Skip to main content

MIMBA ZA PAPO KWA PAPO ZILIVYO HATARI KWA MAMA MWENYE VVU

 


NA ZUHURA JUMA, PEMBA::::


UZAZI ni sehemu ya maisha ya mwanadamu.

Ambapo mwanaume hutoa mbegu na mwanamke hupokea, ndipo hapo anapopatikana mtoto, awe wa kiume ama wa kike.

Kila mmoja anapokuwa na mweza wake, mwisho wa siku wanatumainia watoto na hapo furaha huzidi kutawala ndani ya nyumba na familia kwa ujumla.

Pamoja na kwamba kila mmoja anahitaji watoto katika maisha yake, lakini ni muhumu sana kufuata utaratibu mzuri kwa lengo la kuimarisha afya ya mtoto na mama.

Hii humfanya kuweka hali bora ya kiafya, katika mwili na kuimarisha fuko lake la uzazi kwa kujitayarisha kubeba tena mimba nyengine.

Wapo baadhi ya akinamama hufurahia sana kuzaa papo kwa papo, kwa kile wanachodai kuwa, wamalize haraka na baadae wapumzike bila kujali usalama wa afya zao.

Wafahamu kuwa, kutumia uzazi wa mpango kwa akinamama ni muhimu sana katika kuimarisha afya zao, kwani dini ya kiislamu, imehimiza mtoto kunyonyeshwa miaka miwili.

Qur-an tukufu katika Suratul-Baqarah aya ya 233 imeeleza kuwa ‘Wazazi wa kike wanyonyeshe watoto wao miaka miwili, kwa mwenye kutaka kutimiza kunyonyesha…’

Hiyo inaonesha wazi kwamba, kuachisha mtoto kwa miaka miwili ni muhimu sana kwa akinamama kutokana na faida inayopatikana ndani yake.

HALI IKOJE KWA AKINAMAMA WENYE VVU?

Akinamama wanaoishi na Virusi vya Ukimwi, wanahitaji mapumziko baada ya kujifungua, ili apate kuimarika kiafya pamoja na mtoto wake.

Huku akifuata maelekezo ya daktari wakati gani kwake anaweza kubeba mimba.

Dk, Rahila Salim Omar ambae ni msimamizi wa vituo vya kutoa huduma kwa watu wenye ‘VVU’ anasema, mwili unapotoa kiumbe, unahitaji kujirejesha tena katika hali ya kawaida na ndipo uweze kubeba mimba nyengine.

Wakati wa ujauzito, kinga ya mwili inashuka, kwa hiyo uwezekano wa kupata maambukizi mengine unakuwa ni mkubwa zaidi yeye ama mtoto.

Anafahamisha, afya inakuwa bado haijarudi katika hali yake ya kawaida, hivyo virusi vinaweza kupanda kwa vile kinga yake imeshuka na hatimae kumuambukiza mtoto.

“Hata kama mama mwenye ‘VVU’ tumempima jana, basi akija leo ikiwa tumemgundua na ujauzito, tunampima tena wingi wa virusi, je idadi haijaongezeka?”, anaelezea.

Na ikiwa virusi vimeongezeka, wanampa huduma ya ziada kuweza kumkinga mtoto na maambukizi hayo, ambapo wanampima kila baada ya miezi mitatu, mpaka pale atakapoachisha.

“Kile ndio kipindi ambacho anaweza kumuambukiza mtoto, ama wakati wa ujauzito, wakati wa kujifungua au wakati wa kunyonyesha, ikiwa atakuwa na maradhi au vidonda mdomoni”, anafahamisha.

Wanapendekeza kwamba, baada ya mama kujifungua, akae miaka miwili, ili mwili ujirudi na afya iwe nzuri, ndipo abebe mimba nyengine.

Dk, Rahila anawashauri akinamama hao kabla ya kubeba ujauzito, wafike hospitali, ili wafanyiwe uchunguzi kwamba je, anaweza kubeba mimba nyengine au kinyume chake.

“Wengine wanatwambia na wengine tunakuja kugundua tayari wameshabeba mimba, lakini tunatakiwa tuwapime wingi wa virusi, ikiwa ni kidogo ndipo tuwaruhusu kubeba mimba”, anaeleza.

