenye kanuni) Iwe ni nafasi itakayojazwa kwa mtu kuomba na kufanyiwa usaili”, alisema.

Sambamba na hayo lakini kifungu cha 27 (2) Hakimu yeyote anaweza kutoa hati kumuidhinisha afisa polisi yeyote wa cheo cha Inspekta, kwa msaada au bila msaada kuingia na kupekua mahali popote pale ambapo inashukiwa kuwa kuna gazeti linachapishwa kinyume na Sheria hii linafanya kosa  chini ya Sheria hii au kanuni zozote zilizotungwa ama limefanya, linafanya au linakaribia kufanya kosa, hivyo anaweza kukamata gazeti lolote linalopatikana humo ama kwa  kushuku kuwa kuna gazeti lilichapishwa au linachapishwa pamoja na ushahidi mwingine wowote wa kutenda kosa chini ya Sheria hii au kanuni zozote zilizopo/zitakazopatikana.

“Kifungu hiki hakipo sawa na ni cha ukandamizaji wa uhuru wa habari. Hili ni suala ambalo lalamiko linapaswa lipelekwe katika Bodi ya Ushauri (huduma za habari) litolewe uamuzi, ikishindikana lipelekwe mahakamani na hapo ndipo mahakama itoe hati ya upekuzi.  Polisi wa ngazi yoyote asichukue jukumu la kupekua na kukamata kabla ya lalamiko kuthibitishwa”, alisema Jabir Yunus.

Alisema kuwa Katika zama hizi za utandawazi, kifungu hiki hakistahili kuwapo kwa kuwa hakina maslahi na uhuru wa vyombo vya habari.

Aidha wadau hao walitilia mashaka kifungu cha 30 (i) ambacho kinasema kuwa Endapo Waziri anaona kuwa ni kwa manufaa ya umma au kwa maslahi ya amani na utulivu, anaweza kuamuru kufungiwa kwa gazeti... na gazeti hilo litakoma kuchapishwa kuanzia tarehe iliyotajwa.  



“Waziri amepewa mamlaka makubwa ya kuamua kufungia magazeti. Mamlaka haya yalipaswa kupewa Bodi ya Huduma za Habari baada ya Waziri kuitaarifu bodi kuhusu uamuzi wake wa kulisimamisha/kulifungia gazeti, hivyo walisema kifungu hiki hakina maslahi na uhuru wa habari.

Aidha Makosa ya uchochezi na kashfa yaliyopo Kifungu cha 48 - kinaeleza makosa ikiwa ni pamoja na uchochezi na kashfa kwa mtu yeyote ambaye anachapisha, kuchapisha, kuuza, kusambaza au kutoa chapisho lolote la uchochezi na baada ya kukutwa na hatia mtu huyo faini au kifungo au vyote viwili faini na kifungo vitatolewa na uchapishaji huo utatolewa. itakabidhiwa kwa serikali.

Kifungu hiki kinapunguza sio tu uhuru wa vyombo vya habari lakini pia kinahatarisha uhuru wa kujieleza kwa jumla. Inapendelea zaidi upande wa maslahi ya Serikali na kuzalisha maslahi ya kisiasa.

Hivyo waliomba Maudhui ya kashfa ya vyombo vya habari yadhibitiwe kwa njia ya kiraia badala ya jinai.

Masharti ya Kashfa yametangazwa na Mahakama ya Afrika Mashariki kwa vile ni miongoni mwa masharti yanayokiuka Mkataba wa Jumuiya ya Afrika Mashariki.        

Kuhusiana na Upatikanaji wa taarifa hakuna kifungu cha Sheria haijatoa sehemu ya ufikiaji wa habari ambayo ni muhimu vile vile.

“Tunapendekeza kiwepo kifungu maalum kitakachozungumzia upatikanaji wa habari, walisema wadau hao wa habari.

TAMWA ZANZIBAR

Mapema Dk Mzuri Ali Issa, akitoa maoni yake katika moja ya mkutano wa majadiliano ya sheria mpya ya habari uliofanyika alisema ingawa uhuru wa habari upo lakini unatolewa kwa njia moja na kunyang’anywa kwa njia nyengine.

“Kweli uhuru wa habari upo, lakini upande mwengine haupatikani hivyo sheria mpya ni lazima iweke mazingira mazuri kwa maslahi ya pande zote mbili ya serikali na wanahabari”, alisema.

