Skip to main content

KHADIJA HENOCK: DIWANI WADI YA OLE ATAJA YANAYOMKOSESHA RAHA

 



NA ZUHURA JUMA, PEMBA

“KUTOKANA malezi mazuri niliyolelewa na wazazi wangu, baada ya kumaliza skuli sikujipweteka… nilianza kazi ya kuisaidia jamii na mpaka sasa naendelea”,

…Si maneno ya mtumwengine, bali ni ya Khadija Henock Maziku mkaazi wa shehia ya Mjiniole ambae kwa sasa ndio Diwani wa Wadi ya Ole, Jimbo la Ole wilaya ya Chake chake Pemba.

HARAKARI ZA UONGOZI

Khadija alianza harakati zake za uongonzi tangu mwaka 2007 akiwa katika Jumuiya ya Wanawake (JUWAKAP).

Kwa wakati huo, ambayo ilishirikiana na Shirika la Action Aid, akiwa kama Makamu Mwenyekiti kwa wilaya ya Wete na hatimae kuwa Katibu kwa Mkoa wa Kaskazini Pemba.

Dira ya Jumuiya hiyo ilikuwa ni kumkomboa mwanamke, katika nyanja zote za kisiasa, kijamii na kiuchumi.

Kazi yao ni kuhamasisha wanawake kugombea nafasi za uongozi, ili waondokane na utegemezi huku wakiwa mstari wa mbele kupiga vita vitendo vya ukatili na udhalilishaji.

Mwaka 2009 walifikiwa na mradi wa WEZA kutoka TAMWA, ambao uliwahamasisha wanawake kuanzisha vikundi vya kuweka na kukopa, ambapo walichagua viongozi mbali mbali akiwemo yeye.

Wakati anatoa elimu hiyo kwa wanajamii, alifikisha idadi ya vikundi 16, alivyovianzisha na kuwafikia wanawake  zaidi ya 300.

Lengo lao ni kuwajengea uwezo akinamama, kuaminiana, kukopeshana na kuwagomboa kisiasa na kiuchumi, ambapo walifanikiwa kwa kiasi.

“Nilikuwa naelimisha wanawake wote bila kuchagua chama, niliwaambia kuwa, muhimu ni kwa wanawake kugombea uongozi, tuchangamkie fursa hii”, anaeleza.

Alianza uongozi kwenye Jumuiya, kisha kwenye jamii na sasa kwenye siasa, ambapo awamu iliyopita alipata nafasi ya Diwani wa kuchaguliwa na awamu hii pia amefanikiwa kushika nafasi hiyo.

Alijengewa uwezo ni TAMWA kupitia mradi wa WEZA na Action Aid na amepata mafanikio, na sasa ameingia jimboni kugombea nafasi za uongozi na amefanikiwa.

“Tunaziomba zijitokeze taasisi za kuwaandaa viongozi bora wanawake, na sio bora kiongozi, huku zijipange kumboresha kwani wana umuhimu mkubwa katika kuongoza”, anasema.

Anafafanua kuwa, kuna tofauti kubwa ya uongozi wa mwanamke na mwanaume, kutokana na wanawake kufanya kazi kwa uaminifu na kwa kujitolea.

Aliandaliwa na kuamua kujitolea, hakuogopa vikwazo vyovyote, ambavyo vinawakumba baadhi ya wanawake ambao wanagombea nafasi za uongozi.

“Kwa vile nimeamua, sikuogopa chochote na sikukubwa na kikwazo chochote, hapakuwa na changamoto ambayo ilinifanya niogope,”anaeleza.

Anawaelimisha wanawake wenzake kuhusu mambo mbali mbali ya kijamii, ikiwa ni pamoja na kuanzisha vikundi vya kuweka na kukopa, vya ujasiriamali na kuingia majimboni kusaka uongozi.

HARAKATI ZA KUGOMBEA UDIWANI

Khadija anasema, mwaka 2015 ndio mwaka alioingia wadini,  wa wadi ya Ole na kufanikiwa kuibuka mshindi.