Pamoja na ushauri wanaoutoa kwa akinamama hao, bado kuna baadhi yao wana usiri mkubwa, jambo ambalo linaweza kusababisha maambukizi kwa mtoto, anaezaliwa na yule wa nyuma yake ambae hakuachishwa.

Anasema, wanawafuatilia kwa umakini na wapo vizuri kwenye huduma za mama wajawazito, wanaoishi na VVU, hivyo wanashukuru kwani ni asilimia ndogo sana ya watoto wanaozaliwa na VVU.

Na hiyo ni kwa sababu baadhi ya akinamama hao hawafuati maelekezo ya daktari na kutotumia dawa za ARV kwa usahihi.

Dk. Rahila anasema, ikiwa mama ana VVU anaweza kumuambukiza mtoto wake hasa, ikiwa hakutumia vizuri dawa za ‘ARV’ ambazo zinapunguza idadi ya virusi mwilini.

Kuanzia mwaka 2020 hadi Machi mwaka huu ni watoto wawili tu ambao wameambukizwa VVU na mama zao baada ya kuzaliwa, kati ya vipimo 102 vilivyopimwa kisiwani Pemba.

‘’Vipimo vyetu tunafanya pale mtoto anapofikisha wiki sita baada ya kuzaliwa, miezi tisa na mwaka mmoja na nusu, hivyo tuligundua watoto wawili tu wameambukizwa’’, anasema.

Anaeleza, sababu ya kuambukizwa watoto hao ni kutokana na mama zao kutohudhuria vizuri kliniki na kutofuata hatua zinazotakiwa, ikiwa ni pamoja na kutotumia dawa vizuri.

Dk, Khamis Hamad ambae Msaidizi Meneja Kitengo Shirikishi cha Ukimwi, Kifua kikuu, Homa ya ini na Ukoma, anaeleza, kuwa mama mjamzito ambae anaishi VVU anahitaji zaidi kuzaa kwa mpango.

“Ingawa wajawazito wote kinga yao hupungua, lakini hawa wanaoishi na VVU inapungua zaidi, hivyo anatakiwa apangiwe muda wa kuzaa kulingana na idadi ya virusi alivyonavyo”, anasema.

Kutokana na mimba za papo kwa papo, mwili unakuwa hauwezi kujirudi na unakuwa dhaifu, hivyo mama atakuwa hana mda wa kumshughulikia mtoto alienae, kwa malezi na hata mfumo wa kula.

Mtoto anatakiwa anyonye maziwa ya mama kwa miezi sita bila kumchanganyia chochote, lakini ikiwa mama atabeba mimba nyengine kabla ya wakati unaotakiwa, atamkosema mawanwe haki zinazostahiki.

“Ikiwa ndani ya miezi sita unabeba mimba, unaanza kumkosesha haki ya kumnyonyesha huyu mtoto ulienae, unakosa mda wa kujiandaa kiuchumi na kimwili”, anaeleza.

Hivyo anaanza kuchanganya vyakula huku anaendelea kumnyonyesha, hatima yake ikiwa ziwa la mama lina vidonda na mtoto akiwa ana michubuko mdomboni anamuambukiza.

MAMA WENYE VVU

Maryam Salum mkaazi wa Mabaoni Chake chake, anaeishi na VVU alishawahi kupata elimu kupitia wataalamu wa afya, na sasa amekuwa akifika kliniki, kila anapotaka kubeba ujauzito.

“Najitahidi kufuata ushauri wa daktari, ili kumkinga mtoto wangu dhidi ya maambukizi, kwa sababu unapotaka kubeba mimba unapewa maelekezo na ni vizuri uyafuate”, anafahamisha.

Maryam, baada ya kubeba mimba anatakiwa kutumia dawa vizuri na chakula kizuri kwa lengo la kujenga afya yake na mtoto.

Lengo ni kumkinga mtoto asipate maambukizi ya VVU, na kuongeza idadi ya watu wanaoishi na maambukizi mapya.

Maryam ameolea na mume ambae hana maambukizi, ambapo amezaa mtoto, ambae hana maambukizi na kwa sasa ana miezi tisa anaendelea kumnyonyesha.

