Skip to main content

SIRI YA 'WABAKAJI' KUACHIWA HURU PEMBA, Utetezi wa waliobakwa huwaokoa

 



NA ZUHURA JUMA, PEMBA

WATUHUMIWA wengi wa makosa ya ubakaji wa watoto wa kike kisiwani Pemba huachiwa huru baada ama kesi kumalizikia nje ya mahakama au waliobakwa kuwatetea mahakamani, imefahamika.

Uchunguzi uliofanywa na mwandishi wa gazeti hili kwa kufuatilia mwenendo wa kesi mbali mbali kisiwani humo, umepata ushahidi wa jinsi mabinti wenye umri chini ya miaka 18 waliopata ujauzito wakiwa shuleni, walivyotoa ushahidi mahakamani kwamba hawakubakwa bali walikwenda wenyewe kwa waliowabaka.

Mmoja wa watoto waliopewa mimba wakiwa wadogo lakini wakaenda mahakamani kutoa ushahidi kuwa, hawakubakwa ni Hamida Issa (sio jina lake halisi), ambaye wakati akipata mimba alikuwa anasoma kidato cha pili katika skuli ya Sekondari Piki.

Mahakamani nilisema sijabakwa nilimfuata mwenyewe, kwa sababu sitaki kesi wala sitaki afungwe, sijabakwa bali nilimfuata mwenyewe na nimeridhia, sikulazimishwa na ndio maana sikutaka kutoa ushahidi mahakamani kwa sababu sitaki afungwe,” anasema binti huyo.

Binti huyo mwenye umri wa miaka 16 sasa, alifanyiwa kitendo cha ubakaji mwaka jana katika kijiji cha Mgoli, Shehia ya Piki Wilaya ya Wete na alimtaja aliyemfanyia kitendo hicho kuwa ni Nassor Mohamed Juma, mkazi wa shehia hiyo, ambaye alimlaghai na mwisho wake kumbaka mtoto huyo aliye chini ya uangalizi wa wazazi wake. 

Mtoto huyo anasema, ni kweli alibakwa na kijana huyo na kumsababishia ujauzito, ingawa alipofika mahakamani alikataa kutoa ushahidi kwa makusudi ili kuzuia Nassor asifungwe.

Akizungumza na mwandishi kuhusu kwa nini alifanya alivyofanya huko mahakamani, anasema kwamba hata angetoa ushahidi kijana huyo akafungwa, bado asingeweza kuondoa ukweli kuwa huyo ndiye baba wa mtoto na angetaka kumwona mtoto akitoka chuo cha mafunzo (jela).



“Hata angefungwa ni kazi bure kwa sababu ikiwa ni kunibaka, tayari kashanibaka na mimba kashanipa na nikizaa mtoto atamuona tu akitoka jela, kwa hiyo sikutaka kesi mimi”, anaeleza binti huyo.

Uchunguzi wa mwandishi umeonyesha kwamba kesi ya Hamida ni moja wapo tu ya kesi nyingi za namna ambapo watoto katika Wilaya ya Wete wamekataa kutoa ushahidi na kusababisha kesi hizo kufutwa.

Takwimu za mwaka 2020 za Jeshi la Polisi Wilaya ya Wete zinaonyesha kesi takribani 85 za watoto kudhalilishewa ziliripotiwa, huku kesi 30 zikiwa ni kesi za ubakaji zinazohusisha watoto wenye umri wa kati ya miaka 15-17.

Kati ya hizo kesi 30, zilizoripotiwa, ni kesi nne (4) tu ambazo zilitolewa hukumu huku 17 zikfutwa katika kituo cha Polisi, kesi saba (7) zilifutwa mahakamani na kesi mbili (2) zikiwa katika upelelezi.

Kwa mwaka 2021, takwimu zinaonyesha kwamba kesi zilizoripotiwa zilikuwa 44, huku kesi 28 zikiwa za watoto wenye umri wa miaka 15-17 ambapo ni kesi nne (4) tu ndizo zilizotolewa hukumu kama mwaka 2020, huku kesi 12 zikifutwa Polisi na saba (7) mahakamani na kesi tano (5) upelelezi wake bado unaendelea.

