Skip to main content

SHERIA YA TUME YA UTANGAAZAJI ILIVYOBEBA MANENO YENYE UKAKASI KWA UHURU WA HABARI ZANZIBAR

 



NA HAJI NASSOR, PEMBA:::

ZANZIBAR kama ilivyo eneo jingine lolote ulimwenguni, nayo inavyo vyombo vya habari, ambavyo maudhui yake ni sawa na vile vya mataifa mengine.

Nikukumbushe tu kuwa, kazi za msingi za vyombo vya habari ni kuelemisha, kuburudisha na kuhabarisha ingawa kwa pia ni kukosoa, kupongeza na kuhoji.

Kazi hii hasa ni haki ya kikatiba, katika mataifa mbali mbali, kwa mfano Zanzibar katiba yake ya mwaka 1984 kifungu cha 18 na ile ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya mwaka 1977, ibara 18 imeelezea haki hii.

Kama hivyo ndivyo, unaweza kushangaa kuwa suala la kutoa, kupata na kusambaaza habari ni haki ya kikatiba, sasa iweje kutungwe sheria yenye vifungu au maneno, yenye ukakasi kwa waandishi wa habari.

SHERIA YA TUME YA UTANGAAZAJI ZANZIBAR NO 7 YA MWAKA 1997

Sheria hii ambayo sasa inatimiza umri wa miaka 26, tokea pele ilipotiwa saini na Rais wa wakati huo wa Zanzibar Dk. Salmin Amour Juma, licha ya kufanyiwamarekebisho.

Kwa hakika, lengo kuu la sheria hii, ni kuongoza vyombo vya habari Zanzibar ikiwemo redio, televisheni na vile vyombo vya kisasa vyenye kurusha matangaazo yao, kupitia njia ya mtandaoni.

Sheria hii, kwenye sehemu yake ya kwanza, imeundwa na vifungu vitatu, kwani kile cha nne (4), kimefutwa na kati ya hivyo kimoja kinatoa jina la sheria na maana ya maneno, yaliomo kwenye sheria hiyo.

Sehemu ya pili ya sheria hii, imeundwa na vifungu kuanzia cha tano (5) hadi cha 10, na kubwa zaidi lililopo ni pamoja na uanzishwaji wa Tume ya Utangaazaji Zanzibar ‘TUZ’.



Kwenye sehemu ya tatu ya sheria, imeundwa na vifungu vinne (4) kuanzia cha 11 hadi cha 14, ni eneo lililotajwa zuio la utangaazaji, usiokuwa na leseni, masharti ya kuomba, utoaji wake na kiwango cha matumizi na kuongeza muda.

Sehemu ya nne (4), inaangalia uratibu na usimamizi wa utangaazaji, huku sehemu ya tano, ikundwa na vifungu saba (7) na ikiangalia zaidi amsuala kifedha.

Sehemu ya 6 ya sheria hii ya Utangaazaji Zanzibar nambari 7 ya mwaka 1997, imeundwa na vifungu vitano (5) kuanzia kile cha 26 hadi 30, ambacho, kinaelezea kufutwa kwa sheria nambari 25 ya mwaka 1961.

MANENO YENYE UKAKASI NDANI YA SHERIA HII

Wadau wa habari kila siku, wamekuwa wakirejea maneno yao, wakisema kuwa, neno hutafsiriwa kama lilivyo kwenye maandishi, na wengine wakaenda mbali zaidi kuwa, mtumiaji sio mtunzi.

Kwenye kifungu cha 7 (1) (d) lipo neno lililounda sentensi ‘kudhibiti shughuli za watangaazaji na maadili yao ya utangaazaji pamoja na wafanyabiashara wa vifaa vya utangaaji’.

Mdau wa habari Ali Khamis Haji wa Madungu Chake chake, anasema neno ‘kudhibiti’ linatoa tafsiri ya ukakasi, kwamba suala la kudhiti sio neno rafiki.

‘’Neno kudhibiti linaashiria namna ya kushika, kuweka chini ya ulinzi au wakati mwengine mtu anayefanyakazi chini ya uangalizi fulani, wa tasisi fulani,’’anasema.

