Skip to main content

SHERIA YA MAGAZETI ZANZIBAR MNYORORO MKONGWE KWA UHURU WA HABARI

 


 

 NA HAJI NASSOR, PEMBA:::

Sheria nambari 5 ya Wakala wa Habari, Magazeti na Vitabu ya mwaka 1988, ambayo imefanyiwa marekebisho mwaka 1997, bado baadhi ya vifungu vyake vinaminya uhuru wa habari nchini.

 

Kifungu cha 27 (1) ni miongoni mwa vifungu kinachompa Mamlaka Ofisa yeyote wa Polisi, kukamata gazeti lolote, popote litakapoonekana limechapwa au kuchapishwa au ambalo kwa maoni yake tu, atalituhumu kwamba limechapwa au kuchapishwa kinyume na sheria.

 

Ambapo kifungu cha 27 (3) pia kinampa Mamlaka hakimu kumuamuru Ofisa yeyote wa cheo cha mkaguzi au zaidi, ikiwa ana sababu ya maana ya kuamini kwamba, atachelewa kupata hati ya upekuzi anaweza kutekeleza uwezo alio nao kwa mujibu wa sheria.

 

Vifungu hivi kwa nyakati za sasa, havipaswi kuwepo katika sheria hiyo kutokana na kuwa sio rafiki kwa uhuru wa vyombo vya habari nchini.

 

Wadau mbali mbali, wamekaa pamoja kuvifanyia uchechemuzi baadhi ya vifungu vinavyokandamiza uhuru wa vyombo vya habari, tangu mwaka 2010 ingawa bado vinaendelea kutumika, hali ambayo inawakwaza wanahabari.

 

Lengo la kuvifanyia uchechemuzi vifungu hivyo, ni kuhakikisha kwamba, vinafanyiwa maboresho na vyengine vinaondoshwa kabisa, ili viwape uhuru wanahabari katika kufanya kazi zao.

 

Mwandishi wa habari wa kujitegemea Mohamed Khalfan Ali anasema, sio vizuri kuwepo kifungu hicho kinachompa Mamlaka Ofisa Polisi kwa kutuhumu tu, kwani kitawapa nguvu ya kudhalilisha waandishi na vyombo vya habari.

 

"Hiki kifungu kinapaswa kuondoshwa kabisa, Ofisa Polisi asipewe Mamlaka hayo kwa sababu, watavunjia vyombo vya habari heshima yake na kuvidhalilisha", anasema.

 

Maryam Salum Habib mwandishi wa habari wa Gazeti la Zanzibarleo Pemba anasema, Mamlaka hayo aliyopewa Ofisa wa Polisi anaweza kukamata gazeti, atakapojisikia tu kukamata na sio kwa kufanya kosa.

 

"Kifungu hicho kinampa Mamlaka endapo tu atatuhumu gazeti limechapishwa kinyume na sheria, hivyo akiwa na chuki zake bianafsi anaweza kufanya hivyo, kwa vile kifungu kinamlinda", anafahamisha.

 

Meneja wa radio Jamii Micheweni Ali Massoud Kombo anasema, sio sahihi kwa Ofisa Polisi kupewa Mamlaka hayo, kwani uhuru wa habari, itakuwa bado haujakuwepo nchini.

 

"Ikiwa afisa atakuwa na ugomvi na mwandishi, anaweza kufanya upekuzi au kukamata gazeti, hali ambayo itasababisha taharuki katika vyombo vyetu,’’ anasema.

 

Diwani wa Jimbo la Ole kupitia CCM Khadija Henock Maziku anasema, ilipaswa kifungu kieleze, wakishatuhumu wafanye uchunguzi kwanza, ndipo wakamate gazeti.

 

"Hii ya kuchukua uamuzi wa kukamata gazeti bila kufanya uchunguzi, ni kudhalilisha chombo cha habari na waandishi wake, watakapotuhumu wanatakiwa wafanye upelelezi wa siri, ndipo mengine yaendelee", anashauri. 

 

Anafafanua kuwa, ikiwa watafanya hivyo kutokana na kifungu kinavyoeleza, watawajengea woga waandishi wa habari na kusababisha kufanya kazi zao vibaya.

 

"Baada ya kuthibitisha kuwa kuna ukiukwaji wa sheria ndipo watangaze na kulikamata gazeti, na baadae wawajibishwe lakini sio kwa kutuhumu tu, hiyo sio sawa,’’ anasema.