Katika mazungumzo na gazeti hili, mama wa Hamida, Bi Aisha Ali Hamad (sio jina halisi) mwenye umri wa miaka 45, anasema alifuata hatua zote mpaka kesi kufika mahakamani, ingawa mwisho wa siku mwanawe alikanusha kubakwa mbele ya mahakama na kusema kuwa alikwenda mwenyewe.

“Nilijitahidi kumuelekeza na kumuelewesha mwanangu kuhusu kutoa ushahidi, lakini ilipofika wakati wa kutoa ushahidi alikana mbele ya mahakama, jambo ambalo liliniumiza sana”, anahadithia mama huyo.

Anasema kwa uzoefu wake, watoto wa kike wenye umri huo ni wagumu kutoa ushahidi kwa sababu ni kweli wengine wanawafuata wanaume wenyewe huku wakijua kisheria hawana ridhaa ya kuwa na mahusiano ya kingono na watu wengine.

Mama huyo anaiomba Serikali ifanye utaratibu mwengine wa kuzishtaki kesi za aina hiyo kwa kuchukua ushahidi wa daktari, kwa vile watoto wenye umri huo hawana ridhaa ya kushiriki vitendo vya ngono.

“Serikali isiziache kesi hizi eti kwa sababu mtoto amesema amemfuata mwanaume mwenyewe, mtoto chini ya umri wa miaka 18 kisheria hana ridhaa, hivyo akitaa mtoto, uchukuliwe ushahidi wa daktari”, anafafanua mama huyo.

Hata hivyo, mapendekezo hayo ya mama huyo yanaonekana kuwa na ugumu kwenye utekelezaji kwa vile daktari peke yake anaweza tu kuthibitisha kuingiliwa kwa mwanamke lakini hawezi kuthibitisha ni nani aliyefanya tukio hilo.

Kwa mujibu wa Hakimu wa Mahakama Maalumu ya Kushughulikia Kesi za Udhalilishaji, Ali Abdulrahman Ali, ambaye pia anaifahamu kesi ya Hamida, anasema itakuwa vigumu kwa Mahakama kuwatia hatiani watuhumiwa kwa kutumia ushahidi wa daktari pekee.



“Hatuwezi kumtia hatiani mtuhumiwa kwa ushahidi wa daktari pekee kwa sababu, cheti cha daktari kinaonesha mtoto kutendewa kitendo (ubakaji) na sio kujulikana mtuhumiwa”, anafafanua.

Anaeleza kuwa, ushahidi wa daktani unafafanua tu na ndio maana hawautimii pekee kwa kumtia hatiani mshitakiwa, mpaka pale atakapokiri (kukubali) mtoto kuwa kijana huyo ndiye aliembaka, jambo ambalo kwenye kesi ya Hamida halikuwezekana.

Anataja kesi za kubaka ambazo zimefikishwa mahakamani kuanzia mwaka 2020 hadi 2021 ni 49 huku za watoto kati ya umri wa miaka 15-17 zikiwa 19, ambapo nne washtakiwa wamefungwa, mbili wametozwa faini na kesi 13 zimeondolewa (kufungwa).

Mama Hamida bado anasikitika kuona kwamba mtoto wake amebakwa na kupewa ujauzito, lakini mwisho wa siku anakanusha mwenyewe ushahidi eti anampenda, huku akimuacha mtendaji kosa kudunda mitaani.

“Nikimuona kijana huyo roho inaniuma, kwa sababu ameshamuharibu mwanangu halafu yeye anadunda mtaani, sina raha wala furaha zaidi ya kusemwa na kuchekwa kwa wanafamilia ya kijana huyo”, anasimulia.

Mratibu wa Dawati la Jinsia Wilaya ya Wete, Hassan Khamis, anasema, kesi ya mtoto huyo iliwasumbua sana katika kumtafuta na kumfuatilia kijana huyo ingawa mwisho binti hakuwaunga mkono.

“Mtuhumiwa alikuwa anakimbia, kwa hiyo akionekana sehemu tu, sisi tunapigiwa simu na tunakwenda hatumkuti, siku moja tulimfukuza mpaka mabondeni, tulipomkamata tulikuwa taabani sote”, anaelezea.

