Skip to main content

NDOA KUVUNJIKA, JANGA LA UDHALILISHAJI KWANINI YAWAELEMEE WANAWAKE PEKEE?

 




NA HANIFA SALIM, PEMBA@@@@

UTELEKEZWAJI wa familia ni ukatili wa kijinsia, hali hii husababisha chuki, maradhi, udhalilisha na watoto kukosa haki zao za msingi.

Jukumu la malezi ni la wazazi wote wawili, kupanga matumizi ya rasilimali za familia na mahitaji ya watoto ni jambo la kupewa kipaumbele.

Katika jamii ya sasa, wanawake waliowengi tumeona wakiachwa na waume zao pamoja na watoto, jambo ambalo huleta athari, watoto kukosa haki zao wakati mwengine hata kufanyiwa matendo yasiofaa.

Kutokana na kukosa huko huduma, kutoka kwa familia zao ndipo wanapodhalilishwa kwa kushawishiwa, kupatiwa jambo dogo ambalo alilikosa na alistahiki kupatiwa na familia yake.

ATHARI ZINAZOIKUMBA FAMILIA ILIYOTELEKEZWA

Zipo athari nyingi ambazo huikumba familia ambayo imetelekezwa ikiwemo mama kubeba mzigo mkubwa wa majukumu wa kuwatafutia watoto huduma muhimu kama vile chakula, matibabu, elimu na mengineyo.

Watoto kukosa watu wa kuwadhibiti ambapo huweza kutumbukia katika majanga mbali mbali ikiwemo ubakaji, madawa ya kulevya, ulawiti, uchokoraa na ajira za watoto.

Watoto wengi wanaoacha skuli asilimia kubwa wameonekana kutoka katika familia ambazo zimetelekezwa, mama kukosa nguvu kazi ni sababu ambayo pia inatokana na utelekezwaji wa familia.

Changamoto ni nyingi ambazo humfika mwanamke anapotelekezwa na watoto, wakati mwengine watoto hupatwa maradhi, hukimbia kwenda skuli na madrasa jambo ambalo ni haki yao ya msingi.

WAHANGA WENYEWE

Akizungumza na mwandishi wa Makala, hii mmoja miongoni mwa wahanga wa janga hilo la utelekezwaji mkaazi wa shehia ya Chonga anasema, ni miaka mitano sasa tangu kuachwa na mume wake wa ndoa.

“Mume amenikimbia huu ni mwaka wa tano, nimezunguka katika taasisi zote za sheria kutafuta haki, lakini sina ambacho nimefanikiwa, nimeachwa na watoto wawili wakiume mmoja akiwa ni mlemavu,” anasema.

Anasema, alikwenda kituo cha huduma za sheria, wanawake na watoto, bila ya kupata mafanikio yoyote, hadi alikata tamaa huku mtoto wake mmoja kupoteza maisha.

“Yule mgonjwa ambae ni mlemavu wa akili alinitoka ghafla, mimi mwenyewe nahangaika huku naumwa, ili tupate riski nile na watoto baba yao kanitelekeza muda mrefu”, anaeleza.  

Alipambana kwa juhudi kubwa kufika hadi dawati, wanawake na watoto hakuna ambalo lilifanyika, wala kupata haki yake ambayo aliitegemea.

“Nende wapi nikatafute haki baada ya kumaliza sehemu hizo, ambazo nilikwenda bila ya kupata mafanikio yoyote, na hawa ndio daraja la kufika pale ambapo haki yangu ipo”, anasema.

Anasema vituo vya sheria bado havijawa tayari kuisaidia jamii katika masuala ya utoaji wa huduma, kwani kupitia madhila ambayo aliyapata katika maisha yake, alibaini jambo hilo.

Baada ya kufuatiliwa na kituo cha huduma za sheria, aliambiwa mwanamme ambae ni baba wa watoto wake, yuko kisiwani Unguja.

“Kwani Unguja ni Dubei au kuna umbali gani wakusema sheria haziwezi kumkamata, kama kafanya kosa kubwa la uhujumu uchumi asingetiwa hatiani?, lakini kwa vile ni mimi walishindwa kumpata”, anauliza.

Anasema, aliendelea kudumaa na kukosa haki zake kwa mwanamme ambae aliishi nae kwa muda wa miaka 40, tangu afunge nae ndoa.