“Baada ya kuona kwamba mwaka huo nilifanikiwa kuishika nafasi hiyo, ilipofika mwaka 2020, niligombea tena nafasi hiyo na nashukuru nimefanikiwa”, anaaeleza.

Anasema, anajua kwamba wananchi wameendelea kumchagua kutokana na mambo ya maendeleo aliyoyafanya katika awamu ya kwanza ya uongozi wake wa udiwani.

 

MAFANIKIO

Kuna mafanikio makubwa ikiwa wanawake watagombea nafasi za uongozi kwani ni wasikivu, wenye huruma na kujitolea, hivyo hufanya kazi kwa bidii.

Kabla hajapata nafasi ya udiwani, jamii ilikuwa haijui kwamba kuna mfuko wa mwakilishi na mbunge kwenye majimbo, lakini baada ya kupata nafasi hiyo aliwaeleza wananchi wake.

Anasema, fedha hizo wanaziona kutokana na kazi kubwa anayoifanya katika wadi yake, kwani anahakikisha changamoto zilizopo wanazitatua kupitia fedha hizo.

“Zinapoingia fedha za mfuko wa jimbo tunawaita wananchi wetu, tunawaambia kiasi cha fedha kilichopo, kisha wanaibua changamoto zinazowakabili”, anaeleza.

Baada ya kuibua changamoto hizo, wanazigawa fedha kwa wadi mbili na kutatua matatizo hayo, jambo ambalo lilikuwa halifanyiki kwa madiwani waliopita ambao walikuwa wanaume.

Anafanya maendeleo makubwa katika wadi yake kwa kushirikiana na Mbunge pamoja na Mwakilishi, ambapo tayari ameshajenga vyoo Mjiniole vyenye thamani ya shilingi milioni 26.



‘’Tumepeleka maji katika kijiji cha Makaani kupitia mfuko wa Mwakilishi wenye thamani ya shilingi milioni 12.8 huku akitumia milioni 57 kujenga mabanda ya skuli, chumba cha walimu na computer, kuezeka, kujaza kifusi barabara ya Mbuyuni na Shumindu’’, anaeleleza.

Alisambaza nguzo 12 za umeme kwenye vijiji tofauti pamoja na kupeleka maji katika kijiji cha Markaz Kianga, ambapo huduma ya maji alitumia kiasi cha shilingi milioni 7.

Anasimamia majukumu yake kuhakikisha haki zinapatikana, kwani fedha hizo ni kodi za wananchi.

Anafahamisha, yeye hawezi kufanya jambo kwa maslahi yake binafsi kama wengine waliopita, anajitolea kwa moyo wa imani katika kupeleka mbele gurudumu la maendeleo.

Khadija anaeleza kuwa, wananchi katika wadi yake wanampa mashirikiano makubwa kwa sababu tangu zamani alikuwa na sifa kubwa kutokana na kuwasaidia katika kutatua changamoto mbali mbali.

Mbali na nafasi ya udiwani aliyonayo pia ni mratibu wa wanawake na watoto wa shehia ya Mjiniole, hivyo alikuwa akiibua changamoto zinazowakumba wanawake na watoto na kuzisimamia mpaka wanapata haki zao.

“Tangu mwanzo nilijichanganya na wananchi na kuwasaidia katika kutetea haki zao za msingi na watuhumiwa kupata hatia, hivyo waliniamini na naendelea kuwasaidia”, anaeleza.

CHAGAMOTO ZINAZOWAKUMBA WANAWAKE KUGOMBEA

Mfumo dume ndio unaorejesha nyuma juhudi za wanawake wenye nia ya kugombea nafasi za uongozi ikiwa hawakujikaza, mwaminifu na kusimamia anachokiamini.

“Wengine wanakosa ujasiri, kutokuaminiwa kwenye vyama vyao na kuonekana mwanamme ndie anaeweza kuongoza, na hata akipatiwa nafasi na chama chake, atakuwa ni mtu wa kupangiwa tu na kufuata maelekezo wanayoyataka”, anafafanua.

Lakini ni tofauti na kiongozi yeye ambae alijiandaa, kujiamini na kuwa na uthubutu katika kuwasimamia wanawake wenzake na wananchi kwa ujumla.