Mkurugenzi Mtendaji wa Chama cha Waandishi wa Habari wanawake Tanzania TAMWA-Zanzibar Dk. Mzuri Issa Ali, anasema kwenye sheria za habari, neno ‘kudbiti’ linaleta ukakasi hasa kuelekea uhuru kamili wa habari.

Mchambuzi wa masuala ya sheria za habari Zanzibar Imane Duwe, anasema wakati wa Zanzibar kuwa na sheria mpya ndio huu, na wala kusiwe na maneno kwenye sheria, yanayoashiria uhalifu.

Hata kwenye kifungu hicho (h) lipo neno ‘kutoa maelekezo yoyote kwa biashara ya utangaazaji ambayo kwa maoni yake, itaona inafaa’ kwa mpewa leseni.

Neno kutoa ‘maelekez’o na jengine lile kwa ‘maoni yake itaona inafaa’, haya yamewaibua wadau wa habari na waandishi wa habari wakisema, yanaleta ukakasi.



Na ndio maana mwanasheria wa Shirika la Magazeti ya serikali Juma Khamis Juma, anasema neno moja tu lenye silabi mbili, likitafsiriwa linaweza kusababisha madhara.

‘’Neno ‘maelekezo’ au kwa ‘maoni’ ni hatari kuwemo kwenye maelezo ya sheria, au sentensi inayotoa amri ya jambo, hivyo kuelekea uhuru kamili wa habari, haya yanaukakasi,’’anasema.

Hata mdau wa habari ambae ni Mkuu wa wilaya ya Mkoani kwa sasa Khatib Juma Mjaja, anasema sheria za habari, hazitakiwi kutumika na maneno yenya tafsiri zaidi ya moja.

‘’Ukisema ‘akiona inafaa’, kwa ‘maoni yake’, akihisi, atatoa maelekezo au akisema ‘akiamua’, haya yote yanapingana na katiba na hasa kifungu cha 18,’’anasema.

Kifungu chengeni ni kile cha 15 (2) kuna msamiati kuwa ‘Tume inaweza kila baada ya muda na kwa idhini ya Waziri kwa tangaazo lililochapishwa katika gazeti rasmi, kutaja masharti hayo yatakayotekeleza na mpewa leseni’

Wadau wanassema, neno ‘tume inaweza’ haliaendani na wakati uliopo wa zama za ushirikishwaji na ushiriki na hasa Zanzibar, ikiwa ni nchi inayofuata mfumo wa demokrasia.

Mwandishi Salim Said Salim anasema, neno ‘tume inaweza’, sio sahihi kuwepo kwenye vifungu hasa ambavyo vinasimamia sheria ya habari hapa Zanzibar.

Mratibu wa Internews Zanzibar Zaina Mzee, anasema wakati umefika sasa Zanzibar kuwa na sheria bora na rafiki na yenye maneno yanayoimarisha uhuru wa habari.

‘’Inawezekana leo tunae Katib Mtendaji au waziri mzuri wa habari na pengine asikitumie kifungu hicho vibaya, lakini je kesho na keshokutwa tutakaempata, hatoyatumia atakavyo maneno hayo,’’anahoji.

Ndio maana anasema, ili kuhakikisha Zanzibar kuna kuwa na sheria bora na rafiki, Internews imekuwa ikiwakutanisha wadau, waandishi na wamiliki wa vyombo vya habari, ili kujadili kwa pamoja.



‘’Hamu ya Internews siku moja ni kwa Zanzibar kuwa na sheria bora, rafiki n ainayokuza na kuendeleza uhuru wa habari, ili wananchi wawe na maamuzi sahihi,’’anasema.

Anaamini kukiwepo kwa vyombo vya habari makini, waandishi wakaandika habari makini, zikahaririwa kwa umakini na wananchi watafanya maamuzi makini.

Mwandishi wa ZBC Khadija Kombo anasema, maneno kama hayo yenye ukakasi, ndio yanayoashiria shari baina ya sheria hizo na utendaji kazi wa vyombo vya habari.