Kazi zote za kiume alilazimika kuzifanya ili tu ahifadhi maisha ya ndoa yake pamoja na watoto wake ambao walikua ni walemavu lakini juhudi za kupambania familia yake zilikwisha.



“Samaki niliuza mimi, nazi, Mombasa nilikwenda mimi kufanya biashara, gari ya Ng’ombe nimeendesha, kuni nimekata, nikiendesha gari la ng’ombe huwezi kuamini, niletee Ng’ombe wowote hata awe mkali hatonishinda”, anaeleza.

Yote hayo ambayo yalimkuta alifunzwa na mwanamme huyo ambae alimtelekeza, alijitahidi kwa uwezo wake wote kuhakikisha analinda ndoa yake, lakini hakupata ndoa wala haki yake ambayo aliipigania kwa muda mrefu.

Alizishauri taasisi za sheria kuzisemea haki za wanawake kwa mdomo na vitendo pamoja na kuziangalia kwa kina kwani wanawake waliowengi katika jamii wanaathirika kwa kuachwa na watoto.

Mama mwengine ambae alitelekezwa mkaazi wa shehia ya Msuka Magharibi anasema, aliachwa na mume wake akiwa na watoto wanne wakike.

“Mwanzo alikua anatupatia huduma baada ya kuniacha kindoa lakini sasa hivi ni karibu mwezi wa tisa hatuulizi hata hali zetu, ni mimi mwenyewe ambae napambana na watoto”, anasema.

Alibadilika ikawa watoto hawashuhulikii kwa lolote, apambana na watoto wake kwa kuwatafutia riski kwa kupitia shughuli zake za kilimo ambacho kinamsaidia katika maisha yake.

“Kama si kilimo na kwenda kutafuta nazi nikafanya mafuta nikauza nikapata pesa ya chakula basi tunalala njaa, tunaathirika sana na haya maisha wanawake majukumu ambayo tunaishi na watoto wetu ni magumu mno”, anasema.

WANASHERIA WANASEMAJE

Wakili kutoka chama cha wanasheria Pemba Asha Suleiman Said anasema, mambo yanayopelekea kuongezeka masuala ya utelekezwaji wa wanawake na watoto kwa mujibu wa utafiti uliofanywa na chama chao ni jamii kukosa elimu ya sheria.

Wanawake kuwa na muhali, kwa kuhofia kuwapoteza ndoa zao pale ambapo wanaonesha dalili za manyanyaso na udhalilishaji ambao wanaufanya kwao, kutoyaripoti masuala hayo katika vyombo vya sheria.

Anasema, suala hilo linapotokea wanaoathirika zaidi ni watoto kwani watoto wengi hufanyiwa udhalilishaji kutokana na kukosa malezi na uwangalizi wa wazazi wao.

“Mwanamme anapokuacha akawa hakuhudumikii huo ni utelekezaji linapotokezea suala hili tunachotakiwa wanawake tusikae kimya tuyaripoti katika vyombo vya sheria ikiwemo Idara ya ustawi wa jamii ili kupata haki zetu”,anasema.

OFISI YA WILAYA

Mkuu wa Wilaya ya Micheweni Mgeni Khatib Yahya anasema, kesi za utelekezwaji wa akina mama na watoto ni nyingi sana ambapo kesi hizo zimeonekana kujitokeza zaidi katika maeneo ya ukanda wa pwani.

“Serikali ya Wilaya ndio ambayo inabeba mizigo maana wanatujia akina mama kutwambia leo ya nne hajakula na watoto anakuja kutafuta chakula kwetu, tunachokifanya ni kutafuta mawasiliano ili waweze kutoa huduma”, anasema.

Wanaume walio wengi wameonekana kuwakimbia wake zao pamoja na watoto na kwenda nje ya kisiwa cha Pemba kama vile Tanga, Mombasa, Unguja na Kenya kujenga familia mpya.

“Jamii ya makaazi ya ukanda wa pwani ni wavuvi wanapokwenda ago miezi minne au mitano huziacha familia zao bila ya huruma, na wengine huwaacha kabisa”, anasema.



Anasema jambo hilo linawapa hali ngumu akina mama, kwani hulazimika kutafuta riski ili watoto wao waweze kuishi, hivyo wilaya imechukua hatua za kutoa elimu kwa wanaume wa kila shehia ili kupunguza matendo hayo.  

