Skip to main content

KHADIJA: MJASIRIAMALI ANAYEUSARIFU UKINDU, AKIZALISHA MAKAWA, VIPEPEO VYA ASILI

 


 


NA ZUHURA JUMA, PEMBA::::

NI majira ya saa 6:00 za mchana nikiwa katika harakati zangu za kazi, nilijikuta naibukia katika kijiji cha Tumbe Mashariki Wilaya ya Micheweni Pemba.

Muda huo kijua kilikuwa kinawaka mithili ya moto uliomwagiwa maji kutokana na vuke lililokuwepo.

Wakati macho yangu yakiangaza huku na kule, punde nilimkuta mama mmoja wa makamo, akiwa amekaa pembeni ya mlango wake wa mbele akishona makawa.

Kumbe alikuwa ni mama wa miaka 46 aliejulikana kwa jina la Khadija Sleyum Mtawa anaejishugulisha na ushonaji wa makawa ya nyiti tangu akiwa mtoto.

Bila kujali alinielezea ushonaji wa makawa ya nyiti kwamba ni kazi anayoipenda ambayo inampatia angalau pesa ya sabuni.

Uso wake ukionesha tabasamu anasimulia ni kazi aliyoianza tangu akiwa na miaka 11, wakati huo akiwa darasa la tano mwaka 1985.

Makawa hayo anatengeneza kwa kutumia ukindu mzima uliopasuliwa, rangi na kamba inayojulikana kwa jina la unu ambayo hupatikana kwenye kuti la mnazi.

Kilichomsukuma Khadija kushona makawa ni kutokana na hali ya maisha aliyokuwa nayo katika familia yake na kuona kwamba ipo haja ya kuwasaidia wazazi baadhi ya majukumu.

“Wazazi wangu walikuwa wanajitahidi kutuhudumia na mdogo wangu, lakini kuna baadhi ya vitu nikihitaji huwa hawana uwezo navyo”, anasema Khadija.

Alishona makawa na kuuza, ambapo alipata fedha ya kumsaidia kutatua shida zake na pia kuisaidia familia yake pale inapokuwa na tatizo.

Makawa anayoshona mama huyo ni tofauti na yale ya ukili, kwani yana ubaora wa hali ya juu na yanawavutia watu wengi.

Watu wanayapenda sana makawa ya nyiti kutokana na kuwa yanadumu kwa muda mrefu ukilinganisha na makawa ya ukili, ambapo pia yana muonekano mzuri pindi unavyoyatazama.

“Nanunua ukindu halafu naupasua, nyengine nazipika kwa rangi, kisha zile mbale ndio ninazoshonea makawa kwa kutumia kamba ya unu na hayana kazi kubwa sana ukilinganisha na yale ya ukili”, anaeleza.

Anatengeneza makawa ya rangi mbali mbali pamoja na vipepeyo kwa kutumia ukindu uliopikwa kwa rangi tofauti.

Anasema, ujuzi wa kutengeneza makawa aliupata kwa rafiki yake ambae walikuwa jirani na anamshukuru sana kwa kumfundisha, kwani ujuzi haufi utaendelea kumsaidia.

“Kwa kweli nimefarijika sana kupata ujuzi huu, kwani napata pesa ya kujikwamua na hali ngumu ya maisha, nawanunulia wanangu nguo za sikukuu, kila siku nawapa pesa ya kutumia skuli na nawalipia ada ya madrasa”, anasimulia.

Ingawa pesa anayoipata haikidhi haja lakini hakuna kupata kudogo, kwani maisha yake ni tofauti kabisa na wanawake wengine katika maeneo anayoishi.

“Kujituma kunatusaidia kuwa na muonekano mzuri kila wakati, hivyo nawanasihi wanawake wenzangu tusijipweteke tu, waume watatukimbia”, anaeleza mama huyo.

Mjasiriamali huyo ananunua ukindu kutoka Mkoani Tanga na rangi ananunua kisiwani hapa kwa wafanyabiashara ambao huchukua nchini Kenya.

Anaeleza kuwa, kwa sasa imekuwa ghali sana kutokana na nchi hiyo kukumbwa na ugonjwa wa Corona, kwa sababu wafanyabiashara hawaendi sana.

Mtaji wa mama huyo ni mdogo sana, hali ambayo inasababisha kuzalisha bidhaa kidogo, ambayo haikidhi mahitaji yake kwa sasa.