‘’Kuna faida kubwa kwa mama mwenye ‘VVU’ kuachisha, kwa sababu afya yake sio nzuri, ukilinganisha ya akinamama wasio na VVU’’, anaeleza.

Anatakiwa kulinda afya yake na hatakiwi kuzaa mtoto mwengine hadi pale afya yake, itakapoimarika, kwani ikiwa afya yake sio nzuri kuna uwezekano mkubwa wa kumuambukiza mtoto.

Maryam Said Abdalla mkaazi wa Chake Chake mbae anaishi na VVU, anasema kuna umuhimu mkubwa kwa mama mwenye VVU kutumia uzazi wa mpango hasa kwa vile kinga zao ni tofauti na akinamama wasio na virusi vya Ukimwi.

“Kinga yetu ikishuka zaidi, lile fuko la uzazi linaweza kubeba maambukizi na likamsababishia mtoto maambukizi hayo”, anasema Maryam ambae pia ni Mwenyekiti wa Jumuiya ya watu wanaoisha na VVU Wilaya ya Chake Chake.

Na ndio maana hata kama mama hana maambukizi anatakiwa kuzaa kwa kiasi, kwa sababu atakapomnyonyesha mtoto kwa miaka miwili na kupumzika mwaka mmoja, analifanya fuko la uzazi kurudi pale pale kwenye sehemu yake.

“Hapo kinga yako inakuwa nzuri na damu haipotei, kwani mwenye maambukizi yuko katika hatari ya kubeba maambukizi mengine kutokana na kinga yake kushuka”, anasema.

Ni mwaka wa 16 anaishi na virusi vya ukimwi ingawa anazaa kwa mpango na kufuata ushauri wa daktari kwani ndie anaejua kwamba, virusi alivyonavyo ana uwezo wa kubeba mimba au apate muda zaidi wa kupumzika.

Anasema, hawajapokea kesi ambayo ilitokea kwa sababu mama hakutumia uzazi wa mpango, isipokuwa zinazotokea ni zile ambazo hahudhurii kliniki vizuri na kutotumia dawa.

TUME YA UKIMWI

Ali Mbarouk Omar ambae ni Kaimu Mratibu Tume ya Ukimwi Pemba anasema, ikiwa mama mwenye VVU atazaa papo kwa papo, anapata athari kwa sababu ya kupungua kinga yake ya mwili.

‘’Na kinga ya mwili ikipungua inasababisha kupata magojwa nyemelezi na mtoto anakuwa katika hatari ya kuambukizwa VVU kwa sababu mama hana kinga ya kutosha”, anasema.

NINI KIFANYIKE

Maryam Said Abdalla anawataka akinamama wanaoishi na VVU wafike kwenye kliniki zao ili wafahamishwe jinsi ya kubeba ujauzito kwa ajili ya kumkinga mtoto asipate maambukizi.

“Unapangiwa muda ambao ni stahiki kwako kubeba mimba na pia unapata muda wa kuwashughulikia watoto huku ukiwa na afya bora na nguvu nzuri’’, anaeleza.

Ali Mbarouk Omar ambae ni Mratibu wa Tume ya Ukimwi Pemba anawataka akinamama hao kutumia njia za uzazi wa mpango kuhakikisha wanapata muda wa kupumzika, ili mwili ujirudi katika hali nzuri.

Anasema, ipo haja ya kufuata ushauri wa daktari mara kwa mara, jambo hilo litasaidia kumkinga mtoto na maambukizi ya Virusi vya Ukimwi.

MIKAKATI ILIYOWEKWA KUHAKIKISHA WATOTO WANAZALIWA NA KUKUA SALAMA

Dk, Khamis anaeleza, mikakati ya kitengo ni kuhakikisha kila mama mjamzito ambae anaishi na VVU anatumia dawa za ARV kwa usahihi, ambazo zipo vituo vikubwa vinne vilivyopo kisiwani Pemba.

Wanapewa elimu pamoja na wenza wao, ili ikiwa na yeye ana virusi aweze kutumia dawa kwa sababu, ikiwa mama anatumia dawa lakini mume hatumii, anamuongezea virusi na inasababisha mtoto kupata maambukizi.