Hata kifungu cha 18 (1), kinachompa waziri uwezo wa ‘kukagua’ ingawa kwa kushirikiana na Tume, au mwengine wa wengine kwa ukaguzi au wakaguzi kwa madhumini ya sheria hii.

Hapa neno ‘kukagua’, halijakaa vyema kwa waandishi na wamiliki wa vyombo vya habari, wakisema kazi ya habari haikaguliwi na hasa baada ya mpewa leseni kupewa leseni.

Kwa mfano mwandishi wa mtandaoni Talib Ussi Hamad wa Unguja anasema, neno ‘kukagua’ lina ukakasi mkubwa kuelekea uhuru kamili wa habari.

‘’Kwani isiwe pana neno kutembelea, kukukutana nao, kushauriana lakini suala la kuwepo kwenye kifungu cha sheria neno kukagua, ni kama vile wakati wowote akipenda,’’anaeleza.

Mwandishi Berema Suleiman wa Zenj Fm redio, anasema maneno kama hayo na mengine yanayofana nayo, yanaweza kutumika vibaya na waziri au mwengine atakaepewa mamlaka.

‘’Kwa mfano tunakumbuka wenzetu wa Cloud’s media walivamia usiku na aliyekuwa mkuu wa Mkoa, kwa madai ya kukagua, na tuliona athari iliyojitokeza,’’anafafanua.



Kifungu chengine chenye maneno yenye ukakasi na ukuaji wa wa uhuru wa habari ni cha 27 (1), ambapo waziri husika au mwengine aliyeidhinishwa, anaweza kutoa amri kumtaka mpewa leseni, atangaaze jambo lolote ambalo kwa maoni ya Waziri, lina maslahi kwa umma au uslama wa taifa.

Hapa wadau wa habari wanasema, kifungu hicho kipo kishari shari zaidi, maana kimebainisha uwezo wa Waziri, kumlazimisha mpewa leseni kutangaaza jambo ambalo anaona tu ni kwa maslahi ya umma au usalama wa taifa.

WANANCHI

Omar Haji Kassim na mwenzake Othman Omar Kombo wa Kambini kichokwe, wanasema waandishi wasipokuwa huru, hata wananchi hawatokuwa huru, kufanya uamuzi sahihi.

Mratibu wa Baraza la Taifa la watu wenye ulemavu Mashavu Juma Mabrouk anasema, wanavitarajia mno vyombo vya habari, kuibua changamoto za jamii, na hilo litawezekana ikiwa wako huru.



NINI ATHARI YAKE?

Moja wadau wanasema, ni kuwafanya waandishi wa habari kufanyakazi kwa woga na nidhamu iliyopindukia mipaka, huku ikieleweka kuwa, wao kazi yao ni kuitekeleza Katiba.

Mwandishi wa Mwanahalisi mtandaoni Jabir Idrissa, anasema athari kubwa ni wawekezaji sekta ya habari, kukosa hamu ya uwekezaji, na kundi kubwa kukosa ajira.

Miraji Manzi Kae wa redio Jamii Makunduchi, anasema woga wa waandishi kukosa kufichua maovu, wakati mwengine, hutokana na uwepo wa sheria kandamizi.

NINI KIFANYIKE?

Mwenyekiti wa Klabu ya waandishi wa Habari Zanzibar ‘ZPC’ Abdalla Mfaume, anasema moja ni kuzisemea sheria na vifungu kandamizi, ili waandishi wa habari wafanyekazi zao kama ilivyo, kwa makundi mengine.

Rahma Suleiman wa Gazeti la Nipashe, anasema waandishi na wadau wa habari, waungane kusindikiza mswada wa sheria habari Zanzibar ulipofikia, upelekwe hatua nyingine.

Mchambuzi wa sheria za habari Zanzibar Imane Duwe, anasema maneno kama ‘uwezo wa Mkurugenzi, Waziri, akiona inafaa, akihisi, kwa maoni yake’ kwenye sheria mpya ya habari yasitumike.

Mdhamini wa Baraza la Habari Tanzania MCT-Zanzibar Shifaa Said Hassan, anasema chengine ni kuharakishwa kwa mswaada wa sheria ya habari kufika barazani.

                              Mwisho

Comments