Diwani huyo anasema, ikiwa wanawake wataendelea kubaki nyuma katika kugombea nafasi za uongozi, watashindwa kusimamia maamuzi yao huku wakiendelea kuwa tegemezi.

“Umasikini utatutawala na wanaume watazidi kutumiliki na kutufanyia mambo yasiyostahiki, tuungane mkono pamoja, tusaidiane na lazima tusimamie hili”, anaeleza.

NINI KIFANYIKE

Khadija anawataka wanawake wenzake kufanya kazi kwa bidii, kujitambua na kuwaunga mkono wale ambao wamebahatika kuingia katika nafasi za uongozi.

“Tusidharauliane, tupendane, mpe nguvu mwanamke mwenzako ambazo zitamsaidia katika utendaji wa kazi zake na wanaopata nafasi za uongozi, wasidharau wanawake wenzao tuwasaidie, tuwapende na tuwasikilize”, anafahamisha.

HISTORIA YA KHADIJA

Ameolewa mwaka 1984 na amefanikiwa kupata watoto nane (8), wanawake watatu (3) na wanaume watano (5) na kupata elimu yake ya msingi katika skuli ya Kizimbani Wete hadi kidato cha pili.

Alipata elimu yake ya kidato cha tatu katika skuli ya Sekondari Utaani Wete na baada ya kumaliza hakuendelea na masomo ya elimu ya juu na hatimae kuolewa.

“Kwa vile nilipata mafunzo mazuri kwetu sikujipweteka, nilipoolewa tu nilianza harakati za huku na kule na nilijiunga katika Jumuiya ya Wanawake Mkoa wa Kaskazini Pemba”, anafafanua.

Khadija pia alikuwa kiongozi kwa kada mbali mbali katika jamii ikiwa ni pamoja na katika vikundi vya ushirika na mratibu wa wanawake na watoto shehia ya Mjiniole.

Mume wa Khadija, Mustafa Khamis Bakar anasema mke wake amekuwa mpambanaji kwa wanawake wenzake na watoto kuhakikisha wanapata haki zao.

‘’Nampa mashirikiano makubwa mke wangu kwa sababu anachokifanya ni kizuri sana kwa maslahi ya jamii na Taifa, amekuwa maarufu na ndipo akafanikiwa kupata nafasi ya udiwani’’, anaeleza.

Anaeleza kwa, mke wake anajiamini na hakuwahi kukatishwa tamaa na maneno ya watu na aliendelea kupambana kila hatua kuhakikisha jamii yake inakuwa salama.

Awena Salim Kombo ambae ni mratibu wa Wanawake na watoto shehia ya Kangagani anamfahamu Khadija kwamba ni mwanamke mpambanaji ambae anafanya kazi ya kujitolea kwa jamii yake.

Khadija anafanya kazi ambazo madiwani waliotangulia hawakuzifanya, kwani amekuwa akiwaita wananchi na kuibua changamoto zinazowakabili katika jamii yao na zinapoingizwa fedha za mfuko wa jimbo huzitumia kutatulia changamoto hizo.

“Madiwani waliopita kwa kweli ilikuwa hawafanyi mambo ya kimaendeleo, lakini Khadija kama ameizindua jamii yake, kwa sababu anafanya kazi kubwa kuhakikisha wananchi wanapata huduma stahiki”, anaeleza.

Fatma Ali mkaazi wa shehia hiyo anamkumbuka diwani huyo kuwa ni mwanamke ambae anaisaidia jamii yake kwa hali na mali na ndio maana wananchi wapo karibu na yeye.

“Namkumbuka tangu alipokuwa akielimisha wananchi kuhusiana na mambo ya ujasiriamali, kuelimilisha mambo ya udhalilishaji na ukatili wa kijinsia, hivyo juhudi zake anazitumia na saivi alipopata nafasi ya udiwani”, anasema.

Mratibu wa TAMWA Pemba Fat-hiya Mussa Said anasema, juhudi zao za kuelimisha wanawake kugombea nafasi za uongozi zimeanza kuzaa matunda kwani, mwaka 2020 walijitokeza wengi majimboni mwao kuchukua fomu.