Kilichowashangaza na kuwahuzunisha ni baada ya kuifikisha kesi hiyo mahakamani na hatimae mtoto wa kike kusema hakubakwa bali alikwenda mwenyewe.

Kwa maelezo yake, watoto wenye umri wa miaka 15 hadi 17 wanasumbua sana katika usimamizi na ufuatiliaji kesi, kwa sababu wanakuwa vigeugeu sana na wakati mwengine wanakanusha ushahidi.

 

VIONGOZI WA SERIKALI

Sheha wa Shehia hiyo, Assaa Khamis Mussa, anaeleza kuwa kesi hiyo anaifahamu na iliripotiwa kituo cha Polisi Wete, ingawa mtoto alipofika mahakamani alisema, alimfuata mwenyewe kijana huyo na si kwamba alibakwa kama wazazi wake wanayodai.

“Mtoto aliyefanyiwa kitendo cha ubakaji ndiye shahidi namba moja, hivyo ikiwa amekataa kutoa ushahidi, Mahakama haiwezi kumtia hatiani mtuhumiwa”, anaeleza sheha.

Pia Mkuu wa Idara ya Ustawi wa Jamii Pemba, Omar Mohamed, anasema wamekuwa wakikosa ushirikiano kwa watoto hao wanapofikishwa mahakamani, huenda kuna vitisho dhidi yao kutoka kwa wale wanaowabaka au hawatoi ushirikiano kutokana na kuwalinda wapenzi wao.

“Kwa sababu wanajua kuwa wakitoa ushahidi wa kukiri kutendewa kitendo hicho na wapenzi wao, kuna uwezekano wa wenzao hao kufungwa jela, lakini pia wengine wana tatizo tu la kukosa kujiamini na kushindwa kujieleza mbele za watu”, anafafanua.  

Tatizo hilo limesababisha uwepo wa kiasi kidogo cha kesi zilizoamuliwa, akitoa mfano wa takwimu za Polisi zinazoonyesha kwamba kwa kipindi cha miaka miwili kati ya mwaka 2020 na 2021 jumla ya kesi 58 ziliripoitiwa zinazohusiha watoto kati ya umri wa miaka 15-17.

Katika miaka hiyo miwili, ni kesi nane tu ambazo washitakiwa walihukumiwa ukilinganisha na kesi 43 zilizofutwa ama mahakamani au katika vituo vya Polisi.

WANANCHI

Mkaazi wa Kijiji cha Tundwa kwenye shehia hiyo, Khalfan Juma Ali anaeleza, aghalabu watoto wenye umri huo mara nyingi hulingana kiumri na wenzao huku kukiwa na uwezekano pia wa kuwa na uhusiano wa mapema baina yao.

Akitolea mfano kesi ya mtoto Hamida Issa, anasema licha ya wazazi wake kuwa mstari wa mbele kupigania haki ya mtoto wao, waligonga mwamba baada ya binti kufika mahakamani na kukanusha kuwa alibakwa.

“Kwa kweli umri huu uliowekwa kisheria ni mkubwa kwa sababu huwa wanakubaliana na mtuhumiwa, ndio maana wakawa ni wagumu kutoa ushahidi wanapofika mahakamani”, anaeleza.

Mkaazi wa shehia ya Kiungoni Time Ali Bakari, anasema sababu kubwa inayosababisha watuhumiwa waachiwe bila kufungwa ni shinikizo la wazazi kwani baada tu ya kujulikana mtoto amefanyiwa udhalilishaji, wenyewe ndiyo hushawishi watoto wasifungue kesi.

“Wakisharudi Polisi, wanaambiwa wasitoe ushahidi, ili wasije kugombana familia au majirani, hivyo kwa hali hiyo mtoto hata umuwekee kisu shingoni hasemi ukweli”, anaeleza.

Anahadithia kesi iliyotokea kijijini kwao mwaka huu kuwa, baada ya mtoto kubakwa, wazazi wa pande zote mbili walikubaliana na kukaahidiwa kupewa milioni mbili, hivyo akaamriwa asitoe ushahidi, jambo lililosababisha kesi kufutwa.