Kwa upande wa sheria ya Tume ya Utangazaji ya Zanzibar namba 7 ya mwaka 1997 kama ilivyorekebishwa na sheria namba 1 ya mwaka 2010 wa Muundo wa Tume   Kifungu cha 6(1) Tume ya Utangazaji ni lazima ioneshe vyombo vya habari na mambo yote ya kijinsia.

“Ziko picha zinaoneshwa kwenye televisheni zinawadhalilisha wanawake, baadhi ya mambo hayonekani hivyo kama tume iangalie hilo na kuwachukulia hatua za kisheria wahusika”, alisema.

“Waziri amepewa mamlaka ya kuteua wajumbe zaidi ya wanne wa Tume; hakuna pahali palipopendekezwa uwakilishi wa wadau wala jinsia Ni vizuri kama kabla Waziri hajateua wajumbe wa Tume apate mapendekezo ya wadau.  Kadhalika sifa za wajumbe hawa ziainishwe kwenye Kanuni”, alisema Dk. Mzuri ambae ni Mkurugenzi wa TAMWA Zanzibar alisema Suala la jinsia liangaliwe kwa umuhimu wake.

Pia Dk. Mzuri aligusia kuhusiana na Tume ya uchaguzi, alisema haijawahi tume hiyo kuongozwa na mwanamke, na ni makamu amewahi kutokea kwa nafasi hiyo na kati ya makamishna saba nafasi huwa ni moja tu kwa mwanamke katika vipindi vyote vya tume hiyo.




Sambamba na hilo, lakini alisema kuwa kiujumla wake tume hiyo imekuwa na watendaji wengi wanaume kuliko wanawake jambo ambalo mambo mengi yanayowahusu wanawake hutatuliwa na wanaume hasa katika mchakato mzima wa uchaguzi.

“Wanawake, vijana, watu wenye ulemavu wanakosa nafasi katika uandikishaji, na mambo yote ya uchaguzi jambo ambalo linnahitaji kuangaliwa kwa umakini hasa katika uteuzi na uajiri”, aliongeza Dk. Mzuri.

“Lazima kuwe na mwongozo maalum katika kila hatua ya uchaguzi kuanzia uandikishaji, utoaji wa elimu ya uraia, uteuzi wa wagombea, usimamizi wa uchaguzi, upigaji kura, utoaji wa matokeo na hali ya usalama na kwamba suala la usawa wa kijinsia na ujumuishi liongoze mchakato wote wa uchaguzi kabla, wakati na baada”, aliongeza Dk. Mzuri.

Wadau walisema Tume imepewa mamlaka makubwa ya kuelekeza juu ya aina ya maudhui ambayo vyombo vya habari vya kielektroniki vinapaswa kuyashughulikia. Hivyo, mamlaka haya iliyopewa Tume yanaweza kuathiri uhuru wa vyombo vya habari.

Kazi ya Tume katika sehemu hii inapaswa kuwa ni kushauri tu kuhusu ubora wa maudhui ya kurushwa hewani badala ya kuelekeza.

BARAZA LA HABARI TANZANIA (MCT)

Nae Shifaa Said Hassan, Afisa mdhamini wa Baraza la Habari Tanzania (MCT) upande wa Zanzibar, alisema sheria ya Tume ya uchaguzi Zanzibar (ZEC) alisema ina mapungufu sambamba na kupendekeza baadhi ya mambo kufanyiwa kazi na ZEC kwa lengo la kuleta uwiano wa kijinsia.

“Kwa mfano wanahabari ndio wanaoaminiwa kwenye jamii, hivyo wanapaswa kushirikishwa kikamilifu katika mchakato mzima wa uchaguzi bila ya vikwazo, lakini hapo katikati hukutana na vikwazo vingi hata wakati mwengine havimo kwenye sheria”, alisema.

Aliongeza kuwa Utafiti mdogo wa kupitia Sera ya Jinsia na Ujumiushi (Gender and Social Inclusion Policy) ya (ZEC) ya mwaka 2015 umebaini kuweko kwa mapungufu yaliyosabisha wanawake, vijana na watu wenye ulemavu kutoshiriki ipasavyo katika mchakato wa chaguzi zilizopita, ambayo yanapaswa kufanyiwa kazi ili sheria iwe na mashiko.

