Skip to main content

HAYA NDIO MAAJABU YA MAZIWA YA MAMA KWA MTOTO

 

 


KUTOKA, PEMBA:::::


KILA mwanzoni mwa wiki ya mwezi wa Agosti, ya kila mwaka, dunia huwa na wiki ya unyonyeshaji wa maziwa ya mama.

 

Lengo la wiki hii, huwa ni kusisitiza umuhimu wa maziwa ya mama kwa watoto wachanga na wadogo, kiafya.

 

Afya ni kitu muhimu katika maisha ya mwanadamu na kinyume chake, ni kuzalisha maradhi kadhaa yanayodhoofisha mwili na kiakili.

 

Katika kuhakikisha afya ya mwanadamu inaimarika, msingi wake huanzia tokea mtoto anapokuwa tumboni na mara anapozaliwa, kwa kuhakikisha anapewa mahitaji ya msingi ikiwemo maziwa ya mama.

 

Maziwa ya mama yana kinga kamili ikiwemo ya vitameni A vya kutosha ambavyo huwa ni kinga ya maradhi mbalimbali kwa mtoto mchanga.

 

Ingawa wapo baadhi ya akina mama hawapendi kunyonyesha na huamuwa kumuachisha ziwa mtoto mara tu, anapojifunguwa, kwa sababu tofauti ikiwemo kuhofia maziwa yake kuanguka, kupoteza haiba na muonekano wake.

 

Katika hatuwa ya kumlisha mtoto chini ya miezi sita kunaweza kumsababishia michubuko ndani ya utumbo na kupata gesi kutokana na kuwa utumbo wake hauhimili kusaga vyakula hivyo.

 

Kunyonyesha ni njia moja wapo muafaka ya uwekezaji muhimu na ya gharama nafuu inayoweza kufanywa na mtu yoyote mwenye uwezo wa aina yoyote hata akiwa mlemavu ama masikini.

 

Taifa lolote linahitaji watu wenye afya na wenye uwezo wa kiakili na kimwili katika kuleta maendeleo katika nyanja zote za kiuchumi,kijamii na hata kisiasa.

 

Moja kati ya njia muhimu ya kupata Taifa bora ni kupata msingi wa unyonyeshaji wa maziwa ya mama kwa watoto wachanga.

 

WATAALAMU WA AFYA WANASEMAJE?

Muuguzi wa mama na mtoto wa Hospitali ya Abdalla Mzee Mkoani Pemba, Rabia Mohamed Ussi, anasema kushindwa kuwekeza katika unyonyeshaji, kunachangia kuongeza magonjwa mengi yanayowakumba watoto.

 

Anaainisha kuwa, thari za kutonyonyesha watoto maziwa ya mama hasa kwa watoto moja ni kudumaa akili, kupunguwa kiwango cha ufahamu wa kujifunza na kutambua mambo mbalimbali ambapo huwapunguzia fursa ya kiwango cha kupata elimu.

 

“Viwango duni vya unyonyeshaji humsababishia mama kubeba mimba za papo kwa papo, ambapo hukosa afya mama huyo na kupunguza kufanya kazi za kujikimu kimaisha,’’ anasema.

 

Daktari kutoka Wodi ya wazazi katika hospitali hiyo, Fatma Said Mohamed, anasema unyonyeshaji unampa mtoto mwanzo mzuri wa maisha, huku maziwa ya mama yakiwa mithili ya chanjo ya kwanza kwa mtoto wake.

 

Msimamizi wa kitengo cha lishe Wilaya ya Chake Chake, Harusi Masoud Ali, anasema kufuata utaratibu wa kunyonyesha kwa akina mama, kunawalinda watoto wachanga na maradhi kama vile maradhi ya saratani, pumu na kuharisha.

 

‘’Maradhi haya kwa watoto ni mepesi kupoteza maisha ya watoto hao, maana huwa hawana kinga ya aina yoyote,’’anafafanua.

 

Dokta, Munira Suleiman Khalifa, kutoka kitengo cha lishe Chake chake anasema maziwa ya mama ni rahisi kupatikana, na wanaoamua kuwapa maziwa ya kununua hukumbana na gharama kubwa.