“Zamani ilikuwa sina watoto, lakini baada ya kuolewa na kuzaa majukumu yameongezeka, hivyo pesa ninayoipata ni ndogo sana”, anaeleza.

Mjasiriamali huyo anaeleza, atakapokuwa na fedha za kutosha atanunua ukindu mwingi kwa jumla na kushona makawa mengi ambayo yatampatia tija.

Anahitaji angalau apatiwe shilingi 500,000 ambazo zitamsaidia kusafiri kwenda kununua ukindu kwa jumla na anaamini litamsukuma mbele katika kuendeleza biashara yake.

Kwa upande wa soko anaeleza kuwa, lipo kiasi na zaidi anauza soko la ndani.

Anaamini kwamba, ikiwa atatengeneza makawa mengi, atayapeleka hata katika masoko ya utalii kwa sababu ni makawa adimu kupatikana kutoana na utengenezaji wake.

“Naamini watalii yatawavutia sana makawa haya, kwani ni makawa ya ubunifu na yanawavutia watu wengi wa ndani ya nchi, kila anaeyaona hushangaa na kuhitaji atenenezewe”, anasifia.

Watu wengi hununua kwa ajili ya kufunikia chakula, kupamba ndani ya nyumba, kwa sababu yanapendeza sana na ukiyaona utajiuliza jinsi yalivyoshonwa.

Anafafanua kuwa, kawa moja kubwa anauza shilingi 9,000 na dogo shilingi 7,000 ambapo lililochorwa mauwa ni shilingi 12,000 kubwa kwa sababu hupeleka kwa mchoraji shilingi 3,000 kwa kila kawa moja.

Anasikitika sana kwamba hajawahi kuwafundisha watu utengenezaji wa makawa hayo kutokana na kuwa, wengi wao wanaona ni kazi isiyo na manufaa kwao.

“Ni kweli hii ni kazi isiyo na kipato kikubwa, lakini unapata kupunguza shida zako, kila nikiwambia wanawake wenzangu niwafundishe hawataki”, anasikitika.

Mjasiriamali huyo aliolewa na mume wa kwanza ambae alimuacha baada ya kukaa muda mrefu bila ya kupata kizazi (watoto).

Ingawa kwa sasa ana watoto saba (7), wakike wanne (4) na wakiume watatu (3) tangu alipoolewa tena na mume mwengine mwaka 1994.

Ni mtoto wa kwanza katika familia ya watoto wawili, akiwa yeye na mdogo wake wa kiume ambao walizaliwa hapo hapo Tumbe.

Mume wake Khadija aliejukana kwa jina la Hamad Haji anasema, tangu alipomuoa mke wake anafanya kazi hiyo ingawa kipato ni kidogo sana.

“Nampa mashirikiano sana, lakini tatizo ni mtaji, kwa sababu malighafi anazotumia kutengeneza makawa hayo zinatoka nje ya kisiwa cha Pemba”, anaeleza.

Anasema, ikiwa atapata mtaji wa kutosha basi bidhaa yake hiyo inaweza kumpatia fedha zitakazomsaidia kujikwamua na hali ya maisha.



Tambuu Mwadini Juma mwenye miaka 60 ambae ni mtu wa karibu wa mjasiriamali huyo anasema, anamkumbuka Khadija tangu akiwa mdogo anatengeneza makawa hayo na kuuza.

“Ni mzaliwa wa hapa hapa Tumbe na ameolewa hapa, makawa ni mazuri na watu wanayapenda sana, ni kazi ya ubunifu kwa kweli”, anasifia.

Haji Khamis Haji ambae ni Mratibu wa Mfuko wa Uwezeshaji Wananchi Kiuchumi Pemba anasema, wanaviwezesha vikundi vya wajasiriamali na mtu mmoja mmoja aliyemo kwenye kikundi kwa kuwapatia mikopo na mafunzo.



“Ikiwa mjasiriamali hayumo kwenye kikundi hatumpi mkopo, labda kwa wakulima wa mboga, matunda na wale wanaosafirisha bidhaa kutokana kwa vile sasa kuna mradi wa mboga mboga ambao unawasaidia”, anafafanua.

Mratibu huyo anafahamisha kuwa, kuanzia mwaka 2015 hadi mwaka jana wameshatoa mikopo kwa vikundi na mtu mmoja mmoja alie kwenye kikundi ipatayo 968 ambapo Wilaya ya Micheweni ni mikopo 181 yenye thamani ya shilingi 152,000,000.