VIJANA

Kijana Mohamed Suleiman Said (23) mkaazi wa Shehia ya Kambini anaeleza, sababu ni kwamba wazazi wakishajua kuhusu kesi, wanakubaliana pande zote mbili kumalizika kesi nje ya Mahakama na hivyo siku ya kuitwa mahakamani, mtoto anabadilisha ushahidi.

“Pia inaweza kuwa hivyo kwa sababu ya vitisho kutoka kwa familia ya mvulana au mhusika mwenyewe wa ubakaji, lakini ushahidi wa mtoto aliyefanyiwa ndio wenye nguvu zaidi, kwa hiyo ikiwa atabadilisha au atakataa, mtuhumiwa hawezi kutiwa hatiani”, anasema.  

Kwa upande wake, Salma Hamad Omar (19), mkazi wa Mzambarau Takao, anasema kwa maoni yao watoto wenye umri huo kwa sababu hao wanaume ni wachumba zao, hivyo wanaona shida kusema wamebakwa.

“Wakati mwengine anatishiwa kwa kuambiwa, iwapo atasema, atamfanyia kitu kibaya ajute katika maisha yake yote, hivyo anajiona yupo hatarini atakapotoa ushahidi”, anaeleza.

“Pia anajihisi kwamba akitoa ushahidi itakuwaje? Au huyo kijana akifungwa ndiyo itakuwaje? Kwa hiyo anapofikiria hayo huona hakuna haja kutoa ushahidi”, anasema.

  

Binti mwenye umri wa miaka 17, Maryam Faki Ali, ambaye pia ni mkaazi wa shehia ya Minungwini anaeleza, ajuavyo yeye, watoto wenye umri huo hawapendi kutoa ushahidi kwa sababu huwa kuna makubaliano baina yake na mwanaume.

“Vijana wengi siku hizi hawapendi kuwa ‘single’, kwa hiyo anaweza kukwambia ikiwa unanipenda tufanye mapenzi ili unithibitishie na lazima watafanya, hivyo mwanamke atakapopelekwa mahakamani hatoi ushahidi”, anaeleza.

Anafafanua, mtoto huyo anaona kuwa, akitoa ushahidi wazazi wake na hata jamii kwa ujumla itajua kwamba hajalazimishwa kufanya kitendo hicho bali itakuwa amekiridhia mwenyewe na ndio maana anashindwa kusimama kutoa ushahidi.

WADAU

Mratibu wa Chama cha Waandishi wa Habari Wanawake Tanzania (TAMWA) kwa upande wa Pemba, Fat-hiya Mussa Said, amemuambia mwandishi kuwa watoto hao wana changamoto kubwa ya kukataa kutoa ushahidi mahakamani au kukataa ushahidi ambao wameshautoa vituo vya Polisi kutokana na kutokujielewa.

“Huku tunakotoka hatujawafundisha watoto masuala ya kujiamini, kujithamini, kujitathmini, ili waweze kufikia ndoto zao, sasa wanakwenda kujingiza kwenye mambo mabaya na wanapodhalilishwa wanashindwa kusimulia haki yao”, anasema.

Anasema, wao wanaona kuwapendelea waliowadhalilisha itawasaidia kuolewa au labda ni wazazi wanataka kesi ife na njia wanayoitumia ni kumshawishi mtoto kuharibu ushahidi.

Hafidh Abdi Said Mkurugenzi wa PEGAO Pemba anasema, watoto wenye umri huo tayari wameshajitambua kwa maana hiyo wanafanya makusudi kubakwa na ndio maana wanapoteza ushahidi.

“Kwa vile walichokifanya wanajua kuwa ni makusudi, katika hukumu na wao wawajibishwe kama wanaume, kwa sababu mtoto ambaye amefanyiwa kitendo hicho bila ridhaa yake hawezi kuficha”, anaeleza Hafidh.

VIONGOZI WA DINI

Kiongozi wa Dini ya Kiislamu kutoka Ofisi ya Mufti Pemba, Sheikh Mussa Saleh Ali, anasema, watoto wenye umri huo hawatoi ushahidi wa kweli Polisi au mahakamani kutokana na muhali, vitisho, kurubuniwa na woga wa kimaumbile kutokana na umri wao.