Anawataka wanawake kufuata mfumo wa Khadija katika kuiletea maendeleo jamii yake, ili wazidi kuaminika na kupewa uongozi, jambo ambalo litawafanya wawepo wengi kwenye vyombo vya kutoa maamuzi.

              MWISHO.

 

 

 

 

Comments

BLOG'S VISITORS

DAKTARI MWENGINE CHAKE CHAKE KULA SIKUKUU POLISI, NI KWA TUHUMA ZA KUMBAKA MGONJWA WAKE

NA WAANDISHI WETU, PEMBA::: DAKTARI anaetoa huduma kwa wagonjwa kituo cha afya cha serikali cha  Gombani wilaya ya Chake Chake Pemba, Is-haka Rashid Hadid, anaendelea kushikiliwa na Jeshi la Polisi Mkoa wa kaskazini Pemba, akituhumiwa kumtorosha na kisha kumbaka mtoto wa mwenye umri wa miaka 16, mkaazi wa Gombani. Daktari huyo miaka 35 ni mkaazi wa Kangagani Wilaya ya Wete mkoani humo, ambapo anadaiwa alimchukua mtoto huyo kutoka kwa rafiki yake, na kumpeleka kwenye nyumba anayoishi eneo la Kangagani. Mtoto aliefanyiwa kitendo hicho alisema kuwa, April 21 mwaka huu alikwenda kituo cha afya Gombani, kwa ajili ya matibabu na baada ya kupatiwa huduma na daktari huyo, alimuomba nambari yake ya simu. Alisema ilipofika usiku, walikuwa wanawasiliana kupitia ujumbe mfupi (sms) kwa lengo la kwenda kuchukua dawa nyingine ambazo kwa mchana huo alizikosa hospitalini hapo. "Nilikwenda hospitali kutibiwa, baada ya kufanya mapele katika sehemu zangu za siri, lakini akaniambia mpaka aje da

'MKAPA' NA WENZAKE PEMBA WALAZWA RUMANDE

  NA HAJI NASSOR, PEMBA@@@@ MAHKAMA kuu Zanzibar kisiwani Pemba, chini ya Jaji Ibrahim Mzee Ibrahim, imewapeleka rumande watumuhimwa wanne wanaokabiliwa na tuhuma za kuua kwa makusudi, akiwemo Ali Mussa Omar ‘ Mkapa’ mkaazi wa Wawi wilaya ya Chake chake Pemba. Watuhumiwa wengine walioanza maisha mapya ya rumande ni mtuhumiwa Yassir Mohamed Juma miaka 23, Anuwari Mussa Omar miaka 30 pamoja na mtuhumiwa Yassir Mussa Omar ‘ Makababu ’ miaka 29, wote wakaazi wa shehia ya Wawi, wilaya ya Chake chake Pemba. Awali watuhumiwa hao waliwasili mahakamani hapo, kwa mara ya kwanza, kwa ajili ya kusomewa tuhma zinazowakabili za kumuua kwa maksudi Said Seif Kombo. Ilidaiwa mahakamani hapo na Mwendesha Mashtaka kutoka Ofisi ya Mkurugenzi wa Mashataka Seif Mohamed Khamis akiambatana na mwenzake Mussa Khamis Ali kuwa, watuhumiwa hao kwa pamoja wanadaia kufanya mauwaji hayo kwa maksudi. Ilidai kuwa, watuhumiwa wote kwa pamoja, walitenda kosa hilo Oktoba 16, mwaka huu, baina ya saa 7:00 mchan

HII KALI MBUNGE ASIYA AMKOGESHA MWANANCHI HADHARANI KISA HICHI HAPA......