 

Hafidh Abdi Said ambae ni Mwenyekiti wa CHADEMA Wilaya ya Chake Chake anasema, baadhi ya vifungu vya sheria iliyopo ni kwa maslahi ya wachache, ndio maana zinawakwaza wengine.

 

Anasema, baadhi ya vifungu havipo kumlinda mwandishi na vyombo vya habari, na wala havina maslahi kwao, hivyo kuna haja ya kufanyiwa marekebisho.

 

"Kifungu hicho hakifai kuwepo kwa wakati huu tulionao, kwani waandishi watashindwa kufanya kazi zao na wananchi watakosa haki yao ya kupata habari,’’ anaeleza.

 

Mwanasheria wa serikali Ali Amour Makame anasema kwamba, sio sahihi kifungu hicho kuwepo kwa sababu, kisheria halitakiwi kuwepo neno ‘kwa maoni yake’ na haifai kwa Afisa Polisi kupewa mamlaka hayo kwani, habari inaweza kuwa sahihi kwa mujibu wa maadili yao, lakini yeye isimfurahishe.

 

‘’Elimu za Polisi tunazijua, iweje wapewe mamlaka hayo kwa taaluma nyengine?, hii sio sahihi, kinachoshangaza zaidi ni pale sheria hii ilipoeleza kwamba kwa maoni yake, akituhumu, hichi kitu hakipo kwenye sheria’’, anafafanua.

 

Akielezea kuhusu upekuzi na ukamataji, kifungu hicho kinaenda kinyume na vifungu vya sheria nyengine, ambavyo vinaeleza namna ya kufanya upekuzi na ukamataji wa vitu vinavyodhaniwa kuwa ni makosa.

 

TAMWA –ZANZIBAR, MCT NA INTERNEWS

Fat-hiya Mussa Said ambae ni Mratibu wa TAMWA Pemba anaefahamisha, Polisi wana mamlaka ya kulinda raia na mali zao na kulinda amani ya nchi, ndio maana walipewa mamlaka hayo, lakini kwa wakati wa sasa kifungu hicho kinahitaji maboresho.

 

"Kitakapoboreshwa kifungu hicho, waandishi watakuwa huru kufanya kazi zao za kihabari na wananchi watapata habari, uhuru wa kutoa maoni na kujieleza", anasema.

 

Katibu Mtendaji wa Baraza la Habari Tanzania (MCT) Kajubi Mukajanga anasema, waandishi wasipozielewa sheria zao, mchakato wa kupitisha utakuwa kwenye mikono ya wanasheria na wanasiasa na hivyo watapendekeza wanavyotaka.

 

Afisa Mdhamini MCT Zanzibar Shifaa Said Hassan anasema, pamoja na kuzieleza sheria hizo na mapungufu yake tangu 2010, lakini bado inaendelea kutumika, jambo ambalo linawapa wakati mgumu katika kuendeleza tasnia ya habari nchini.

 

"Haya mamlaka aliyopewa Ofisa Polisi sio sahihi kwa kweli na wala haileti picha nzuri, mimi naona ni udhalilishaji wa waandishi na vyombo vyetu, tuendelee kuzisemea sheria hizi ili vifungu vinavyotukwaza viondoshwe", anafafanua Shifaa.

 

"Ni miaka 12 sasa harakati za kupigania uwepo wa sheria nzuri za habari zinafanyika kwa maslahi ya jamii na Taifa kwa ujumla, lakini bado hatujafikia tunapopataka", anasema  Zanziba Mzee Mratibu wa Internews Zanzibar wakati akizungumza na waandishi wa habari mjini Zanzibar.

 

Anasema, kuna vifungu vingi ambavyo vinahitaji kufanyiwa marekebisho ikiwemo cha 27 (1), (3), kwani vinawanyima waandishi uhuru na kuwakosesha wananchi haki ya kutoa maoni na kujieleza.

 

Ndio maana Internews kwa sasa imeshirikiana na wadau wake ikiwemo MCT, TAMWA Zaznibar na waandishi wa habari, ili kuviibua vifungu vyenye kero na kufanyiwa marekebisho.