ASASI YA VIJANA ZANZIBAR WANAZUNGUMZAJE (ZYF)

Dadi Kombo, alisema kuwa sera hiyo si rafiki sana kwa kuwa kwenye Makamishna hakuna kijana ambae yuko katika nafasi hizo muhimu za juu.

“Kundi la vijana ndilo kubwa na la wanawake hapa Tanzania mbali na zile nafasi za muda za tume hasa wakati wa uchaguzi basi makundi hayo mawili hakuna yanavyofaidika kwa kuwa nafasi nyingi zimehodhiwa na wanaume na watu wa rika kubwa”, alisema.

Alisema kama wao wadau walibaini mapungufu mbalimbali ikiwamo kutokuwa na mwongozo na mpango mkakati wa kuitekeleza sera ya jinsia na ujumuishi ambayo imeundwa maalum kwa ajili ya kuangalia ujumuishi na haki za kijinsia.

Aidha alisema, vijana na watu wenye ulemavu zinazingatiwa katika mchakato mzima wa uchaguzi ili demokrasia siyo tu itendeke bali ionekane kuwa inatendeka.

Dadi alisema ili kuhakikisha usawa wa kijisia na ujumuishi unafikiwa kwa kila hatua ya uchaguzi ZEC inapaswa kukutana na wadau wa masuala ya jinsia, vijana na watu wa makundi yote pamoja na wanahabari mara kwa mara ili kuona hali ikoje na kuweka mpango wa utekelezaji ili pia kusaidia katika ukusanyaji wa takwimu kama sera na sheria zilivyosema kuwa ZEC itakuwa na mfumo madhubuti wa ukusanyaji wa takwimu (Systematically Data Collection).

JUMUIYA YA WANAWAKE WENYE ULEMAVU ZANZIBAR (JUWAUZA)

Mwenyekiti wa JUWAUZA, Salma Saadat alisema pia katika utafiti wamebaini uwepo wa kamati ya maadili ya ZEC, ni wa muda mfupi, huundwa wakati wa uchaguzi na uhai wake humalizika mara tu baada ya uchaguzi kwisha.

Aidha alisema kamati hiyo haijawekewa mwongozo wa kushughulikia malalamiko wala haina mwongozo wa kutatua vitendo vya udhalilishaji wanavyofanyiwa wanawake, vijana na watu wenye ulemavu na wanahabari wakati wa uchaguzi.

“Kuna wanawake au wanahabari walifanyiwa vitendo vya udhalilishaji wakati wa uchaguzi lakini hawajui waende wapi kupeleka kesi zao, kwa sababu kamati haina mwongozo wa kutatua kesi za mtu mmoja mmoja.

Hivyo alipendekeza sera na sheria ziweke miongozo na mpango kazi ili ikidhi haja kwa wanawake, vijana na watu wenye ulemavu kushiriki ipasavyo katika mchakato mzima wa uchaguzi kama wapiga kura, wagombea, wafuatiliaji ilani na sera za vyama na hata kuhakikisha kuwa usalama wao unalindwa vyema.

Mapema Afisa mwandamizi wa JUWAUZA, Haura Shamte, alisema kuwa sera ya Tume ya uchaguzi ni nzuri sana nay a kupigiwa mfano si kwa Afrika hata duniani kwa ujumla.

Alisema nchi kadhaa zimekopia namna ya uzuri wa sera ya Tume ya uchaguzi Zanzibar, lakini utekelezaji wake bado ni mdogo ukilinganisha na uzuri wake.



“Sera yetu ya uchaguzi Zanzibar ni nzuri, lakini haitekelezwi hivyo tutapeleka mapendekezo yetu ikiwa ni pamoja na kutaka makamishna wa tume kuongezeka idadi ya wanawake”, alisema.

Aidha alisema kuwa wanakusudia kuishawishi tume kungalia nafasi mbalimbali kama za rasilimali watu juu ya kuwashirikisha wanawake, vijana na watu wenye ulemavu hasa ikizingatiwa kuwa ni taasisi muhimu inayowagusa watu wengi.

MTANDAO WA JINSIA ZANZIBAR (ZGC)

Asha Aboud Mzee ambae ni Mwenyekiti wa Mtandao wa jinsia Zanzibar (ZGC) alisema wakati umefika sasa tume kuitathmini sheria ya habari, Tume ya utangazaji nay a Baraza la wawakilishi namna ya ufanyaji kazi wake.