  NA HAJI NASSOR, PEMBA MBUNGE wa viti maalum nafasi za wanawake mkoa wa kaskazini Pemba Asiya Sharif Omar, amewataka wananchi wa kijiji cha taifu, shehia ya Kinyasini jimbo la Gando wilaya ya Wete Pemba, kuyalinda miundombinu ya maji safi na salama, ili yawe endelevu kwao. Kauli hiyo ameitoa wakati alipokuwa akizungumza na mwandishi wa habari hizi, mara baada ya kuwasili kijijini humo, na kumkogesha mwananchi mmoja kama ishara ya uzinduzi wa mradi wa maji safi na salama, ulioasisiwa na mbunge wa Jimbo la Gando. Alisema, hawana mbadala kwa sasa bali ni kuilinda miundombinu ya huduma hiyo, hasa baada ya mbunge wa wao Salim Mussa Omar, kuwarejeshea huduma hiyo. Alieleza kuwa, inafahamika kuwa kwa miaka 14 waliikosa huduma hiyo hasa kwa vile viongozi waliokuwepo hawakujali kuwatatulia tatizo hilo, hadi juzi ilipofanywa na mbunge wao. “Baada ya huduma hii sasa kurejeshwa na mbunge wa jimbo la Gando, kazi iliyobakia kwenu wananchi ni kila mmoja kuwa mlinzi wa miundombinu hii,’’ali

TUHMA ZA DAKTARI PEMBA KUCHIWA HURU: POLISI KASKAZINI KUTOA TAARIFA RASMI LEO

  NA HAJI NASSOR, PEMBA KAMANDA wa Polisi mkoa wa kaskazini Pemba, Juma Saad Khamis, amesema leo Mei 9, mwaka huu atatoa taarifa rasmi, juu ya kuendelea kumshikilia au kumpa dhamana ya Polisi, daktari wa Kituo cha Afya Gombani Is-haka Rashid Hadid, anayetuhumiwa kwa ubakaji. Alisema, kwa vile alikuwa katika mapumziko mafupi, haelewi jambo lolote linaloendelea kwa mtuhumiwa huyo, juu ya kuendelea kushikiliwa kwake kituoni hapo. Alieleza kuwa, leo Mei 6 (jana), hajapata taarifa za ndani za mtuhumiwa, huyo na kuwataka wananchi na wanaharakati, wasubirie hadi Jumatatu ijayo. Akizungumza na waandishi wa habari kwa nyakati tofauti Kamanda huyo, alisema hana taarifa zozote za kupewa dhamana mtuhumiwa ndani ya kituo chake cha Polisi au kuendelea kuwepo. ‘’Ilikuwa mimi sipo kazini kwa muda, kuanzia anakamatwa hadi anafikishwa Polisi, kwa sasa siwezi kueleza jambo lolote kwa mtuhumiwa huyo, hadi Jumatatu,’’alieleza. Aidha Kamanda huyo alieleza kuwa, kwa sasa hawezi kutoa ufafan

MADAKTARI KUTOKA CHINA WAOKOA MAISHA YA MTOTO PEMBA

  HABIBA ZARALI, PEMBA TIMU ya 32 ya madaktari wa kichina katika hospitali ya Abdalla Mzee Mkoani wamefanikiwa kufanya upasuaji mkubwa wa mtoto mwenye umri wa miaka 15 mkaazi wa Chole Kengeja, baada ya kuchomwa na jiti sehemu ya njia zake za mfumo wa uzazi. Mtoto huyo ambae alianguka hivi karibuni katika mti na baadae kuchomwa na jiti hilo na kumsababishia kutokwa na damu nyingi katika sehemu ya nyonga, alifanyiwa upasuaji uliodumu kwa muda wa saa tatu na   kuokolewa maisha yake. Akizungumza mara baada ya operesheni huo kiongozi wa timu hiyo Dr Jiang Jinhua, alisema mara baada ya mtoto huyo kufikishwa hospitalini hapo na kufanyiwa vipimo na kuonekana   ilibidi apatiwe rufaa ya kwenda katika hospitali nzuri yenye kutibu tatizo lake huko nchini Kuwado ambapo haikuwezekana kutokana na hali ya umaskini wa f amilia ya mtoto huyo . Alisema timu ya madaktari hao itaendelea kutowa huduma za matibabu   kwa wananchi kisiwani humo,   ili kuwaondolea gharama ya kutafuta matibabu nje ya nch