“Yeye itakuwa anatumia dawa lakini mume wake anamuongezea mzigo kila siku, hivyo wote ni vyema wakatumia dawa ili kumnusuru mtoto asipate maambukizi”, anaeleza daktari huyo.

Anafahamisha, wanawafuatilia vya kutosha wanaoishi na virusi vya ukimwi katika kuhakikisha wanatumia dawa kwa usahihi.

Uzazi wa mpango ni muhimu kwa mama mwenye VVU kwani inampa nafasi ya kurudisha afya yake katika hali nzuri na kupata nafasi ya kumuhudumia mtoto wake vizuri, ili asipate maambukizi.

                                                     MWISHO.

Comments

BLOG'S VISITORS

DAKTARI MWENGINE CHAKE CHAKE KULA SIKUKUU POLISI, NI KWA TUHUMA ZA KUMBAKA MGONJWA WAKE

NA WAANDISHI WETU, PEMBA::: DAKTARI anaetoa huduma kwa wagonjwa kituo cha afya cha serikali cha  Gombani wilaya ya Chake Chake Pemba, Is-haka Rashid Hadid, anaendelea kushikiliwa na Jeshi la Polisi Mkoa wa kaskazini Pemba, akituhumiwa kumtorosha na kisha kumbaka mtoto wa mwenye umri wa miaka 16, mkaazi wa Gombani. Daktari huyo miaka 35 ni mkaazi wa Kangagani Wilaya ya Wete mkoani humo, ambapo anadaiwa alimchukua mtoto huyo kutoka kwa rafiki yake, na kumpeleka kwenye nyumba anayoishi eneo la Kangagani. Mtoto aliefanyiwa kitendo hicho alisema kuwa, April 21 mwaka huu alikwenda kituo cha afya Gombani, kwa ajili ya matibabu na baada ya kupatiwa huduma na daktari huyo, alimuomba nambari yake ya simu. Alisema ilipofika usiku, walikuwa wanawasiliana kupitia ujumbe mfupi (sms) kwa lengo la kwenda kuchukua dawa nyingine ambazo kwa mchana huo alizikosa hospitalini hapo. "Nilikwenda hospitali kutibiwa, baada ya kufanya mapele katika sehemu zangu za siri, lakini akaniambia mpaka aje da

'MKAPA' NA WENZAKE PEMBA WALAZWA RUMANDE

  NA HAJI NASSOR, PEMBA@@@@ MAHKAMA kuu Zanzibar kisiwani Pemba, chini ya Jaji Ibrahim Mzee Ibrahim, imewapeleka rumande watumuhimwa wanne wanaokabiliwa na tuhuma za kuua kwa makusudi, akiwemo Ali Mussa Omar ‘ Mkapa’ mkaazi wa Wawi wilaya ya Chake chake Pemba. Watuhumiwa wengine walioanza maisha mapya ya rumande ni mtuhumiwa Yassir Mohamed Juma miaka 23, Anuwari Mussa Omar miaka 30 pamoja na mtuhumiwa Yassir Mussa Omar ‘ Makababu ’ miaka 29, wote wakaazi wa shehia ya Wawi, wilaya ya Chake chake Pemba. Awali watuhumiwa hao waliwasili mahakamani hapo, kwa mara ya kwanza, kwa ajili ya kusomewa tuhma zinazowakabili za kumuua kwa maksudi Said Seif Kombo. Ilidaiwa mahakamani hapo na Mwendesha Mashtaka kutoka Ofisi ya Mkurugenzi wa Mashataka Seif Mohamed Khamis akiambatana na mwenzake Mussa Khamis Ali kuwa, watuhumiwa hao kwa pamoja wanadaia kufanya mauwaji hayo kwa maksudi. Ilidai kuwa, watuhumiwa wote kwa pamoja, walitenda kosa hilo Oktoba 16, mwaka huu, baina ya saa 7:00 mchan

HII KALI MBUNGE ASIYA AMKOGESHA MWANANCHI HADHARANI KISA HICHI HAPA......