Alisema yapo mambo mengi yanayohitaji kuhimizwa utekelezwaji wake jambo ambalo litaonesha namna ya ushiriki wa makundi yote katika tume ya uchaguzi.

“Wanawake, vijana, watu wenye ulemavu na wanahabari wanaotupa taarifa wanakosa nafasi katika mambo yengi na yanapokuwa hayo ni ya muda mfupi tu hivyo tunaomba sera na sheria yake penye mapungufu itekelezwe kwa udhati kabisa na kuwekwa takwimu sahihi za ushiriki wa makundi hayo”, alisema.

Aidha Wadau wamependekeza Sera ya Jinsia na Ujumishi ya ZEC ipitiwe tena pamoja na kuipangia mpango kazi ili iweze kutekelezeka, jambo ambalo litaweka fursa sawa kwa makundi hayo.

KUFANYIWA MAREKEBISHO YA KATIBA

Vile vile katika mapendekezo wadau wameomba katiba ya Zanzibar ya mwaka 1984 ifanyiwe marekebisho ili wanawake waweze kuteuliwa kwenye nafasi ya Makamishna wa Tume ya Uchaguzi Zanzibar, kwa sababu katiba iliyopo sasa haimlazimishi Rais wa Zanzibar kuzingatia usawa wa jinsia wakati wa kuteua Makamishna wa Tume hiyo.

“Tunafahamu kuwa mamlaka ya uteuzi wa makamishna siyo wa ZEC kwa kuwa imeainishwa katika Katiba ya nchi kwamba mwenyekiti na wajumbe wengine wawili watateuliwa na rais, ambapo kati ya hao lazima mmoja awe jaji na wajumbe wengine wanne watatoka katika vyama vya siasa.

“Ili kuhakikisha kwamba ZEC inasimamia vyema Sera yake ya Jinsia na Ujumuishi ilisema kwamba mara kwa mara itakua inapendekeza kufanya marekebisho ya katiba ili masuala ya jinsia na ujumuishi yaingie katika katiba na kuifanya sera hii itekelezeke, hivyo tunashauri hatua hiyo ifanywe mapema iwezekanavyo kabla ya uchaguzi mkuu mwingine kwa sababu kumalizika kwa uchaguzi ni mwanzo wa uchaguzi mwingine,” alisisitiza Bi Asha Aboud.

SHERIA NA MIKATABA MBALIMBALI YA KIMATAIFA

Ni ukweli usiopingika kuwa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar bado haijatekeleza vyema matakwa ya katiba ya Zanzibar ya mwaka 1982 juu ya haki na fursa sawa kwa baadhi ya mmabo hasa nafasi za wanawake katika serikali na vyombo vya maamuzi.

Hayo yalikuja baada ya wanawake wengi kunyimwa fursa ya kupata nafasi ya kugombea majimboni katika uchaguzi mkuu wa mwaka 2020.

Hata hivyo, Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Hussein Ali Mwinyi, amekuwa akiwachagua wanawake kama alivyoahidi katika teuzi zake mbalimbali za nyadhifa za juu serikalini.

Kwa mfano Ibara ya 8 kifungu cha 111 (b) kinasema ni lazima kukuza katika ngazi zote za mfumo wa elimu, ikijumuisha watoto wote wakiwa na umri mdogo, ikiheshimu haki za watu wenye ulemavu.

Pia ibara hiyohiyo kifungu cha 4 kinasema ili kuhakikisha haki hii inapatikana nchi zilizoridhia mkataba zitachukua hatua zinazofaa kuajiri watu maalumu, wakiwemo watu wenye ulemavu wenye utaalamu na mkundi mengine ya pembezoni.

Aidha kifungu cha 5 kinaeleza nchi zilizoridhia mkataba zitahakikisha kwamba watu wenye ulemavu wanaweza kupata haki yao ya kiraia ikiwemo hilo la kuchagua na kuchaguliwa bila ya ubaguzi kwa misingi sawa na wengine, ili kufikia hatua hii nchi zilizoridhia mkataba zitahakikisha kwamba mahitaji ya watu wenye ulemavu yanashughulikiwa.