Mchungaji Zeno Marandu kutoka Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT) Chake Chake amemueleza mwandishi kwamba kesi za udhalilishaji zimekuwa zikikosa kupata hukumu kutokana na watoto hao kukataa kutoa ushahidi, kutokujielewa au muhali uliopo ndani ya jamii, kwani asilimia kubwa ya vitendo hivyo vinatokea ndani ya familia.

 

                                                       MWISHO. 

 

Comments

BLOG'S VISITORS

DAKTARI MWENGINE CHAKE CHAKE KULA SIKUKUU POLISI, NI KWA TUHUMA ZA KUMBAKA MGONJWA WAKE

NA WAANDISHI WETU, PEMBA::: DAKTARI anaetoa huduma kwa wagonjwa kituo cha afya cha serikali cha  Gombani wilaya ya Chake Chake Pemba, Is-haka Rashid Hadid, anaendelea kushikiliwa na Jeshi la Polisi Mkoa wa kaskazini Pemba, akituhumiwa kumtorosha na kisha kumbaka mtoto wa mwenye umri wa miaka 16, mkaazi wa Gombani. Daktari huyo miaka 35 ni mkaazi wa Kangagani Wilaya ya Wete mkoani humo, ambapo anadaiwa alimchukua mtoto huyo kutoka kwa rafiki yake, na kumpeleka kwenye nyumba anayoishi eneo la Kangagani. Mtoto aliefanyiwa kitendo hicho alisema kuwa, April 21 mwaka huu alikwenda kituo cha afya Gombani, kwa ajili ya matibabu na baada ya kupatiwa huduma na daktari huyo, alimuomba nambari yake ya simu. Alisema ilipofika usiku, walikuwa wanawasiliana kupitia ujumbe mfupi (sms) kwa lengo la kwenda kuchukua dawa nyingine ambazo kwa mchana huo alizikosa hospitalini hapo. "Nilikwenda hospitali kutibiwa, baada ya kufanya mapele katika sehemu zangu za siri, lakini akaniambia mpaka aje da

'MKAPA' NA WENZAKE PEMBA WALAZWA RUMANDE

  NA HAJI NASSOR, PEMBA@@@@ MAHKAMA kuu Zanzibar kisiwani Pemba, chini ya Jaji Ibrahim Mzee Ibrahim, imewapeleka rumande watumuhimwa wanne wanaokabiliwa na tuhuma za kuua kwa makusudi, akiwemo Ali Mussa Omar ‘ Mkapa’ mkaazi wa Wawi wilaya ya Chake chake Pemba. Watuhumiwa wengine walioanza maisha mapya ya rumande ni mtuhumiwa Yassir Mohamed Juma miaka 23, Anuwari Mussa Omar miaka 30 pamoja na mtuhumiwa Yassir Mussa Omar ‘ Makababu ’ miaka 29, wote wakaazi wa shehia ya Wawi, wilaya ya Chake chake Pemba. Awali watuhumiwa hao waliwasili mahakamani hapo, kwa mara ya kwanza, kwa ajili ya kusomewa tuhma zinazowakabili za kumuua kwa maksudi Said Seif Kombo. Ilidaiwa mahakamani hapo na Mwendesha Mashtaka kutoka Ofisi ya Mkurugenzi wa Mashataka Seif Mohamed Khamis akiambatana na mwenzake Mussa Khamis Ali kuwa, watuhumiwa hao kwa pamoja wanadaia kufanya mauwaji hayo kwa maksudi. Ilidai kuwa, watuhumiwa wote kwa pamoja, walitenda kosa hilo Oktoba 16, mwaka huu, baina ya saa 7:00 mchan

HII KALI MBUNGE ASIYA AMKOGESHA MWANANCHI HADHARANI KISA HICHI HAPA......