 



WHO

Shirika la Afya Duniani ‘WHO’ linasema mtoto mchanga ana umri wa tangu pale anapozaliwa mpaka anapotimiza mwaka mmoja, wakati mtoto mdogo ni yule wa umri wa kuanzia mwaka mmoja hadi miaka miwili.

 

Kwa hiyo, unyonyeshaji maziwa ya mama unaweza kuelezewa kwa ujumla kuwa ni njia asilia ya uzalishaji watoto wachanga na wadogo ambao pamoja na kula maziwa hayo mtoto anapata virutubishi vingi vya kinga ya mwili.

 

Vilevile kitendo cha Unyonyeshaji ni muhimu kwani huimarisha uhusiano baina ya mama na mtoto na kumjengea mama na mwanawe kujiamini zaidi.

 

MTOTO ANATAKIWA ANYONYESHWE VIPI

 

Mratibu wa lishe Wilaya ya Mkoani, Mwajine Khamis Mjaka, anasema ili mtoto aweze kufaidika na maziwa ya mama anatakiwa kunyonyeshwa ipasavyo kila anapohitaji mtoto na sio anapohitaji mama.

 

Anasema mama anaponyonyesha anatakiwa kumuweka mtoto wake vizuri kichwa kiwe juu ya mkono wa mama, tumbo la mtoto ligusane na tumbo la mama.

 

‘’Nyato ya ziwa yenye rangi nyeusi ikae katika mdomo wa mtoto, na mama aliteke vizuri ziwa lake na kuacha tabia ya kulikamata ziwa hilo kwa kubana vidole kama mkasi,’’anafafanua.

 

Anasema mtoto anahitaji kupata maziwa ya mama hata kama yuko kazini, mama huyo anapaswa kuyakamuwa maziwa yanayomtosha kwa muda wote hadi atakaporudi.

 

“Wazazi wana kawaida ya kuwaacha watoto wao bila ya kunyonya kwa muda mrefu na kumpa vyakula vyengine wakati uwezo wa kuyakamuwa maziwa na akapewa upo hata kama mama hayupo,”anasema.

 


Mama yanapokamuliwa yana uwezo wa kukaa kwa saa nane, ama yanaweza kuhifadhiwa katika friji kwa saa 24 na iwapo yatagandishwa yanakaa hadi saa 72.

 

“Unapoyayeyusha maziwa ya mama yaliyoganda kwa kuyaweka katika friji unatakiwa kuyatia katika chombo kisha kukitia katika maji ya moto chombo hicho hadi yapate umoto unaohitajika na sio kuyateleka maziwa hayo,”alifahamisha.

 

 UMUHIMU WA MAZIWA YA MAMA

Mratibu wa mama na mtoto wilaya ya Mkoani Moza Mohamed Ali anasema, licha ya maziwa ya mama kuonekana ni mepesi lakini yana virutubisho muhimu na kiasi kikubwa cha maji ya kutosha.

 

‘’Maji ni kwa ajili ya kukata kiu ya mtoto, chakula na mafuta ambapo kitaalamu inashauriwa watoto wasipewe maji wala chakula chochote mpaka baada ya miezi sita,’’anasema.

 

Maziwa ya mwanzo yenye rangi ya njano, yanayotoka kwa siku tatu baada ya kujifungua ni muhimu na lishe bora kwa watoto, kwani yanakinga mwili kwa mtoto (immunity).

 

     FAIDA ZA UNYONYESHAJI

Moja ni kuimarisha uhusiano baina ya mama na mtoto, kuwaondolea watoto maradhi mbalimbali, kuzidisha ufahamu pamoja na kuwasababisha kujiamini.

 

Watoto wanaonyonyeshwa kwa kipindi cha miezi sita ya mwanzo bila ya kupewa maji hupata madini chuma ya kutosha na kukingwa na upungufu wa wekundu wa damu kwa kipindi chote cha miezi sita.

 

Mama anaponyonyesha mara kwa mara usiku na mchana mwili wake hutengeneze maziwa kwa wingi zaidi, kwani kadiri mama anavyonyonyesha anaongeza uwezo wa kuzalisha maziwa mengi.

 




Mkuu wa kitengo cha lishe cha wizara ya afya Pemba Raya Mkoko Hassan, anasema elimu duni ya unyonyeshaji wa maziwa ya mama, inachangia ongezeko la ugonjwa wa utapiamlo kwa watoto.

