Skip to main content

SMZ yakumbushwa kuzifanyia marekebisho Sheria zinazominya uhuru wa habari Zanzibar


NA NAFDA HINDI, ZANZIBAR

Mkurugenzi wa Chama cha waandishi wa habari wanawake Tanzania Znz Dk Mzuri Issa amesema kuwepo kwa uhuru wa habari na kujieleza ni haki ya msingi ya binadamu ambayo itachochea kuleta maendeleo.

Dk Mzuri ameyasema hayo wakati akifunguwa mkutano wa uchambuzi wa sheria zinazokwaza uhuru wa habari Zanzibar uliowashirikisha wadau wa masuala ya habari na waandishi wahabari uliofanyika katika Ofisi za Tamwa Tunguu, Wilaya ya Kati, Mkoa wa Kusini Unguja.

Amesema suala la kupata habari kwa Zanzibar limeanzia tokea enzi za karne zilizopita, kinachorudisha nyuma kwa sasa kutopata habari ni kuwepo sheria zisizo rafiki kwa waandishi wahabari na hata wananchi.

“Zanzibar ni kitovu cha Utamaduni wakupata habari, na hata waandishi wahabari wanawake walianzia Zanzibar enzi hizo,’’ Dk Mzuri Issa.

Akiwasilisha ripoti hiyo ya Uchambuzi wa sheria zinazokwaza uhuru wa habari Muhadhir kutoka Chuo Kikuu cha Zanzibar (ZU) Said Suleiman amesema kuna baadhi ya sheria zimepitwa na wakati hasa katika ulimwengu huu wa sayansi na teknolijia ipo haja ya kufanyiwa marekebisho kwa sababu zinakwamisha uhuru wa habari na kujieleza.

Akizitaja baadhi ya sheria hizo amesema ni  pamoja na Sheria ya Usajili wa habari, magazeti na vitabu no 5 (1988) iliofanyiwa marekebisho na sheria no 8 {1997), Sheria ya Tume ya  Utangazaji Zanzibar no 7 (1997) iliyorekebishwa na sheria no 1 (2010), Sheria ya Makosa ya Mtandao (2018), Sheria ya Adhabu (2004) no 6 iliyofanyiwa marekebisho na sheria (2018) na nyenginezo.

 Mapema Afisa Mradi wa Uhuru wa habari kutoka TAMWA,Zanzibar Zaina Mzee amesema kwa miaka mingi Sheria hii ya habari imekuwa kikwazo kwa waandishi wahabari na vyombo vya habari kwa ujumla kufanya kazi kwa ufanisi.

Nae Mjumbe wa bodi kutoka TAMWA,ZNZ Shifaa Said amesema wakati umefika sasa kwa waandishi wahabari kutumia vyema kalamu zao kuikumbusha Serikali  namna gani sheria zilizopo zinavyoathiri uhuru wa kupata habari.

“ Ni wakati sasa waandishi wahabari kutumia kalamu zenu kuonesha kwa namna ambavyo sheria zilizopo zinavyoathiri tasnia ya habari na zinahitaji kufanyiwa marekebisho kwa maslahi ya umma,” Shifaa Said.

Mwandishi mwandamizi kutoka Zanzibar Salim Said Salim amesema ni Utamaduni wa watu wa Zanzibar ulianzia enzi za kale kupenda kupokea habari kupitia njia tofauti hivyo ni vyema kuendelezwa kwa kuepuka vikwazo kupitia sheria za habari.

“Wazanzibar walipenda kupata habari kama njia moja ya mawasiliano kupitia njia tofauti, tukiwa kwenye usafiri wa majini (baharini) kulikuwa na mabomba ambayo yanatowa taarifa kwa abiria,” Salim Said.

Jabir Idrisa amesema Enzi za utawala wa Kisultan Zanzibar kulikuwa na magazeti Zaidi ya 50 ukilinganisha na hali iliopo sasa kuna gazeti moja pekee linalomilikiwa na Serikali hivyo marekebisho ya sheria yanahitajika ili kutoa nafasi kwa raia kumiliki magazeti binafsi.

 Mradi wa kuimarisha masuala ya uhuru wa habari wa miaka miwili wenye lengo la kuendeleza mapitio ya uhuru wa Sheria za habari (ARFEL), Unaofadhiliwa na Common Wealth Foundation.

 

   

 

Comments