Skip to main content

WATAALAMU WA SHERIA WAIPA KAZI IDARA YA KATIBA NA MSAADA WA KISHERIA

 

           


 
                  

NA HAJI NASSOR, PEMBA

WATAALAMU wa sheria Zanzibar, wameitaka Idara ya Katiba na Msaada wa sheria Zanzibar, kuongeza jitihada za elimu ili kusaidia kubadili mawazo, mitazamo na uwelewa wa watu maskini, ili kuongeza matumizi ya huduma za msaada wa kisheria.

 Walisema, Idara inapaswa kuweka kipaumbele cha pekee cha kutoa mafunzo hayo, ili kuona walengwa wa mfumo wa kutoa elimu, ushauri na msaada wa kisheria ambao ni watu maskini wanafaidika nao.

Kwa mujibu wa tafsiri ya ripoti ya tathmini ya awali ya hali halisi ya msaada wa kisheria Zanzibar ya mwaka 2020, iliyotolewa na wizara ya Katiba na sheria, walisema azma ya uwepo wa msaada wa kisheria ni kwa watu wasio na uwezo.

Wataalamu hao kwenye ripoti hiyo walisema, suala la utoaji wa msaada wa kisheria linazingatiwa kuwa ni miongoni mwa viashiria vya msingi ya upatikanaji haki.

Walieleza kuwa, taifa lolote lile duniani haliwezi kufurahia uwepo wa baadhi ya haki za binadamu bila ya kunawiri mfumo wa utoaji wa msaada wa kisheria.

Aliyekuwa Jaji Mkuu wa Zanzibar Omar Othman Makungu, kwenye ripoti hiyo alisema wasaidizi wa sheria na watoa msaada wa sheria wanafanyakazi kubwa ya kuisaidia jamii kuwapa ufahamu wa sheria.

Wakili wa serikali Mwandamizi Afisi ya Mkurugenzi wa Mashataka Ali Rajab, alisema bado watoa msaada wa kisheria hawajawafikia ipasavyo watu katika maeneo hasa ya vijijini, ambao wengi wao hawana uwezo wa kulipia gharama za mawakili.

“Jengine ambalo ni kasoro inaonekana watoa msaada wa kisheria wengi wao ni waajiriwa wa serikalini au sekta binafsi, hivyo hawana muda mwafaka wa kutoa huduma,’’alieleza.




Rais mstaafu wa chama cha mawakili Zanzibar Omar Said Shaaban, alisema sasa mawakili hawana tena mtazamo mbaya kwa watoa msaada wa kisheria, kama ilivyokuwa hapo mwanzo.

Wakili wa mahakama kuu Pemba Khalfan Amour Mohamed, alisema wananchi walio wengi waliopo Pemba, hawajafurahia utoaji wa huduma za msaada wa kisheria kutokana na jiografia ya kisiwa chenyewe.

Aidha Mkurugenzi wa Jumuiya ya wanasheria wanawake Zanzibar ‘ZAFELA’ Jamila Mahamoud, alisema wasaidizi wa sheria hawana muda wa kutosha wa kuwahudumia watu katika maeneo yao.

“ZAFELA imegundua kuwa, wasaidi wa sheria waliopata mafunzo na ZLSC hawakai katika maeneo ambayo walipojisajili wakati wanaomba mafunzo hayo,’’alifafanua.

Katika ripoti hiyo, wataalamu hao wa sheria walipendekeza kuwa, wakati umefika sasa kuongeza ufahamu wa watoaji wa masaada wa kisheria ili kutambuliwa rasmi.

Hata hivyo walipendekeza kuwa, ni vyema watoa msaada wa kisheria kushirikiana kwa karibu na mawakili katika ofisi zao, ili kutoa huduma za kujitolea kwa ufanisi zaidi.

Akizungumza hivi karibuni Mkurugenzi wa Idara ya Katiba na msaada wa kisheria Zanzibar, Hanifa Ramadhn Said, alisema licha ya uchanga wa idara, wameshafanya makubwa, ikiwa ni pamoja na elimu kwa jamii.

“Hivi sasa karibu kila shehia tumeshaifikia, nab ado tunaendelea kukutana na jamii, ili kuwapa elimu na ushauri wa kisheria tena bila ya malipo,’’alieleza.

Ripoti hiyo ya tathmini ya awali ya hali halisi ya msaada wa kisheria Zanzibar, inaangalia taarifa za awali kuhusiana na historia, hadhi, asili ya shughuli za masaada wa kisheria hapa Zanzibar.

Ambapo ripoti hiyo, itasaidia kubainisha mambo yatakayoimarisha huduma za utoaji msaada wa kisheria pamoja na kupendekeza mfumo mzuri, utakaopelekea kupatika kwa urahisi kwa watu wote.

                      Mwisho

 

 

 

 

Comments