 

 Kwa Zanzibar kati ya watoto 100 ni watoto 30 pekee, ndio wanaonyonyeshwa kikamilifu bila ya kupewa aina yoyote ya chakula, 70 sio rasmi.

 

“Ni muhimu kunyonyesha mtoto titi moja kati ya dakika 20 hadi 30 kwa wakati mmoja, ili amalize maziwa yote kabla ya kumpa jengine, hii itamuwezesha kushiba na kulala muda mrefu,”anasema.

 

JAMII INASEMAJE

 

Maryam Nassor (70) wa Mkoani, anasema enzi zake wakati akizaa utaalamu huo wa kunyonyesha mtoto miezi sita bila ya kumpa hata maji, haukuwepo.

 

Anaona kwa vile wataalamu wa afya wanalihimiza hilo, basi hakuna shaka ni jambo zuri kwa afya ya watoto na ni jema kwa wazazi kuufuata utaratibu huo.

 

“Zamani maradhi kwa watoto yalikuwa mengi na vifo vilikuwa vikitokea mara kwa mara, inawezekana ilikuwa inatokana tatizo la kulishwa mapema,”anaeleza.

 

Sabiha Juma (45) wa Kiwani anasema, kati ya watoto wake watano, ni wawili wa mwisho ndio aliowanyonyesha miezi sita   bila ya kuwapa hata maji, ingawa tofauti anaiona ikiwemo kwenye ufahamu wa kusoma.

 

Salma Suleiman (27) wa Uweleni  anasema elimu ya unyonyeshaji anaipata kupitia klinik ya mama na mtoto na kushauri akina mama kufuata maelekezo ya wataalamu wa afya.

 

Suleiman Hamad (65) wa Mtambile anasema kila zama zinazokuja zina utaalamu ulioboreka zaidi ya uliopita ,ni wajibu wa jamii kusikiliza na kufanyia kazi ili mafanikio kuatikana.

 


Juma Saidi wa Makombeni anasema ni wajibu wa kina baba kutowa huduma stahiki ikiwemo ya kula kwa akina mama ili waweze kunyonyesha watoto miezi sita bila kupewa chakula.

 

TATHMINI UNICEF/WHO

Tathmini iliyotolewa mwaka 2017 kwa ushirikiano wa UNICEF, Shirika la Afya Duniani (WHO) na mradi wa kimataifa wa unyonyeshaji inaonyesha kuwa, hakuna nchi inayokidhi kikamilifu viwango vya unyonyeshaji vilivokuwa vimependekezwa.

 

Viwango vya unyonyeshaji vilivyofanyiwa tathmini katika nchi 194, vimebaini kwamba asilimia 40 tu ya watoto walio chini ya umri wa miezi sita, wananyonyeshwa maziwa ya mama pekee bila kitu kingine na nchi 23 pekee duniani, ndizo zenye kiwango cha unyonyeshaji pekee wa zaidi ya asilimia 60.

 

Aidha tathmini imebaini kuwa, uwekezaji wa dola 4.70 kwa kila mtoto mchanga unahitajika ili kuongeza kiwango cha unyonyeshaji pekee kwa watoto walio chini ya miezi sita ili kufikia asilimia 50 ifikapo 2025.

 

Vifo vingi vya watoto wadogo huchangiwa kwa kutokupata kunyonya maziwa ya mama ipasavyo jambo ambalo husababisha kukosa kinga mwilini ikiwemo vitamin ‘A’ ambavyo ni kinga ya maradhi kwa mtoto.

 

Imebainika kuwa katika nchi tano kati ya hizo ni za mataifa makubwa kiuchumi, lakini ni yenye dharura kama vile China, India, Indonesia ,Mexico, Nigeria kadiri ya watoto 236,000 hufariki kwa mwaka.

 

Kwa mujibu wa UNICEF na WHO “Tathimini inaonyesha kwamba ongezeko la kiwango cha unyonyeshaji wa maziwa ya mama pekee linaweza kuokoa maisha ya watoto 820,000 kila mwakana na hivyo kuzalisha pato zaidi la dola bilioni 302.” 

 

Mwisho

 

 

Comments