  NA HAJI NASSOR, PEMBA MBUNGE wa viti maalum nafasi za wanawake mkoa wa kaskazini Pemba Asiya Sharif Omar, amewataka wananchi wa kijiji cha taifu, shehia ya Kinyasini jimbo la Gando wilaya ya Wete Pemba, kuyalinda miundombinu ya maji safi na salama, ili yawe endelevu kwao. Kauli hiyo ameitoa wakati alipokuwa akizungumza na mwandishi wa habari hizi, mara baada ya kuwasili kijijini humo, na kumkogesha mwananchi mmoja kama ishara ya uzinduzi wa mradi wa maji safi na salama, ulioasisiwa na mbunge wa Jimbo la Gando. Alisema, hawana mbadala kwa sasa bali ni kuilinda miundombinu ya huduma hiyo, hasa baada ya mbunge wa wao Salim Mussa Omar, kuwarejeshea huduma hiyo. Alieleza kuwa, inafahamika kuwa kwa miaka 14 waliikosa huduma hiyo hasa kwa vile viongozi waliokuwepo hawakujali kuwatatulia tatizo hilo, hadi juzi ilipofanywa na mbunge wao. “Baada ya huduma hii sasa kurejeshwa na mbunge wa jimbo la Gando, kazi iliyobakia kwenu wananchi ni kila mmoja kuwa mlinzi wa miundombinu hii,’’ali

TUHMA ZA DAKTARI PEMBA KUCHIWA HURU: POLISI KASKAZINI KUTOA TAARIFA RASMI LEO

  NA HAJI NASSOR, PEMBA KAMANDA wa Polisi mkoa wa kaskazini Pemba, Juma Saad Khamis, amesema leo Mei 9, mwaka huu atatoa taarifa rasmi, juu ya kuendelea kumshikilia au kumpa dhamana ya Polisi, daktari wa Kituo cha Afya Gombani Is-haka Rashid Hadid, anayetuhumiwa kwa ubakaji. Alisema, kwa vile alikuwa katika mapumziko mafupi, haelewi jambo lolote linaloendelea kwa mtuhumiwa huyo, juu ya kuendelea kushikiliwa kwake kituoni hapo. Alieleza kuwa, leo Mei 6 (jana), hajapata taarifa za ndani za mtuhumiwa, huyo na kuwataka wananchi na wanaharakati, wasubirie hadi Jumatatu ijayo. Akizungumza na waandishi wa habari kwa nyakati tofauti Kamanda huyo, alisema hana taarifa zozote za kupewa dhamana mtuhumiwa ndani ya kituo chake cha Polisi au kuendelea kuwepo. ‘’Ilikuwa mimi sipo kazini kwa muda, kuanzia anakamatwa hadi anafikishwa Polisi, kwa sasa siwezi kueleza jambo lolote kwa mtuhumiwa huyo, hadi Jumatatu,’’alieleza. Aidha Kamanda huyo alieleza kuwa, kwa sasa hawezi kutoa ufafan

MADAKTARI KUTOKA CHINA WAOKOA MAISHA YA MTOTO PEMBA

  HABIBA ZARALI, PEMBA TIMU ya 32 ya madaktari wa kichina katika hospitali ya Abdalla Mzee Mkoani wamefanikiwa kufanya upasuaji mkubwa wa mtoto mwenye umri wa miaka 15 mkaazi wa Chole Kengeja, baada ya kuchomwa na jiti sehemu ya njia zake za mfumo wa uzazi. Mtoto huyo ambae alianguka hivi karibuni katika mti na baadae kuchomwa na jiti hilo na kumsababishia kutokwa na damu nyingi katika sehemu ya nyonga, alifanyiwa upasuaji uliodumu kwa muda wa saa tatu na   kuokolewa maisha yake. Akizungumza mara baada ya operesheni huo kiongozi wa timu hiyo Dr Jiang Jinhua, alisema mara baada ya mtoto huyo kufikishwa hospitalini hapo na kufanyiwa vipimo na kuonekana   ilibidi apatiwe rufaa ya kwenda katika hospitali nzuri yenye kutibu tatizo lake huko nchini Kuwado ambapo haikuwezekana kutokana na hali ya umaskini wa f amilia ya mtoto huyo . Alisema timu ya madaktari hao itaendelea kutowa huduma za matibabu   kwa wananchi kisiwani humo,   ili kuwaondolea gharama ya kutafuta matibabu nje ya nch