 

‘’Nguzo kubwa ya kuleta mabadiliko katika kila jambo, basi ni kufanya kazi kwa karibu na vyombo vya habari, kama tunavyofanya sisi Internews juu ya upatikanaji wa sheria rafiki ya habari Zanzibar,’’anasema Zaina.

 

Hata hivyo, amewasisitiza waandishi kuendea kutengeneza vipindi, Makala, ujumbe mfupi mfupi na habari za kawaida, ili kuvieleza vifungu kandamizi kwa uhuru wa habari

 

ATHARI ZA VIFUNGU KANDAMIZI KW AUHURU W AHABARI ZANZIBAR

 

Hanifa Salim Mohamed ambae ni mwandishi wa gazeti la Zanzibarleo Pemba anasema, athari zinazoweza kujitokeza ni pamoja na waandishi kufanya kazi kwa hofu, hali ambayo itasababisha kutofanya kazi vizuri.

 

"Itakuwa hatuko huru katika utendaji wa kazi zetu, kwa sababu tutafanya kazi kwa woga na hii itapelekea kushindwa kuibua yale ambayo yanaikwaza jamii", anasema.

 

Hafidh Abdi Said ambae ni Mwenyekiti wa CHADEMA Wilaya ya Chake Chake anasema athari yake ni kwamba, watu watashindwa kutoa maoni yao kwani watahofia kukamatwa pamoja vyombo hivyo vya habari kufungwa, hivyo hata maendeleo yatakuwa ni duni.

 

"Vyombo vya habari ndivyo ambavyo vinaleta maendeleo katika nchi yeyote duniani lakini ikiwa kutakuwa na sheria ambazo ni kandamizi, tusitegemee kuleta mabadiliko ya kimaendeleo", anasema.

 

Mratibu wa TAMWA Pemba Fat-hiya Mussa Said anasema, athari itakayojitokeza ni kwamba watu watakosa haki yao ya kujieleza na kupata habari.

 

"Vyombo vya habari vinapokuwa huru na hata wananchi watakuwa huru kuelezea yale yanayowakwaza na hapo ndipo yatakapotatuliwa na kufikia pale tunapopataka ambayo ni nchi yenye Maendeleo", anaeleza.

 

Mwanasheria wa Shirika la Magazeti ya serikali Zanzibar Juma Khamis Juma, anafafanua kuwa, wananchi watakosa taarifa ambazo ni haki yao kuzipata kwa mujibu wa Katiba.

 

‘’Sio habari zote zitakazoandikwa zitawafurahisha hao Maofisa Polisi na wengine, kwa hiyo ikiwa ana chuki na chombo au mwandishi wa habari, atalikamata gazeti na kulisababisha lisifanye kazi zake’’, anafafanua.

 

Tatu Abdalla Mselem ambae ni Mratibu wa TUJIPE Pemba anasema, waandishi wa habari itakuwa hawafanyi kazi zao vizuri kwa sababu watakuwa na hofu katika kukusanya, kuandika na kurusha habari zao.

 

‘’Ilikuwa mamlaka kisheria wapewe wanahabari wenyewe kwani Ofisa Polisi anaweza kuwa na chuki zake binafsi akatumia mamlaka anayopewa, Maafisa hao wachukuliwe kama wadau na sio kupewa mamlaka kwani chombo cha habari ni cha kujitegemea’’, anaeleza.

 

NINI KIFANYIKE

Mkuu wa taaluma wa Chuo cha uandishi wa habari na mawasiliano ya Umma Zanzibar Imane Duwe, anasema kwanza kufutwa kwa sheria hiyo kongwe na kuwa na sheria rafiki kw auhuru wa habari.

 

Mwananchi Asha Salim Ali mkaazi wa Wete anasema, ili kuwe na uhuru wa vyombo vya habari kuna haja ya kuvifanyia maboresho vifungu vyote vinavyominya uhuru wa habari.

 

Khamis Mohamed mkaazi wa Gombani Chake Chake anafahamisha kuwa, Ofisa wa Polisi asipewe mamlaka hayo na badala yake iundwe bodi maalumu ya kuweza kuchunguza tuhuma na itakapothibitika chombo kimekiuka sheria ndipo kichukuliwe hatua.

 

"Mimi iliyonishangaza ni hii kwamba Ofisa Polisi hata akituhumu tu anaweza kukamata gazeti au hata kitabu cha mwandishi, kwa kweli hii sio sahihi hata kidogo", anafahamisha.