USTAWI WA JAMII

Mkuu wa Idara ya maendeleo ya jamii jinsia na watoto Pemba Mwanaisha Ali Massoud anasema, mwezi Julai 2021 hadi Juni 2022 wamepokea malalamiko ya kesi 126, kati ya malalamiko hayo 71 walalamikaji wamepata haki zao.

“Wanapokuja walalamikaji tunawasikiliza kwa kina halafu tukawapa ushauri ili kuona wanashirikiana wazazi wa pande mbili katika malezi ya watoto wao”, anasema.

Kupitia makala hii anaishauri jamii kuwa na subira katika uwendeshaji mzima wa familia zao, kuzitumia familia zao kuweza kupata suluhu juu ya matatizo walionayo.

Wazazi wanapofanya migogoro ndani ya familia zao watambue ndio kizingiti kikubwa cha familia kukosa maendeleo ya haraka hivyo, lazima wanandoa wawe makini huku wakitambua kwamba waathirika wakubwa ni wanawake na watoto.

TAMWA

Mratibu wa Chama cha waandishi wa habari wanawake Tanzania (TAMWA) Pemba Fat-hiya Mussa Said anasema, wamekua wakiwasaidia wanawake ambao wametelekezwa kwa kuwapa ushauri wa kupeleka malalamiko yao Idara ya ustawi wa jamii.

“Tunawaunganisha na Idara ya ustawi wa jamii, mahakama ya kadhi ili waweze kupata haki zao, mwaka jana hatukua na kesi utelekezwaji kwani sisi zaidi tunashuhulikia kesi za udhalilishaji wa kingono”, anasema.

Anasema, mwaka 2021 walipokea kesi 61 kwa Wilaya ya Wete, 48 Mkoani, huku akiwataka akina baba kufahamu kwamba familia hulelewa katika pande mbili hivyo aliwanasihi wawe na subra pamoja na kuwapatia huduma watoto wao licha ya kuwa ndoa imeshavunjika.

WANANCHI WANASEMAJE?

Fatma Hamad Khamis mkaazi wa Gombani anasema, wanaume wamekosa huruma na mapenzi kwa wanawake na watoto wao kwani majukumu yote ya familia huwaachia na kuona kwamba ni adabu ambayo humpa mwanamke baada ya kuachana.

‘’Wanaume wanapokutaka watakufuata kwa mahaba, lakini kinyume chake hutokezea ambapo kutatokea mfarakano wa ndoa yao, wanatuacha na watoto bila ya kuelewa kwamba watoto wanahitaji huduma kutoka kwa baba’’, anasema.

Abdalla Mohamed Ramadhan mkaazi wa machomane, anasema wapo wanaume ambao wamekosa uwelewa wa kutambua majukumu yao pale ambapo wameachana.

‘’Mwanamke uapomuacha na watoto unamuachia mzigo mkubwa ambao yeye hatoweza kuumudu, nawashauri wanaume wenzangu wajenge utamaduni wa kuwapatia huduma watoto hata pale wanapotengana’’, anasema.

Salama Kassim Haji mkaazi wa Mwambe anasema, familia inapotelekezwa kinachotokezea ni kuwaathiri watoto kufanyiwa udhalilishawaji na watu wabaya kutokana na kukosa huduma stahiki ambazo walizikosa.

NINI KIFANYIKE?

Ni vyema jamii kuzitumia familia zao kuleta suluhu katika kutatua matatizo yao ili kuepusha uvunjifu wa ndoa na kuongezekeza idadi kubwa ya malalamiko ya kesi za utekelezwaji wa wanawake na watoto ndani ya jamii.

 

Kwani jamii ya sasa imeonekana kutokuzitumia familia zao kutatua changamoto kama ilivokua zamani jambo ambalo linachangia kwa kiasi kikubwa uvunjifu wa ndoa.

 


Vile vile kuwa na subra katika uendeshaji wa familia, wazazi watambue wanapofanya migogoro ndani ya familia kutakuwa na kizingiti cha kutokupata maendeleo ya haraka.