Fat-hiya Mussa Said ambae ni Mratibu wa Chama cha Waandishi wa Habari Wanawake Tanzania (TAMWA) kwa upande wa Pemba anasema, kawaida wanawawezesha wajasiriamali wa vikundi vya shehia ambazo zimefikiwa na mradi wao wa kuwawezesha wanawake kiuchumi (WEZA).

“Mjasiriamali huyu anatakiwa ajiunge kwenye vikundi vya kuweka na kukopa, ili apate fedha za mkopo zitakazomsaidia kujikwamua na changamoto zinazomkabili”, anafahamisha.

Alimtaka mjasiriamali huyo ajifunze zaidi na awe tayari kujifunza mambo mbali mbali sambamba na kuchangamkia fursa za masoko.

Wajasiriamali wadogo wadogo kisiwani Pemba wamekuwa wakikabiliwa na changamoto mbali mbali zinazosababisha kuwakwamisha katika shughuli zao, licha ya kuwa na lengo la kujikwamua.

                                     MWISHO.

     

 

 

 

 

Comments

BLOG'S VISITORS

DAKTARI MWENGINE CHAKE CHAKE KULA SIKUKUU POLISI, NI KWA TUHUMA ZA KUMBAKA MGONJWA WAKE

NA WAANDISHI WETU, PEMBA::: DAKTARI anaetoa huduma kwa wagonjwa kituo cha afya cha serikali cha  Gombani wilaya ya Chake Chake Pemba, Is-haka Rashid Hadid, anaendelea kushikiliwa na Jeshi la Polisi Mkoa wa kaskazini Pemba, akituhumiwa kumtorosha na kisha kumbaka mtoto wa mwenye umri wa miaka 16, mkaazi wa Gombani. Daktari huyo miaka 35 ni mkaazi wa Kangagani Wilaya ya Wete mkoani humo, ambapo anadaiwa alimchukua mtoto huyo kutoka kwa rafiki yake, na kumpeleka kwenye nyumba anayoishi eneo la Kangagani. Mtoto aliefanyiwa kitendo hicho alisema kuwa, April 21 mwaka huu alikwenda kituo cha afya Gombani, kwa ajili ya matibabu na baada ya kupatiwa huduma na daktari huyo, alimuomba nambari yake ya simu. Alisema ilipofika usiku, walikuwa wanawasiliana kupitia ujumbe mfupi (sms) kwa lengo la kwenda kuchukua dawa nyingine ambazo kwa mchana huo alizikosa hospitalini hapo. "Nilikwenda hospitali kutibiwa, baada ya kufanya mapele katika sehemu zangu za siri, lakini akaniambia mpaka aje da

'MKAPA' NA WENZAKE PEMBA WALAZWA RUMANDE

  NA HAJI NASSOR, PEMBA@@@@ MAHKAMA kuu Zanzibar kisiwani Pemba, chini ya Jaji Ibrahim Mzee Ibrahim, imewapeleka rumande watumuhimwa wanne wanaokabiliwa na tuhuma za kuua kwa makusudi, akiwemo Ali Mussa Omar ‘ Mkapa’ mkaazi wa Wawi wilaya ya Chake chake Pemba. Watuhumiwa wengine walioanza maisha mapya ya rumande ni mtuhumiwa Yassir Mohamed Juma miaka 23, Anuwari Mussa Omar miaka 30 pamoja na mtuhumiwa Yassir Mussa Omar ‘ Makababu ’ miaka 29, wote wakaazi wa shehia ya Wawi, wilaya ya Chake chake Pemba. Awali watuhumiwa hao waliwasili mahakamani hapo, kwa mara ya kwanza, kwa ajili ya kusomewa tuhma zinazowakabili za kumuua kwa maksudi Said Seif Kombo. Ilidaiwa mahakamani hapo na Mwendesha Mashtaka kutoka Ofisi ya Mkurugenzi wa Mashataka Seif Mohamed Khamis akiambatana na mwenzake Mussa Khamis Ali kuwa, watuhumiwa hao kwa pamoja wanadaia kufanya mauwaji hayo kwa maksudi. Ilidai kuwa, watuhumiwa wote kwa pamoja, walitenda kosa hilo Oktoba 16, mwaka huu, baina ya saa 7:00 mchan

HII KALI MBUNGE ASIYA AMKOGESHA MWANANCHI HADHARANI KISA HICHI HAPA......