 

Mwanasheria Ali Amour Makame anashauri, gazeti hilo litakapokamatwa libaki kwa Mrajisi katika uchunguzi wake ndipo aweze kubaini kwamba habari gani sio sahihi lakini sio kupewa mamlaka hayo askari yeyote.

 

Ali Massoud Kombo anasema, Jeshi la Polisi lisipewe Mamlaka hayo, hivyo wadau waendelee kutoa mapendekezo ili kuhakikisha vyombo vya habari vinakuwa huru na hapo ndipo vitafanya kazi zao vizuri.

 

Baadhi ya vifungu vya sheria ya Wakala wa Habari, Magazeti na Vitabu bado vinaminya uhuru wa vyombo vya habari, hivyo kuna haja ya kufanyiwa maboresho ili waandishi wafanye kazi zao vizuri.

 

                                                       MWISHO.

 

 

 

Comments

BLOG'S VISITORS

DAKTARI MWENGINE CHAKE CHAKE KULA SIKUKUU POLISI, NI KWA TUHUMA ZA KUMBAKA MGONJWA WAKE

NA WAANDISHI WETU, PEMBA::: DAKTARI anaetoa huduma kwa wagonjwa kituo cha afya cha serikali cha  Gombani wilaya ya Chake Chake Pemba, Is-haka Rashid Hadid, anaendelea kushikiliwa na Jeshi la Polisi Mkoa wa kaskazini Pemba, akituhumiwa kumtorosha na kisha kumbaka mtoto wa mwenye umri wa miaka 16, mkaazi wa Gombani. Daktari huyo miaka 35 ni mkaazi wa Kangagani Wilaya ya Wete mkoani humo, ambapo anadaiwa alimchukua mtoto huyo kutoka kwa rafiki yake, na kumpeleka kwenye nyumba anayoishi eneo la Kangagani. Mtoto aliefanyiwa kitendo hicho alisema kuwa, April 21 mwaka huu alikwenda kituo cha afya Gombani, kwa ajili ya matibabu na baada ya kupatiwa huduma na daktari huyo, alimuomba nambari yake ya simu. Alisema ilipofika usiku, walikuwa wanawasiliana kupitia ujumbe mfupi (sms) kwa lengo la kwenda kuchukua dawa nyingine ambazo kwa mchana huo alizikosa hospitalini hapo. "Nilikwenda hospitali kutibiwa, baada ya kufanya mapele katika sehemu zangu za siri, lakini akaniambia mpaka aje da

'MKAPA' NA WENZAKE PEMBA WALAZWA RUMANDE

  NA HAJI NASSOR, PEMBA@@@@ MAHKAMA kuu Zanzibar kisiwani Pemba, chini ya Jaji Ibrahim Mzee Ibrahim, imewapeleka rumande watumuhimwa wanne wanaokabiliwa na tuhuma za kuua kwa makusudi, akiwemo Ali Mussa Omar ‘ Mkapa’ mkaazi wa Wawi wilaya ya Chake chake Pemba. Watuhumiwa wengine walioanza maisha mapya ya rumande ni mtuhumiwa Yassir Mohamed Juma miaka 23, Anuwari Mussa Omar miaka 30 pamoja na mtuhumiwa Yassir Mussa Omar ‘ Makababu ’ miaka 29, wote wakaazi wa shehia ya Wawi, wilaya ya Chake chake Pemba. Awali watuhumiwa hao waliwasili mahakamani hapo, kwa mara ya kwanza, kwa ajili ya kusomewa tuhma zinazowakabili za kumuua kwa maksudi Said Seif Kombo. Ilidaiwa mahakamani hapo na Mwendesha Mashtaka kutoka Ofisi ya Mkurugenzi wa Mashataka Seif Mohamed Khamis akiambatana na mwenzake Mussa Khamis Ali kuwa, watuhumiwa hao kwa pamoja wanadaia kufanya mauwaji hayo kwa maksudi. Ilidai kuwa, watuhumiwa wote kwa pamoja, walitenda kosa hilo Oktoba 16, mwaka huu, baina ya saa 7:00 mchan

HII KALI MBUNGE ASIYA AMKOGESHA MWANANCHI HADHARANI KISA HICHI HAPA......