Kimsingi mengi ya hayo yanahitaji kufanyiwa kazi kwa weledi kabisa ili kuona makundi yote yanajumuishwa sambamba na kuwawekea mazingira mazuri wanahabari ambao nao hawataathiri mitazamo ya serikali kwa njia moja ama nyengine kwani lengo ni kuwa pande zote mbili zifanye kazi kwa maslahi ya mapana ya nchi na wananchi wake.

Hivyo, ili kuleta mabadiliko, Serikali inahitaji kuchukua juhudi za makusudi kuzifanyia kazi sheria kinzani zinazohusiana na mambo ya habari kama sheria ya Tume ya Utangazaji ya Zanzibar, Sheria ya habari ya Zanzibar na sheria ya Baraza la wawakilishi ya Zanzibar ambazo zote zina haki za msingi na kikatiba.

                        MWISHO 

Comments

BLOG'S VISITORS

DAKTARI MWENGINE CHAKE CHAKE KULA SIKUKUU POLISI, NI KWA TUHUMA ZA KUMBAKA MGONJWA WAKE

NA WAANDISHI WETU, PEMBA::: DAKTARI anaetoa huduma kwa wagonjwa kituo cha afya cha serikali cha  Gombani wilaya ya Chake Chake Pemba, Is-haka Rashid Hadid, anaendelea kushikiliwa na Jeshi la Polisi Mkoa wa kaskazini Pemba, akituhumiwa kumtorosha na kisha kumbaka mtoto wa mwenye umri wa miaka 16, mkaazi wa Gombani. Daktari huyo miaka 35 ni mkaazi wa Kangagani Wilaya ya Wete mkoani humo, ambapo anadaiwa alimchukua mtoto huyo kutoka kwa rafiki yake, na kumpeleka kwenye nyumba anayoishi eneo la Kangagani. Mtoto aliefanyiwa kitendo hicho alisema kuwa, April 21 mwaka huu alikwenda kituo cha afya Gombani, kwa ajili ya matibabu na baada ya kupatiwa huduma na daktari huyo, alimuomba nambari yake ya simu. Alisema ilipofika usiku, walikuwa wanawasiliana kupitia ujumbe mfupi (sms) kwa lengo la kwenda kuchukua dawa nyingine ambazo kwa mchana huo alizikosa hospitalini hapo. "Nilikwenda hospitali kutibiwa, baada ya kufanya mapele katika sehemu zangu za siri, lakini akaniambia mpaka aje da

'MKAPA' NA WENZAKE PEMBA WALAZWA RUMANDE

  NA HAJI NASSOR, PEMBA@@@@ MAHKAMA kuu Zanzibar kisiwani Pemba, chini ya Jaji Ibrahim Mzee Ibrahim, imewapeleka rumande watumuhimwa wanne wanaokabiliwa na tuhuma za kuua kwa makusudi, akiwemo Ali Mussa Omar ‘ Mkapa’ mkaazi wa Wawi wilaya ya Chake chake Pemba. Watuhumiwa wengine walioanza maisha mapya ya rumande ni mtuhumiwa Yassir Mohamed Juma miaka 23, Anuwari Mussa Omar miaka 30 pamoja na mtuhumiwa Yassir Mussa Omar ‘ Makababu ’ miaka 29, wote wakaazi wa shehia ya Wawi, wilaya ya Chake chake Pemba. Awali watuhumiwa hao waliwasili mahakamani hapo, kwa mara ya kwanza, kwa ajili ya kusomewa tuhma zinazowakabili za kumuua kwa maksudi Said Seif Kombo. Ilidaiwa mahakamani hapo na Mwendesha Mashtaka kutoka Ofisi ya Mkurugenzi wa Mashataka Seif Mohamed Khamis akiambatana na mwenzake Mussa Khamis Ali kuwa, watuhumiwa hao kwa pamoja wanadaia kufanya mauwaji hayo kwa maksudi. Ilidai kuwa, watuhumiwa wote kwa pamoja, walitenda kosa hilo Oktoba 16, mwaka huu, baina ya saa 7:00 mchan

HII KALI MBUNGE ASIYA AMKOGESHA MWANANCHI HADHARANI KISA HICHI HAPA......