  NA HAJI NASSOR, PEMBA MBUNGE wa viti maalum nafasi za wanawake mkoa wa kaskazini Pemba Asiya Sharif Omar, amewataka wananchi wa kijiji cha taifu, shehia ya Kinyasini jimbo la Gando wilaya ya Wete Pemba, kuyalinda miundombinu ya maji safi na salama, ili yawe endelevu kwao. Kauli hiyo ameitoa wakati alipokuwa akizungumza na mwandishi wa habari hizi, mara baada ya kuwasili kijijini humo, na kumkogesha mwananchi mmoja kama ishara ya uzinduzi wa mradi wa maji safi na salama, ulioasisiwa na mbunge wa Jimbo la Gando. Alisema, hawana mbadala kwa sasa bali ni kuilinda miundombinu ya huduma hiyo, hasa baada ya mbunge wa wao Salim Mussa Omar, kuwarejeshea huduma hiyo. Alieleza kuwa, inafahamika kuwa kwa miaka 14 waliikosa huduma hiyo hasa kwa vile viongozi waliokuwepo hawakujali kuwatatulia tatizo hilo, hadi juzi ilipofanywa na mbunge wao. “Baada ya huduma hii sasa kurejeshwa na mbunge wa jimbo la Gando, kazi iliyobakia kwenu wananchi ni kila mmoja kuwa mlinzi wa miundombinu hii,’’ali

TUHMA ZA DAKTARI PEMBA KUCHIWA HURU: POLISI KASKAZINI KUTOA TAARIFA RASMI LEO

  NA HAJI NASSOR, PEMBA KAMANDA wa Polisi mkoa wa kaskazini Pemba, Juma Saad Khamis, amesema leo Mei 9, mwaka huu atatoa taarifa rasmi, juu ya kuendelea kumshikilia au kumpa dhamana ya Polisi, daktari wa Kituo cha Afya Gombani Is-haka Rashid Hadid, anayetuhumiwa kwa ubakaji. Alisema, kwa vile alikuwa katika mapumziko mafupi, haelewi jambo lolote linaloendelea kwa mtuhumiwa huyo, juu ya kuendelea kushikiliwa kwake kituoni hapo. Alieleza kuwa, leo Mei 6 (jana), hajapata taarifa za ndani za mtuhumiwa, huyo na kuwataka wananchi na wanaharakati, wasubirie hadi Jumatatu ijayo. Akizungumza na waandishi wa habari kwa nyakati tofauti Kamanda huyo, alisema hana taarifa zozote za kupewa dhamana mtuhumiwa ndani ya kituo chake cha Polisi au kuendelea kuwepo. ‘’Ilikuwa mimi sipo kazini kwa muda, kuanzia anakamatwa hadi anafikishwa Polisi, kwa sasa siwezi kueleza jambo lolote kwa mtuhumiwa huyo, hadi Jumatatu,’’alieleza. Aidha Kamanda huyo alieleza kuwa, kwa sasa hawezi kutoa ufafan

MADAKTARI KUTOKA CHINA WAOKOA MAISHA YA MTOTO PEMBA

  HABIBA ZARALI, PEMBA TIMU ya 32 ya madaktari wa kichina katika hospitali ya Abdalla Mzee Mkoani wamefanikiwa kufanya upasuaji mkubwa wa mtoto mwenye umri wa miaka 15 mkaazi wa Chole Kengeja, baada ya kuchomwa na jiti sehemu ya njia zake za mfumo wa uzazi. Mtoto huyo ambae alianguka hivi karibuni katika mti na baadae kuchomwa na jiti hilo na kumsababishia kutokwa na damu nyingi katika sehemu ya nyonga, alifanyiwa upasuaji uliodumu kwa muda wa saa tatu na   kuokolewa maisha yake. Akizungumza mara baada ya operesheni huo kiongozi wa timu hiyo Dr Jiang Jinhua, alisema mara baada ya mtoto huyo kufikishwa hospitalini hapo na kufanyiwa vipimo na kuonekana   ilibidi apatiwe rufaa ya kwenda katika hospitali nzuri yenye kutibu tatizo lake huko nchini Kuwado ambapo haikuwezekana kutokana na hali ya umaskini wa f amilia ya mtoto huyo . Alisema timu ya madaktari hao itaendelea kutowa huduma za matibabu   kwa wananchi kisiwani humo,   ili kuwaondolea gharama ya kutafuta matibabu nje ya nch