 

SERIKALI KUU

Akisoma hutuba ya mwaka wa fedha 2022/2023 ukumbi wa Baraza la Wawakilishi, Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Riziki Pembe Juma, alisema kwa mwaka huo walipokea malalamiko 373 ya ukiukwaji wa haki za watoto na kuyafanyia kazi.

 

Kati ya hayo, yaliyopokelewa Unguja yalikuwa 151 na Pemba 222, ambapo yanayohusu matunzo ya huduma yalikuwa ni 211 Unguja 79 na Pemba 132, na 162 ya mvutano wa malezi wakati kwa Unguja yalikuwa 72 na Pemba 90.

 

Malalamiko 167 yalipatiwa ufumbuzi na malalamiko 25 yalitolewa rufaa kwenda mahakamani, wahusika 100 walikubaliana kifamilia na 81 wanaendelea na hatua.

 

 

                                       MWISHO.

 

 

 

 

 

 

Comments

BLOG'S VISITORS

DAKTARI MWENGINE CHAKE CHAKE KULA SIKUKUU POLISI, NI KWA TUHUMA ZA KUMBAKA MGONJWA WAKE

NA WAANDISHI WETU, PEMBA::: DAKTARI anaetoa huduma kwa wagonjwa kituo cha afya cha serikali cha  Gombani wilaya ya Chake Chake Pemba, Is-haka Rashid Hadid, anaendelea kushikiliwa na Jeshi la Polisi Mkoa wa kaskazini Pemba, akituhumiwa kumtorosha na kisha kumbaka mtoto wa mwenye umri wa miaka 16, mkaazi wa Gombani. Daktari huyo miaka 35 ni mkaazi wa Kangagani Wilaya ya Wete mkoani humo, ambapo anadaiwa alimchukua mtoto huyo kutoka kwa rafiki yake, na kumpeleka kwenye nyumba anayoishi eneo la Kangagani. Mtoto aliefanyiwa kitendo hicho alisema kuwa, April 21 mwaka huu alikwenda kituo cha afya Gombani, kwa ajili ya matibabu na baada ya kupatiwa huduma na daktari huyo, alimuomba nambari yake ya simu. Alisema ilipofika usiku, walikuwa wanawasiliana kupitia ujumbe mfupi (sms) kwa lengo la kwenda kuchukua dawa nyingine ambazo kwa mchana huo alizikosa hospitalini hapo. "Nilikwenda hospitali kutibiwa, baada ya kufanya mapele katika sehemu zangu za siri, lakini akaniambia mpaka aje da

'MKAPA' NA WENZAKE PEMBA WALAZWA RUMANDE

  NA HAJI NASSOR, PEMBA@@@@ MAHKAMA kuu Zanzibar kisiwani Pemba, chini ya Jaji Ibrahim Mzee Ibrahim, imewapeleka rumande watumuhimwa wanne wanaokabiliwa na tuhuma za kuua kwa makusudi, akiwemo Ali Mussa Omar ‘ Mkapa’ mkaazi wa Wawi wilaya ya Chake chake Pemba. Watuhumiwa wengine walioanza maisha mapya ya rumande ni mtuhumiwa Yassir Mohamed Juma miaka 23, Anuwari Mussa Omar miaka 30 pamoja na mtuhumiwa Yassir Mussa Omar ‘ Makababu ’ miaka 29, wote wakaazi wa shehia ya Wawi, wilaya ya Chake chake Pemba. Awali watuhumiwa hao waliwasili mahakamani hapo, kwa mara ya kwanza, kwa ajili ya kusomewa tuhma zinazowakabili za kumuua kwa maksudi Said Seif Kombo. Ilidaiwa mahakamani hapo na Mwendesha Mashtaka kutoka Ofisi ya Mkurugenzi wa Mashataka Seif Mohamed Khamis akiambatana na mwenzake Mussa Khamis Ali kuwa, watuhumiwa hao kwa pamoja wanadaia kufanya mauwaji hayo kwa maksudi. Ilidai kuwa, watuhumiwa wote kwa pamoja, walitenda kosa hilo Oktoba 16, mwaka huu, baina ya saa 7:00 mchan

HII KALI MBUNGE ASIYA AMKOGESHA MWANANCHI HADHARANI KISA HICHI HAPA......