  NA HAJI NASSOR, PEMBA MBUNGE wa viti maalum nafasi za wanawake mkoa wa kaskazini Pemba Asiya Sharif Omar, amewataka wananchi wa kijiji cha taifu, shehia ya Kinyasini jimbo la Gando wilaya ya Wete Pemba, kuyalinda miundombinu ya maji safi na salama, ili yawe endelevu kwao. Kauli hiyo ameitoa wakati alipokuwa akizungumza na mwandishi wa habari hizi, mara baada ya kuwasili kijijini humo, na kumkogesha mwananchi mmoja kama ishara ya uzinduzi wa mradi wa maji safi na salama, ulioasisiwa na mbunge wa Jimbo la Gando. Alisema, hawana mbadala kwa sasa bali ni kuilinda miundombinu ya huduma hiyo, hasa baada ya mbunge wa wao Salim Mussa Omar, kuwarejeshea huduma hiyo. Alieleza kuwa, inafahamika kuwa kwa miaka 14 waliikosa huduma hiyo hasa kwa vile viongozi waliokuwepo hawakujali kuwatatulia tatizo hilo, hadi juzi ilipofanywa na mbunge wao. “Baada ya huduma hii sasa kurejeshwa na mbunge wa jimbo la Gando, kazi iliyobakia kwenu wananchi ni kila mmoja kuwa mlinzi wa miundombinu hii,’’ali

TUHMA ZA DAKTARI PEMBA KUCHIWA HURU: POLISI KASKAZINI KUTOA TAARIFA RASMI LEO

  NA HAJI NASSOR, PEMBA KAMANDA wa Polisi mkoa wa kaskazini Pemba, Juma Saad Khamis, amesema leo Mei 9, mwaka huu atatoa taarifa rasmi, juu ya kuendelea kumshikilia au kumpa dhamana ya Polisi, daktari wa Kituo cha Afya Gombani Is-haka Rashid Hadid, anayetuhumiwa kwa ubakaji. Alisema, kwa vile alikuwa katika mapumziko mafupi, haelewi jambo lolote linaloendelea kwa mtuhumiwa huyo, juu ya kuendelea kushikiliwa kwake kituoni hapo. Alieleza kuwa, leo Mei 6 (jana), hajapata taarifa za ndani za mtuhumiwa, huyo na kuwataka wananchi na wanaharakati, wasubirie hadi Jumatatu ijayo. Akizungumza na waandishi wa habari kwa nyakati tofauti Kamanda huyo, alisema hana taarifa zozote za kupewa dhamana mtuhumiwa ndani ya kituo chake cha Polisi au kuendelea kuwepo. ‘’Ilikuwa mimi sipo kazini kwa muda, kuanzia anakamatwa hadi anafikishwa Polisi, kwa sasa siwezi kueleza jambo lolote kwa mtuhumiwa huyo, hadi Jumatatu,’’alieleza. Aidha Kamanda huyo alieleza kuwa, kwa sasa hawezi kutoa ufafan

MADAKTARI KUTOKA CHINA WAOKOA MAISHA YA MTOTO PEMBA

  HABIBA ZARALI, PEMBA TIMU ya 32 ya madaktari wa kichina katika hospitali ya Abdalla Mzee Mkoani wamefanikiwa kufanya upasuaji mkubwa wa mtoto mwenye umri wa miaka 15 mkaazi wa Chole Kengeja, baada ya kuchomwa na jiti sehemu ya njia zake za mfumo wa uzazi. Mtoto huyo ambae alianguka hivi karibuni katika mti na baadae kuchomwa na jiti hilo na kumsababishia kutokwa na damu nyingi katika sehemu ya nyonga, alifanyiwa upasuaji uliodumu kwa muda wa saa tatu na   kuokolewa maisha yake. Akizungumza mara baada ya operesheni huo kiongozi wa timu hiyo Dr Jiang Jinhua, alisema mara baada ya mtoto huyo kufikishwa hospitalini hapo na kufanyiwa vipimo na kuonekana   ilibidi apatiwe rufaa ya kwenda katika hospitali nzuri yenye kutibu tatizo lake huko nchini Kuwado ambapo haikuwezekana kutokana na hali ya umaskini wa f amilia ya mtoto huyo . Alisema timu ya madaktari hao itaendelea kutowa huduma za matibabu   kwa wananchi kisiwani humo,   ili kuwaondolea gharama ya kutafuta matibabu nje ya nch