  NA HAJI NASSOR, PEMBA MBUNGE wa viti maalum nafasi za wanawake mkoa wa kaskazini Pemba Asiya Sharif Omar, amewataka wananchi wa kijiji cha taifu, shehia ya Kinyasini jimbo la Gando wilaya ya Wete Pemba, kuyalinda miundombinu ya maji safi na salama, ili yawe endelevu kwao. Kauli hiyo ameitoa wakati alipokuwa akizungumza na mwandishi wa habari hizi, mara baada ya kuwasili kijijini humo, na kumkogesha mwananchi mmoja kama ishara ya uzinduzi wa mradi wa maji safi na salama, ulioasisiwa na mbunge wa Jimbo la Gando. Alisema, hawana mbadala kwa sasa bali ni kuilinda miundombinu ya huduma hiyo, hasa baada ya mbunge wa wao Salim Mussa Omar, kuwarejeshea huduma hiyo. Alieleza kuwa, inafahamika kuwa kwa miaka 14 waliikosa huduma hiyo hasa kwa vile viongozi waliokuwepo hawakujali kuwatatulia tatizo hilo, hadi juzi ilipofanywa na mbunge wao. “Baada ya huduma hii sasa kurejeshwa na mbunge wa jimbo la Gando, kazi iliyobakia kwenu wananchi ni kila mmoja kuwa mlinzi wa miundombinu hii,’’ali

TUHMA ZA DAKTARI PEMBA KUCHIWA HURU: POLISI KASKAZINI KUTOA TAARIFA RASMI LEO

  NA HAJI NASSOR, PEMBA KAMANDA wa Polisi mkoa wa kaskazini Pemba, Juma Saad Khamis, amesema leo Mei 9, mwaka huu atatoa taarifa rasmi, juu ya kuendelea kumshikilia au kumpa dhamana ya Polisi, daktari wa Kituo cha Afya Gombani Is-haka Rashid Hadid, anayetuhumiwa kwa ubakaji. Alisema, kwa vile alikuwa katika mapumziko mafupi, haelewi jambo lolote linaloendelea kwa mtuhumiwa huyo, juu ya kuendelea kushikiliwa kwake kituoni hapo. Alieleza kuwa, leo Mei 6 (jana), hajapata taarifa za ndani za mtuhumiwa, huyo na kuwataka wananchi na wanaharakati, wasubirie hadi Jumatatu ijayo. Akizungumza na waandishi wa habari kwa nyakati tofauti Kamanda huyo, alisema hana taarifa zozote za kupewa dhamana mtuhumiwa ndani ya kituo chake cha Polisi au kuendelea kuwepo. ‘’Ilikuwa mimi sipo kazini kwa muda, kuanzia anakamatwa hadi anafikishwa Polisi, kwa sasa siwezi kueleza jambo lolote kwa mtuhumiwa huyo, hadi Jumatatu,’’alieleza. Aidha Kamanda huyo alieleza kuwa, kwa sasa hawezi kutoa ufafan

MADAKTARI KUTOKA CHINA WAOKOA MAISHA YA MTOTO PEMBA

  HABIBA ZARALI, PEMBA TIMU ya 32 ya madaktari wa kichina katika hospitali ya Abdalla Mzee Mkoani wamefanikiwa kufanya upasuaji mkubwa wa mtoto mwenye umri wa miaka 15 mkaazi wa Chole Kengeja, baada ya kuchomwa na jiti sehemu ya njia zake za mfumo wa uzazi. Mtoto huyo ambae alianguka hivi karibuni katika mti na baadae kuchomwa na jiti hilo na kumsababishia kutokwa na damu nyingi katika sehemu ya nyonga, alifanyiwa upasuaji uliodumu kwa muda wa saa tatu na   kuokolewa maisha yake. Akizungumza mara baada ya operesheni huo kiongozi wa timu hiyo Dr Jiang Jinhua, alisema mara baada ya mtoto huyo kufikishwa hospitalini hapo na kufanyiwa vipimo na kuonekana   ilibidi apatiwe rufaa ya kwenda katika hospitali nzuri yenye kutibu tatizo lake huko nchini Kuwado ambapo haikuwezekana kutokana na hali ya umaskini wa f amilia ya mtoto huyo . Alisema timu ya madaktari hao itaendelea kutowa huduma za matibabu   kwa wananchi kisiwani humo,   ili kuwaondolea gharama ya kutafuta matibabu nje ya nch