  NA HAJI NASSOR, PEMBA MBUNGE wa viti maalum nafasi za wanawake mkoa wa kaskazini Pemba Asiya Sharif Omar, amewataka wananchi wa kijiji cha taifu, shehia ya Kinyasini jimbo la Gando wilaya ya Wete Pemba, kuyalinda miundombinu ya maji safi na salama, ili yawe endelevu kwao. Kauli hiyo ameitoa wakati alipokuwa akizungumza na mwandishi wa habari hizi, mara baada ya kuwasili kijijini humo, na kumkogesha mwananchi mmoja kama ishara ya uzinduzi wa mradi wa maji safi na salama, ulioasisiwa na mbunge wa Jimbo la Gando. Alisema, hawana mbadala kwa sasa bali ni kuilinda miundombinu ya huduma hiyo, hasa baada ya mbunge wa wao Salim Mussa Omar, kuwarejeshea huduma hiyo. Alieleza kuwa, inafahamika kuwa kwa miaka 14 waliikosa huduma hiyo hasa kwa vile viongozi waliokuwepo hawakujali kuwatatulia tatizo hilo, hadi juzi ilipofanywa na mbunge wao. “Baada ya huduma hii sasa kurejeshwa na mbunge wa jimbo la Gando, kazi iliyobakia kwenu wananchi ni kila mmoja kuwa mlinzi wa miundombinu hii,’’ali

TUHMA ZA DAKTARI PEMBA KUCHIWA HURU: POLISI KASKAZINI KUTOA TAARIFA RASMI LEO

  NA HAJI NASSOR, PEMBA KAMANDA wa Polisi mkoa wa kaskazini Pemba, Juma Saad Khamis, amesema leo Mei 9, mwaka huu atatoa taarifa rasmi, juu ya kuendelea kumshikilia au kumpa dhamana ya Polisi, daktari wa Kituo cha Afya Gombani Is-haka Rashid Hadid, anayetuhumiwa kwa ubakaji. Alisema, kwa vile alikuwa katika mapumziko mafupi, haelewi jambo lolote linaloendelea kwa mtuhumiwa huyo, juu ya kuendelea kushikiliwa kwake kituoni hapo. Alieleza kuwa, leo Mei 6 (jana), hajapata taarifa za ndani za mtuhumiwa, huyo na kuwataka wananchi na wanaharakati, wasubirie hadi Jumatatu ijayo. Akizungumza na waandishi wa habari kwa nyakati tofauti Kamanda huyo, alisema hana taarifa zozote za kupewa dhamana mtuhumiwa ndani ya kituo chake cha Polisi au kuendelea kuwepo. ‘’Ilikuwa mimi sipo kazini kwa muda, kuanzia anakamatwa hadi anafikishwa Polisi, kwa sasa siwezi kueleza jambo lolote kwa mtuhumiwa huyo, hadi Jumatatu,’’alieleza. Aidha Kamanda huyo alieleza kuwa, kwa sasa hawezi kutoa ufafan

MADAKTARI KUTOKA CHINA WAOKOA MAISHA YA MTOTO PEMBA

  HABIBA ZARALI, PEMBA TIMU ya 32 ya madaktari wa kichina katika hospitali ya Abdalla Mzee Mkoani wamefanikiwa kufanya upasuaji mkubwa wa mtoto mwenye umri wa miaka 15 mkaazi wa Chole Kengeja, baada ya kuchomwa na jiti sehemu ya njia zake za mfumo wa uzazi. Mtoto huyo ambae alianguka hivi karibuni katika mti na baadae kuchomwa na jiti hilo na kumsababishia kutokwa na damu nyingi katika sehemu ya nyonga, alifanyiwa upasuaji uliodumu kwa muda wa saa tatu na   kuokolewa maisha yake. Akizungumza mara baada ya operesheni huo kiongozi wa timu hiyo Dr Jiang Jinhua, alisema mara baada ya mtoto huyo kufikishwa hospitalini hapo na kufanyiwa vipimo na kuonekana   ilibidi apatiwe rufaa ya kwenda katika hospitali nzuri yenye kutibu tatizo lake huko nchini Kuwado ambapo haikuwezekana kutokana na hali ya umaskini wa f amilia ya mtoto huyo . Alisema timu ya madaktari hao itaendelea kutowa huduma za matibabu   kwa wananchi kisiwani humo,   ili kuwaondolea gharama ya kutafuta matibabu nje ya nch