  NA HAJI NASSOR, PEMBA MBUNGE wa viti maalum nafasi za wanawake mkoa wa kaskazini Pemba Asiya Sharif Omar, amewataka wananchi wa kijiji cha taifu, shehia ya Kinyasini jimbo la Gando wilaya ya Wete Pemba, kuyalinda miundombinu ya maji safi na salama, ili yawe endelevu kwao. Kauli hiyo ameitoa wakati alipokuwa akizungumza na mwandishi wa habari hizi, mara baada ya kuwasili kijijini humo, na kumkogesha mwananchi mmoja kama ishara ya uzinduzi wa mradi wa maji safi na salama, ulioasisiwa na mbunge wa Jimbo la Gando. Alisema, hawana mbadala kwa sasa bali ni kuilinda miundombinu ya huduma hiyo, hasa baada ya mbunge wa wao Salim Mussa Omar, kuwarejeshea huduma hiyo. Alieleza kuwa, inafahamika kuwa kwa miaka 14 waliikosa huduma hiyo hasa kwa vile viongozi waliokuwepo hawakujali kuwatatulia tatizo hilo, hadi juzi ilipofanywa na mbunge wao. “Baada ya huduma hii sasa kurejeshwa na mbunge wa jimbo la Gando, kazi iliyobakia kwenu wananchi ni kila mmoja kuwa mlinzi wa miundombinu hii,’’ali

TUHMA ZA DAKTARI PEMBA KUCHIWA HURU: POLISI KASKAZINI KUTOA TAARIFA RASMI LEO

  NA HAJI NASSOR, PEMBA KAMANDA wa Polisi mkoa wa kaskazini Pemba, Juma Saad Khamis, amesema leo Mei 9, mwaka huu atatoa taarifa rasmi, juu ya kuendelea kumshikilia au kumpa dhamana ya Polisi, daktari wa Kituo cha Afya Gombani Is-haka Rashid Hadid, anayetuhumiwa kwa ubakaji. Alisema, kwa vile alikuwa katika mapumziko mafupi, haelewi jambo lolote linaloendelea kwa mtuhumiwa huyo, juu ya kuendelea kushikiliwa kwake kituoni hapo. Alieleza kuwa, leo Mei 6 (jana), hajapata taarifa za ndani za mtuhumiwa, huyo na kuwataka wananchi na wanaharakati, wasubirie hadi Jumatatu ijayo. Akizungumza na waandishi wa habari kwa nyakati tofauti Kamanda huyo, alisema hana taarifa zozote za kupewa dhamana mtuhumiwa ndani ya kituo chake cha Polisi au kuendelea kuwepo. ‘’Ilikuwa mimi sipo kazini kwa muda, kuanzia anakamatwa hadi anafikishwa Polisi, kwa sasa siwezi kueleza jambo lolote kwa mtuhumiwa huyo, hadi Jumatatu,’’alieleza. Aidha Kamanda huyo alieleza kuwa, kwa sasa hawezi kutoa ufafan

MADAKTARI KUTOKA CHINA WAOKOA MAISHA YA MTOTO PEMBA

  HABIBA ZARALI, PEMBA TIMU ya 32 ya madaktari wa kichina katika hospitali ya Abdalla Mzee Mkoani wamefanikiwa kufanya upasuaji mkubwa wa mtoto mwenye umri wa miaka 15 mkaazi wa Chole Kengeja, baada ya kuchomwa na jiti sehemu ya njia zake za mfumo wa uzazi. Mtoto huyo ambae alianguka hivi karibuni katika mti na baadae kuchomwa na jiti hilo na kumsababishia kutokwa na damu nyingi katika sehemu ya nyonga, alifanyiwa upasuaji uliodumu kwa muda wa saa tatu na   kuokolewa maisha yake. Akizungumza mara baada ya operesheni huo kiongozi wa timu hiyo Dr Jiang Jinhua, alisema mara baada ya mtoto huyo kufikishwa hospitalini hapo na kufanyiwa vipimo na kuonekana   ilibidi apatiwe rufaa ya kwenda katika hospitali nzuri yenye kutibu tatizo lake huko nchini Kuwado ambapo haikuwezekana kutokana na hali ya umaskini wa f amilia ya mtoto huyo . Alisema timu ya madaktari hao itaendelea kutowa huduma za matibabu   kwa wananchi kisiwani humo,   ili kuwaondolea gharama ya kutafuta matibabu nje ya nch